Saturday, August 5, 2017

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 12


ILIPOISHIA:
Alikuwa ni msichana mzuri sana, upande wa nyuma alikuwa amejazia huku kiuno chake kikiwa kimegawanyika, kama nyigu ambao kule kijijini tulikuwa tukiwaogopa kutokana na sumu yao wanapokung’ata.
Suruali ya jeans aliyovaa, ililifanya umbo lake lijichonge vizuri, ghafla akageuka, akanibamba nikiwa namtazama kwa nyuma, nikazidi kujisikia aibu.
SASA ENDELEA...
“Mbona unaniangalia hivyo?”
“Mimi?” Nilijifanya kuvunga, akanisogelea na kunipiga kakibao kepesi begani huku tabasamu pana likiwa limechanua kwenye kwenye uso wake. Na mimi nikawa nacheka huku aibu zikiwa zimenijaa.”
“Dar es Salaam unaishi sehemu gani?” aliniuliza swali ambalo lilikuwa gumu sana kulijibu kwani ukweli ni kwamba sikuwa naijua Dar wala sikuwahi kufika kabla. Nikawa nababaika mwenyewe, akajiongeza na kuniuliza:
“Kwani hii ndiyo mara yako ya kwanza kufika Dar?”
“Ndiyo,” nilijibu harakaharaka kwa sababu alikuwa amenipunguzia sana kazi ya kumjibu. Akaniambia kwamba yeye anaishi na wazazi wake Kijitonyama. Akaniambia kwamba alikuwa amemaliza chuo akisomea uhasibu na alikuwa anatoka Mbeya kuwasalimu bibi na babu yake wa upande wa mama.
“Wanaishi Mbeya sehemu gani?” nilimuuliza, akaniambia wanaishi Katumba, njia panda ya kwenda Mwakaleli. Maeneo hayo sikuwa nimewahi kufika zaidi ya kusikia tu kwa watu,  nikawa natingisha kichwa kumkubalia. Akaendelea kunieleza kwamba mama yake alikuwa Mnyakyusa lakini baba yake alikuwa ni mtu kutoka Mkoa wa Pwani ingawa hakunieleza ni kabila gani.
Hatimaye dakika kumi ziliisha, dereva akaanza kupiga honi akitupa ishara kwamba muda wa kuingia kwenye basi umefika. Kwa hizo dakika chache nilizokaa na msichana huyo, niligundua kwamba alikuwa mcheshi, mchangamfu na asiye na maringo kama walivyo wasichana wengi warembo kama yeye.
“Lakini hujaniambia unaitwa nani.”
“Unataka kujua jina langu?”
“Ndiyo.”
“Sitaki,” alisema huku akinipiga tena begani, akaanza kukimbia kuelekea kwenye basi. Sikuelewa kitendo hicho kilikuwa na maana gani, wakati anakimbia nilishuhudua kitu kingine ambacho kiliusisimua sana moyo wangu, mpaka nikawa najiuliza zile hisia nilizokuwa nazisikia kwa wakati huo zilikuwa na maana gani?
Kwa kifupi nilijisikia raha sana kufahamiana na msichana huyo. Niliendelea kumtazama akikimbia mpaka alipofika kwenye ngazi za kupanga kwenye basi, akageuka na kunitazama kisha akapanda ngazi. Na mimi nilitembea harakaharaka huku nikiendelea kuchekacheka mwenyewe, mkononi nikiwa na kopo la soda ambayo nilikua nimeinywa nusu.
Nilipopanda na kuingia ndani ya gari, ndugu zangu wote walishangaa kuniona nikiwa na soda ya kopo, tena nikinywa kwa mrija.
Niliwaona wote walivyomeza mate, wakawa wanaulizana nimeipata wapi soda hiyo? Sikuwajali kwa sababu bado nilikuwa na hasira nao, nikakaa kwenye siti yangu, nikageuka na kumtazama yule msichana ambaye mpaka muda huo hakuwa amenitajia jina lake, nikashtuka tena kugundua kwamba kumbe alikuwa ametulia akinitazama kila nilichokuwa nakifanya.
Macho yangu na yake yalipogongana, aliachia tabasamu hafifu halafu eti na yeye akakwepesha macho yake kwa aibu, yaani mwanzo mimi ndiyo nilikuwa nakwepesha macho yangu lakini ghafla na yeye alianza kukwepesha macho yake kwa aibu. Dereva aliondoa gari na safari ikaendelea.
Safari hii umakini ulikuwa ukinipungua sana kichwani mwangu kwani mara kwa mara tulikuwa tukitazamana na yule msichana na kuishia kuchekacheka tu. Nashukuru hakuna jambo lolote baya lililotokea mpaka tulipoanza kuingia mjini.
Tulipofika Kibaha, gari lilisimama na yule abiria aliyekuwa amekaa pembeni yangu, alisimama na kushuka, harakaharaka nikamuona yule msichana akikusanya kila kitu chake na kuja kukaa pembeni yangu. Aliponisogelea tu, nilianza tena kusikia harufu ya manukato aliyojipulizia, ambayo kiukweli yalinivutia sana.
Akakaa pembeni yangu na kuniegamia kimtindo kabla ya kujiweka vizuri kwenye siti yake.
“Yule niliyekaa naye hata stori hana, muda wote analala tu bora nikae na wewe,” alisema huku akinipigapiga begani, nikawa natabasamu tu kwani kiukweli hata mimi nilikuwa napenda kukaa naye siti moja.
“Ulisema unataka kujua jina langu?” alianzisha mazungumzo, niikamjibu kwa kutingisha kichwa, akaniambia ananipa mtihani nitafute mwenyewe jina lake. Kiufupi ni kwamba, kwa muda mfupi tu niliokaa naye, alionesha kupenda sana urafiki wetu uendelee, jambo ambalo hata mimi nilikuwa nalipenda ingawa mara kwa mara nilikuwa najishtukia.
Hata nilipokuwa nacheka, sikuwa napenda ayaone meno yangu kwani ya kwake yalikuwa meupe sana na masafi lakini kwangu mimi, hata sikuwa nakumbuka mara ya mwisho kupiga mswaki ni lini, si unajua tena maisha ya kijijini.
“Una simu?” aliniuliza swali ambalo lilinifanya nijisikie tena aibu. Sikuwa na simu, sikuwahi kumiliki wala sikuwa najua namna ya kuitumia, nikawa natingisha kichwa kukataa, akaniambia alikuwa na simu mbili lakini hiyo nyingine hakuwa akiitumia kwa sababu ilikuwa ya kizamani.
“Basi nipe mimi,” nilisema kwa utani kwani nilijua ni jambo ambalo haliwezekani, akacheka na kufungua kibegi chake kidogo, akatoa simu ndogo aina ya Nokia ya tochi na kunipa.
“Chukua utakuwa unatumia,” alisema. Nikapigwa na butwaa nikiwa ni kama siamini. Kuna wakati nilihisi kwamba pengine alikuwa akinitania lakini mwenyewe alisisitiza kwamba  ni kweli amenipa. Muda huo, tayari gari lilikuwa limeshawasili Ubungo, sikuwa napajua zaidi ya kusikia tu watu wakisema hapo ndiyo ubungo.
Tayari giza lilishaanza kuingia, taa nyingi zilizokuwa zinawaka kila upande zikanifanya nijihisi kama nilikuwa kwenye ndoto.
Waliosema mjini kuzuri hawakukosea, Dar ilikuwa na tofauti kubwa sana na kule kijijini nilikozaliwa na kukulia, kila kitu kilikuwa kigeni kwangu. Wakati nikiendelea kushangaashangaa, nilisikia mama akiniambia kwamba natakiwa kuwa makini kuchukua mizigo iliyokuwa imewekwa kwenye buti.
Harakaharaka nikateremka na abiria wengine, hata sikukumbuka nilipotezana saa ngapi na yule dada, ushamba wa mjini ulinipa mchecheto mkubwa ndani ya moyo wangu, nikaenda mpaka kwenye buti nikiwa na wale ndugu zangu wengine ambao nao walikuwa wakishangaashangaa, tukafanikiwa kushusha mizigo yetu yote na kuiweka pembeni.
“Twendeni nilisikia sauti ya baba akizungumza, kugeuka pembeni, sote tulipigwa na butwaa kumuona baba akiwa anafungua milango ya teksi. Hakuna aliyejua baba alifika saa ngapi Dar es Salaam kwa sababu kama aliweza mpaka kuzungumza na dereva wa teksi na kukaa pale wakitusubiri, maana yake ni kwamba aliwahi sana kufika.
“Unajua wewe huna akili kabisa,” baba alianza kunifokea baada ya kumaliza kupakiza mizigo kwenye teksi, nikawa nashangaa kwa nini baba ananiambia maneno hayo.
“Yule uliyekuwa umekaa naye kwenye basi ni nani?”
“Ni rafiki yangu.”
‘Unamjua wewe? Na hicho alichokupa una uhakika gani kama ni simu? Ujinga wako utaiponza familianzima,” alisema maneno ambayo yalinishangaza sana.

Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...