Wednesday, August 30, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 25


ILIPOISHIA:
Harakaharaka, huku akilia, aliwaita walinzi ambao nao walimuita daktari wa familia hiyo, muda mfupi baadaye wote wakawa wamejaa ndani ya chumba hicho wakijaribu kuokoa maisha ya msichana huyo lakini ilionesha kwamba tayari walikuwa wamechelewa.
SASA ENDELEA...
Shenaiza alikuwa akitapatapa, akirusharusha mikono na miguu, mapovu mengi yaliyochanganyikana na damu yakimtoka mdomoni na puani, harakaharaka Shenaiza alitolewa kwenye chumba alichokuwa amefungiwa na kulazwa juu ya kitanda cha magurudumu, akakimbizwa kwa kasi mpaka nje na kupakizwa kwenye gari.
Muda mfupi baadaye, gari lililombeba lilikuwa tayari lipo barabarani, likikimbia kwa kasi kubwa, taa zote za mbele zikiwa zimewashwa huku yule daktari akiwa bize kuhakikisha anaokoa maisha ya Shenaiza.
Japokuwa baba wa msichana huyo mrembo hakuwepo nchini kwa muda huo, tayari taarifa zilimfikia huko alikokuwa juu ya kilichomtokea binti yake.
Naye akajikuta akichanganyikiwa mno kwani Shenaiza alikuwa mtu muhimu sana kwake. Bila yeye, mambo yake mengi yangekwama, jambo ambalo hakuwa tayari kuona linatokea. Muda hohuo aliwapigia simu wasaidizi wake na kuwaambia ni lazima wafanye kila kinachowezekana kuhakikisha anapona.
Baada ya kufikishwa hospitalini, harakaharaka Shenaiza alilazwa juu ya kitanda chenye magurudumu, akakimbizwa kupelekwa kwenye wodi ya wagonjwa mahututi, madaktari kadhaa, wakisaidiana na yule daktari wa familia, walianza kuhaha kuhakikisha wanaokoa maisha ya msichana huyo.
*** 
“Lakini mimi sijafa Shenaiza, mimi niko hai.”
“Ungekuwa hai ndiyo ungekuwa huku? Acha kujidanganya Jamal!”
“Hapana sijafa! Mimi sijafa! Niko haiii,” nilisema kwa sauti kubwa iliyofuatiwa na kilio.
“Sasa unalia nini Jamal? Kwani kufa ni jambo la ajabu? Mbona mimi mwenyewe nimeamua kuyakatisha maisha yangu?”

“Hapana, mimi bado nina ndoto zangu nyingi sana sijazitimiza maishani. Isitoshe umri wangu bado mdogo, familia yangu haijafaidi matunda yangu hata kidogo, bado sijaoa wala sina mtoto hata mmoja, itakuwaje nife?”
“Kwani wote wanaokufa wanapenda wenyewe kufa? Usikufuru Jamal, inabidi umshukuru Mungu kwa kila kitu, naamini hakuna kilichoharibika, si utakuwa hapa na mimi?”
“Hapana Shenaiza, hapanaaa!” nilizidi kupingana naye, akazidi kuning’ang’aniza kwamba eti nilikuwa tayari nimekufa na hilo halikuwa tatizo kubwa kwa sababu hata yeye aliamua mwenyewe kufa.
Bado akili yangu ilikuwa na maswali mengi yaliyokosa majibu. Unajua mtihani ambao Mungu ametupa sisi wanadamu, ni kushindwa kuelewa kinachotokea baada ya mtu kufa. Kama angekuwepo mtu hata mmoja, ambaye angekuwa na uwezo wa kuelezea kwa ufasaha kinachotokea baada ya mtu kufa, pengine angewasaidia sana binadamu kupunguza hofu ya kifo inayowatesa.
Kwangu mimi hali ni tofauti, hata sielewi nitumie maneno gani kuelezea kilichotokea lakini naamini kwamba ukiendelea kunifuatilia msomaji wangu, utaelewa ni nini hasa kilichotokea na pengine kitakusaidia na wewe kuweza kuyaelewa maisha na kifo katika upeo mpana zaidi, pengine kuliko ulivyokuwa unafikiria mwanzo.
Bado mjadala mkubwa kati yangu na Shenaiza, ulikuwa ni juu ya suala la kifo. Msichana huyo alikuwa akisisitiza kwamba mimi na yeye tumekufa na ndiyo maana tulikuwa kule lakini mimi nikawa naendelea kumbishia kwamba sijafa kwa sababu bado nilikuwa na akili zangu timamu.
Nilikuwa naelewa vizuri kila kilichokuwa kinaendelea, jambo ambalo bado hakuna ushahidi wa kutosha kwamba wafu huwa wanaelewa kinachoendelea. Nitakuja kulifafanua hili zaidi hapo baadaye.
Basi ile safari ambayo hata sijui mwisho wake ulikuwa ni wapi, iliendelea, treni lilizidi kuchanja mbuga, moshi ukazidi kuongezeka mle ndani sambamba na kelele za vyuma kugongana. Hata hivyo, bado niliweza kumsikia vizuri Shenaiza kwa kila alichokuwa anakizungumza.
Bado nilikuwa na hamu ya kutaka kujua ni nini kilichotokea mpaka na yeye aseme amekufa kwa sababu mpaka muda huo, bado nilikuwa gizani. Nilifumba macho na kujaribu kuvuta picha kwa nguvu, nikashtuka kuliko kawaida kujikuta nimetokezea kwenye wodi nyingine tofauti na ile ambayo mwili wangu ulikuwepo.
Nilipotazama vizuri ndani ya wodi hiyo, kama ilivyokuwa mwanzo kule kwenye ile wodi niliyokuwa nimelazwa, madaktari wengi walikuwa wakihangaika kuokoa maisha ya mtu aliyekuwa amelala juu ya kitanda, akionesha kabisa kwamba alikuwa kwenye hatua za mwisho za uhai wake.
Nilipomtazama vizuri mtu huyo, hakuwa mwingine bali Shenaiza ambaye sekunde chache zilizopita nilikuwa nimekaa naye kwenye siti moja ya treni la ajabu. Ni hapo ndipo nilipoelewa kile alichokuwa anakisema Shenaiza kwamba ameamua kuyakatisha maisha yake.
Madaktari walikuwa wakihangaika mno, Shenaiza akaunganishwa kwenye mashine ya kumsaidia kupumua huku dripu nyingi zikitiririka kwa kasi kuingia kwenye mishipa yake ya damu.
Kibaya zaidi, kadiri muda ulivyokuwa unazidi kusonga mbele ndivyo mashine maalum ya kusoma mapigo ya moyo aliyokuwa ameunganishiwa msichana huyo na kuunganishwa kwenye kompyuta, ilivyokuwa ikionesha kwamba mapigo yake ya moyo yalikuwa yakishuka kwa kasi kubwa, jambo ambalo lilimaanisha kwamba muda mfupi baadaye, mapigo ya moyo yatasimama kabisa na kukata roho.
“Hapana! Hapana... Shenaiza noooo!” nilipiga kelele kwa sauti kubwa, nikajikuta muda huohuo nimehama kutoka kule hospitalini mpaka ndani ya treni, nikageuka kumtazama Shenaiza, nikamuona akiwa amejikunyata na kujiinamia, kama anayesubiri jambo fulani litokee.
Sijui nilipata wapi nguvu lakini nilijikuta nikimshika Shenaiza na kuanza kumtingisha kwa nguvu, akashtuka kwa nguvu na kunitolea macho akionesha kukasirishwa na kitendo changu cha kumshtua.
Wakati ananitazama, alianza kupiga chafya mfululizo, akili yangu ilihama tena na kurudi wodini, nikapigwa na butwaa baada ya kumuona mgonjwa akipiga chafya mfululizo huku damu ikimtoka puani na mdomoni kwa mabongemabonge!
“She is back into her consciousness! Ooh thanks God! She was almost dead!” (Amerejewa na fahamu zake! Ooh ahsante Mungu, alishafikia hatua ya kufa) nilimsikia daktari mmoja akipaza sauti mle wodini, nikaona nyuso za wote waliokuwemo ndani ya wodi hiyo ya wagonjwa mahututi zikianza kuonesha matumaini makubwa, tofauti kabisa na mwanzo.
Harakaharaka Shenaiza alizungukwa pale kitandani, kazi ya kunusuru maisha yake ikazidi kupamba moto. Nikiwa naendelea kushangaashangaa, nilishtuka nikiguswa begani, akili zangu zikarudi tena kule kwenye treni.
“Kwa nini umeniokoa? Ungeniacha nife,” alisema Shenaiza huku akilia, nikatanua mikono yangu kama ishara ya kumkumbatia, akajilaza kifuani kwangu na kunikumbatia kwa nguvu huku akiendelea kulia.
Nikiwa katika hali ileile, nilishtuka muda mfupi baadaye na kujikuta nikiwa nimejikumbatia mwenyewe. Shenaiza hakuwepo tena, nikageuka huku na kule, hakukuwa na mtu mwingine yeyote kwenye lile treni, nilibaki peke yangu huku mwanga wa ile taa iliyokuwa ndani ya behewa nililokaa ukizidi kufifia, muda mfupi baadaye giza nene likatanda kila mahali.
“Jamal! Jamal! Jamal!” nilishtuka baada ya kuisikia tena ile sauti nzito ya kutetemeka, iliyoniita kwa mara ya kwanza kabisa, ikiniita tena, ikafuatiwa na vicheko vya kutisha vya watu wengi, nikawa nageuka huku na kule lakini sikuona chochote zaidi ya giza nene, hofu kubwa ikatanda moyoni mwangu.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...