Thursday, August 3, 2017

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 10


ILIPOISHIA:
“Kuna tukio baya linataka kutokea, kuwa makini,” nilisikia sauti ya baba ikiniongelesha sikioni mwangu, nikageuka huku na kule, baba hakuwepo, nikajua kwa vyovyote lazima alikuwa ameona jambo ndiyo maana akanipa tahadhari, nikajiweka vizuri kitini, nikawa natazama huku na kule.
SASA ENDELEA...
Niliingiza mkono mfukoni na kutoa ile dawa aliyonipa baba, nikaishika ili chochote kikitokea iwe rahisi kufanya kama nilivyoelekezwa. Tukaanza kuteremka kwenye mteremko mrefu, wenye konakona nyingi na makorongo ya kutisha wa Kitonga.
Nilielewa kwa sababu gani eneo hilo lilikuwa maarufu sana, barabara ilikuwa imechomngwa pembezoni mwa milima na mawe makubwa, hali iliyofanya kama upande mmoja kukiwa na ukuta wa mlima basi upande wa pili kuna bonde refu sana.
Yaani kwa kutazama tu urefu wa yale makorongo, nilijikuta nikihisi kizunguzungu, nikawa najiuliza ikitokea dereva akakosea na kupeleka gari kwenye yale makorongo nini kitatokea? Sikupata majibu.
Safari iliendelea, dereva akawa amepunguza sana mwendo, abiria wote ndani ya gari wakiwa kimya kabisa. Nadhani kila mmoja alikuwa na kumbukumbu ya kilichotokea Mlima Nyoka. Ghafla tulishtuka baada ya kuona kuna lori la mafuta, tena likiwa na trela kwa nyuma, likija kwa kasi kubwa nyuma yetu.


Tulishtushwa na kishindo kikubwa kilichosikika nyuma, wote tukageuka na kusimama kwenye siti, tukawa tunatazama nini kinachoendelea? Inavyoonesha, lile lori lilikuwa limepasuka tairi la mbele na kumshinda dereva, sasa likawa linayumba barabara nzima.
Abiria wote walianza kupiga kelele kwenye lile basi, hakuna ambaye alijua nini kitatokea kwa sababu kama lile gari lori lingeendelea kuja kwa mwendo ule, lingeligonga basi letu kwa nyuma na kwa ile kasi yake, maana yake lingeturushia kwenye korongo refu na kutuangukia kwa juu.
Sijui kama kuna mtu angepona, ukizingatia kwamba lilikuwa ni lori la mafuta na lilionesha kuwa na mzigo. Nilichokifanya, kwa haraka nilimnyunyizia ule unga dereva ambaye bado hakuwa akijua afanye nini. Nilipomnyunyizia tu, nilimuona akibadili gia haraka, akaongeza mwendo na kulifanya basi lianze kushuka mteremko ule kwa kasi kubwa.
Kuongeza kasi kwa ghafla kuliwafanya abiria wengine wazidi kuchanganyikiwa, kelele zikazidi ndani ya basi, lile lori nalo likawa linazidi kuja kwa kasi kubwa nyuma yetu.
Wakati dereva akizidi kukanyaga mafuta na kulifanya basi lishuke kwa kasi ya ajabu mteremko ule hatari, ghafla tulishtukia lori jingine likiwa limepaki mbele yetu, dereva na utingo wake wakiwa wamekata matawi ya miti na kusambaza barabarani, ishara kwamba lilikuwa limeharibika.
Kwa kasi ambayo gari tulilopanda lilikuwa likishuka nayo, hata mimi mwenyewe sikuamini kama dereva ataweza kulimudu na kulikweopa lile lori mbele yetu.
Hata hivyo, dereva alitumia kile ambacho wengi huita uwezo binafsi, bila kupunguza mwendo hata kidogo, alizungusha usukani kwa kasi, gari likageuka kama linaenda kugonga jiwe kubwa lililokuwa pemebini ya barabara, kisha akazungusha tena usukani kwa kasi, gari likageuka tena upande wa pili.
Kitendo kile kililifanya basi letu lipenye kwenye uwazi mwembamba uliokuwepo kati ya lile gari lililoharibika na ukuta wa upande wa pili, kufumba na kufumbua likapita pale katikati kwa kasi kubwa na kulipita lile gari bovu, dereva akaanza kupunguza mwendo huku akibadilisha gia.
Sekunde chache baadaye, kilisikika kishindo kikubwa nyuma yetu, lile lori la mafuta lilikuwa limeligonga lile lori jingine bovu kwa nyuma na kulisukuma mita kadhaa kabla ya yote mawili kuangukia kwenye korongo refu, watu wote wakawa hawaamini kilichotokea.
Cha ajabu sasa, wakati watu wote wakitazama kilichotokea kule nyuma, nilishtuka kugundua kwamba kumbe aliyekuwa akiendesha gari hakuwa yule dereva wetu bali baba, macho yakanitoka pima nikiwa siamini ninachokiona. Alipogundua kwamba namtazama, naye alinigeukia na kunitazama kwa sekunde chache, akawa aanendelea kubadili gia huku akifunga breki.
Mbele kidogo kulikuwana uwazi pembeni ya barabara ambao uliwekwa maalum kwa ajili ya magari yanayoharibika njiani, akaendelea kufunga breki na hatimaye, akalisimamisha kabisa basi letu. Wakati watu bado wakiwa bize kushangaa kule nyuma, alifungua mlango wa dereva, akashuka huku akiendelea kunitazama na kunionesha ishara kwamba nisiseme chochote.
Akapotea kwenye upeo wa macho yangu na kuniacha na maswali mengi yasiyo na majibu. Cha ajabu kingine, aliposhuka, pale kwenye siti ya dereva alikuwa amekaa dereva yuleyule, tena akiwa amefunga na mkanda kabisa lakini kama ilivyokuwa mara ya kwanza, naye alionesha kushtuka kama mtu aliyekuwa amelala usingizi mzito. Akageuka huku na kule, macho yangu na yake yakagongana.
‘Kwani kumetokea nini?” aliniuliza kwa sauti ya chini huku akitaka mtu mwingine yeyote asielewe. Nadhani hata yeye alishagundua kwamba kuna mambo yasiyo ya kawaida yalikuwa yakiendelea.
“Ajali, ajali mbaya sana,” nilimjibu huku nikimuonesha kule nyuma tulikotoka ambako moshi mzito mweusi ulikuwa ukifuka kutoka bondeni. Tayari abiria wengi walikuwa wameshashuka kwenye basi na kuanza kurudi kule eneo la tukio. Harakaharaka dereva alifungua mlango na kushuka, na mimi ikabidi nishuke tena safari hii nilipitia pale kwenye mlango wa dereva.
Tukawa tunakimbilia pale eneo la tukio. Trela moja la lile lori la mafuta, lilikuwa limekatika na kuanguka katikati ya barabara kimshazari, jambo lililofanya mawasiliano kati ya pande hizo mbili za barabara yakatike. Hakukuwa na gari ambalo lingeweza kuvuka tena mpaka trela lile liondolewe.
Ajali ilikuwa mbaya kiasi cha kumfanya kila mmoja aliyeshuhudia, ainue mikono yake juu na kumshukuru Mungu kwa sababu kama isingekuwa miujiza iliyotokea, ilibidi basi letu ndiyo ligongwe na kuangukia kule bondeni kisha kuanza kuungua kama ilivyokuwa imetokea.
Tukiwa bado tunaendelea kushangaa kilichotokea, tulishangaa kuona mtu akitoka ndani ya lile lori la mafuta lakini mwili wake wote ukiteketea kwa moto, akawa anajaribu kukimbia lakini hakufika mbali, moto ukamzidi na kumfanya aanguke chini.
Kwa jinsi magari hayo yalivyodondokea chini bondeni, hakuna mtu yeyote ambaye angewahi kwenda kumsaidia yule mtu kwa sababu kwanza eneo lenyewe lilikuwa haliwezi kupitika kirahisi, watu wakawa wanapiga kelele huku tukimshuhudia yule mtu ambaye sijui ndiyo alikuwa dereva au utingo wa gari lililopata ajali akiteketea bila msaada wowote.
Muda mfupi baadaye, magari mengine mengi yalishawasili eneo hilo na kwa sababu barabara ilikuwa imefungwa, yalisimama na kupanga foleni ndefu, abiria na madereva wakawa wanashuka kuja kujionea kilichotokea.
Kila aliyekuwa anaona kilichotokea, alikuwa haamini kabisa. Ilikuwa ajali mbaya mno ambayo kama ingehusisha gari la abiria, sidhani kama kuna mtu yeyote angetoka salama.
Kwa kuwa tulikuwa nyuma ya muda na bado tulikuw ana safari ndefu, ilibidi turudi kwenye basi letu, dereva naye akawa anaonekana kuwa na maswali mengi kuliko majibu.
Japokuwa kwa mara nyingine abiria wote walikuwa wakimsifia kwa jinsi alivyoweza kuepusha ajali ile, mwenyewe alikuwa akijua kutoka ndani ya moyo wake kwamba siyo yeye aliyefanya kazi hiyo na hakuwa akijua chochote kilichotokea.
Tulirudi kwenye basi na baada ya kuhakikisha abiria wote wameingia, dereva aliondoa gari kwa mwendo wa taratibu, gumzo kubwa ndani ya basi likawa ni juu ya ajali hiyo. Wakati watu wakiendelea kujadiliana kuhusu ajali hiyo, mimi bado nilikuwa na maswali mengi mno kuhusu baba.
Bado sikuwa na majibu na hakukuwa na mtu yeyote wa kunijibu zaidi ya baba mwenyewe. Jambo kubwa ambalo lilikuwa likijirudia ndani ya kichwa changu, lilikuwa ni je, kweli baba ni mchawi?
“Unasemaje?” nilisikia sauti ya baba akiniuliza kwa ukali, nikageuka huku na kule lakini baba hakuwepo.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...