Thursday, October 26, 2017

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 49


ILIPOISHIA:
Nilipofika, na mimi nilijifanya ni mwombolezaji wa kawaida tu, nikawasalimia baadhi ya watu kisha nikajichanganya na waombolezaji wengine. Ghafla nilishtuka baada ya kuona kitu ambacho sikukitarajia, nikahisi kijasho chembamba kikianza kunitoka, mara hirizi yangu ikaanza kunibana kwa nguvu, kufumba na kufumbua kamba yake ikakatika, ikadondoka chini!
SASA ENDELEA...
“Mungu wangu!” nilijikuta nimetamka kwa sauti, hali iliyofanya watu wote washtuke, hata wale ambao hawakuwa wameniona nikiwasili eneo hilo, waligeuka na kunitazama, nikajihisi mwili ukiishiwa nguvu na kunyong’onyea kama nimepigwa na shoti ya umeme.
Sikujua nifanye nini kwa wakati huo, watu wakawa bado wamenikazia macho, kila mtu akiwa na shauku kubwa ya kutaka kujua mimi ni nani na nini kimetokea mpaka nikashtuka kiasi hicho.
“Wasalimu watu wote kwa heshima kisha wape pole,” nilisikia sauti ya baba masikioni mwangu, ghafla nikajikuta nimepata nguvu na kuwa na imani kubwa kwamba hata iweje, baba ameshajua kinachoendelea kwa hiyo atanisaidia.

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 47


ILIPOISHIA:
“Nataka nikalale na dada Shenaiza,” alisema kwa sauti ya kudeka huku akinisogelea na kujilaza kifuani kwangu, nikapitisha mkono wangu na kumshika kiunoni, nikamuona akiruka kama aliyepigwa na shoti ya umeme.
SASA ENDELEA...
“No! Usifanye hivyo,” alisema Firyaal huku akinitoa mkono kwa staili ya ‘sitaki nataka’, nikamvutia kwangu na kusababisha tuwe tunatazamana katika umbali usiozidi nchi tano, kiasi cha kila mmoja kuwa anazisikia pumzi za mwenzake.
“This is not the right time,” (Huu siyo muda muafaka) alisema huku akiipitisha mikono yake na kunishika shingoni, kwa mara nyingine nikamshika kiunoni, akashtuka tena, safari hii kwa nguvu zaidi na kufumba macho yake mazuri, tukagusanisha ndimi zetu na kuanza kuwaiga njiwa wanavyoyalisha makinda yao.
Jambo la ajabu lilitokea kwenye hisia zangu, nikawa nahisi kama nipo kwenye ulimwengu mwingine wa tofauti kabisa, tuliendelea kugandana kama ruba kwa sekunde chache, kelele za kitasa cha chumba alichokuwa amelala Raya ndizo zilizotushtua.
Harakaharaka nikamuachia Firyaal na kumuonesha kwa ishara kwamba aende chumbani alikokuwa amelala dada yake, kweli alifanya hivyo, akakimbia kwa kunyata wakati mimi nikienda kumfungulia Raya.

Wednesday, October 25, 2017

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 48


ILIPOISHIA:
Nilichopanga kichwani, ni kuchukua maelekezo vizuri kwa yule mtu aliyesema marehemu ni jirani yake kisha kwenda kwanza mpaka eneo la ajali na baada ya hapo, nitakwenda Tumbi kujionea hali ya mgonjwa na hiyo maiti kama nitapata nafasi. Nilikuwa na shauku kubwa ya kujua kila kitu maana moyo wangu ulikuwa na hatia kubwa, hasa kutokana na jinsi taarifa za ajali ile zilivyowaumiza mioyo abiria wengi.
SASA ENDELEA...
Safari iliendelea na hatimaye tukawasili Kibaha, gari liliposimama tu, nilimuwahi yule abiria aliyekuwa akisimulia kuhusu ile ajali, nikamsalimu na kumuomba anielekeze ulipo msiba kwa sababu aliyefariki ni ndugu yangu.
“Ni Mlandizi, ukishuka tu pale kituoni, uliza mtu yeyote eti kwenye msiba wa mtoto aliyekufa kwenye ajali ni wapi? Huwezi kupoteza, mtoto alikuwa anafahamika sana yule kutokana na jinsi alivyokuwa na heshima,” alisema yule abiria, nikamshukuru.
Nilipoachana naye, nilimfuata dereva ili anielekeze sehemu gari lilipopata ajali kwani kuna muda nilimsikia akisema kwamba eneo hilo ni baya sana, ajali huwa zinatokea mara kwa mara. Eneo lenyewe nilikuwa nalifahamu lakini sikujua naweza kufikaje.

Seven Days ih Hell (Siku Saba Kuzimu)- 46


ILIPOISHIA:
“Ulisema unasomea IT, hebu chukua ile laptop pale uje hapa unisaidie kitu,” nilimtega, naye ni kama alikuwa akiisubiri nafasi hiyo, harakaharaka aliinuka pale alipokuwa amekaa, akaenda kuchukua laptop ya Shamila na kuja nayo kwenye lile kochi nililokuwa nimekaa, akaja kukaa karibu kabisa na mimi kiasi cha kunifanya niwe nalisikia joto la mwili wake, lililonakshiwa kwa manukato mazuri aliyokuwa amejipulizia.
Mara mlango wa jikoni ukafunguliwa.
SASA ENDELEA...
“Vipi?” Shamila aliuliza huku akiwa ni kama ameshtuka f’lani hivi kuniona nikiwa nimekaa jirani namna ile na Firyaal.
“Kuna kazi namuelekeza anisaidie.”
“Ooh! Tena huyo atakufaa zaidi, si amesema anajuajua mambo ya IT?”
“Ndiyo japo bado sijathibitisha,” nilisema huku nikijifanya kumkandamiza Firyaal ili kuua soo, naye ni kama alijua kilichokuwa ndani ya akili yangu, akatulia kiasi cha kufanya iwe vigumu kwa Shamila kuelewa kilichokuwa kikiendelea kati yangu na msichana huyo mdogo lakini mrembo.
Akaenda kwenye friji na kuchukua baadhi ya vifaa kisha akarudi jikoni, akaniacha nikiwa bize nikijifanya namuelekeza kitu Firyaal ambaye naye alikuwa akiitikia kwa umakini, alipoingia jikoni tukatazamana.

Tuesday, October 24, 2017

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 47


ILIPOISHIA:
“Broo vipi unaenda?” alisema huku akisimamisha Bajaj yake jirani kabisa na pale nilipokuwa nimesimama, nadhani kwa sababu ya kigiza kile cha alfajiri hakuwa ameniona vizuri, aliniponisemesha na mimi kumtazama usoni, niliona jinsi alivyoshtuka, akataka kuondoa Bajaj yake haraka lakini alishachelewa.
SASA ENDELEA...
Nilishika bomba la Bajaj yake na kuingia, nikakaa siti ya nyuma, akawa ni kama amepagawa maana hakujua kama akimbie na Bajaj au aiache akimbie kwa miguu.
“Simama kwa usalama wako,” niliongea kwa sauti ya mamlaka, nikamuona jinsi alivyokuwa akihangaika, kijasho chembamba. Hakuwa tayari kusimama, inaonesha alikuwa akiniogopa sana, nilichoamua kukifanya ilikuwa ni kumtumia kutimiza mahitaji yangu.
Nilivuta pumzi ndefu na kuzibana kama baba alivyonielekeza, nikaweka utulivu kidogo kisha nikamuamrisha kunipeleka Ubungo. Nilifanya hivyo kwa kuzungumza moyoni maana ndivyo nilivyoelekezwa, nikamuona akizidi kuichochea Bajaj yake.
Hata hivyo, njia aliyokuwa anapita, ilikuwa ni ileile tuliyoipita jana wake wakati tukielekea Ubungo kupanda magari ya kwenda Kibaha. Alizidi kuongeza kasi, akawa anakimbia kama mshale, mwenyewe alidhani ananikimbia lakini kumbe tayari nilishaingia ndani ya akili yake.
Huwa si kawaida ya Bajaj kukimbia spidi kubwa na kuyapita magari lakini siku hiyo iliwezekana. Baada ya dakika kadhaa za kukimbia kwa kasi kubwa kwenye lami, hatimaye tuliwasili Ubungo, nikavuta tena pumzi na kumpa amri ya kusimama kwenye kituo cha mafuta.

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 45


ILIPOISHIA:
Nguo maalum aliyofunikwa upande wa kichwani, ilifanya iwe vigumu kwa mtu yeyote kumtambua, tukaendelea kusonga mbele mpaka tulipofika kwenye geti la kutokea nje ya hospitali, hapo tukakumbana na kipingamizi ambacho hakuna aliyekitegemea, mapigo ya moyo wangu yakawa yananienda mbio kuliko kawaida.
SASA ENDELEA...
“Haroo! Mnaenda wapi usiku? Harafu hao wagonjwa mbona mumewafunika sura, wafunueni, hima,” alisema askari aliyekuwa amevalia sare maalum, mkononi akiwa ameshika bunduki. Ilibidi Shamila atumie mbinu ya ziada kumtuliza kwani tayari alishaonesha wasiwasi nao.
“Kamanda, ina maana hata mimi hunijui? Hiki hapa ni kitambulisho changu, naitwa Shamila, nawapeleka wagonjwa wangu hapo kwenye maabara za Lancet hapo nje kwenye kipimo cha MRI, si unajua humu ndani hakuna na isitoshe kesho asubuhi kutakuwa na foleni kubwa sana,” alisema Shamila kwa lafudhi laini ambayo ilimfanya yule mlinzi awe anamtazama tu usoni.
“Ooh! Nesi Shamira, kumbe ni wewe, basi wapereke ila ukitoka basi uje hapa nina mazungumzo na wewe kidogo sawa nesi,” alisema mlinzi huyo kwa lafudhi ambayo ilionesha dhahiri kwamba ni Mkurya, kwa kutambua udhaifu wake, Shamila alimbania kijicho kimoja, akawa anachekacheka mwenyewe na kwenda kufungua geti.

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na hatia)- 46


ILIPOISHIA:
Tangu nizaliwe, sikuwahi kuchinja hata kuku tu, achilia mbali ndege tuliokuwa tukiwawinda kule kijijini kwetu lakini sasa eti nilikuwa natakiwa nimchinje binadamu, mtoto asiye na hatia yoyote ili nifaulu mtihani na kuwa mwanachama kamili, nilijikuta nikitetemeka kuliko kawaida.
Nilikichomoa kisu pale kiunoni nilipokiweka, mikono ikawa inatetemeka kuliko kawaida, nikawa namtazama mtoto yule usoni, nilijikuta nikiingiwa na huruma isiyo ya kawaida.
SASA ENDELEA...
Kisu kikadondoka na kwenda kujikita kwenye udongo. Nikamuona Mkuu akinikata jicho la ukali, akatembea kwa hatua zenye vishindo vizito mpaka pale nilipokuwa nimesimama, akainama kwa tabu na kukichomoa kile kisu, akanishikisha mkononi.
Baada ya hapo aliingiza mkono kwenye kimkoba chake kidogo cha ngozi, akatoa kichupa kilichokuwa na ungaunga mweusi, akamimina kwenye viganja vya mikono yake kisha akanipulizia usoni bila kusema chochote, nikapiga chafya mbili mfululizo kisha nikaanza kuona kama akili zangu zinabadilika jinsi ya ufanyaji kazi wake.
Hata sijui nini kiliendelea lakini baadaye akili zangu zilipokuja kukaa sawa, nilikuwa nimeshika kisu kwa nguvu huku mwili wangu ukiwa umetapakaa damu, watu wote wakawa wanashangilia kwa nguvu.

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 44


ILIPOISHIA:
Ilibidi Raya abaki palepale hospitalini mpaka usiku ili iwe rahisi kufanya kazi yetu, muda ukazidi kuyoyoma na hatimaye giza likaingia, ule muda tuliokuwa tukiusubiri kwa hamu ukawa umewadia.
SASA ENDELEA...
“Tunakusikiliza wewe Shamila!”
“Yaah! Inabidi mnisikilize kwa makini vinginevyo hakuna kitakachofanikiwa.”
“Tunaanzia wapi?” nilimuuliza Shamila huku mapigo ya moyo wangu yakinienda mbio.
“Tulia Jamal, mbona una haraka namna hiyo,” alisema Shamila, nikashusha pumzi ndefu na kutulia, hakuna muda ambao nilikuwa nahitaji msaada wake kama huo na kubwa zaidi, sikuwa mimi tu ambaye nilikuwa nahitaji msaada wake, bali Shenaiza pia.
Shamila aliingia kwenye chumba cha kubadilishia nguo, muda mfupi baadaye alitoka akiwa na gauni jingine, akampa Raya na kumuelekeza kuingia kule ndani kwenda kubadilisha nguo. Kweli akatii alichoambiwa, muda mfupi baadaye akatoka akiwa ndani ya mavazi ya kinesi, usingeweza kumtambua kwamba hakuwa nesi.

Monday, October 23, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 43


ILIPOISHIA:
Kauli yake hiyo ilitufurahisha sana mimi na Shamila, tukawa na uhakika kwamba sasa kazi itakuwa nyepesi kwa sababu tayari tutakuwa na mtu kutoka ndani kabisa, ambaye angetusaidia kutimiza lengo letu la kupambana na mtu huyo hatari.
SASA ENDELEA...
“Kwa hiyo tunaanzia wapi?” nilimuuliza Shamila, akawa ni kama anayetafakari kitu kisha akaniambia ameshapata majibu.
“Ngoja niende kwanza na huyu binti nikampe hiyo hard disk yake,” alisema Shamila.
“Utaweza kuichomoa kwenye kompyuta?”
“Mimi naweza, nasomea Information Technology niko mwaka wa pili,” alisema Firyaal ambaye alikuwa amefanana sana na Shenaiza, yaani hata bila kuuliza ungemjua tu kwamba ni ndugu yake.
“Sijamaliza kukopi data ninazozihitaji lakini.”
“Nitakusaidia pia, ninayo ‘back up’ kubwa tu nyumbani, naweza kuhamisha data zote na kukuletea,” alisema msichana huyo, nikawa namtazama usoni kwani aliyokuwa akiyasema hayakuwa yakifanana na umri wake.
Kwa kumtazama alionekana kama msichana mdogo ambaye kwa makadirio ungeweza kudhani yupo kidato cha pili au cha tatu lakini kumbe tayari alishafika kidato cha sita na sasa alikuwa chuoni.

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 42


ILIPOISHIA:
“Una..ta..ka kufa...nya ni...ni,” sikumalizia kauli yangu, akawa tayari ameshafika pale kitandani, tukagusanisha ndimi zetu huku Shamila akionesha kweli kudhamiria kile alichokitaka. Hakuogopa kabisa kwamba pale ni wodini.
SASA ENDELEA...
Nilijaribu kumzuia lakini haikusaidia kitu, alishadhamiria na kwa ilivyoonesha, alikuwa tayari kufanya chochote ili apate alichokuwa anakitaka. Tuliendelea kugusanisha ndimi   zetu huku mikono yake laini ikitalii kwenye viunga mbalimbali vya mwili wangu, nikaanza kuhisi hali ya tofauti.
Unajua jambo ambalo nitaendelea kulisema kila siku, hakuna jambo baya kama kuyajaribu mapenzi. Wazee wetu waliosema kwamba mapenzi hayajaribiwi, walikuwa sahihi kabisa. Wakati naanza uhusiano wa kimapenzi na Shamila, nilikuwa najua kabisa kwamba tayari ninaye Raya ambaye ananipenda sana na tumeshaahidiana vitu vingi, tena kibaya zaidi mimi ndiyo nikiwa mwanaume wa kwanza maishani mwake.
Akilini mwangu nilijua kwamba hata nikimkubalia Shamila, haiwezi kuwa na tatizo lolote kwa sababu kiukweli sikuwa nimempenda kutoka ndani ya moyo wangu na nilipanga kumtumia kama daraja tu la kunifanya nipate nilichokuwa nakitaka kwa urahisi.

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...