Tuesday, August 22, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 20


ILIPOSHIA:
Mpaka muda huo nilikuwa nimeshindwa kabisa kujizuia nisiendelee kuporomokea kule chini, kwa mbali nikaanza kuliona shimo kubwa ambalo ukubwa wake hata sijui nifananishe na nini lakini kwa kifupi lilikuwa kubwa mno, lisilo na mwisho, moto mkali ukiwa unawaka ndani yake. Kibaya zaidi, na mimi nilikuwa nikiendelea kuporomoka kuelekea ndani ya shimo hilo, nikajua huo ndiyo mwisho wangu.
SASA ENDELEA...
“Jamal! Jamal! Don’t go my love, come back to me! Come back Jamal,” (Jamal! Jamal! Usiende mpenzi wangu, rudi kwangu! Rudi kwangu Jamal) wakati nikiendelea kuporomokea kule kwenye lile shimo kubwa lililokuwa na moto mkali ambao siwezi kuuelezea, nilisikia sauti ikiniita.
Tofauti na sauti za kutishatisha nilizokuwa nikizisikia, hii ilionesha dhahiri kwamba siyo ngeni masikioni mwangu. Ilikuwa ni sauti ambayo niliitambua kuwa ni ya Raya, msichana aliyetokea kunipenda kwa moyo wake wote.
Raya alikuwa akipaza sauti huku akilia, maneno aliyokuwa akiniambia yalinichoma sana moyoni mwangu.
Katika hali ambayo sijui niielezeeje, nilijikuta nikipata nguvu kubwa kutoka ndani, nikajipindua kwa nguvu na kujikuta ile kasi ya kuporomokea kule chini inapungua, nikazidi kufurukuta kupambana na ile nguvu kubwa iliyokuwa inanivuta na hatimaye nikajikuta nikiangukia sehemu nyingine tofauti kabisa na kule nilikokuwa nikielekea.

Pale nilipoangukia, palikuwa na unyevunyevu mkubwa chini utafikiri nimekanyaga matope lakini giza lilikuwa nene pengine hata kule nilikotoka, nikawa naangaza macho huku na kule lakini sikuweza kuona chochote. Ukimya wa ajabu ukatanda kiasi cha kunifanya nianze kuyasikia mapigo ya moyo wangu yalivyokuwa yakinidunda.
Kufumba na kufumbua, nilijikuta nimerudi pale nilipokuwepo mwanzoni kabisa, kwenye kona ya ile wodi niliyolazwa. Kama ilivyokuwa mwanzo, nilikuwa nauona mwili wangu ukiwa umelazwa pale kitandani lakini tofauti na awali, safari hii nilikuta ubize mle ndani ya wodi ukiwa umeongezeka sana.
Madaktari walikuwa wakipigana vikumbo, kila nesi alikuwa bize kuhakikisha anaokoa maisha yangu. Sikuelewa nini kimetokea mpaka ubize uongezeke kiasi kile lakini niliwasikia baadhi ya madaktari wakijadiliana kwamba kilichonitokea kilikuwa kitu adimu sana.
“His heartbeats almost stopped but now they are stabilizing, ooh my God he was dead!” (Mapigo ya moyo wake yalisimama kabisa lakini sasa naona yameanza kurudi kwenye hali yake ya kawaida, ooh Mungu wangu, alikuwa tayari amekufa).
“It’s my eleventh year in this career and I have never witnessed something like this,” (Huu ni mwaka wangu wa kumi na moja nafanya kazi hii, sijawahi kushuhudia tukio kama hili) alisema daktari mmoja, kila mtu akawa anaendelea kuzungumza lake.
Bado niliendelea kujiuliza maswali mengi bila majibu lakini kwa jinsi mazungumzo hayo yalivyokuwa yakiendelea, inaonesha nilikuwa nimetokewa na jambo baya sana. Nikiwa bado palepale kwenye kona ya ile wodi, nikiangalia kila kilichokuwa kinaendelea mle ndani, niliisikia tena ile sauti niliyoisikia muda mfupi uliopita, tena ikizungumza maneno yaleyale.
“Jamal! Jamal! Don’t go my love, come back to me! Come back Jamal,” (Jamal! Jamal! Usiende mpenzi wangu, rudi kwangu! Rudi kwangu Jamal).
Ilikuwa ni sauti ya Raya na ilionesha ikitokea nje ya ile wodi. Nilijikuta nikiwa na shauku ya kutaka kumuona Raya, ile kuwaza tu kwamba nataka kumuona, nilijikuta tayari namtazama lakini katika mazingira ambayo yalionesha kwamba yeye pamoja na watu wengine wote waliokuwa wamemzunguka, hawakuwa na taarifa juu ya uwepo wangu mahali pale.
“Jamal is dead! (Jamal amekufa) Nitakuwa mgeni wa nani mimii? Eeeh Mungu, kwa nini mimi? Why?”
“Raya ukilia sana unakufuru. Wewe unajua jinsi Jamal alivyo rafiki yangu kipenzi lakini mwenzio bado sitaki kuamini kama ni kweli ametangulia mbele za haki. Hebu jikaze, tunaweza kuwa tunamchulia akafa kweli.”
“Usinipe moyo Justice, wote tumeshuhudia mashine ya kusoma mapigo yake ya moyo ikishuka mpaka mwisho kuonesha kwamba mapigo yake ya moyo yamesimama, madaktari wamefanya kila kitu na kujiridhisha kwamba amekufa, ina maana huamini tu?”
“Angekuwa ameshakufa angezungushiwa shuka la kijani pale kitandani kwake na madaktari wote ungeona wameshatoka chumba cha wagonjwa mahututi, mimi naamini bado yupo hai,” Justice na Raya walikuwa wakizungumza pale nje, Raya akilia kwa uchungu huku wafanyakazi wenzao kadhaa pamoja na watu wengine, wakisaidiana kumtuliza msichana huyo.
Pembeni kulikuwa na kundi lingine la watu ambao siwafahamu vizuri, lakini nao walionesha kufika pale kwa sababu yangu, muda mwingi wakawa wanajadiliana huku wakiwatazama akina Raya.
Niliwaona pia waandishi wawili wa habari, mmoja nadhani alikuwa anatoka kwenye kituo cha runinga na mwingine wa magazeti. Niliwatambua hivyo kutokana na jinsi walivyokuwa wamevaa na zana za kazi ambazo kila mmoja alikuwa amebeba. Nilijaribu kuangaza huku na kule kuangalia kama nitamuona Shenaiza lakini hakuwepo eneo hilo.
Nilitamani sana kujua ukweli wa mambo yote ambayo Shenaiza alikuwa akinificha lakini sikujua nitaanzia wapi. Yeye ndiye aliyekuwa chanzo cha matatizo yote yaliyonitokea lakini cha ajabu ni kwamba hata mimi, muathirika namba moja wa mambo yote yale yaliyokuwa yakiendelea kutokea, nilikuwa sielewi hasa nini kilichojificha nyuma ya pazia.
Kwa tafsiri nyepesi nyepesi, kama Mungu angeamua kunichukua moja kwa moja, ningeacha maswali mengi sana ambayo hakuna mtu yeyote ambaye angeweza kuyajibu, zaidi ya Shenaiza mwenyewe. Hali ilikuwa ya simanzi kubwa pale nje ya hospitali, niliwaona watu wengine wakizungumza na simu, kila mmoja akilitaja jina langu.
Maneno mengi yalikuwa yakiendelea kumtoka Raya, akiendelea kulia kwa uchungu kiasi cha kufikia hatua ya kukufuru. Kwa juujuu tu, kupitia maelezo yake pamoja na yale niliyoyasikia kule ndani kwa madaktari, nilielewa kilichokuwa kimetokea.
Ilionesha kwamba, kuna muda mapigo ya moyo wangu yalisimama, kwa tafsiri nyepesi, kuna muda nilikufa! Lilikuwa ni jambo la ajabu ambalo lilinitisha sana. Sikuelewa ni muda gani nilikuwa nimekufa kwa sababu muda wote nilikuwa timamu na nilikuwa naelewa kila kilichokuwa kinaendelea.
Sikukumbuka muda ambao pengine nilipoteza fahamu au sikuwa naelewa kinachoendelea! Nasisitiza tena, muda wote nilikuwa na akili zangu timamu. Nilijisikia uchungu sana kwa jinsi Raya alivyokuwa akilia, ukichanganya na hofu kubwa niliyokuwa nayo, nilijikuta nikianza kutokwa na machozi. Ajabu ni kwamba, wakati mimi nikiendelea kulia, wale madaktari pale kitandani walishtuka baada ya kuona mwili wangu nao ukitokwa na machozi, wakawa wanatazamana. Nikiwa naendelea kulia, nilipaliwa na mate, hali iliyofanya nikohoe mfululizo, ajabu zaidi, na ule mwili wangu pale kitandani ukakohoa, madaktari wakazidi kupigwa na butwaa, wakawa wanatazamana wakiwa ni kama hawaamini kilichokuwa kinatokea.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...