Tuesday, September 5, 2017

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 35



ILIPOISHIA:
NIKIWA bado hata sijui nini cha kufanya, nilishtukia nikifungwa mikono na miguu, nikajaribu kukurupuka lakini sikuweza kufanya chochote, ikabidi nitulie na kuanza kumtazama ni nani aliyenifanyia kitendo hicho na alikuwa na lengo gani kwangu maana niliona kifo changu kikiwa kimewadia. Na hata kama ningeuawa, kila mtu angeamini aliyekufa ni mbwa mkubwa.

SASA ENDELEA...
“MIMI sipendi mtu mkaidi, siku nyingine nitakuacha uwe mbwa koko, unafikiri unaweza kunikimbia mimi?” alikuwa ni Isri, akiwa anahema huku jasho likimvuja kwa wingi. Nilitaka nimuombe msamaha lakini sauti haikutoka, nikawa naendelea kutokwa na machozi kwa wingi.
Aliniinamia pale chini, akanionyesha ishara nifumbue mdomo, nikafanya hivyo, akaingiza mkono mfukoni na kutoa kichupa kilichokuwa na maji, akayamimina yote mdomoni mwangu. Yalikuwa machungu sana lakini nilivumilia, akanionyesha ishara kwamba niyameze.
Nilifanya hivyo, nikahisi kama mwili wangu wote unawaka moto kwa maumivu lakini kufumba na kufumbua, nilijikuta nikibadilika na kurudi kwenye hali yangu ya kawaida. Alinifungua ile kamba ya shingoni kisha mikononi na miguuni, akaniambia nisimame lakini nilishindwa kufanya hivyo kwani sikuwa na nguo hata moja mwilini, akafungua kimfuko alichobeba mgongoni na kunirushia nguo zangu.


Yaani kama kuna mtu anabisha uchawi haupo kwenye hii dunia, basi anajidanganya sana, kuna uchawi na wachawi na wengine wana uwezo mkubwa kuliko unavyoweza kufikiri. Sijui hata hizo nguo nilizivua saa ngapi na yeye alizipata wapi, sikutaka kuhoji, harakaharaka nilizivaa huku nikitazama huku na kule kama hakuna mtu yeyote anayetuona.
Bado mwili wangu ulikuwa na harufu ya mbwa-mbwa na mikono ilikuwa imechubuka nadhani ni kwa sababu ya kukimbia kama mbwa.
“Kwa nini unanifanyia hivi Isri? Kosa langu ni nini?”
“Sasa kwani mimi nimekufanyaje? Badala unishukuru unaanza kunilaumu tena.”
“Nikushukuru! Nikushukuru kwa lipi,” nilisema kwa hasira huku nikimsogelea Isri mwilini, mwili wangu ukitetemeka kwa jazba.
“Unataka kufanya nini Togo!”
“Nataka unieleze, kwa nini umenifanyia hivi? Unanijua au unanisikia?” niliwaka kwa jazba. Miongoni mwa vitu ambavyo nilikuwa najivunia na hata wenzangu kule kijijini walikuwa wakiniogopa, ni ubavu niliokuwa nao. Hakukuwahi kutokea ugomvi wowote wa kupigana halafu nikashindwa ingawa ilikuwa si rahisi kunikuta nikipigana mpaka mtu anichokoze sana.
“Mimi ni nani kwako?” Isri aliniuliza swali ambalo kidogo lilizifanya jazba zangu zitulie. Aliniuliza swali hilo kwa mara nyingine, halafu akaniuliza kama naamini yeye anaweza kunifanyia jambo baya kwa makusudi kwa jinsi alivyokuwa ananipenda mpaka kufikia hatua ya kunipa mwili wake wa thamani. Akaniuliza kama nimesahau mapenzi makubwa aliyonionyesha tangu siku ya kwanza ananiona, nikajikuta nikishusha pumzi ndefu na kujiinamia, mwili ukianza kupunguza kutetemeka.
“Twende huku,” alisema huku akinishika mkono, nilitaka kujichomoa lakini moyo ukasita, nikawa mpole kama kondoo anayepelekwa machinjioni, nikamfuata mpaka chini ya mwembe mkubwa uliokuwa jirani na pale tulipokuwa. Akaniambia nimpe mkono wangu wa kushoto, akaugeuza na kuutazama kwa muda kwenye upande wa nyuma wenye kucha.
“Unauona huu mshipa wa damu,” aliniambia huku akinionyeshea mshipa mkubwa wa damu uliokuwa unaonekana. Akaniambia kwamba nikifika nyumbani, kabla sijaingia ndani, natakiwa kuchukua kitu chenye ncha kali, iwe sindano au wembe na kujitoboa kwenye huo mshipa ili damu itoke.
“Damu ikiwa inatoka, hakikisha unaipakaza kwenye kingo mbili za mlango kisha ndiyo uingie ndani na usitoke mpaka giza liingie,” aliniambia huku akinipa pole kwa yote yaliyotokea, sikumjibu kitu kwani bado sikuwa najua nini itakuwa hatma yangu.
Baada ya hapo, aliniambia nifumbe macho, nikatii alichokisema, akaniambia nisifumbue mpaka atakaponiambia. Ghafla nikaanza kuhisi kama kimbunga kikali kinavuma pale chini ya mwembe tulipokuwa, sikuelewa tena kilichoendelea mpaka niliposikia sauti za watu ninaowafahamu wakilitaja jina langu, akiwemo Isri mwenyewe.
Ikawa ni kama nimetoka kwenye usingizi mzito ambao hata sielewi ulitokea wapi, nilipofumbua macho, nilishtuka mno kujikuta nipo nje ya nyumba ya akina Rahma huku mama na ndugu zangu wakiwa wamenizunguka lakin Isri hakuwepo. Yaani kuna mambo mengine yanatokea hata ukiulizwa yametokeaje, huwezi kuelezea.
“Vipi? Mbona umelala nje?” mama aliniuliza huku akiniinua. Sikutaka kuwa na maelezo marefu maana kila mtu angeniona mwendawazimu kama ningesimulia kila kitu kilichotokea. Kwa bahati nzuri, baba alitoka na kuja hadi pale nilipokuwa, nikiwa bado nimekaa chini kwenye maua.
Akanitazama usoni kwa makini kisha akawaambia ndugu zangu pamoja na mama wakaendelee na usafi kwa sababu ndiyo kwanza walikuwa wametoka kuamka na walikuwa wakifanya usafi wa mazingira na nyumba.
Waliondoka kwa shingo upande, mara kwa mara wakawa wanageuka na kunitazama, wakiwa na maswali mengi yasiyo na majibu. Walichokuwa wanakijua wao ni kwamba nilikuwa nimekamatwa na polisi na kwa jinsi taratibu za kisheria zilivyo, isingekuwa rahisi mimi kutoka bila kuja kuwekewa dhamana na hakukuwa na mtu mwingine wa kufanya hivyo zaidi ya baba na baba yake Rahma.
“Hebu simama,” alisema baba huku akinipa mkono, na mimi nikampa mkono wa kushoto. Wakati akinivuta kuniinua, nilimuona akiukazia macho mshipa wangu wa mkononi, uleule ambao Isri aliniambia nikifika nyumbani, kabla sijaingia ndani niutoboe kisha damu nizipake kwenye kingo za mlango.
“Umefanya nini? Hebu tuone?” alisema baba huku akizidi kuuvutia ule mkono wangu kwake, akautazama ule mshipa kwa sekunde kadhaa kisha nikamuona akiingiza mkono wake mmoja mfukoni, akatoa pochi yake na kuipekuakwa mkono mmoja, huku ule mwingine akiwa bado amenishikilia.
Nikamuona akitoa sindano ya kushonea nguo iliyokuwa na uzi mweusi, nikiwa bado najiuliza anataka kufanya nini, nilishtukia akinitoboa, nikaruka kwa maumivu, damu nyingi ikawa inaruka kwa kasi. Harakaharaka, akiwa bado amenishikilia, nilimuona baba akitoa kichupa kidogo mfukoni, cha ajabu eti akawa anakinga damu ambayo licha ya kutobolewa sehemu ndogo, ilikuwa ikiendelea kuruka kwa nguvu.
Sikuelewa kulikuwa na uhusiano gani kati ya ule mshipa wangu, damu iliyokuwa inanitoka na kile alichokisema Isri. Kile kichupa kidogo kilikaribia kujaa lakini cha ajabu, damu yenyewe ilikuwa nyeusi tii. Ilipopungua kutoka, baba aliniachia, akakifunga kile kikopo na bila kunisemesha kitu aliingia ndani haraka na kuniacha palepale nje.
Ndugu zangu waliokuwa wakiendelea kunitazama kwa macho ya kuibia, walibaki kunishangaa tu. Kwa kuwa baba hakuniambia chochote, na tayari Isri alikuwa amenipa maelezo fulani, nilijifuta ile damu iliyokuwa ikiendelea kunivuja, safari hii ikiwa imepungua, harakaharaka nikasogea mlangoni na kuipaka kwenye kingo za mlango, nikawa nageuka huku na kule kuhakikisha hakuna anayeona ninachokifanya.
Nilipofanya kitendo hicho tu, nilisikia kama masikio yamezibuka hivi, nikawa nasikia sauti za ajabuajabu kama miluzi hivi ambayo awali sikuwa naisikia, nikajikuta nikilazimika kuziba masikio kwa mikono, nikaingia ndani.
Cha ajabu, nilipoingia ndani tu, ile miluzi ilikoma kusikika, nikarudi kwenye hali yangu ya kawaida ingawa bado damu ilikuwa ikinitoka kidogo.
“Togoooo!” Rahma ambaye ndiyo kwanza alikuwa akitoka chumbani kwake baada ya kuamka, alisema huku akinikimbilia pale koridoni nilipokuwepo, akaja na kunikumbatia kwa nguvu huku akipiga kelele, akasema eti haamini kama ameniona.
“Mbona unatoka damu?”
“Nimeumia,” nilimjibu kwa mkato, akanipa pole sana na kunishika mkono, akawa ananipeleka kule chumbani kwake. Mwili wangu ulikuwa mchafu na nilikuwa nanuka lakini mwenyewe hakujali. Furaha aliyokuwa nayo, iliweza kabisa kuumaliza uchovu wa asubuhi aliokuwa nao, uso wake ukachangamka mno, akawa anatembea kwa madaha huku akijinyonganyonga.
Kabla ya kupatwa na yale matatizo siku iliyopita, hatukuwa tumeonana na Rahma kwa sababu asubuhi aliwahi sana kuamka na kuondoka na mama yake kufuatilia mambo ya chuo, hatukupata muda wa kuwa pamoja.
“Togoo!” nilisikia baba akiniita kwa sauti ya juu akiwa amesimama kwenye mlango wa chumba anacholala na mama.
“Naam baba,” niliitikia huku nikijaribu kumtoa Rahma maana alikuwa amenishika kimahaba, baba akaja mbiombio na kunishika mkono, akamwambia Rahma kuna kazi hatujamaliza kwa hiyo anisubiri, alinishika mkono na kuanza kunivuta kuelekea nje lakini tulipofika kwenye kingo za mlango tu, jambo la ajabu lilitokea.
Je, nini kitafuatia? Usikose Jumatatu kwenye Gazeti la Championi Jumatatu.


No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...