Monday, September 3, 2018

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 6


ILIPOISHIA:
Nilitafuta sehemu nzuri, upande wa nyuma kabisa wa shamba hilo kubwa, nikajificha na kuanza kupanga namna ya kwenda kutimiza azma yangu. Ilikuwa ni lazima nimuokoe Saima kwa gharama yoyote, hasa ukizingatia kwamba ndani ya tumbo lake, alikuwa na kiumbe, mwanangu mtarajiwa, ambaye angekuja kuyabadilisha kabisa maisha yangu na kunifanya na mimi nianze kuitwa baba.
SASA ENDELEA...
Nikiwa bado palepale mafichoni, usingizi ukikizonga kichwa changu kutokana na ukweli kwamba sikuwa nimelala hata kidogo usiku kucha, nilisikia muungurumo wa pikipiki zaidi ya moja kutokea upande wa nyuma wa shamba kubwa.
Nilijiweka sawa, ‘chuma’ changu nikakikamata vizuri mkononi kwa ajili ya chochote kwani japokuwa nilikuwa sehemu ambayo naujua isingekuwa rahisi kwa mtu yeyote kuniona, nilikuwa nafahamu vizuri jinsi Mute anavyoendesha shughuli zake. Alikuwa na intelijensia ya hali ya juu pengine kuliko hata vyombo vingi vya usalama.
Nikiri kwamba japokuwa ni kweli nilikuwa na matatizo makubwa na Mute, lakini ni yeye ndiye aliyenifundisha kila kitu nilichokuwa nakifanya. Nikiwa kwake, ndiko nilikojifunza kutumia bunduki, mbinu za mapigano ya mwilini au kwa kitaalamu ‘martial arts’, kutumia silaha nyingine mbalimbali na sehemu muhimu unazotakiwa kuwa nazo makini unapotaka kupigana na mtu, iwe ni silaha au kwa mikono.
Unajua tofauti kubwa kati ya raia wa kawaida na askari aliyepitia mafunzo, ni kwamba raia wa kawaida unaweza kuwa unajua kwamba ukimpiga ngumi usoni adui yako, utampasua na kumtoa damu au kumng’oa meno lakini hutaweza kuzuia asiendelee kupambana na wewe lakini askari anajua kabisa akikupiga sehemu gani, unaweza kudondoka na kupoteza fahamu papo hapo, au pengine kufa kabisa.

Sikuwa askari lakini kwa mafunzo niliyoyapata bila hiyari yangu nikiwa chini ya mikono ya Mute, nilikuwa na ujuzi pengine kuliko hata askari wenye mafunzo ya kawaida na pengine hiyo ndiyo sababu iliyofanya niwe tishio kwa watu waliokuwa wananijua.
Licha ya yote hayo, bado kuna kosa kubwa sana alikuwa amelifanya Mute kwenye maisha yangu, kwa sababu kwanza mbinu zilizotumika mpaka nikawa mfuasi wake, hazikuwa sahihi, unajua kazi hizi za hatari bora mtu aamue mwenyewe kuwa mtu mbaya lakini siyo kuingizwa ukiwa hujui chochote na ndiyo maana chuki yangu kwake ilikuwa kubwa mno kiasi cha kujiapiza kwamba siku nikikutana naye, lazima nitautoa uhai wake, tena kwa mikono yangu mwenyewe.
Kule upande wa nyuma wa shamba lile nilikokuwepo, kulikuwa na njia ndogo ambayo nakumbuka kabla mimi na Mute hatujaingia kwenye haya matatizo makubwa, tulikuwa tukiitumia kuingia na kutoka mle shambani hasa kwenye ‘misheni’ maalum ambazo zinatakiwa kufanyika kwa usiri mkubwa.
Muungurumo ulizidi kusogea, na mimi nikawa najaribu kunyanyua shingo yangu kutoka pale kwenye maficho yangu, kujaribu kutazama ni nini kilichokuwa kinaendelea.
Nikashtuka kuona pikipiki kubwa tatu zikija kwa kasi kubwa, na kati ya hizo, ya kwanza ilikuwa na watu wawili, nyingine ilikuwa na watu wawili na nyingine ilikuwa na watu watatu.
Kwa jinsi nilivyokuwa naujua utendaji kazi wa vijana wa Mute, nilijua pale lazima kuna mtu ametoka kutekwa au kuna jambo lisilo la kawaida limetokea kwa sababu pia kulikuwa na sheria nyingine inayoagiza kwamba mnapoenda kwenye kazi, lazima pikipiki moja ibebe watu wawili, dereva na abiria ambaye kimsingi ndiye aliyekuwa akikaa na silaha ili likitokea la kutokea, dereva yeye kazi yake iwe ni kukimbia na yule abiria wa nyuma kazi yake iwe ni kujihami.
Ilikuwa ni makosa pikipiki kuwa na dereva peke yake au kuwa na zaidi ya watu wawili kwa hiyo nikajua lazima kuna jambo. Kama muda ule ndiyo walikuwa wakiwasili pale Kibaha, maana yake ni kwamba walikuwa wamefanya tukio usiku wa manane na eneo la mbali lililowalazimu kutembea umbali mrefu ili kuwahi kuukwepa mkono wa kisheria.
Basi macho yangu yote niliyaelekeza kwenye ile pikipiki iliyokuwa na watu watatu kwa sababu kwa hesabu zangu, nilijua kwamba lazima pikipiki zote zilikuwa na watu wawili kama ilivyo kawaida, sasa huyu mtu wa tatu ni nani? Nikawa natafuta majibu.
Nilipoitazama ile pikipiki vizuri, niligundua kwamba yule mtu wa tatu, alikuwa mwanamke na kwa jinsi ilivyoonesha, ni kama alikuwa ameteswa kwa muda mrefu kwani hata kukaa mwenyewe hakuweza, badala yake mtu aliyekuwa nyuma yake ndiyo akawa amemshikilia. Kwa maana hiyo ni kwamba alikuwa amekalishwa katikati, mbele dereva na nyuma mtu mwingine.
Pia nguo zake zilikuwa zimelowa kwa damu na wakati nazidi kukazia macho, moyo wangu ulinilipuka mno baada ya kugundua kwamba blauzi aliyokuwa amevaa, japokuwa ilikuwa imelowa damu, ilikuwa ikifanana sana na blauzi ya kipenzi cha moyo wangu, Saima.
Kumbukumbu zangu zilinionesha kwamba ndiyo aliyokuwa amevaa siku ya mwisho wakati anatekwa na kuchukuliwa kwa nguvu kutoka kule nyumbani, kabla ya baadaye nyumba yenyewe kuchomwa moto.
“No! Haiwezekani, haiwezekani,” nilisema huku nikitetemeka kuliko kawaida. Nilijisikia uchungu usiomithilika ndani ya moyo wangu, kwa nini wamfanyie vile Saima wangu?
Amewakosea nini mpaka wamteke na kumtesa kiasi kile? Kama shida ya Mute ilikuwa ni mimi, kwa nini asinichukue na kwenda kunifanya chochote anachokitaka? Kwa nini wamfanye vile Saima, tena akiwa na ujauzito wangu?
Wamasai wana kitu kinaitwa mori! Yaani kijana wa Kimasai akipandisha mori, anaweza hata kupambana na simba na akamuua kwa mikono yake.
Basi na mimi japokuwa sikuwa Mmasai, nilijikuta nikipandwa na mori, mapigo ya moyo yakawa yananienda mbio kuliko kawaida, mwili nikahisi ukiwa na nguvu za ajabu, hofu yote ikaniisha na nikajiapiza kwamba ama zangu, ama zao! Nife mimi, au wafe wao wote lakini siwezi kukubali kumuona Saima wangu katika hali ile.
Japokuwa pale nilipokuwa nimekaa palikuwa ni juu kidogo, kwenye tawi la mti mkubwa, nilijirusha mpaka chini na cha ajabu hata sikufikiria mara mbili nitadondokea sehemu gani, kwa bahati nzuri pale chini palikuwa pameliwa matuta ya viazi, kwa hiyo ikawa ahueni kwangu.
Kishindo cha kuruka kwangu, kiliwashtua wale vijana wa Mute, nikamuona mmoja akiwapa ishara wenzake, wale waliokuwa wamembeba Saima wakazidi kuongeza kasi huku wale wengine wakigeuza pikipiki zao na kutazama kule nilikokuwepo, ambako ndiko kishindo kilipotokea.
Nilitambua kwamba malengo yao ni kuhakikisha misheni ya kumuingiza Saima ndani ya lile shamba inafanikiwa na ndiyo maana wale wengine waliongeza mwendo na sasa wakawa wamekaribia kwenye geti dogo la nyuma, huku wale wengine wakijiandaa kukabiliana na chochote kilichokuwa kinataka kuvuruga misheni yao.
Kwa sababu tayari nilishajua lengo lao, na mimi niliamua kupiga hatua moja zaidi kichwani mwangu, na kuhakikisha nazuia Saima asiingizwe mle ndani. Kwa kawaida, bunduki ikiwa na risasi, ili ufyatue risasi ni lazima kwanza uzivute risasi kwenye chemba kisha ndiyo uvute ‘trigger’ ili kuruhusu risasi itoke.
Na kisheria, kama bunduki haitumiki, risasi hazitakiwi kukaa kwenye chemba kwa sababu ni hatari sana, zinaweza kukulipukia hata wewe mwenyewe kwa bahati mbaya endapo ukigusa ‘trigger’ hata kwa bahati mbaya.
Kama umewahi kufuatilia kwa makini, hata kwenye filamu za mapigano, kabla mtu hajafyatua risasi, ni lazima kwanza aikoki bunduki au bastola yake, kile kitendo cha kukoki ndiyo kinachozivuta risasi kutoka kwenye ‘magazini’ na kuziingiza kwenye chemba.
Ni kitendo ambacho kinachukua sekunde kadhaa tu, lakini kwa akili ya mtu kama mimi, ninapokuwa na ‘bomba’ mkononi, sekunde moja pekee ilikuwa inatosha kufanya tukio la kushangaza. Maana yangu ni kwamba, wakati mimi nilishaikoki bunduki yangu na kuzijaza risasi kwenye chemba, wale wafuasi wa Mute bado walikuwa hawajafanya hivyo kwa sababu nilikuwa ni kama nimewashtukiza.
Kwa hiyo ule muda wa sekunde kadhaa za kushuka kwenye pikipiki, kuweka sawa bunduki zao na kuzikoki, ulitosha kunifanya niwe nimeshawatangulia mbele hatua kadhaa, kwa hiyo nilichokifanya, nilimlenga yule dereva aliyekuwa anaongeza mwendo kuelekea kwenye lile geti dogo.
Nadhani nilichokifanya hawakukitegemea kabisa kutokana na jinsi nilivyoweza kufanya ‘timing’ sahihi ya muda, basi yule mwenzao alipiga yowe kwa nguvu, pikipiki ikayumba na kupoteza mwelekeo, wakadondoka kama mzigo. Nilijua lazima Saima naye anaweza kuumia lakini ilikuwa ni bora nusu shari kuliko shari kamili.
Kilichofuatia baada ya hapo, ilikuwa ni mvua ya risasi, mitutu zaidi ya minne ilielekezwa kwangu, kila mmoja akawa ananifyatulia risasi. Wasichokijua wengi ni kwamba vita ya kurushiana risasi siyo sawa na kupigana ngumi, kwamba wewe unarusha na mwenzako anarusha kwa wakati huohuo! Ilikuwa ni lazima kutumia akili, mwenzako akiwa anakushambulia wewe unaji-cover kwenye eneo ambalo risasi haziwezi kukupata, kisha na yeye akizubaa kidogo na wewe unashambulia kwani pale unakuwa umeushika uhai wako mkononi, akifanya uzembe kidogo tu, basi unakuponyoka.
Sasa sijui ni kwa sababu ya ‘kupaniki’ au nini, wale wafuasi wa Mute ambao nilikuwa naamini kwamba nao wanazo mbinu kama nilizonazo mimi, walikuwa wakishambulia tu bila ku-take cover.
Kwa hiyo nilichokifanya kabla risasi ya kwanza haijafyatuliwa, niliwahi kuruka na kulala chini, nyuma ya matofali ambayo ilionesha yalisalia wakati wa ujenzi wa ukuta, kwa hiyo risasi zote zilikuwa zikiishia kwenye matofali hayo, wakawa wananishambulia huku wakinisogelea ‘kibwegebwege’, nikaona huo ndiyo muda wa kukamilisha kile kilichonifanya nifunge safari mpaka eneo hilo.
Ghafla niliinuka huku ‘bomba’ likiwa mkononi, kidole kikiwa kwenye ‘trigger’, nikazichekesha kwa mtindo wa kufagia kutoka kushoto kwenda kulia lakini ghafla nilihisi kitu kikipenya kwenye mwili wangu, damu zikaruka kama bomba lililopasuka, ghafla nikaanza kuhisi kama kizunguzungu.

Je, nini kitafuatia? Usikose Jumatatu kwenye Championi Jumatatu.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...