Monday, September 3, 2018

SEVEN DAYS IN HELL (SIKU SABA KUZIMU)- 64


ILIPOISHIA:
“Tulia jamal, mbona una haraka, nimesema leo ndiyo leo na watu wote watatujua sisi ni akina nani. Shenaiza na Firyaal, naomba mkaze mioyo yenu maana kinachoenda kutokea kwa baba yenu siyo kizuri lakini lazima tufanye hivi,” alisema Junaitha, akawasha gari, tukaondoka huku ile difenda ikitufuata kwa nyuma.
SASA ENDELEA...
Msafara uliendelea na safari mpaka tulipofika Kurasini, tukakata kushoto na kuiacha barabara ya lami, nikaikumbuka vizuri njia hiyo kwani ndiyo tuliyopita siku ile tulipoenda nyumbani kwa akina Shenaiza.
Tulipoingia kwenye barabara hiyo, ile difenda iliyokuwa nyuma, ilituwashia taa, nikamuona Junaitha akipunguza mwendo na kupaki pembeni, ile difenda nayo ikapunguza mwendo na kusimama. Yule askari aliyekuwa na nyotanyota begani akamsogelea Junaitha.
“Kumbe mlikuwa mnamaanisha huyu mzee Loris?”
“Ndiyo, kwani maelezo yote si yanajitosheleza afande?”
“Ni hatari sana kwa kweli, hata sidhani kama itawezekana.”
“Kwani mheshimiwa, wananchi wanapoletamalalamiko kwenu, tena mazito kama haya, wakiwa na ushahidi wa kila kitu, ni nani anayeweza kuwasaidia kama siyo jeshi la polisi?”
“Wewe ni nani unayeuliza maswali ya namna hiyo? Isitoshe sizungumzi na wewe, naongea na huyu mama aliyeleta taarifa.”

“Naitwa Richard Bukos, ni mwandishi wa habari kutoka Kitengo Maalum cha Oparesheni Fichua Maovu (OFM),” majibu yale ya yule mwandishi wa habari ambaye tulikuwa naye ndani ya lile gari, Toyota Alphard, yalimshtua mno yule askari. Ni kama hakutegemea kama kulikuwa na mwandishi wa habari mle ndani, tena akiwa na vitendea kazi vyote.
“Kwa nini mmekuja na waandishi wa habari?” alimgeukia Junaitha na kumuuliza swali hilo, akionesha kutofurahishwa kabisa na uwepo wa Bukos eneo lile.
“Kwani kuna tatizo gani afande? Tunataka Watanzania wote wajue kinachoendelea,” alijibu kwa kujiamini, nikamuona akigeuka na kurudi kule kwa wenzake bila kuzungumza kitu. Shenaiza alinigeukia, tukatazamana kisha wote tukageuka na kumtazama Bukos kisha tukageukia kule kwenye ile difenda. Tukamuona yule askari akijadiliana na wenzake, wakiwa ni kama wanalaumiana kitu.
Muda mfupi baadaye, tulimuona akitoa simu ya upepo (Radio Call), akaibonyeza na kuanza kuzungumza na watu wa upande wa pili. Mpaka muda huo sikuwa nimeelewa ni nini hasa kilichomfanya aonekane kusitasita.
“Kwani kuna nini kinaendelea?”
“Inaonekana wanamjua huyu mzee,” alisema Junaitha, yule askari akawa anazungumza na simu huku akisogea pale kwenye gari. Alipomaliza kuzungumza, alimgeukia Junaitha.
“Huku ni kama mmetuleta uwanja wa vita, hatuwezi kuingia kichwakichwa, hata nyie humo ndani ya gari, itabidi gariligeuzwe na kwenda kupaki kule barabarani, mbali kabisa, tunaenda kuuwasha moto ambao haitakuwa rahisi kuuzima, umenielewa?” alisema askari huyo, sautikutoka kwenye simu yake ya upepo ikawa inasikika, askari wengine wakipeana maelekezo.
Imebidi niombe msaada kutoka makao makuu, kuna wenzetu wanakuja ila nakuonya siku nyingine lazima uwe unatoa taarifa ambazo zimekamilika. Wewe mwandishi wa habari itabidi ukae mstari wa mbele kabisa wa mapambano, si unajifanya unajua kufuatilia matukio magumu?” alisema huku akigeuka na kuondoka.
Kwa muda wote huo, Firyaal na Shenaiza ambao walikuwa wamekumbatiana, walikuwa kimya kabisa, Raya na Shamila nao walikuwa kimya, wakitazama kila kilichokuwa kinaendelea.
“Wasitake kututisha bwana, wanataka tukasimame barabarani ili iweje? Watakuwa wanataka kutuchezea mchezo mchafu hawa.”
“Hapana, alichokisema ni kweli, kule ndani kwetu kuna walinzi wengi wenye bunduki wanamlinda baba na kama amerudi ulinzi huwa unaongezwa zaidi, kuna kamera kila sehemu,” alisema Shenaiza na kuungwa mkono na mdogo wake, Firyaal.
Yule askari ambaye alikuwa amesogea pembeni, alianza kumuonesha ishara Junaitha kwamba ageuze gari, kufuatia maelezo yale ya Shenaiza na Firyaal, ilibidi tugeuze tu, tukaanza kurudi kule tulikotoka ambapo tulilipita lile gari la polisi ambalo lilikuwa limewasha taa za mbele na za juu.
Wale askari waliokuwa ndani ya gari hilo, wote walishashuka na kutawanyika eneo lile na kadiri muda ulivyokuwa unazidi kusonga mbele, ndivyo eneo lote lilivyokuwa linaonekana kama uwanja wa vita.
Junaitha aliendesha gari mpaka barabarani, akatafuta sehemu nzuri nakupaki, yule askari akawa anatembea kwa kasi kutufuata.
“Kuna yeyote anayeifahamu vizuri ngome ya Loris na mazingira yake ya ndani?”
“Ndiyo, tuko na binti yake mdogo, yeye anaweza kuwa msaada mkubwa kuwaongoza,” alisema Junaitha akimuonesha Firyaal.
“Basi itabidi tuongozane naye,” alisema, mapigo ya moyo wangu yakanilipuka paah! Yaani wao wenyewe walishasema kwamba pale ni uwanja wa vita halafu safari hii wanataka eti Firyaal ndiyo awaongoze. Wao wamevaa nguo maalum za kuzuia risasi (bullet proof) lakini Firyaal yeye amevaa blauzi tu!
“Haiwezekani.”
“Haiwezekani nini?”
“Haiwezekani Firyaal ndiyo awaongoze, bora hata mimi ndiyo niwaongoze.”
“Kwani wewe unayafahamu mazingira ya mle ndani?”
“Hapana, nitamuuliza akinielekeza na mimi nitawaelekeza.”
“Mbona unataka kuleta mzaha kwenye mambo ‘serious’ we kijana, hebu usiingilie kazi yetu,” alisema yule askarikwa sauti yenye mamlaka, nikageuka na kumtazama Firyaal, tukawa tunatazamana. Sijui kwa nini roho yangu ilikuwa ikinienda mbio kiasi hicho, nilishahisikwamba kuna jambo baya linaenda kutokea mbele yetu.
“Junaitha, do something!” (Junaitha, fanya chochote) nilimwambia Junaithan, akanigeukia na kunitazama.
“Kwani wasiwasi wako ni nini Jamal.”
“Vita haina macho, wanaweza kumpiga risasi Firyaal.”
“Siku zote huwa nakufundisha namna ya kuishinda hofu ndani ya moyo wako, kwa nini ufikirie mabaya tu?”
“Kama wasiwasi wako ni huo, tutamvalisha ‘bullet proof’ na kofia ngumu ya chuma, atakuwa salama,” alisema yule askari, akageuka na kuondoka zake.
“Usiwe na wasiwasi Jamal, nitakuwa sawa. Ni lazima tushirikiane nao ili kukomesha ushetani anaoufanya baba,” alisema Firyaal kwa kujiamini, nikakosa cha kujibu. Ukimya ulitawala mle ndani ya gari, kila mmoja akawa anawaza lake.
Muda mfupi baadaye, tulizinduliwa na ving’ora vya magari manne ya polisi yaliyokuwa yanakuja kwa kasi kubwa, yote yakiwa yamewasha taa za mbele, ndani yake kukiwa na askari wengi wenye silaha.
Yote yakaiacha barabara ya lami na kuingia kwenye barabara ya vumbikwa kasi kubwa, yakaenda kusimama jirani na lile la kwanza na hata kabla hayajasimama, askari wote tayari walikuwa wameshashuka kwa kuruka. Ungeweza kufananisha kila kitunafilamu ya mapigano.
Yule askari aliyekuwa akizungumzana sisi mara kwa mara, alianza kutoa maelezo, akawapanga katika makundi mawili, kila mmoja akiwa na bunduki mkononi, akawa anawaelekeza nini cha kufanya na baada ya kilammoja kujipanga kwenye sehemu yake, alitufuata pale kwenye gari, tulipokuwa tumekaa, tukishuhudia kila kitu kilichokuwa kinaendelea.
Mkononi alikuwa ameshika koti maalum la kuzuia risasi na kofia ngumu ya polisi kama alivyokuwa ametuahidi, mapigo ya moyo wangu yakawa yanazidi kunienda mbio. Cha ajabu, Firyaal yeye uso wake ulikuwa umejawa na tabasamu pana, akasogea mpaka pale kwenye gari na kutuambia kuwa muda wa kazi umewadia.
“Wewe mpigapicha itabidi ukae kwa mbali maana hatuna vifaa vya kutosha vya kukukinga na risasi, binti njoo nikuelekeze namna ya kuvaa,” alisema akimuoneshea Firyaal, harakaharaka akashuka kwenye gari, ikabidi na mimi nishuke.
“Dont worry Jamal, each and everything is going to be okay!” (Usiwe na wasiwasi Jamal, kila kitu kitakuwa sawa) alisema Firyaal na kunisogelea, akanikumbatia na kunibusu mdomoni huku kila mtu akishuhudia. Sikujali, nilikuwa nampenda sana Firyaal na sikuwa tayari kuona jambo lolote baya linamtokea, hasa kabla ya mimi na yeye kukutana na kumaliza kile tulichokuwa tayari tumekianza.

Je, nini kitafuatia? Usikose Ijumaa kwenye Gazeti la Championi Ijumaa.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...