Monday, July 24, 2017

Seven Days In Hell (Siku Saba Kuzimu)- 6


ILIPOISHIA:
Mara simu yake ilianza kuita mfululizo, akaishika na kutazama namba ya mpigaji lakini katika hali ambayo sikuielewa, aliiachia simu hiyo, ikadondoka chini na kufunguka betri ikaangukia kivyake, mfuniko kivyake na simu nayo kivyake. Akaanza kuangua kilio kwa uchungu huku akiniomba nimsaidie, nilibaki nimepigwa na butwaa.
SASA ENDELEA…
“Nikusaidie nini Shenaiza?” nilimuuliza huku nikiiokota ile simu na kuiunganisha upya.
“Nakuomba usiniache, fanya kila kinachowezekana unitoroshe hapa hospitalini usiku huuhuu, watakuja kunimalizia,” alisema msichana huyo na kuzidi kunichanganya.
“Watakuja kukumalizia? Akina nani? Na Kwa nini tutoroke wakati hali yako bado siyo nzuri?”
“Naomba ufanye nilichokuomba mengine utaenda kuyajua mbele ya safari,” alisema msichana huyo huku akiendelea kulia.
Nikiwa bado nimeduwaa, nikiwa sijui cha kufanya, nilishtuka kumuona akichomoa sindano ya dripu aliyokuwa amechomwa mkononi mwake na kusababisha damu zianze kumtoka mkononi, akajikongoja huku akionesha kuwa na maumivu makali, akanitaka nimpe bega langu ili apate balansi ya kutembea.
Sikuwa na cha kufanya zaidi ya kukubaliana na matakwa yake, japokuwa nilikuwa najua kwamba ninachokifanya ni hatari sana lakini sikuwa na namna zaidi ya kumsaidia msichana huyo ingawa mpaka muda huo sikuwa najua nini kinachomsumbua.
Huku damu zikimvuja na kudondokea sakafuni, nilimsaidia kutembea, tukatoka mpaka nje ya wodi hiyo huku mara kwa mara nikigeuka nyuma kutazama kama hakuna mtu aliyekuwa akitufuatilia.
Kwa bahati nzuri, kwa kuwa muda ulikuwa umeenda sana, madaktari wengi walishaondoka sambamba na manesi ambapo waliosalia walikuwa ni wale wenye ‘shift’ ya usiku ambao nao hawakuwa wengi.
“Heeei! Mnakwenda wapi usiku wote huu,” mwanaume wa makamo ambaye bila hata kuuliza tulijua ni mlinzi wa hospitali hiyo kutokana na kuvalia sare huku mkononi akiwa na kirungu, alituuliza huku akifunga geti la kutokea nje.
Ilibidi nimdanganye kwamba nilimleta mgonjwa wangu kutibiwa majeraha aliyoyapata kwenye ajali lakini hatukumkuta daktari kwa kuwa alishaondoka, nikamdanganya kwamba tunaenda kujaribu kwenye hospitali nyingine lakini hakutaka kuelewa. Akasema hawezi kuturuhusu kutoka mpaka tupate kibali kutoka kwa daktari aliyekuwa zamu usiku huo.
Shenaiza ni kama alijua kilichokuwa ndani ya akili yangu kwani alianza kuugulia kama anayesikia maumivu makali, nikatumia kigezo hicho kuendelea kumshawishi yule mlinzi aturuhusu na alipozidi kukomaa, nilichomoa noti moja ya shilingi elfu kumi na kumshikisha, nikamuona akiachia tabasamu na kututaka kuwa makini.
Akafungua geti ambapo breki ya kwanza ilikuwa ni kwenye kituo cha teksi kilichokuwa nje ya hospitali hiyo, tukaingia kwenye teksi moja na kuondoka huku nikimuelekeza dereva kutupeleka nyumbani kwangu, Mikocheni.
Kwa kuwa ulikuwa ni usiku na hakukuwa na foleni, haikutuchukua muda mrefu tukawa tayari tumeshawasili Mikocheni, nilipotaka kumlipa dereva teksi fedha zake tulizokubaliana, Shenaiza ambaye muda wote alikuwa amejilaza huku kichwa chake akiwa amekiweka kwenye mapaja yangu, aliniambia nisilipe.
“Nina fedha za akiba kwenye pochi yangu ndogo, hebu fungua,” aliniambia, kweli nikafungua pochi yake ndogo aliyokuwa ameiweka kwenye mfuko wa gauni refu alilokuwa amelivaa. Nilipoifungua, nilishangaa kukuta kuna noti kadhaa za dola miamia za Kimarekani na noti mbili za shilingi elfu kumi, zote mpya.
Nikatoa na kumpa dereva na kutaka kurudisha pochi mahali pale lakini aliniambia kwamba nikae nayo mimi, nikakubali na kuiweka kwenye mfuko wa suruali niliyokuwa nimeivaa.
Wakati wa kushuka, kama ilivyokuwa wakati wa kupanda, ilibidi yule dereva teksi anisaidie kumtoa Shenaiza ambaye bado alikuwa akiugulia maumivu makali, akapitisha mkono wake kwenye bega langu na nikawa namsaidia kutembea kuelekea ndani kwangu.
Nilifungua mlango na kumkaribisha ndani, japokuwa alikuwa kwenye maumivu makali, nilimuona akiachia tabasamu hafifu kisha akanisifia: ”Mh! Jamani wewe msafi hadi raha, inatakiwa umpate mwanamke msafi kama wewe ndiyo awe mke wako ndiyo mtaendana,” alisema huku akikodolea macho huku na kule ndani ya sebule yangu.
Japokuwa sikuwa nimeoa lakini hakuna kitu nilichokuwa nakipenda kama kuiweka nyumba yangu katika hali ya usafi, kuanzia sebuleni mpaka chumbani huku nikinunua vitu vingi vya kisasa.
Nilimsaidia Shenaiza kukaa pale sebuleni kwenye sofa kisha nikamvua viatu alivyokuwa amevaa pamoja na koti alilovaa juu ya gauni lake na mtandio aliokuwa amejizibia lile jeraha la kichwani.
“Shenaiza mwenzio naogopa kulala na wewe ukiwa kwenye hali hiyo, ukizidiwa usiku itakuwaje? Kwa nini tusiende hospitali nyingine? Hapa siyo mbali na Hospitali ya Kairuki,” nilimwambia lakini alikataa katakata na kuniambia kwamba hospitalini haikuwa sehemu salama kwake kwa wakati huo.
“Basi kuna rafiki yangu anaishi hapo mtaa wa pili ni daktari lakini bado hajaajiriwa, anafanya ‘field’ hapo Kairuki, unaonaje nikamuite aje kutusaidia?”
“Hapana usijali, nitakuwa sawa kwa sababu kama ni damu nimeshaongezewa ya kutosha, ondoa hofu,” alisema huku akiinua mkono wake taratibu na kunigusa kwenye shavu langu la upande wa kushoto, akawa ananivutia pale alipokuwa amekaa.
Kwa tahadhari kubwa nikiogopa nisije nikamtonesha majeraha yake, niliulanisha mwili wangu, akanivutia mpaka nilipomsogelea kabisa, akanibusu kwenye shavu langu na kuninong’oneza.
“Ahsante sana kwa msaada wako, ni Mungu pekee ndiye atakayekulipa, upo tofauti sana,” nilitabasamu na kumtazama, macho yetu yakagongana, naye akaachia tabasamu hafifu.
Kwa kuwa sikuwa nimekula chochote, ilibidi nimuage kwamba naenda kubahatisha kama nitapa chipsi kwenye banda lililokuwa mtaa wa pili kutoka pale nilipokuwa naishi. Nilitoka huku Shenaiza akinisisitiza niwahi kurudi pia nifunge mlango kwa nje ikiwa ni pamoja na kuzima taa zote. Sikujua kwa sababu gani bado alikuwa na hofu kubwa kiasi hicho. Nilifanya kama alivyoniambia na kutoka, nikafunga mlango kisha nikafunga na geti la chuma kwa nje na kuondoka kuelekea mtaa wa pili.
Kwa bahati nzuri nilikuta bado hawajafunga, nikaagiza chipsi sahani mbili na vipande vya kuku kwani nilitaka nikambembeleze Shenaiza naye ale japo kidogo. Dakika kadhaa baadaye chakula changu kilikuwa tayari, nikalipa na kuanza kuondoka huku nikijitahidi kutembea haraka kwani nilipoteza muda mwingi pale kusubiria chakula.
Katika hali ambayo sikuitegemea, nilipotokeza kwenye uchochoro wa kuelekea kwangu, kwa mbali niliwaona wanaume kama watatu hivi wakiwa wamesimama mlangoni kwangu, mmoja akiwa anagonga mlango kwa nguvu.
“Mungu wangu, akina nani tena hao usiku wote huu?” nilijiuliza huku nikirudi nyuma na kujibanza pale uchochoroni, nikawaona wale wanaume wakiendelea kugonga mlango kwa nguvu. Ugongaji wao ulionesha dhahiri kwamba hawakuwa wamekuja kwa heri, nikawa natetemeka nikiwa sijui nitafanya nini.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.
Nifollow kwenye mitandao ya kijamii kwa:
Facebook: Hash Power
Instagram: Hashpower7113
Twitter: Hash- Power.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...