Tuesday, July 25, 2017

Graves of the Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 7


ILIPOISHIA:
WALE wageni waliaga na kuondoka, baba akatuita tena ndani na kuanza kuhesabu fedha zilizopatikana. Zilikuwa ni shilingi milioni mbili na laki tatu, akasema zingetosha kabisa kwa safari yetu. Tukakubaliana kwamba tumalizie maandalizi na asubuhi ya siku ya pili tuianze safari ya kuelekea jijini Dar es Salaam.
SASA ENDELEA...
KWELI usiku huo hakuna hata aliyepata lepe la usingizi, ‘kimuhemuhe’ cha safari kilitufanya tukae macho mpaka jogoo la kwanza lilipokuwa linawika. Baba alituagiza kwamba tubebe vile vitu vya muhimu tu kwa sababu maisha ya kijijini yalikuwa tofauti sana na maisha ya mjini.
Akatuambia vitu vingine tuviache palepale na vitakuwa salama kwa sababu kuna walinzi anawaacha kwa ajili ya kutulindia mji wetu. Aliposema walinzi sikumuelewa kwa haraka anamaanisha nini, akili nyingine zikanituma kuamini kwamba labda watakuwa ni mgambo lakini nilijiuliza anaweza kuwaacha mgambo ndiyo walinde nyumba yetu wakati hawakuwa wakielewana? Sikupata majibu.
Saa kumi na nusu za usiku, tulitoka na kuanza kutembea kuelekea stendi, kila mmoja akiwa na mzigo wake. Tukaenda mpaka stendi ambapo tulipanda gari la kwanza kabisa ambalo lilikuwa likielekea Mbeya mjini, lakini cha ajabu, wakati wote tumeshapanda kwenye gari, baba yeye alibaki chini.

Tukawa tunasubiri na yeye apande lakini hakufanya hivyo, sanasana tukamuona akiwa anazungumza na mama, kupitia dirisha la gari lile tulilokuwa tumepanda, nadhani alikuwa akimpa maelekezo muhimu sana kwa sababu muda wote mama alikuwa akitingisha kichwa kuashiria kuelewa kile alichokuwa akiambiwa.
Baada ya kumaliza kuzungumza na mama, baba alikuja moja kwa moja pale nilipokuwa nimekaa mimi, akanipa mkono na kuniambia kwamba tutangulie yeye atafuata, akaniambia ananiamini mimi zaidi kwa hiyo lazima niwe makini kuwalinda ndugu zangu.
Nilijisikia fahari sana kwa jinsi baba alivyokuwa akinipa kipaumbele kwenye mambo ya msingi japokuwa nilikuwa na kaka zangu na mimi ndiyo nilikuwa mdogo. Baada ya dakika chache, dereva aliingia ndani ya gari, akawasha na safari ya kutoka Makongorosi kuelekea Mbeya mjini ikaanza.
Safari haikuwa nyepesi, kwa sababu sehemu kubwa ya njia ya kutokea Chunya kuelekea Mbeya mjini, ni milima na mabonde makubwa, ikiambatana na miteremko ambayo kama dereva hayupo makini hamuwezi kufika salama. Ukizingatia na lile giza la alfajiri ile, kila mmoja alikuwa akiomba moyoni tufike salama. Baada ya safari ndefu, hatimaye tuliwasili Mbalizi, gari likashusha baadhi ya abiria na kuingia Barabara Kuu ya Mbeya-Tunduma ambayo ni ya lami, likaendelea na safari ya kuelekea Mbeya Mjini.
Nikiri kwamba hiyo ndiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza kufika mjini na kila kitu kwangu kilikuwa kigeni. Sikuwahi kuona barabara ya lami, sikuwahi kuona magari mengi ya kila aina wala sikuwahi kuona nyumba nzuri na za kisasa, nyingine zikiwa na maghorofa.
Ilikuwa ni safari ambayo iliufurahisha mno moyo wangu, nikawa nachekacheka tu mwenyewe. Hali ilikuwa hivyohivyo kwa ndugu zangu wengine ambao nao walikuwa na ushamba ulioonekana waziwazi kwenye sura zao. Safari yetu ilienda kuishia kwenye Stendi Kuu ya Mabasi ya Mbeya au maarufu kama Mbeya Terminal.
Cha ajabu, wakati gari likikata kona kuelekea sehemu ya kushushia abiria, nilimuona baba akiwa chini, akilitazama gari tulilokuwa tumepanda. Nikabaki na maswali mengi yasiyokuwa na majibu, kwamba alifikaje kabla yetu? Kumbukumbu zangu zilinionyesha kwamba kule Chunya, stendi kulikuwa na gari moja tu ambalo ndiyo hilo ambalo sisi tulipanda.
Na safari nzima, hatukupitwa na gari lingine lolote, wala chombo kingine cha usafiri, si bodaboda wala Bajaj, sasa baba alifikaje pale kabla yetu? Yalikuwa ni maswali ambayo sikuwa na majibu yake. Lakini cha ajabu, nilipomgeukia mama wala hakuonyesha kushtushwa na uwepo wa baba eneo lile, nikamuona akimpungia mkono kama anayemwambia ‘tuko hapa’.
Gari liliposimama, baba ndiye aliyekuwa akitupokea mizigo, ndugu zangu wote walionekana kuchukulia uwepo wa baba eneo lile kama kitu cha kawaida, kwa kifupi hakuna aliyekuwa na akili ya udadisi kama niliyokuwa nayo mimi, nadhani ndiyo maana baba alikuwa akinipenda zaidi yao.
Alitupokea mizigo na kutusaidia kushuka, tukasimama pembeni ya gari, mimi nikawa namtazama nikiwa sina majibu ya maswali yangu kabisa. Mimi na ndugu zangu wote tulikuwa tumechafuka miili yetu kwa sababu ya kusafiri kwenye barabara ya vumbi kutoka Chunya lakini baba yeye alikuwa msafi kabisa.
“Tunasafiri na basi lile pale,” alisema baba kwa sauti ambayo wote tuliisikia vizuri, akatuonyesha kwenye basi kubwa lililokuwa limeinama upande wa mbele kama ndege ya kijeshi, wote tukawa tunalitazama basi lile kwani muundo wake ulikuwa wa aina yake na sidhani kama kuna yeyote kati yetu ambaye aliwahi kuliona basi kama hilo kwa macho.
Basi tulibeba vifurushi vyetu na kuanza kumfuata baba ambaye alitupeleka mpaka kwenye lile basi, yeye akawa wa kwanza kuingia, akawa anatusaidia kupanda ngazi mmoja baada ya mwingine. Wa mwisho alikuwa mama ambaye alikuwa na mzigo mkubwa, baada ya kuingia, baba alianza kusoma namba za siti zilizokuwa zimeandikwa upande wa juu wa basi hilo kubwa, mpaka alipozipata.
Kila mtu alikuwa na siti yake, akawa anatuelekeza sehemu za kukaa, akampa mama tiketi zetu wote kisha nikamuona akizungumza naye mambo fulani, akaingiza mkono mfukoni na kutoa noti kadhaa za shilingi elfu kumikumi, mama akamshukuru, kisha akamuinamia sikioni na kumuongelesha mambo ambayo hakuna aliyesikia.
Wakati akimnong’oneza mama, macho ya baba yalikuwa kwangu, nilipoona ananiangalia, ikabidi nikwepeshe macho yangu kwani tulifundishwa kwamba siyo heshima kuwatazama baba na mama wanapokuwa na mazungumzo yao ya siri.
Baada ya hapo, alikuja pale nilipokuwa nimekaa, akaniinamia na kurudia kuniambia maneno yaleyale aliyoniambia wakati tukiondoka kule Chunya. Aliniambia kwamba ukimtoa mama, mimi ndiye niliyepaswa kuwa mkuu wa msafara na lazima nihakikishe tunafika salama salmini tuendako, akanipigapiga mgongoni kisha akanipa mkono.
Alifanya hivyohivyo kwa ndugu zangu wengine pia, akawapa mkono mmoja baada ya mwingine kisha akarudi kwangu na kuniambia kwamba tutangulie yeye anafuata.
“Lakini baba... sisi wote ni wageni huko tunakoenda, kwa nini usikae na sisi kwenye hili basi? Tukipotea je?” nilimuuliza, swali lililomfanya anitazame usoni kwa makini, nikakwepesha macho yangu kwa sababu baba alikuwa na hali fulani ambayo akikukazia macho lazima utazame pembeni.
“Kwani kutoka Chunya kuja hapa nani alikuwa wa kwanza kufika?” aliniuliza, swali lililonifanya nipate nafasi ya kutoa dukuduku nililokuwa nalo moyoni.
“Tena nilitaka kukuuliza, kwani ulikuja na usafiri gani na kwa nini wewe hujachafuka kama sisi?”
‘Wewe ni mwanaume, lazima ujifunze kuwa na akiba ya maneno, siyo kila unachokiona ukizungumze au uulize, sijakuzaa kuja kuwa msindikizaji maishani mwako,” alisema kwa sauti ya chini ambayo ni mimi tu niliyeisikia lakini iliyokuwa imebeba ujumbe mzito sana ndani yake, nikashusha pumzi na kukaa vizuri kwenye siti yangu.
Tayari dereva alishaanza kupiga ‘resi’ nyingi na kupiga honi, kuonyesha kwamba muda mfupi baadaye safari ingeanza. Baba akatembea harakaharaka kuelekea kwenye mlango wa kushukia, akateremka mpaka chini na kusimama upande ule tuliokuwa tumekaa, gari likaanza kuondoka ambapo alitupungua mikono, na sisi tukafanya hivyo.
Safari ikaanza, hiyo ilikuwa ni karibu saa kumi na mbili na nusu, basi likaanza kuchanja mbuga kuelekea Dar es Salaam.
Baada ya kusafiri umbali mfupi, tukiwa tumefika eneo maarufu liitwalo Mlima Nyoka, lililokuwa kilometa chache kutoka Uyole mjini, tulishangaa kuanza kuona gari likiyumbayumba. Nilikuwa nikisikia sifa za eneo hilo mara kwa mara kwamba magari mengi, hasa ya abiria yalikuwa yakipata ajali na kuua abiria wengi, mapigo ya moyo yakawa yananienda mbio kuliko kawaida.
Kulikuwa na mteremko mkali wenye kona za hatari, na baada ya kuvuka daraja kulikuwa na mlima mkali pia, jambo ambalo lilimaanisha kama dereva akishindwa kulimudu gari, ajali yake ingekuwa si ya mchezo. Dereva alizidi kuyumba huku gari likiongeza kasi, hali iliyofanya abiria waanze kupiga kelele kwa nguvu, wengi wakilitaja jina la Mungu.
Gari lilizidi kuongeza kasi, likawa linashuka kwenye mteremko huo kwa kasi kubwa huku likiendelea kuyumba huku na kule, kelele ndani ya basi zikazidi kuongezeka.

Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

1 comment:

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...