Tuesday, July 18, 2017

MAKABURI YA WASIO NA HATIA (GRAVES OF THE INNOCENTS)- 2


ILIPOISHIA:
Tulipokaribia nyumbani kwa mzee huyo, baba alinionesha ishara kwamba nisimame, nikafanya hivyo, tukawa tunasikia sauti za watu wengi wakilia kutoka nyumbani kwa mzee huyo, baba akanionesha ishara kama anayesema ‘unaona?’, nikashika mdomo kwa mshangao. Sikutaka kuamini kwamba kweli mzee Mwankuga alikuwa amefariki dunia.
SASA ENDELEA...
Nilijikuta nikishusha lile furushi la dawa na panga, nikawa nataka niende kushuhudia mwenyewe kama ni kweli lakini baba aliniambia nisithubutu kufanya hivyo, hasa kutokana na uhasama uliokuwepo kati yetu na familia hiyo. Bado niliendelea kuwa na shauku kubwa ya kutaka kujua kama ni kweli yule mzee amekufa.
Ilibidi baba anishike mkono, tukaenda mpaka nyumbani ambapo baba aliingia kwenye chumba chake cha uganga na kuanza kuchambua zile dawa tulizotoka nazo porini. Ni kama alijua kwamba nitamtoroka na kurudi kule msibani kwenda kushuhudia kilichotokea kwani aliniambia nikae palepale, nimuangalie jinsi alivyokuwa akichambua dawa.
Kweli nilitii maagizo yake, nikakaa pale lakini bado nilikuwa na shauku kubwa ya kutaka kujua kilichoendelea. Nilipomuona baba amezama kwenye kazi yake hiyo, niliinuka na kuanza kuelekea mlangoni, akaniwahi na kuniuliza ninakokwenda.

“Naenda kujisaidia baba,” nilimdanganya baba, akanitazama usoni kisha akaendelea na kazi yake. Nilitoka na kwenda chooni ambako nako nilizunguka nyuma, nikatokomea huko na kwenda kutokea upande wa pili, nyumbani kwa mzee Mwankuga.

Kwa kuwa watu walikuwa wengi, hakuna aliyenitazama vizuri, kwa hiyo nikapata nafasi ya kujichanganya na waombolezaji ambao kadiri muda ulivyokuwa unazidi kusonga mbele ndivyo walivyokuwa wakizidi kuongezeka.
“Kwani alikuwa anaumwa?”
“Hapana alikuwa mzima wa afya kabisa na alikuwa akiendelea na kazi zake, mara akaanza kulalamika kwamba kichwa kinamuuma sana, damu zikawa zinamtoka puani na mdomoni, ghafla akadondoka na kugeuza macho, muda mfupi baadaye moyo wake ukasimama,” nilimsikia ndugu mmoja wa Mwankuga akimuelezea mmoja wa waombolezaji.
Ni hapo ndipo nilipoamini kwamba kweli Mwankuga alikuwa amekufa, kwa kuhofia kuonekana na watu, hasa ndugu zake ambao kama nilivyosema tangu awali hatukuwa na uhusiano nao mzuri, nilirudi kinyumenyume, kisha nikaondoka haraka kurudi nyumbani.
Nilimkuta baba akiwa amesimama nje ya nyumba yetu, akinitazama, nadhani alishashtukia kwamba nimemtoroka, aliponiona tu natokeza, akanibana kwa maswali magumu.
“Ulikuwa wapi?”
Nilikosa cha kujibu, nikawa najiumauma, baba akaniambia nina bahati sana vinginevyo angenifunza adabu, tukaingia ndani ambapo tulienda mpaka kule kwenye chumba cha uganga, baba akanikalisha chini na kuanza kuzungumza na mimi.
“Unajua wewe ndiyo mwanangu kipenzi na sasa umeshakuwa mkubwa, sina sababu ya kuendelea tena kukuficha mambo yangu ndiyo maana leo nimekuonesha baadhi ya mambo.
“Dunia imebadilika sana mwanangu, binadamu tunaishi kwa ubaya sana, hakuna anayemtakia mwenzake mema, watu wanawaonea wengine bila sababu, watu wasio na hatia wanakufa kila siku, ukienda makaburini, yaliyojaa ni makaburi ya watu wasio na hatia! Kila mmoja lazima ajilinde mwenyewe na ukishaweza kujilinda mwenyewe, unaweza pia kuwalinda wenzako,” alisema baba, maneno ambayo yaliniingia lakini bado sikuwa naelewa kile alichokuwa anakimaanisha.
Bado nilikuwa nataka ufafanuzi wa kifo cha mzee Mwankuga kwa sababu kwa akili yangu, niliona kama hakuwa amefanya jambo lolote kubwa kustahili adhabu ya kifo. Ni kama baba aliyaona mawazo yangu, akaniambia anajua najiuliza maswali mengi yasiyo na majibu kuhusu kilichotokea kule msituni.
“Kuna yule rafiki yako aliyekufa kwa kutumbukia kwenye kisima mwaka jana, unamkumbuka?”
“Alfred? Ndiyo namkumbuka,” nilimjibu baba huku nikiwa na shauku ya kutaka kusikia anachotaka kukisema. Akaniambia mazingira ya kifo cha Alfred, yalikuwa yamejaa utata wa hali ya juu na kwamba baada ya kuchunguza kwa kina, aligundua kwamba Alfred hakufa kifo cha kawaida, bali aliuawa.
Akaendelea kuniambia kwamba hata huko kuuawa kwenyewe, japokuwa kila mtu alikuwa anajua ni kweli amekufa na kuzikwa, lakini ukweli ni kwamba hakuwa amekufa bali alichukuliwa msukule.
“Kwani kuna tofauti gani kati ya mtu aliyekufa na mtu aliyechukuliwa msukule?” Nilimuuliza baba, akaniambia kwamba mtu aliyekufa kwa kifo cha amri ya Mungu, huwa mwili unatengana na roho, mwili unaenda kuzikwa kaburini na huo ndiyo unakuwa mwisho wa maisha ya kawaida ya hapa duniani.
Akaniambia pia kwamba kwa kawaida, nafsi au roho ya mtu huwa haiishi ila baada ya kutengana na mwili, huhama kutoka kwenye ulimwengu wa kawaida na kwenda kwenye ulimwengu mwingine. Nilipotaka kumuuliza kuhusu huo ulimwengu mwingine, aliniambia kwamba atanifafanulia siku nyingine.
Akaendelea kunieleza kwamba mtu anayechukuliwa msukule, huwa hafi bali anabadilishwa kichawi kiasi cha kila mmoja kuamini kwamba ni kweli amekufa lakini kinachotokea, huwa anachukuliwa na wachawi na kwenda kutumikishwa kichawi kwenye kazi mbalimbali, mpaka siku ambayo atakufa kwa amri ya Mungu lakini kwa kipindi chote hicho, huwa anaishi kama msukule.
“Sasa mbona Alfred alipokufa tulienda kumzika makaburini na hata siku ya kuaga mwili wake, wote tulipita kwenye jeneza lake na mimi mwenyewe nilimshuhudia akiwa amelala ndani ya jeneza?”
“Ni vigumu sana kunielewa hiki ninachokisema kwa maneno, lakini nataka nikuhakikishie kwamba rafiki yako hakufa na aliyefanya yote hayo ni huyu mshenzi Mwankuga,” alisema baba akionesha kuwa na jazba, akaendelea kunieleza kwamba, licha ya Alfred, walikuwepo watu wengine wengi tu ambao wengine waliuawa kwelikweli lakini kwa ushirikina, ikiwa ni uonevu unaofanywa na wachawi hasa wanapokaribia kutoa makafara yao, na wengine huchukuliwa misukule.
Bado sikuwa namuelewa anachokisema, akaniambia anataka akanithibitishie kwamba Alfred hakufa. Aliacha kila alichokuwa anakifanya, tukatoka nje ambapo watu walikuwa wakizidi kufurika kwenye msiba wa Mwankuga na sasa vilio vya wanawake vilikuwa vikizidi kuongezeka.
Wala baba hakujali chochote, tukatoka na kuelekea makaburini ambayo yalikuwa eneo maarufu linalofahamika kama msalabani, nilikuwa na shauku kubwa ya kutaka kujionea mwenyewe kile alichokuwa anakisema baba kama ni kweli.
“Unakumbuka alizikwa kwenye kaburi gani?” baba aliniuliza, nikamwambia nakumbuka vizuri kwa sababu enzi za uhai wake, Alfred alikuwa rafiki yangu mkubwa na kifo chake cha ghafla, kiliniumiza mno moyo wangu. Kwa kuwa hata siku ya mazishi yake nilikuwepo mpaka makaburini, nilikuwa nalikumbuka vizuri kaburi lake.
Nikamuongoza baba mpaka kwenye kaburi la Alfred ambalo juu yake kulikuwa na msalaba ulioandikwa jina lake kamili, tarehe ya kuzaliwa na tarehe ya kufa kwake. Akaniambia niwe makini kwa kila atakachokuwa anakifanya, nikatingisha kichwa huku hofu kubwa ikiwa imetanda ndani ya moyo wangu kwani kiukweli nilikuwa nikiogopa sana makaburi na maiti.

Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...