Tuesday, October 24, 2017

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na hatia)- 46


ILIPOISHIA:
Tangu nizaliwe, sikuwahi kuchinja hata kuku tu, achilia mbali ndege tuliokuwa tukiwawinda kule kijijini kwetu lakini sasa eti nilikuwa natakiwa nimchinje binadamu, mtoto asiye na hatia yoyote ili nifaulu mtihani na kuwa mwanachama kamili, nilijikuta nikitetemeka kuliko kawaida.
Nilikichomoa kisu pale kiunoni nilipokiweka, mikono ikawa inatetemeka kuliko kawaida, nikawa namtazama mtoto yule usoni, nilijikuta nikiingiwa na huruma isiyo ya kawaida.
SASA ENDELEA...
Kisu kikadondoka na kwenda kujikita kwenye udongo. Nikamuona Mkuu akinikata jicho la ukali, akatembea kwa hatua zenye vishindo vizito mpaka pale nilipokuwa nimesimama, akainama kwa tabu na kukichomoa kile kisu, akanishikisha mkononi.
Baada ya hapo aliingiza mkono kwenye kimkoba chake kidogo cha ngozi, akatoa kichupa kilichokuwa na ungaunga mweusi, akamimina kwenye viganja vya mikono yake kisha akanipulizia usoni bila kusema chochote, nikapiga chafya mbili mfululizo kisha nikaanza kuona kama akili zangu zinabadilika jinsi ya ufanyaji kazi wake.
Hata sijui nini kiliendelea lakini baadaye akili zangu zilipokuja kukaa sawa, nilikuwa nimeshika kisu kwa nguvu huku mwili wangu ukiwa umetapakaa damu, watu wote wakawa wanashangilia kwa nguvu.

Yule mtoto hakuwepo tena pale kwenye kile kitanda cha miti, nadhani alishaondolewa maana niliwaona watu wengine kadhaa wakiwa wamezunguka pale ambapo jana yake palikuwa na furushi la nyama, wakawa ni kama kuna kazi wanaifanya, hakuna hata aliyegeuka nyuma.
Mkuu alinisogelea huku uso wake ukiwa na tabasamu pana, sikuwahi kumuona akiwa na furaha kama aliyokuwa nayo, akaja na kunishika kichwani kama mtoto anavyomsalimia mkubwa wake, akanishika pia kifuani kisha akainama na kunishika vidole gumba vya miguu.
Alipoinuka, alifungua kimkoba chake, akatoa hirizi nyeusi na kunifunga kwenye mkono wa kushoto, akaniambia kwamba hicho ndiyo kitambulisho na silaha yangu na kwamba maelekezo mengine nitapewa na watu walionizidi, watu wote wakapiga makofi kwa nguvu na kuanza kuimba nyimbo za ajabuajabu huku wakicheza kwa mtindo ambao hata sikuuelewa.
Nilimuona baba akija mpaka pale katikati, akatoa salamu kwa Mkuu kisha akanikumbatia kwa nguvu. Hakujali zile damu nilizokuwa nazo, akakichukua kile kisu na kukifuta damu kisha akakichomesha kwenye mshipi wake kiunoni, akanishika mkono huku akiendelea kucheza sawa na wale watu wengine, akanipeleka mpaka sehemu aliyokuwa amekaa yeye na baba yake Rahma.
Sauti ya pembe la ng’ombe ilisikika kisha watu mbalimbali wakaanza kuja pale nilipokuwa pamoja na baba na baba yake Rahma, wakawa wananisogelea kisha wanainamisha vichwa vyao kama ishara ya heshima.
Baba aliniambia kwamba hiyo ni ishara ya kukaribishwa kwenye ulimwengu wao na kila mwanachama mpya anayetimiza masharti, huwa anafanyiwa hivyo. Waliendelea kuja kwa wingi lakini wengi sura zao zilikuwa ngeni kabisa kwangu.
Kulikuwa na wazee, watu wa makamo, vijana kama mimi na watoto wadogo, wanaume kwa wanawake. Wengine walikuwa ni wasichana wazuri tu ambao wala usingeweza kudhania kwamba nao wanahusika na yale mambo. Wengine walikuwa ni watu wazima wenye heshima zao.
Unajua watu wengi huwa wakisikia neno ‘mchawi’, tafsiri ambayo wanaijenga vichwani mwao, ni mtu fulani wa ajabuajabu, anayetisha, aliyezeeka au aliyedhoofika mwili. Ukweli ni kwamba mchawi hana alama, mwingine unaweza kuwa unamuona kama bosi fulani, au mwingine unamuona kama msichana mrembo, mzee wa heshima au mtoto mdogo lakini kumbe akawa anahusika na mambo hayo.
Wakati wakiendelea kuja, mara nilimuona Isri akitokezea, akanitazama na mimi nikamtazama, tukatazamana kwa sekunde kadhaa, tukio ambalo baba aliliona ‘mubashara’, akanigeukia na kunitazama usoni, nikaacha kumtazama Isri na kumtazama baba kisha harakaharaka nikakwepesha macho yangu.
Isri alisogea mbele kisha akainamisha kichwa kama wale wengine wote kisha tararibu akaondoka na kutoa nafasi kwa watu wengine kuendelea na zoezi hilo. Zoezi likaendelea na baadaye, nilishtuka kuziona sura za watu ambao niliwakumbuka vizuri.
Wa kwanza alikuwa ni yule bibi kizee aliyenizabua kibao siku nilipokuwa mahabusu, usiku walioingia na kuanza kuwanga ndani ya chumba cha mahabusu. Nakumbuka siku aliponipiga na kunisababisha maumivu makali, nilijiapiza kwamba siku nitakayokutana naye lazima nilipize kisasi.
Wakati akinisogelea, nilitazama kushoto na kulia, baba akawa ameshajua ninachotaka kukifanya, akanionesha ishara kwamba sitakiwi kufanya chochote. Yule bibi naye ni kama alinikumbuka, aliponitazama vizuri usoni akawa ni kama ameshtuka, akasogea kwa kujihami na kutoa ishara kwangu huku akinitazama kwa macho ya kuibia, moyoni nikajiapiza kwamba ipo siku yake lazima nilipe kisasi.
Nyuma yake alikuwa ameongozana na wale watu wote alioingia nao siku ile mahabusu, wote wakawa wananitazama kwa macho yenye ujumbe fulani, mwisho akatokeza yule ambaye nilisababisha akanasa ndani ya mahabusu kisha mimi nikatoka kimiujiza.
Tofauti na wenzake wote, huyu alionesha kuwa na hasira na mimi maana jicho alilonikata, mpaka nilijishtukia, baba na baba yake Rahma wakawa wanacheka. Ni kama walikuwa wanajua kila kitu kinachoendelea. Basi pilikapilika ziliendelea kama kawaida, ukafika muda wa chakula ambapo sikuogopa sana kama siku ya kwanza.
Baada ya hapo, ulifika muda wa kucheza ngoma za kienyeji na baadaye tulitawanyika, sikujua nimefikaje nyumbani lakini nilichokuwa nakikumbuka ni kwamba baba na baba yake rahma walinishika mikono, wakawa wanaagana na wenzao na muda mfupi baadaye, nilijikuta nikiwa kwenye kona ya chumba nilichokuwa nalala.
Ni hapo ndipo nilipopata muda wa kutosha kuanza kutafakari kilichotokea, nilijihisi kuwa na hatia kubwa ndani ya moyo wangu na nikajiapiza kwamba lazima asubuhi niende Kibaha kufuatilia taarifa za ile ajali na kuona nini hasa ambacho watu wengine watakiona.
Sikupata hata lepe la usingizi, nikawa najiuliza maswali mengi yasiyo na majibu, mara kwa mara nikawa naitazama ile hirizi niliyopewa na Mkuu na kuvalishwa kwenye mkono wangu. Ilikuwa nyeusi tii, ikiwa imefungwa kwa kamba nyekundu.
Kwa kuwa muda ulikuwa umeenda sana, muda mfupi baadaye kulianza kupambazuka, kwa kuwa sikuwa nimelala kabisa, nilienda bafuni kutaka kujimwagia maji kupunguza uchovu lakini ghafla nilikumbuka kwamba baba aliniambia sitakiwi kugusa maji kwa muda wa siku saba.
Ikabidi nijifutefute tu usoni na miguuni na kwenye yale madoa ya damu kisha nikarudi chumbani kwangu, nikaanza kujiandaa kuelekea Kibaha. Sikuwa na nauli na sikutaka kumuaga mtu yeyote, nilitaka kwenda kujionea nini hasa kilichotokea.
Wakati natoka kwa kunyata, nilipitia sebuleni, nikafungua droo ambayo wenyeji wetu huwa wanaweza chenji zinazobaki kwenye manunuzi yao, niliijua kwa sababu mara kadhaa nilimuona Rahma akichukua fedha, nikachukua noti mbili za shilingi elfu mojamoja, nikanyata na kutoka mpaka nje.
Tofauti ambayo niliiona dhahiri, safari hii nilikuwa najiamini sana, sikuwa Togo yule wa saa chache zilizopita, mara kwa mara nikawa najishika pale mkononi kuhakikisha kinga yangu ipo sehemu yake.
Nilipofika mita kadhaa kutoka kwenye geti kubwa, nilimuona yule kijana aliyekuwa akinicheka mara kwa mara kwamba eti mimi ni muuaji. Nilikumbuka maneno aliyoyatoa jioni iliyopita wakati nikiwa na baba na baba Rahma tukielekea kule eneo la tukio, nikaona huo ndiyo muda muafaka wa kumaliza hasira zangu.
“Broo vipi unaenda?” alisema huku akisimamisha Bajaj yake jirani kabisa na pale nilipokuwa nimesimama, nadhani kwa sababu ya kigiza kile cha alfajiri hakuwa ameniona vizuri, aliniponisemesha na mimi kumtazama usoni, niliona jinsi alivyoshtuka, akataka kuondoa Bajaj yake haraka lakini alishachelewa.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...