Saturday, December 31, 2016

SEVEN DAYS IN HELL! (SIKU SABA KUZIMU)-1

Damu nyingi zilikuwa zinanitoka upande wa kushoto wa kifua changu kiasi cha kunifanya nilowe chapachapa. Nilijitahidi kuinuka pale nilipokuwa nimelala huku damu nyingi zikiendelea kunitoka lakini maumivu makali yalinirudisha chini.



Kwa kutumia mikono yangu miwili, nilijaribu kuminya pale kwenye jeraha kubwa ili kuzuia damu isiendelee kunimwagika lakini nilijikuta mikono ikikosa nguvu, kadiri muda ulivyokuwa unasonga mbele ndivyo nilivyokuwa nazidi kuishiwa nguvu.


Watu wengi walianza kukimbilia pale nilipokuwa nimeanguka na kunizunguka, niliwasikia wengine wakishindwa kuficha hisia zao na kuanza kuangua vilio wakilitaja jina langu. Nadhani hali waliyoniona nayo iliwafanya waamini kwamba siwezi kabisa kupona kutokana na damu zilivyokuwa zinaendelea kunimwagika mithili ya bomba lililopasuka.
Nikiwa kwenye maumivu makali, nilijigeuza na kuanza kutazama angani, upeo wa macho yangu ukagota kwenye mawingu meupe na ya bluu yaliyokuwa yakilipendezesha anga, nikabaki nimetulia nikiwa kwenye hali hiyo.
Kelele za watu wengi waliokuwa wanazidi kuongezeka eneo la tukio kunishangaa, zilianza kupungua taratibu masikioni mwangu, zikazidi kupungua na baadaye nikawa nasikia kama watu wananong’ona. Kwa mbali nilisikia mlio wa ving’ora ambavyo hata hivyo sikujua ni vya nini.
Nikiwa naendelea kutazama angani, taswira ndani ya mboni za macho yangu ilianza kufifia taratibu na kadiri muda ulivyokuwa unazidi kusonga mbele ndivyo nayo ilivyozidi kufifia, japokuwa ilikuwa ni mchana, kigiza kikaanza kutanda kwenye macho yangu.
Nakumbuka neno la mwisho nililofanikiwa kulisema, ingawa ilikuwa ni kwa taabu kubwa kutokanana midomo yangu kuwa mizito, ilikuwa ni: Mungu nisaidie! Nikafumba macho na giza totoro likatawala kila sehemu, sikuelewa tena kilichoendelea baada ya hapo!
Katika hali ambayo sikuitegemea na ambayo mpaka leo huwa siwezi kuifafanua, muda mfupi baadaye nilijikuta nikizinduka lakini nikiwa kwenye hali ya tofauti kabisa. Nilizinduka nikiwa palepale nilipokuwa nimelala awali lakini katika hali ya ajabu, nilikuwa mwepesi sana.
Nikajikuta nikianza kupaa taratibu kuelekea juu. Nikiwa juu kidogo, niligeuka na kutazama pale nilipokuwa nimeangukia, nikashangaa kuona bado mwili wangu ulikuwa umelala palepale, damu nyingi zikiendelea kutoka kwenye jeraha la kifuani, tena safari hii zikitoka kwa mabongemabonge.
“Mungu wangu! Hiki ni kitu gani tena?” nilijikuta nikisema kwa sauti ya chini, ungeweza kudhani nilikuwa kwenye ndoto lakini haikuwa hivyo. Nilijiuliza kama mwili wangu bado ulikuwa pale chini, mimi niliyekuwa napaa nilikuwa ni nani?Sikupata majibu.
Niliendelea kupaa kuelekea juu mpaka nikafikia umbali wa mita kadhaa, ulioniwezesha kuona vizuri kila kitu kilichokuwa kinaendelea eneo la tukio. Niliwaona watuwakizidi kumiminika kwa wingi eneo la tukio, wengine wakishika vichwa vyao baada ya kuuona mwili wangu ukiwa kwenye hali ile.
Niliwaona watu kadhaa ambao nilikuwa nikiwafahamu wakiwa na nyuso za huzuni kali, wengine wakiangua vilio kwa nguvu. Nilimuona rafiki yangu na mfanyakazi mwenzangu ambaye muda mfupi kabla ya tukio nilikuwa naye, Justice akiwa analia kwa uchungu mno huku akilitaja jina langu.
Nilimuona pia Raya, msichana ambaye naye tulikuwa tukifanya naye kazi na ambaye alikuwa anapenda sana kuwa karibu na mimi ingawa mara kwa mara nilikuwa nikimkwepa (nitaeleza zaidi kuhusu msichana huyu baadaye), naweza kusema yeye ndiye aliyekuwa na hali mbaya kuliko watu wengine wote kwani alikuwa akilia kwa sauti ya juu huku akilitaja jina langu kiasi cha kusababisha muda mfupi baadaye aanguke na kupoteza fahamu.
Niliwaona pia baadhi ya watu wakiupiga picha mwili wangu kwa kutumia simu zao za mikononi, niliwaona pia waandishi kadhaa wa habari ambao nao walikuwa wakipiga picha nyingi eneo la tukio, za mnato na za video.
Muda mfupi baadaye, walifika askari wanne waliokuwa wamepakizana kwenye pikipiki mbili, maarufu kama tigo ambao niliwaona wakianza kuwarudisha watu nyuma kutoka pale mwili wangu ulipokuwa umelala.
Mmoja wao alisogea jirani kabisa, nikamuona akiuchunguza mwili wangu kisha akaugusa shingoni kama anayesikiliza mapigo ya moyo, nikamuona akiinuka na kuwasogelea wenzake, wakawa wanazungumza jambo ambalo sikuelewa ni nini. Mmoja akatoa simu ya upepo (radio call) na akawa anazungumza na upande wa pili.
Nikiwa bado naendelea kushangaa kwani kila kitu kilikuwa kigeni kwangu, nilianza kusikia ving’ora kwa mbali, nikakumbuka kwamba kabla sijapoteza fahamu kutokana na kutokwa na damu nyingi, nilivisikia tena ving’ora hivyo lakini tofauti yake ni kwamba sasa nilikuwa na uwezo wa kuona kila kilichokuwa kinaendelea.
Lilikuwa ni gari la kubebea wagonjwa (ambulance) ambalo lilikuwa likija kwa kasi eneo lile mwili wangu ulipokuwepo. Nyuma yake lilikuwa limeongozana na difenda ya polisi ambayo niliitambua kwa urahisi kutokana na namba zake za usajili na maandishi yaliyokuwa ubavuni yaliyosomeka ‘Police’.
Wale askari waliokuwepo eneo la tukio waliwatawanya watu upande ule ile ambulance ilikokuwa inatokea, gari likasogea mpaka jirani kabisa na pale mwili wangu ulipokuwepo.
Likasimama ambapo manesi wanne waliovalia nguo nyeupe waliteremka wakiwa na machela, sambamba na askari kadhaa waliokuwa kwenye ile difenda, wote wakasogea na kuuzunguka mwili wangu.
Wakasaidiana kuuinua mwili wangu pale chini na kuulaza kwenye machela kisha wakauingiza kwenye ambulance. Nilimuona Justice naye akipanda. Raya yeye alipakizwa kwenye lile gari la polisi akiwa hajitambui.
Gari likaondoka kwa kasi kubwa likifuatiwa na difenda kwa nyuma, wale askari wa pikipiki waliendelea kuwepo pale eneo la tukio kwa dakika kadhaa wakiwa makini kuwasikiliza watu walichokuwa wanakisema huku wakiwahoji wengine kadhaa.
Kwa muda wote huo, bado nilikuwa najiuliza kilichotokea bila kupata majibu, sikuelewa nipo kwenye hali gani kwa sababu kama ni mwili wangu, tayari ulishapakizwa kwenye ambulance na kukimbizwa hospitali lakini nilishangaa mimi bado nipo eneo lile nikielea angani.
Nilijiuliza ule mwili wangu unapelekwa wapi lakini pia sikupata majibu. Ghafla nilipata wazo la kuifukuzia ile ambulance ili nijue wanaupeleka wapi mwili wangu. Wazo nililoona linafaa, ilikuwa ni kushuka chini na kuchukua bodaboda kwani niliamini kutokana na foleni iliyokuwepo na kasi ya ambulance, ni usafiri huo pekee ndiyo unaoweza kuniwahisha.
Nilishuka jirani kabisa na pale mwili wangu ulipokuwepo muda mfupi uliopita, watu wakawa wameshaanza kutawanyika huku wengine wakijikusanya vikundivikundi pembeni na kujadiliana kuhusu kilichotokea. Nilimsikia mzee mmoja akiwaambia wenzake: “Kwa hali aliyonayo, hawezi kupona, lazima afe.”
Nikashtuka sana kusikia kauli hiyo kwa sababu sikujua wanamzungumzia nani kwamba lazima afe wakati mimi bado nilikuwa hai na nilikuwa nawasikia wanachokisema.
Sikutaka kupoteza muda, harakaharaka nilisogea pembeni ya barabara na kupunga mkono kusimamisha bodaboda, japokuwa dereva alikuwa akija upande wangu, nilishangaa akinipita kama hajaniona. Akaja wa pili naye licha ya kumpungia mkono kwa nguvu hakusimama, akanipita kwa kasi.
Nilijitazama vizuri mwilini kwani nilihisi huenda wanaogopa kusimama kutokana na mwili wangu kulowa damu lakini kituambacho pia nilishindwa kukielewa, shati nililokuwa nimevaa halikuwa na hata tone la damu. Lilikuwa ni shati lilelile ambalo mwili wangu wakati unatolewa eneo lile lilikuwa halitamaniki kwa damu.
Nilishindwa kuelewa ni nini hasa kimetokea, nikajitazama vizuri mwili wangu na kugundua kwamba ulikuwa na hali fulani kama ya kung’aa kusiko kwa kawaida, nilijishika pale kifuani lakini hapakuwa na alama kwamba nilikuwa nimejeruhiwa vibaya, nikazidi kuchanganyikiwa.
Ilibidi nisogee mpaka kwenye maegesho ya bodaboda nikiamini pale itakuwa rahisi kuzungumza na dereva yoyote ili aniwahishe kabla ile ambulance haijapotea kabisa. Nilipopiga hatua moja nilijiona kuwa mwepesi sana halafu tambo lilikuwa refu sana tofauti na kawaida. Sehemu ambayo ningetembea hata hatua ishirini, nilipiga hatua mbili tu, nikawa nimeshafika pale kwenye bodaboda.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...