SIMULIZI

MAKABURI YA NUNGWI- NUNGWI GRAVES
MWANGWI ­­wa vilio na simanzi kutoka kwa watu waliopoteza maisha baada ya meli kuzama kwenye mkondo wa bahari wa Nungwi, Zanzibar,  uliambaa kwenye maji na kwenda kugota kwenye ukuta wa chini ya bahari, mahali palipokuwa na maelfu ya makaburi yaliyochongwa kwenye mwamba mgumu kuhitimisha safari ya wote waliopoteza maisha yao kwenye ajali hiyo ya kihistoria.

 Kwa binadamu wa kawaida, wenye macho yanayoweza kutofautisha giza na mwanga pekee, hiyo ilikuwa ni ajali ya bahati mbaya kama zilivyo ajali nyingine lakini kwa wale wenye uwezo wa kuona zaidi  ya upeo wa  kawaida wa binadamu (beyond normal vision), haikuwa ajali ya bahati mbaya bali kitu kikubwa zaidi kilichopangwa na kuratibiwa kwa umakini wa hali ya juu.

“Babu! Mbona nasikia vilio vya watu wengi sana! Kwani kuna nini?” kijana mdogo anayefundishwa imani za kishirikina, Kahungo,  alikuwa akimuuliza babu yake.
“Hivyo ni vilio vya roho zilizopokonywa miili yao bila kujiandaa.“
“Unamaanisha nini babu?”
“Ili binadamu akamilike anapaswa kuwa na mwili na roho, vitu hivi vinapotengana, binadamu hufa.  Sasa hawa wametenganishwa miili na roho ghafla kwenye ajali bila hata kujiandaa na ndiyo maana wanalia sana.”

“Sasa mbona wanazikwa wakiwa hai? Kwa nini wengine wanalia sana wakati wengine hawalii? Na hawa waliokuwa wanachimba makaburi huku chini ya bahari walikuwa wanatumia vifaa gani?”

”Hawazikwi wakiwa hai. Zile unazoziona ndiyo roho, zinapambana kurudi kwenye miili yao inayoelea juu ya maji lakini zinashindwa. Wanaolia sana ni wale ambao kwenye maisha yao walimsahau Mungu na wakazama dhambini! Wale unaowaona hawalii ni wale ambao walikuwa wanafuata maagizo ya Mungu. Waliochimba makaburi haya ya Nungwi walitumia kitu chepesi sana, walitumia maarifa ya giza!”

“Maarifa ya giza? Lakini mbona hata misalaba inayowekwa kwenye makaburi haya siyo kama ile tuliyozoea kuiona kule duniani? Naona kama ni mifupa ya binadamu imefungwa na kutengenezwa misalaba,“ Kahungo alizidi kumhoji babu yake kwani kila alichokuwa anakiona kilikuwa kinamshangaza.
“Hizi ni kanuni za nguvu za giza! Mbona hushangai mimi na wewe kufika huku chini ya bahari bila ya kuwa na mitungi  ya gesi wala nini na bado tunapumua kama kawaida?”

“Mh! Kweli dunia ina mambo. Halafu nilisikia kuna wazamiaji kutoka Kusini mwa Afrika walishindwa kufika huku, mbona sisi tumefika kirahisi na bado naona watu wengi tu wakiendelea na shughuli za mazishi?”

“Hii dunia mjukuu wangu tunafaidi sisi wenye nguvu za giza! Hakuna kinachotushinda na ndiyo maana nataka nikuandae na wewe ufuate nyayo zangu, si unaona mimi nimeshakuwa mzee! Kuna kazi sana mpaka kufikia huku tulipo, inakubidi uvuke ngazi nyingi sana. Wengi hata ngazi ya kwanza hushindwa kuivuka.”   

“Kwani hapa tulipo panaitwaje babu?”
“Nungwi! Kuna mkondo bahari wenye nguvu sana hapa na kuna wakati maji huwa yanachemka. Kutokana na maajabu ya hapa ndiyo maana wachawi waliamua kuweka kituo chao kikuu. Maji yanapishana kwa ngazi kuanzia juu hadi chini.

“Unataka kusema hiki ni kituo cha wachawi?”
“Eee! Wengi watashangaa kwa sababu ya ajali iliyotokea, lakini ukweli ni kwamba Nungwi ipo kwa miaka mingi iliyopita. Hii siyo ajali ya kwanza kutokea hapa. Mimi tangu nikiwa mdogo nilikuwa nakuja hapa kuongeza nguvu za kichawi na nilikuwa nikishuhudia ajali kubwa kuliko hata hii.”

 Maelezo ya babu yake yalimshangaza mno Kahungo. Alizoea kusikia au kusoma hadithi za kutisha kwenye vitabu lakini sasa alikuwa eneo la tukio akishuhudia mwenyewe kila kitu. Babu yake akazidi kumfafanulia mambo.

“Siyo binadamu wote unaowaona duniani wanaishi kihalali, wengi hawafuati maagizo na mafundisho ya Mungu! Wanavunja amri zake kwa makusudi. Wanaabudu sanamu na kutukuza dhambi! Hawaogopi kufa wala adhabu za kaburi! Watu kama hawa wakiingia kwenye mitego ya nguvu za giza hawaponi!

“Sisi (wachawi) huwa tunasaidia kuwafikisha kwa urahisi kuzimu kwa kuwapitisha kwanza kwenye malago ya wachawi ambapo hutumikishwa kwa kipindi fulani kisha kuachwa waendelee na safari zao. Miongoni mwa njia za kuwasaidia wafike upesi kwenye safari zao ni kuwazika chini ya bahari.

“Babu! Unataka kusema makaburi chini ya bahari yapo hapa Nungwi pekee?”
“Yapo sehemu nyingine nyingi, lakini kwa miaka mingi hapa ndiyo kwenye makaburi maarufu na mengi zaidi, ndiyo maana hata mkondo bahari wa hapa una nguvu kubwa na husababisha ajali nyingi na kubwa kuliko sehemu nyingine.”

“Aaah! Mbona  unanichanganya! Kwani kilichoanza kuwepo hapa Nungwi ni makaburi ya chini ya bahari au mkondo wenye nguvu unaosababisha ajali?”

Swali lile lilimfanya yule mzee amkazie macho mjukuu wake huku akiwa ni kama ambaye hakutegemea kulisikia kutoka kwake. Aliachia tabasamu hafifu kisha akasema:

“Naona umekua siku hizi mjukuu wangu kwani unauliza maswali ambayo hata mimi nilipokuwa na umri kama wako sikuweza kuyafikiria. Kwa kuwa una hamu ya maarifa juu ya ulimwengu usioonekana kwa macho ya kawaida, nitakufafanulia kila kitu.”

“Cha kwanza kuwepo kilikuwa ni kituo kikuu cha wachawi miaka mingi sana iliyopita. Kutokana na nguvu za giza zinazozalishwa chini ya bahari kila wachawi kutoka sehemu mbalimbali wanapokutana, maji yalikuwa yakivurugika sana na kuchemka, ndiyo mkondo wa bahari ukaanza kutokea taratibu kisha ukawa unazidi kuongezeka nguvu.

“Mkondo huo ulianza kusababisha ajali nyingi kwa wasafiri wa majini na kupoteza maelfu ya roho za watu, waliokuwa wanakufa wakawa wanaletwa kuzikwa huku chini, ndiyo yakatokea makaburi haya ambayo yalizidi kuongezeka wingi kwa kadiri ajali zilivyokuwa zinazidi kutokea.”

Baada ya kukaa kule chini ya bahari kwa saa nyingi akishuhudia mauzamauza mengi ya kichawi, Kahungo alimuomba babu yake waondoke kwani moyo wake ulishindwa kuvumilia yale aliyokuwa anayaona na kuyasikia. Wakashikana mikono na babu yake kisha wakafanya ishara za kichawi, Kahungo akaambiwa afumbe macho kama alivyofanya awali wakati wa kuja. Kufumba na kufumbua wakajikuta wako mchangani, ufukweni mwa bahari.

Baada ya kutoka kule chini ya bahari na kujikuta wakiwa ufukweni mwa bahari, Kahungo na babu yake waliwalikuta watu wengi wakiendelea na kazi ya kuopoa kile wakichoamini ni miili ya ndugu zao waliozama kwenye ajali ya meli iliyotokea katika mkondo bahari wa Nungwi.

“Babu hawa wanafanya nini?”
“Wawaokoa ndugu zao waliokufa kwenye ajali.”
“Sasa mbona wanabeba vipande vya migomba?”
“Shhhh! Usiongee chochote, watakusikia. Nyamaza!“ babu yake Kahungo alimnyamazisha mjukuu wake. Alipoona hataki kutulia, alifungua kimkoba chake cha ngozi na kutoa unga fulani mweusi, akajimiminia kidogo kiganjani kisha akaupulizia usoni mwa Kahungo. 

 “Hebu fikicha macho yako,“ alisema babu yake Kahungo.  Alipofanya vile alivyoambiwa, alishangaa kuona mambo aliyokuwa anayaona awali yakipotea ghafla, akaanza kuona  kawaida kama wengine walivyokuwa wanaona.

 “Babu roho inaniuma sana, hivi kama kweli Mungu yupo kwa nini anaruhusu haya yatokee kwa waja wake?”
“Kahungo mjukuu wangu! Jifunze kuwa na roho ngumu, angalia mpaka unamkufuru Mungu wako! Kila jambo linatokea kwa sababu. Badala ya kumlaumu Allah tunapaswa kumshukuru kwa kila kitu.”

“Lakini babu, hivi kwa nini wachawi wanakuwa na uwezo wa kuwadhuru wengine kuliko kuwasaidia? Tazama kila  jambo baya siku hizi linahusishwa na uchawi au dini ya shetani. Kwa nini?”
“Aah, hayo maswali yako utaenda kuniuliza nyumbani, hapa tujadili haya yanayoonekana mbele yetu tu.”

“Sawa, lakini hoja yangu nilikuwa nataka kukuuliza kuwa kama wachawi wote wakikutana kwa kikao cha dharura, hawawezi kutafuta mbinu za kusaidia uokoaji maana kule chini ya bahari bado watu wengi wapo hai.”

Hilo haliwezekani mjukuu wangu! Ingekuwa watu wote wanaamini uchawi tungekuwa na nguvu za kufanya hivyo lakini serikali na dini za kisasa  haziutambui kabisa uchawi, hivyo kuukosesha nguvu ya pamoja.”

“Kwani babu wewe unaabudu dini gani?
“Mi namuabudu Mungu, dini au madhehebu ni kama njia tu ambazo zote zinaelekea sehemu moja.”
“Siyo kweli, ungekuwa unamuabudu Mungu usingekuwa unashiriki kwenye michezo ya nguvu za giza.”

“Kuwa mwelewa mjukuu wangu. Mungu ndiye aliyeumba vitu vyote, vyenye uhai na visivyo na uhai, binadamu na majini. Hizi nguvu zenyewe zinazotumika na wachawi au wafuasi wa jamii za siri kama Masoni na Illuminati zinatoka kwa Mungu, sema watu wengi huwa hawaelewi, tatizo kubwa la binadamu wanaoishi duniani leo ni ukosefu wa maarifa.”

Wakati Kahungo na babu yake wakiendelea kuzungumza ufukweni mwa bahari wakiwa wamekaa juu ya mchanga, lilikuja kundi la vijana kadhaa na kuwazunguka.

“We mzee wewe! Yaani sisi tunahangaika kuwaokoa ndugu zetu waliokufa kwenye ajali ya meli wewe umekaa na kijukuu chako mnapiga soga? Una akili kweli wewe? Badala ya kuja kutusaidia unaleta ujinga wako hapa,” kijana mmoja alisema kwa jazba, wale wenzake wakadakia na kuanza kuzomea.

Kahungo na babu yake walitazamana, wakiwa bado hawajakubaliana nini cha kufanya, wale vijana waliwainua juujuu na kuanza kuwasukuma kuelekea kule shughuli za uokoaji zilikokuwa zinafanyika.

“Kahungo!“
“Naam babu,” aliitikia na alipomtazama babu yake, alimkonyeza na kumpa ishara ya nini cha kufanya. Kwa kasi kubwa Kahungo alitekeleza, kufumba na kufumbua wale vijana wakajikuta wamebeba magogo mawili, moja kubwa na jingine dogo.
“Hee! Kumetokea nini?“
“Wamejigeuza kuwa magogo, he kumbe wachawi?  Mungu wangu… tumekwisha!”
“Acheni  kuogopa  nyie, tufanyeni dua haraka kisha haya magogo tukayachome moto,“ alisema mmoja wao lakini kabla hawajatekeleza, kulitokea upepo mkali  uliokuwa unavuma kutokea baharini, ukazoa mchanga  mwingi na kuzunguka kama kimbunga. Kufumba na kufumbua yale magogo nayo yakatoweka kimiujiza.
Kutokana na woga, wale vijana walitimua mbio, kila mmoja akashika njia yake huku wakipiga mayowe ya kuomba msaada.

“Babu kwani pale kumetokea nini mpaka tukaondoka kirahisi namna ile?”
“Wale watoto wanataka kucheza na moto. Unajua tulikuwa na uwezo wa kuwadhuru lakini kwa sababu tupo kwenye msiba mzito nimeamua kuwasamehe.
Tulichokifanya pale ni kuhama kwa kutumia nguvu za giza kutoka dunia ya kawaida hadi dunia ya giza inayoongozwa na nguvu za kichawi, ndiyo maana tulipoondoka walijikuta wamebeba magogo kisha nayo yakachukuliwa na kimbunga.

“Kwa hiyo hapa hawatuoni?”
“Hawatuoni, si ndiyo maana wametupita hapahapa wakati wakikimbia?”
“Sasa  babu kwa nini huu uwezo mkubwa ulionao usiutumie kuisaidia serikali kwenye mambo ya maendeleo au kuokoa waathirika wa majanga kama hili badala ya kuishia kuwatesa na kuwatishia maisha watu?”

“Unajua maswali yako yanachosha sana. Nimeshakwambia ni kwa sababu serikali na watu wake hawaamini katika uchawi. Lakini siku inakuja ambapo dunia yote itakuwa na imani moja, hapo ndipo haya unayoyauliza mara kwa mara yatakapotimia.”

“Babu mbona nimewahi kusikia kuwa hicho unachokisema ndiyo sera kuu ya dini ya shetani ya Masoni? Hiyo si ndiyo New World Order?”

“Kwa nza nikurekebishe… Masoni siyo dini ya shetani, mimi nimekuwa mwanachama wake tangu nikiwa mdogo lakini mafundisho yote yanasisitiza kumpenda Mungu na kutii amri zake, nawashangaa wanaosema ni dini ya shetani.”

 “Pamoja na hayo bado hujajibu swali langu.”
“Vyovyote unavyofikiria lakini wakati unakuja ambapo dunia nzima itakuwa na dini moja, na hapo ndipo haya unayoyataka yatakapotimia.”

”Lakini babu unajua mi bado roho inaniuma sana juu ya wale watu wanaoteseka chini ya bahari, naomba unipeleke tena labda naweza kupata wazo la nini cha kufanya ili kuwasaidia.”

Bila hiyana, babu yake Kahungo alimuelekeza mjukuu wake kitu cha kufanya, akamwambia afumbe macho mpaka atakapomwambia afumbue. Baada ya sekunde chache, tayari walikuwa chini ya bahari, kwenye mkondo bahari wa Nungwi, eneo ambalo walikuwepo muda mfupi uliopita.

 Shughuli za mazishi zilikuwa bado zikiendelea huku vilio vikizidi kuongezeka kwa kadiri muda ulivyokuwa unaenda.

“Babu nakuomba kwa huruma yako tuwaokoe hawa watoto wadogo wanaotaka kuzikwa hai, angalau nao wakayafaidi maisha ya duniani kabla ya kuletwa tena huku makaburini.”

“Kwa kuwa umeng’ang’ania sana, ngoja nikaongee na Barthaayin, akikubali ndiyo tutaifanya hiyo kazi.”
“Kwani huyo Barthaayin ndiyo nani?”

“Ni mfalme wa roho ya mauti anayefanya kazi na Zirail. Binadamu wanapokufa yeye ndiyo hufanya kazi ya kuwahamisha kutoka kwenye ulimwengu wa roho kisha kuwaweka tayari kwa ajili ya safari ya kuzimu au peponi. Waliokuwa wanatenda amali njema wakati wa uhai wao huelekea peponi wakati watenda maovu huelekea kuzimu,” alisema babu na kuondoka kwa kasi.

Akamuacha Kahungo akiwa anayafikiria maelezo aliyompa juu ya huyo Barthaayin. Baada ya muda, babu alirejea huku sura yake ikiwa na tabasamu hafifu. Akamwambia kuwa mkuu wa roho ya mauti ameridhia ombi lake la kuwatoa baadhi ya watoto kutoka kwenye janga la umauti. Kauli ile ilimfurahisha sana, bila kupoteza muda akamsogelea babu na kumuuliza wanaanzia wapi.

“Lakini amesema idadi yao lazima iwe witiri na zaidi amependekeza watoto wa kiume saba ndiyo waachiwe huru, warejee kwenye familia zao,” alisema babu yake huku akitoa vitu kama dawa za kienyeji kutoka kwenye mkoba wake mdogo. Baada ya hapo akamwacha palepale alipokuwa, akamwambia kuwa bado hakuwa na nguvu za kutosha kuingia kwenye hali ya umauti na kurejea.

“Ili kumuokoa mtu ambaye ameshaionja roho ya mauti lazima na wewe umfuate hukohuko, kisha utoke naye. Usipokuwa na nguvu za kutosha unaweza kubakia hukohuko,” alisema babu yake huku akisisitizia kuwa makini na kuondoa hofu ndani ya moyo wake.

Alimwambia kuwa ili muujiza wowote utokee, sharti binadamu aishinde hofu na kuitawala akili yake. Alibaki ameshika tama akitaka kuona kama kweli kile alichokuwa anakisema kinawezekana. Baada ya kuagana naye,  alipotea kimiujiza. Baada ya kama dakika mbili tangu alipopotea, alianza kusikia vilio vya watoto wa kiume kutokea ndani ya ukuta wa bahari.

 Japokuwa babu yake alimsisitiza kupambana na hofu, alijikuta akitetemeka mwenyewe. 

4 comments:

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...