Monday, September 3, 2018

SEVEN DAYS IN HELL (SIKU SABA KUZIMU)- 65


ILIPOISHIA:
“Dont worry Jamal, each and everything is going to be okay!” (Usiwe na wasiwasi Jamal, kila kitu kitakuwa sawa) alisema Firyaal na kunisogelea, akanikumbatia na kunibusu mdomoni huku kila mtu akishuhudia. Sikujali, nilikuwa nampenda sana Firyaal na sikuwa tayari kuona jambo lolote baya linamtokea, hasa kabla ya mimi na yeye kukutana na kumaliza kile tulichokuwa tayari tumekianza.
SASA ENDELEA...

“Inabidi ubaki usaidiane na hawa askari, bado kuna kazi kubwa mbele yetu. Nakukumbusha tu kwamba huonekani na mtu yeyote kwa hiyo utakuwa na nafasi ya kuyafanya hata yale ambayo watu wa kawaida hawayawezi, ni lazima Loris akamatwe, umepigwa risasi na Firyaal naye amepigwa risasi, haiwezekani iwe ni kwa ajili ya kazi bure,” alisema Junaitha, sauti ambayo ilipenya vilivyo masikioni mwangu, akawa ni kama amezidi kuniongezea hasira.

Wale askari walipoingia, wengine ilibidi wabaki nje, wakatawanyika kule ndani kwa tahadhari kubwa na muda mfupi baaddaye, mvua nyingine ya risasi ikaanza kumwagika.
Nilishindwa kuelewa ni kwa sababu gani nyumba hiyo ilikuwa ikilindwa kiasi hicho, nikasikia sauti ya Junaitha masikioni mwangu akinielekeza kusonga mbele haraka mpaka pale walipokuwepo walinzi wengine waliokuwa wakifyatua risasi kwa kasi.


Nilipiga hatua mbili tu, bila kuonekana na mtu nikawa tayari nimeshafika kwenye geti la pili ambalo nalo lilikuwa na vyumba viwili vya walinzi kama kule mwanzo lakini tofauti yao, hawa hawakuwa ghorofani, vyumba vyao vilikuwa vya chini.

Kwenye chumba cha kwanza kilichokuwa upande wa kusini, kulikuwana walinzi wawili ambao tofauti na wale wa nje, hawa walikuwa wamevalia sare maalum, kwa kasi ya ajabu nikawashika vichwa na kuwagonganisha kwa nguvu, wote wakadondoka chini kama mizigo.

Nikainama na kushika shingo ya wa kwanza, nikaigeuza kwa kasi, sauti ya mfupa ukiteguka ikasikika, nikamfuata na yule wa pili, naye nikafanya hivyohivyo! Nikasikia sauti ya Junaitha ikinipongeza na kunielekeza kuelekea upande wa pili ambapo bado risasi zilikuwa zikiendelea kumiminwa.

Nilipoingiatu, kwa mbali nilishuhudia askari wengine wawili wakipigwa risasi na kudondoka chini, kwa jazba nikamshika wa kwanza na kumrushia ukutani na bunduki yake, kwa kuwa alikuwa ameshika sehemu ya kufyatulia risasi ‘trigger’, risasi kadhaa zilimiminika kwenye kifua cha mwenzake, nikammalizia kwa kuvunja shingo yake, eneo lote likawa kimya.

Sikuwa mimi ambaye najijua, roho ya mauti ilikuwa imenijaa kiasi kwamba kupoteza uhai wa mtu niliona kuwa kitu chepesi mno. Mpaka muda huo nilikuwa nimeshawanyonga walinzi kadhaa lakini bado nilikuwa na hamu ya kuendelea kuua tena na tena.
Nikawaona askari wengine wakiburuza miili ya wenzao na kuisogeza pembeni huku wengine wakija kwa kasi kubwa. Kwa muda wote huo hakuna aliyekuwa anajua kwamba mimi ndiyo nilikuwa mstari wa mbele, nikiwasafishia njia, wakawa wanaendelea kukimbilia ndani huku wakifyatua risasi.

Wakafika kwenye geti la pili na kulivunja, wakaingia ndani. Wakati wao wanahangaika kufungua geti, mimi nilikimbia na kuingia mpaka ndani kabisa, nikapigwa na butwaa kwa jinsi jengo hilo lilivyokuwa limejengwa.

Japokuwa kwa nje lilikuwa linaonekana kama jengo la kawaida tu, ndani ilikuwa ni zaidi ya ngome. Kulikuwana nyumba karibu saba, tena zote za kifahari, zikiwa zimejengwa kwa mtindo wa kuzunguka na kutengeneza kama duara hivi, huku kila moja ikiwa imezungukwa na mandhari nzuri sana.

Upande wa Magharibi kulikuwa kama na godauni hivi likiwa limezungushiwa nyaya za umeme, huku mlangoni kukiwa na walinzi wawili wenye bunduki ambao nao waliposikia ile mvua ya risasi, walikaa mkao wa kujihami.

Kwa hesabu za harakaharaka, mle ndani kulikuwa na zaidi ya watu kumi na mbili na miongoni mwao, walikuwepo wanawake watatu ambao kwa kuwatazama tu walikuwa wakifanana sana na Firyaal na Shenaiza, kuanzia rangi ya ngozi zao na watoto wa kiume wawili ambao hata bila kuuliza niligundua kwamba walikuwa ni wadogo zao Firyaal na Shenaiza.

Lakini pia kulikuwa na wanaume wengine kama wanne hivi, wenye miili mikubwa wakiwa na bunduki mikononi, nadhani ndiyo walikuwa walinzi wa mwisho wa familia hiyo. Wakiwa katika hali ya taharuki, walishtukia askari wengi wakiwavamia, wakiwa na silaha na yule kiongozi akasikika akitoa amri kwamba wote wasalimu amri vinginevyo watawapiga risasi.

Kwa jinsi askari walivyokuwa wamefanikiwa kuingia mpaka ndani kabisa, wale walinzi walijikuta wakikosa cha kufanya zaidi ya kusalimu amri, wakainua mikono juu huku wakitupa bunduki zao, wale wanawake nikawaona wote wakiwakimbilia watoto wao na kuwakumbatia, wakajikunyata chini huku wakipiga kelele.

Kwa kuwa askari wote walikuwa na mafunzo ya kazi zao, hawakushughulika sana na wale wanawake na watoto, wakawaweka chini ya ulinzi wale walinzi wote waliokuwa wameinua mikono juu, wote wakafungwa pingu na kulazwa chini.

Bado nilikuwa na shauku ya kutaka kujua mle ndani ya lile godauni lililokuwa likilindwa vikali mlikuwa na nini? Wakati hayo yakiendelea, tulishtushwa ghafla na mlio mkali wa gari lililoonesha kwamba linaondoka kwa kasi kubwa.

Kwa kasi ya ajabu nilianza kukimbia kuelekea kule muungurumo huo ulikokuwa unatokea, baadhi ya askari nao wakafanya hivyo.

Kumbe ile ngome ilikuwa na mlango mwingine wa dharura upande wa nyuma ambako nako kulikuwa na walinzi kadhaa wenye silaha, nikamuona mwanaume mwenye asili ya kiasi, mweupe, mnene, mrefu na mwenye nywele zenye mvi kiasi, akiwa katikati ya mabaunsa wanne, kila mmoja akiwa na bunduki, wakiwa ndani ya gari dogo lakini la kifahari ambalo nyuma lilikuwa wazi, Jeep.

“Mungu wangu,” nilijisemea kwa sababu kwa kumtazama tu, nilijua lazima huyo ndiyo baba yao akina Firyaal na Shenaiza na hapo alikuwa akijaribu kutoroka. Tayari geti lilikuwa limefunguliwa na zilihitajika sekunde chache tu kwa ile kasi yao, wawe tayari wameshatoka nje, jambo ambalo sikuwa tayari kuona likitokea.

Kwa uwezo wa nguvu za kipekee nilizokuwa nazo, niliwahi getini bila kuonekana na mtu yeyote, ndani ya hizo sekunde chache tu na mimi nikalifunga lile geti haraka. Kwa kasi waliyokuwa nayo, dereva alikanyaga breki lakini gari liliserereka na kwenda kulibamiza geti, ukuta wa juu ukabomoka na tofali kubwa likadondokea mbele ya gari hilo, likatua kwenye kichwa cha dereva na kumpasua.

Ungeweza kufananisha kila kitu na movi ya kusisimua ya mapigano, tayari askari nao walishafika na kulizingira lile gari ambalo bado lilikuwa likiendelea kunguruma, huku damu nyingi zikimwagika kutoka kwenye kichwa cha dereva.

Kwa jinsi kila kitu kilivyotokea kwa kasi kubwa, hata wale walinzi wa Loris walishindwa cha kufanya, wakazitupa silaha zao na kujisalimisha, wakawekwa chini ya ulinzi na kufungwa pingu, wote wakalazwa chini isipokuwa Loris ambaye ilibidi askari wawili wenye miili mikubwa wamshike huku na kule, akiwa amefungwa pingu kwani naye hakuwa mtu wa mchezomchezo.

Japokuwa alionesha kuwa umri umeenda, lakini alikuwa na mwili mkubwa wa mazoezi, mikono yake ikiwa na misuli kuonesha kwamba siyo mtu ambaye unaweza kumdhibiti kwa urahisi.

Wale walinzi wengine walirudishwa na kwenda kuchanganywa na wale wenzao, Loris akapelekwa moja kwa moja kwenye gari la polisi chini ya ulinzi mkali, akakalishwa chini.
Kazi iliyokuwa imesalia, ilikuwa ni kuvunja lile godauni kuangalia ndani kulikuwa na nini? Nilikuwa na shauku kubwa ya kujua kilichokuwemo mle ndani kwani kwa jinsi nilivyosikia stori za mzee huyo na mazingira ya ile ngome yake aliyokuwa akiishi, achilia mbali ulinzi wa hali ya juu, ilionesha ana mambo mengi sana maovu.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.


No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...