Thursday, February 1, 2018

SEVEN DAYS IN HELL (SIKU SABA KUZIMU)- 59



ILIPOISHIA:
Maneno yake yalinipa nguvu sana, akaniambia kwamba aliwalaza usingizi mzito kwa makusudi wale wengine ili tukamalizie kazi ya kumzindua Shenaiza lakini akanipa taarifa ambazo zilinishtua mno. Aliniambia baba yake Shenaiza amejizatiti vilivyo kwa nguvu za nje na ndani na ili tufanikishe azma yetu, ilikuwa ni lazima mtu mmoja kati yetu afe.
“Afe?”
“Ndiyo, lazima afe mtu kwenye kafara.”
SASA ENDELEA...
“Sasa mambo ya makafara yanaingiaje tena hapa? Kama ni hivyo basi mimi najitoa.”
“Ukijitoa maana yake wewe ndiyo utakufa. Wasiwasi wa nini na wewe ni mwanaume? Hebu acha woga, nitakufundisha cha kufanya wala usiwe na wasiwasi,” alisema Junaitha lakini kiukweli alikuwa amenichanganya mno.
Mmoja kati yetu lazima afe? Nani sasa! Kama siyo mimi ni nani? Raya? Haiwezekani. Shenaiza? Hapana. Shamila? Noo! Au Firyaal? Nilijiuliza maswali mengi ambayo yote hayakuwa na majibu. Nilichokifanya ilikuwa ni kujaribu kupambana na hofu ambayo sasa ilikuwa inanitafuna ndani kwa ndani.

Hakuna kitu ambacho binadamu hawezi kukizoea kama kifo! Miaka yote watu wanakufa lakini kwa nini kila mtu anapokufa kunakuwa na msiba mzito kwa watu wanaomzunguka? Ni dhahiri kwamba kifo hakizoeleki.
“Mbona kama umepoteza umakini Jamal? Kwani wewe unaelewa nini kuhusu kifo?” aliniuliza Junaitha, swali ambalo lilinizindua kutoka kwenye lindi la mawazo.
“Kifo? Kifo si ni kufa?”
“Ndiyo ni kufa, unaelewa nini kuhusu kufa?”
“Mtu anakufa na huo ndiyo unakuwa mwisho wa maisha yake,” nilimjibu Junaitha, nikiwa nimemkodolea macho.
“Huna haja ya kuogopa kuhusu kifo kwa sababu kinachotokea inakuwa ni kuhama tu kutoka kwenye ulimwengu mmoja kwenda kwenye ulimwengu mwingine, ni kama hivi tu sisi tunavyofanya lakini tofauti yake ukifa unakuwa huwezi kurudia kwenye mwili wako lakini hakuna tofauti sana.”
“Sijakuelewa.”
“Utanielewa tu wala usiwe na haraka, sitaki kabisa kusikia ukiogopa kuhusu kifo, umenielewa?”
“Nitaachaje kuogopa Junaitha?”
“Sasa unaogopa nini? Mbona huogopi tunavyohama kutoka ulimwengu mmoja kwenda mwingine?” alisema Junaitha lakini bado alichokuwa anakisema hakikuingia kabisa akilini mwangu.
“Hebu tuachane na haya mambo kwanza, tuna kazi kubwa mbele yetu,” alisema, akanibusu mdomoni, nikashusha pumzi ndefu na kuinuka pale tulipokuwa tumelala, naye akainuka, tukatoka na kuelekea kwenye chumba alichokuwa amelala Shenaiza.
“Hebu niambie ukweli, hujawahi kufanya mapenzi na huyu msichana kweli?” Junaitha aliniuliza, akimaanisha Shenaiza, nikamjibu kwa kutingisha tu kichwa.
“Hebu nitazame usoni,” alisema Junaitha lakini sikutaka kumtazama kwa sababu ambazo nazijua mwenyewe.
“Kwa nini tusimalize kazi kwanza halafu hayo mengine yatafuata baadaye?” nilisema huku nikionesha kutofurahishwa na swali lake, ilivoonesha naye hakutaka kuniudhi kwani alibadilisha mada haraka.
“Simama kwa kule,” aliniambia, akinioneshea upande uliokuwa na miguu ya Shenaiza, nikafanya kama alivyoniambia. Yeye alisimama upande wa kichwani kwa msichana huyo, akapiga magoti na kunitaka na mimi nifanye hivyohivyo.
“Katika vidole vyako kumi vya mikono, nataka kila kimoja kiguse kidole cha Shenaiza na ushikilie hivyohivyo, usiachie,” aliniambia, nikafanya kama alivyoniambia. Kweli nilishika vidole vyote vya Shenaiza, nikawa namtazama Junaitha kusubiri maelekezo zaidi.
“Fumba macho,” alisema Junaitha na kusisitiza kwamba nisimuachie vidole wala nisifumbue macho, nikamsikia akianza kuongea maneno ambayo hata sijui ni ya lugha gani au yalikuwa yakimaanisha nini, akaendelea kuyarudiarudia na kadiri alivyokuwa anazidi kuongea ndivyo sauti yake ilivyoanza kuwa ya kutisha, ikawa inasikika kama ile aliyoitoa kule kwenye ulimwengu mwingine ambayo ama kwa hakika ilikuwa ikitisha.
Nilianza kuhisi vitu kama upepo mkali ukivuma mle ndani, sikuelewa umetokea wapi, ukabadilisha na kuanza kuwa kama kimbunga kikali, vitu vikawa vinapeperushwa huku na kule. Upepo ulizidi kuwa mkali, Junaitha naye aliendelea kuyarudiarudia maneno yake kwa ukali, mara ikaanza kusikika miungurumo ya ajabu mle ndani, ikafuatiwa na radi kubwa iliyopiga kwa nguvu kubwa mno, nilijikuta nikipoteza mwelekeo, nikarushwa mpaka ukutani, nikajibamiza na kudondoka chini.
Ninachoshukuru ni kwamba sikufumbua macho kama Junaitha alivyoniambia, nikajikuta nimepoteza fahamu, nikawa sielewi kinachoendelea.
“Wewe ni nani?”
“Na wewe ni nani?” nilijikuta nikirejewa na fahamu lakini nusunusu, jitu kubwa ambalo sikuweza kuona mwisho wake, lilikuwa limesimama mbele yangu, likiniuliza kwa sauti nzito. Cha ajabu, eti wala sikuogopa chochote na badala ya kujibu, na mimi nikaliuliza swali.
“Kwa nini mnaingilia mambo yasiyowahusu? Mnamjua huyu binti? Kwa nini mnataka kumsaidia?”
“Na nyie kwa nini mnamtesa? Si ameshawaambia hataki kushirikiana nanyi?”
“Wewe ndiyo unamsemea? Kwa nini asiseme mwenyewe?”
“Nasema mwenyewe sasa, sitaki kushirikiana na nyie, Jamal nisaidie baba?” sauti ambayo niliitambua vyema kwamba ni ya Shenaiza ilisikika lakini nilipogeuka huku na kule, sikumuona zaidi ya lile jitu.
“Unasemaje wewe?”
“Nimesema sitaki kushirikiana na nyie, niacheni na maisha yangu,” sauti ya Shenaiza ilisikika tena, ghafla ikasikika tena radi kali ambayo safari hii niliona kama imepiga jirani kabisa na pale nilipokuwa.
Fahamu zikanirudia vizuri, nikajikuta nimelala sakafuni, huku Shenaiza akipiga kelele kwa nguvu pale kitandani, Junaitha akikazana kumtuliza.
“Njoo unisaidie Jamal, inuka njoo,” alisema Junaitha, nikainuka pale sakafuni kwa kujikongoja, nikasogea pale nilipokuwa nimesimama awali, Junaitha akaniambia nimshikilie Shenaiza ambaye alikuwa akirusha miguu na kutapatapa.
“Tulia Shenaiza, kila kitu kitakuwa sawa,” alisema Junaitha, msichana huyo ambaye muda wote alikuwa amefumba macho, alifumbua na ghafla akawa ni kama amezinduka, macho yake yakatua kwangu.
“Jamal!”
“Shenaiza.”
“Hapa ni wapi na nimefikaje?”
“Ooh! Ahsante kazi imekamilika,” alisema Junaitha huku akimuachia Shenaiza, akawa anajifuta jasho jingi lililokuwa linamtoka.
“Na huyu ni nani?”
“Tulia Shenaiza, kwanza pole kwa yote yaliyokutokea, pumzika kwanza utajua kila kitu,” nilimwambia, akawa bado ni kama ana mawenge, akawa ananitazama mimi, anamtazama Junaitha, anakitazama kile chumba, anajitazama yeye mwenyewe katika namna ya kushangaa sana.
“Inabidi nikamuogeshee maji ya maiti, amka binti,” alisema Junaitha na kumshika mkono Shenaiza ambaye bado alikuwa ameduwaa. Kiukweli hata mimi nilikuwa na maswali mengi sana lakini ilibidi nijikaze ili Shenaiza atulie. Nilishangaa kwamba iweje ndani ya muda mfupi tu namna hiyo, kutokee mambo ya kutisha kiasi kile mle ndani halafu watu waliopo nje wasijue chochote?
Nini kimefanyika mpaka Shenaiza ambaye kwa siku kadhaa alikuwa amepoteza kabisa fahamu, leo arudiwe na fahamu zake kama hakuna kilichotokea? Wanaosema uchawi haupo, nawapa pole. Uchawi upo na una nguvu kwelikweli.
“Njoo kwanza Jamal,” alisema Shenaiza baada ya kuwa ameshasimama kwa msaada wa Junaitha, mwili wake ukiwa hauna nguvu kabisa. Nilimsogelea, akanikumbatia kwa nguvu na kunibusu mdomoni, tukio ambalo Junaitha alilishuhudia ‘laivu’.
“Nakupenda sana, naamini wewe ndiyo umeyapigania maisha yangu mpaka muda huu,” alisema, nikamuona Junaitha akimshika mkono bila kusema kitu na kuanza kumvuta kuelekea bafuni.
Mate ya Shenaiza yalikuwa machungu kuliko klorokwin, nikawa najikaza tu huku nikijitahidi kuachia tabasamu kwenye uso wangu. Junaitha alimkokota mpaka bafuni na kufunga mlango kwa ndani, nikabaki nimesimama pale koridoni.
Ghafla nikaanza kusikia sauti ya Firyaal akilia kama mtu anayekabwa na kitu, nikakurupuka mpaka kwenye kile chumba walichokuwa wamelala wote, nikafunga breki za ghafla mlangoni, nikiwa siamini kile nilichokuwa nakiona.
Je, nini kitaendelea? Usikose next issue.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...