Friday, February 2, 2018

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 64



ILIPOISHIA:
Tukiwa tunaendelea kuchanja mbuga, baba akiwa mbele na baba yake Rahma akiwa nyuma, mara tulianza kusikia sauti za ajabu kutoka ndani ya pori lile, huku kukiwa na purukushani kubwa, mapigo ya moyo wangu yalilipuka na kuanza kunienda mbio kuliko kawaida.
SASA ENDELEA...
“Nakufaaa! Naku...fa...aa,” sauti ya mwanamke ilisikika, aliporudia mara ya pili kuimba msaada, sauti yake ilikuwa ikikwamakwama na muda mfupi baadaye akaanza kukoroma kuonesha kwamba mtu au watu waliokuwa wakitaka kumdhuru tayari walishafanikisha lengo lao.
Tofauti na hali niliyokuwa nayo mimi, baba na baba yake Rahma hawakuonesha kushtuka chochote, yaani ilikuwa ni kama hakuna kilichotokea na wala hakuna aliyeshughulika kwa chochote.
Muda mfupi baadaye, harufu ya damu mbichi ilitawala eneo lote lile, milio ya bundi na midege mingine ya ajabu ikazidi kuifanya hali iwe ya kutisha mno. Baba aliendelea kupiga hatua ndefundefu, hukumoyo wangu ukiwa umepondwapondwa kwa hofu na mshtuko, na mimi nikawa naongeza mwendo, miguu yangu ikitetemeka kuliko kawaida.

“Unaogopa nini? Hili linaitwa pori la kafara, huku ndiyo watu wanakokuja kutolea makafara ili mambo yao yafanikiwe,” alisema baba yake Rahma huku tukiendelea kusonga mbele, sikumjibu chochote maana bado nilikuwa natetemeka sana.
Jambo ambalo mpaka leo huwa silipatii majibu, ni kwa nini watu wenye imani za giza hawaoni hatari kabisa kuyakatisha maisha ya mtu mwingine? Ni kweli kwamba sote tutakufa na kifo hakiepukiki lakini kwa nini uyakatishe maisha ya mtu mwingine kwa sababu zako binafsi?
Japokuwa na mimi nimefanya sana huo mchezo, natamani kama utokee muujiza nguvu zote za giza zipotee. Ukweli ambao watu wengi hawaujui, katika vifo vinavyotokea kila siku, iwe ni kwa ajali, magonjwa, watu kujinyonga au kuuana, nguvu za giza zinahusika kwa asilimia kubwa sana.
Kuna matukio mengine unaweza kuona kama ni kifo cha kawaida tu lakini mtu mwenye uwezo wa kuona mambo kwa jicho la tatu, anakuwa anaelewa mchezo mzima ulivyotokea. Si kila kifo kinachotokea kipo kama unavyoweza kudhani, humu duniani kuna mambo mengi sana yaliyojificha na kuna watu wanawaonea sana wenzao na kundi kubwa linaloonewa sana, ni wale watu wasio na imani thabiti ndani ya mioyo yao.
Basi tulifika mpaka barabarani, kwa kuwa muda ulikuwa umeenda sana, hakukuwa na magari yoyote yaliyokuwa yakipita, barabara ilikuwa kimya kabisa. Nilitegemea baba atasema tutafute sehemu ya kuondokea kama kawaida yetu maana nilikuwa nimchoka sana lakini safari hii alizungumza kitu cha tofauti.
Alisemakwa sababu tulikuwa tumebeba kitu cha muhimu sana, ilikuwa ni lazima tufike nyumbani kwa njia za kawaida. Aliposema tumebeba kitu muhimu sikumuelewa kwa sababu kiukweli hakuna hata mmoja kati yetu aliyekuwa na mzigo wowote. Tulianza kutembea pembezoni mwa barabara ileile ya lami tuliyojia, huku wote tukiwa kimya kabisa. Utaratibu wetu ulikuwa uleule, baba mbele, mimi katikati na baba Rahma nyuma.
Kwa bahati nzuri, tulipofika mbele kidogo, kuna Fuso lilikuwa likitokea upande wa mashambani, likiwa na shehena ya mananasi, kama ujuavyo tena Bagamoyo kunalimwa sana matunda.
Harakaharaka baba alimpungia mkono dereva, akasimamisha gari kabla hajaingia kwenye barabara ya lami, akamfuata na kuzungumza naye ambapo sekunde chache baadaye, baba alitupa ishara kwamba tupande.
Nadhani walishakubaliana, ikawa ahueni maana nilikuwa nikiiwazia sana ile safari. Gari lilikuwa limejaza mananasi mpaka juu kabisa, ikabidi tupande na kukaa juu ya mabomba na kujishikilia vizuri, dereva akaliingiza gari kwenye barabara ya lami na safari ikaendelea.
Japokuwa kule juu kulikuw ana upepo mkali unaochoma mpaka ndani ya kifua, ilibidi tuvumilie maana ilikuwa bora kuliko kutembea kwa miguu. Baada ya kama dakika hamsini hivi, tuliwasili jijini Dar, tukateremka kwenye kituo cha Mwenge, tukamshukuru sana yule dereva, yeye akaendelea na safari yake na sisi tukaanza kutembea kuelekea nyumbani.
Kitu kingine ambacho nilijifunza lakini nisingependa kukizungumzia sana leo, maduka mengi, hasa yale makubwa, yanakuwa na ulinzi wa nguvu za giza hasa nyakati za usiku ambapo kama una uwezo wa kuona mambo yaliyojificha, unaweza kustaajabu sana.
Hii dunia ina mambo mengi sana yaliyojificha, kama nioivyosema, sitaki kuelezea sana kuhusu hili. Basi tuliendelea na safari yetu mpaka tulipofika nyumbani, tayari ilishagonga saa tisa na nusu.
“Unatakiwa kuwa mtulivu na msiri, hakuna kitu cha ajabu tena kwako, umenielewa,” baba aliniambia kwa kauli ya msisitizo wakati tukiagana kwa ajili ya kila mmoja kwenda kulala lakini sikumuelewa anamaanisha nini.
“Kuanzia leo utakuwa unalala peke yako, chumba chako kinatakiwa kuwa kimefungwa muda wote na usiruhusu watu kuingiaingia, hata awe nani, umenielewa?” alisema baba, baba yake Rahma akawa anatingisha kichwa kuonesha kwamba anaunga mkono kile alichokisema baba.
Bado sikuwa naelewa kwa nini wananiambia vile, baba akahitimisha kwa kuniambia kwamba eti hategemei kunisikia nikifanya jambo lolote la ajabu. Tuliagana, nikaingia chumbani kwangu, kweli yule ndugu yangu niliyekuwa nalala naye siku mojamoja hakuwepo, kwa hiyo nilikuwa peke yangu.
Kwa jinsi nilivyokuwa nimechoka, sikutaka hata kufanya kitu kitu chochote, nikavua nguo zote, nikazima taa na kujilaza kitandani. Mwili wangu ulikuwa na maumivu sehemu mbalimbali, lakini pale yule mwanamke aliponichanja usiku huo palikuwa na maumivu makali zaidi.
Nikiwa bado natafakari mambo chungu nzima yaliyotokea kwa siku nzima, nilisikia kitu kilichonishtua sana. Chini ya kitanda changu kulikuwa kama na purukushani fulani hivi kwa mbali, ikabidi harakaharaka niinuke na kwenda kuwasha taa.
Nikainama chini kwa tahadhari kubwa na kuchungulia uvunguni, katika hali ambayo sikuitegemea kabisa, nilikiona kile kimfuko kilichotengenezwa kwa kipande cha gunia, nilichokionakule kwa yule mtaalamu kikiwa chini ya kitanda changu.
Ni kimfuko hichohicho ndicho yule mtaalamu tuliyetoka kwake usiku huo, alichomuweka yule nyoka mdogo baada ya kumlambisha damu yangu. Kilichonishtua zaidi, kimfuko kilikuwa tupu, kwa akili za harakaharaka nikahisi kwamba lazima zile purukushani nilizokuwa nazisikia, zilikuwa ni za yule nyoka akihangaika kutoka.
Sasa kimfuko kimefikaje chumbani kwangu? Na kama kile nilichokuwa nakihisi ni kweli, yule nyoka alikuwa mle ndani, ningelalaje? Nilijikuta usingizi wote ukiniisha, harakaharaka nikapanda juu ya kitanda na kukaa kwenye uchago wa kitanda ili hata akipanda kitandani, asiweze kunifikia.
Ni hapo ndipo nilipoanza kuelewa kauli za baba zilikuwa na maana gani, kuanzia ile ya kule njiani kwamba ‘tumebeba kitu muhimu sana’, mpaka yale maneno aliyoyazungumza muda mfupi uliopita kabla kila mmoja hajaenda kulala.
Nilijiapiza kwamba sitalala mpaka kupambazuke, na ukizingatia tayari muda ulishaenda sana, niliona isiwe tabu. Lakini waliosema usingizi ndugu yake kifo hawakukosea, hata sijui nini kilitokea, nilipokuja kushtuka baadaye, nilijikuta nimelala kitandani na kibaya zaidi, hata taa ilikuwa imezimwa.
Mshtuko nilioupata ulikuwa hauelezeki, nikafumbua macho na kuyakodoa kama nitaona chochote lakini nilijitahidi nisitingishike hata sehemu moja kwenye mwili wangu. Nikiwa nimejikausha kama gogo, nilihisi hali fulani kwenye ile sehemu yule mwanamke aliponichanja usiku huo.
Nilihisi kama kuna kitu kinanilamba hivi, nikaanza kutetemeka huku nikiendelea kujikausha nisisababishe mtikisiko wa aina yoyote, nilipozidi kuvuta utulivu, nikahisi kuna kitu cha baridi kinatingishikatingisha upande ule niliokuwa nalambwa, mapigo ya moyo yakawa yanadunda kama nimetoka kukimbia mbio za mita mia moja.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...