Monday, January 29, 2018

DOUBLE LIFE (Maisha Mara Mbili)- 2



ILIPOISHIA:
Naamua kuendelea kujilaza, vishindo vinazidi kusogea na sasa vinasikika mita chache tu kutoka pale nilipojilaza, naamua kuushinda usingizi na kuyafumbua macho yangu, napigwa na butwaa na ninachokiona mbele ya macho yangu.
SASA ENDELEA...
“Iqram! Ni wewe au naota? Ooh Mungu wangu,” msichana mrembo mwenye mchanganyiko wa damu kama chotara wa Kizungu na Kiafrika, anashuka kutoka kwenye mgongo wa farasi mkubwa mweupe aliyekuwa amesimama mita chache kutoka pale nilipokuwa nimejilaza.
Kumbe vile vishindo vilikuwa ni vya farasi huyo mkubwa lakini mzuri, kwa wale wenye mazoea ya kwenda ufukweni, hasa nyakati za jioni watakuwa mashahidi kwamba mara chache unaweza kukutana na mtu au watu waliopanda farasi, wanaokimbia nao ufukweni wakipunga upepo wa bahari.
Sikuwa nimezoea kuwaona farasi kwa karibu, nikawa namshangaa huku nikijiuliza maswali mengi ndani ya kichwa changu kuhusu mnyama huyo. Ni kama nilisahau kabisa uwepo wa msichana huyo mrembo.

“Iqram! Iqram!” alisema, safari hii akiwa ameshateremka kwenye yule farasi, akanisogelea na kuniinamia pale chini. Nilimtazama, macho yake na yangu yakakutana, sura yake haikuwa ngeni kabisa machoni mwangu ingawa sikuweza kabisa kukumbuka nilimuona wapi.
Kingine kilichonishangaza, ni kwamba aliniita jina ambalo mara kwa mara ndilo nililokuwa nikiamini kwamba ndiyo jina langu halisi ingawa watu wote, hata wazazi wangu walikuwa wakikataa kwamba hilo siyo jina langu.
Kwa mujibu wa mtu ambaye alikuwa akisema kwamba ndiye mama yangu mzazi, nilipozaliwa nilipewa jina la Davis na watu wote wanaonifahamu walikuwa wakinijua kwa jina hilo.
Mara kwa mara nilikuwa nikiingia kwenye ugomvi mkubwa na ‘wazazi’ wangu, nikiwaambia kwamba mimi jina langu siyo Davis, naitwa Iqram na hilo ndiyo jina nililopewa nilipozaliwa, hiyo ikawa miongoni mwa sababu za wao kuamini kwamba huenda kweli nilikuwa na matatizo ya akili.
“Umeniitaje?”
“Swali gani hilo, kwani wewe jina lako siyo Iqram? Mbona upo huku? Kwa nini una hali hiyo Iqram? Nini kimekusibu jamani?” alisema yule msichana huku akishindwa kuzizuia hisia zake, machozi yakawa yanamtoka kwa uchungu.
“Samahani, unaweza kunikumbusha wewe ni nani?” nilimuuliza swali lililomfanya ashtuke, akanitazama vizuri huku akijifuta machozi yake. Sijui kwa nini alishtuka kiasi hicho baada ya mimi kumuuliza swali.
“Akili yako imepatwa na tatizo gani Iqram?”
“Mbona sina tatizo lolote? Watu wote wananiita Davis, wewe umejuaje kama mimi naitwa Iqram?” nilimuuliza swali lingine, nadhani kwa jinsi nilivyokuwa nikiongea na yeye alianza kupatwa na wasiwasi kama akili yangu ipo sawa maana hakunijibu zaidi ya kunitazama kwa macho yake mazuri ambayo sasa yalikuwa yamebadilika rangi na kuwa mekundu.
“Mbona hunijibu?”
“Upo ‘siriasi’ na hayo maswali yako? Umenisahau au hunijui? Iqram, unajua ni kwa kiasi gani nimehangaika kukutafuta? Yaani kwanza hata siamini kama ni wewe, tafadhali naomba usinifanyie hivyo,” alisema huku akianza tena kulia.
Katika hali ambayo sikuitegemea, bila kujali hali yangu niliyokuwa nayo, aliniinamia pale chini na kunibusu, nikashtuka kidogo, machozi yake ya moto yakawa yananidondokea mwilini, harufu ya pafyumu yake ikapenya kwenye pua zangu na kunifanya nishtuke zaidi.
Ilikuwa ni harufu ya pafyumu ambayo nilikuwa naijua ingawa sikukumbuka nimewahi kukutana nayo wapi. Tofauti kabisa na watu wote niliokuwa nikikutana nao nikiwa kwenye hali hiyo, msichana huyo mrembo hakuonesha kuwa na hata chembe ya kinyaa juu yangu.
“Umepatwa na nini Iqram?” aliendelea kusema huku akilia, mara kwa mara akinibusu, nikawa namtazama usoni huku nikiendelea kujiuliza maswali yaliyokosa majibu. Msichanahuyu mrembo ni nani? Amelijuaje jina langu la Iqram? Kwa nini ameguswa sana na hali aliyonikuta nayo? Nilijiuliza maswali mengi yaliyokosa majibu.
Nilitamani kuendelea kumuuliza lakini niliogopa kuendelea kuonekana mwendawazimu, isitoshe msichana mwenyewe alionesha kuguswa sana na hali yangu na kadiri nilivyokuwa nikizidi kuzungumza naye, ilionesha kama ndivyo alivyokuwa akizidi kuumia kwa hiyo nilichoamua ilikuwa ni kuendelea kujiuliza maswali kimyakimya.
“Baba na mama watafurahi sana wakikuona, wamehangaika sana juu yangu chanzo cha yote ikiwa ni wewe, namshukuru Mungu kwa kunileta huku ufukweni jioni hii,” alisema huku akinishika mkono.
“Twende nyumbani kwetu, leo itakuwa ni siku ya kipekee sana,” alisema huku akiinuka akiwa bado ameushikilia mkono wangu. Bado sikuwa naelewa kinachoendelea, nikajikuta nimesimama lakini maumivu makali ya miguu yalinifanya nirudi tena pale chini.
Miguu ilikuwa ikiuma sana, pia nilikuwa na majeraha mengi ya kukanyaga vitu vyenye ncha kali na vipande vya chupa, ukichanganya na yale maumivu ya kutembea kwa miguu umbali mrefu kila siku, nilikuwa kama mlemavu wa miguu.
“Vipi tena? Miguu inakuuma? Hebu nione...” alisema huku akiinama na kuitazama miguu yangu.
“Mungu wangu! Mbona upo hivi?” alisema huku akijiziba mdomo kwa kiganja chake cha mkono kuonesha ni kwa kiasi gani alikuwa ameshtuka kutokana na miguu yangu ilivyokuwa.
“Ok, nataka unishikilie nikupandishe kwenye farasi, tukifika nyumbani kwetu daktari wa familia yetu atakusaidia na nakuhakikishia utapona na kuwa sawa,” alisema, mimi bado nikawa namtazama usoni, akili zangu zikiwa zinawaza mambo mengine tofauti kabisa.
Kuna wakati kama nilikuwa nakaribia kumkumbuka hivi lakini kumbukumbu zikawa zinapotea, ilinibidi nikubaliane naye, kweli akaninyanyua tena. Hakuwa na nguvu za kuweza kunimudu lakini na mimi nikawa najitahidi, akanipandisha kwenye mgongo wa yule farasi mkubwa ambaye bado alikuwa amesimama palepale, na yeye akapanda na kukaa nyuma yangu, nikawa nalisikia joto la mwili wake na kunifanya nijihisi kama nimefufuka kutoka katika wafu.
Tayari kigiza kilishaanza kuingia, akamgeuza yule farasi, akazichezesha hatamu zake na kuanza kukimbia, huku kigiza kikizidi kuingia.
***
MIAKA 11 ILIYOPITA
Vwawa, Mbozi
Ilikuwa ni Jumatatu kama zilivyo Jumatatu nyingine zote, niliamshwa usingizi na sauti ya mama yangu aliyekuwa akinisisitiza kuwahi kuamka ili nisichelewe shuleni. Huo ndiyo uliokuwa utaratibu wa kila siku, mama yangu alikuwa akipenda sana niwahi shuleni na alikuwa akinisisitiza kwamba elimu ndiyo kitu pekee kitakachokuja kunifanya niweze kuyamudu maisha yangu, hata kipindi ambacho wao watakuwa wameshaondoka kwenye uso wa hii dunia.
Baada ya kumaliza kujiandaa, nilitoka haraka na kuchukua baiskeli yangu ndogo, ambayo mama alininunulia baada ya kufanya maajabu kwenye mtihani wa darasa la nne, kipindi hicho nikiwa bado mdogo kabisa ambapo niliibuka na kuwa mshindi wa kwanza kwa mkoa mzima wa Mbeya.
Mama alifurahishwa sana na heshima niliyokuwa nimemletea, kama zawadi ndiyo akaenda kuninunulia baiskeli hiyo. Kwa kipindi hicho, mtoto, tena mwanafunzi kumiliki baiskeli ndogo ya kisasa, wengi wanapenda kuziita ‘sport’, ilikuwa ni lazima utoke kwenye familia inayojimudu kisawasawa kiuchumi.
Basi nilipanda kweye baiskeli yangu, begi langu la daftari likiwa mgongoni, safari ya kuelekea shule ikaanza huku nikiwa na furaha kama kawaida yangu. Miongoni mwa sifa za kipekee nilizokuwa nazo, ni kwamba muda wote nilikuwa napenda sana kufurahi na hiyo ilisababisha niwe na marafiki wengi sana, kuanzia wanafunzi wenzangu mpaka walimu.
Ilikuwa ni nadra sana kunikuta nimenuna, muda wote tabasamu pana lilikuwa limechanua kwenye uso wangu. Nadhani hiyo ilichangiwa pia na aina ya maisha tuliyokuwa tukiishi, familia yetu ilikuwa na amani na upendo mkubwa sana. Kila nilichokuwa nakihitaji nilikuwa nikikipata kwa wakati, kwa hiyo kitu kitwacho shida kwangu ulikuwa ni msamiati mgeni.
Ili kufika shuleni nilikokuwa nasoma, Mwenge Primary School, ilikuwa ni lazima uvuke barabara kubwa ya lami ya Mbeya-Tunduma. Kwa wale waliowahi kuitumia barabara hii, watakuwa wanaelewa vizuri kwani ni miongoni mwa barabara kubwa zinazounganisha nchi moja na nyingine.
Ni barabara hii ndiyo iliyokuwa ikiziunganisha Tanzania na Zambia, kwa hiyo muda wote ilikuwa ‘bize’ sana, magari ya kila aina yalikuwa yakipita, tena kwa kasi kubwa, mengine yakielekea upande wa Tunduma na mengine upande wa Mbeya.
Basi nikiwa na baiskeli yangu, nilipofika njiani, nilikutana na rafiki yangu mmoja kipenzi, Mungu aipumzishe roho yake mahali pema peponi. Jina lake alikuwa akiitwa Wilson, alikuwa rafiki yangu kipenzi sana kiasi kwamba darasani tulikuwa tukikaa dawati moja.
Japokuwa baiskeli yangu haikuwa na sehemu ya kumpakiza mtu, nilipomuona Wilson nilisimama ili apande kwa nyuma, yaani kwenye tairi la nyuma kuna ‘msumari’ mmoja mrefu  unaotoa sapoti ya tairi kuzunguka, kwa hiyo kama baiskeli haina kiti cha nyuma, mtu anaweza kusimama kwenye msumari huu, kwa kuacha upenyo mdogo katikati ya miguu kuruhusu tairi lizunguke, halafu anakuwa amesimama na kumshikilia dereva mabegani kisha safari inaendelea.
Kwa waliopitia maisha ya ‘utundu’ kama mimi wanaweza kuwa wananielewa vizuri  ninaposema hivi, basi hivyo ndivyo ilivyotokea, nilimpakia Wilson na safari ya kuelekea shule ikaendelea, huku tukipiga stori za hapa na pale, tukicheka na kufurahi kama kawaida yetu.
Dakika chache baadaye, tayari tulikuwa tumewasili eneo maarufu ambapo barabara ya vumbi inakatisha kwenye barabara kuu ya Mbeya-Tunduma. Ni jirani kabisa na kituo kikuu cha polisi cha Vwawa.
Siku zote ninapovuka barabara huwa nipo makini sana lakini sijui nini kilitokea siku hiyo, tukiwa tunaendelea kupiga stori, akili zikiwa hazipo kabisa kwamba sasa tunavuka kwenye barabara kubwa ya lami, tena yenye shughuli kibao, nilishtukia honi kali za lori zikipigwa, zikifuatiwa na kelele za vyuma vya breki kusuguana na matairi, sambamba na matairi kusuguana na lami, kikasikika kishindo kikubwa kisha giza nene likatanda kwenye upeo wa macho yangu. Sikuelewa tena kilichoendelea.
Je, nini kitafuatia? Usikose Jumatatu kwenye Championi Jumatatu.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...