Thursday, December 21, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 55


ILIPOISHIA:
“Ukitaka kuendelea kuishi, kazi ni moja tu, tunataka utuoneshe Shenaiza alipo na pia utuambie mbinu zote za kishirikina ulizomfanyia baba yake alipokuja kwako kuomba kinga ya kufanikisha mambo yake ya kishetani,” alisema Junaitha, mwanamke huyo akaanza upya kulia huku akitingisha kichwa chake, hali iliyozidi kunifanya nikose majibu. Aliendelea kulia na mara akaanza tena kutoa muungurumo kama mnyama mkali wa porini, akawa anafurukuta kwa nguvu.
SASA ENDELEA...
“Usitake kututisha hapa na ukiendelea na upuuzi wako nitakuua kwa mikono yangu mwenyewe, unajua ni kwa kiasi gani nina hasira na wewe?” alisema Junaitha kwa sauti nzito ya kunguruma, ambayo sikuwahi kumsikia hata siku moja, yule mwanamke mzee akanywea na kurudi kwenye hali yake ya kawaida lakini bado alikuwa akilia huku akitingisha kichwa, akionesha hayupo tayari kuzungumza kitu chochote.
“Wala sikulazimishi, uchaguzi ni wako, ukitaka kuendelea kuishi ni lazima uzungumze na ukitaka kufa endelea kukataa.”
“Hata nikizungumza nitakufa tu, hawezi kuniacha, ataniua.”
“Nani, unamzungumzia nani?”
Badala ya kujibu, yule mwanamke alionesha kwa ishara, Junaitha na mimi tukageuka kutazama kule alikokuwa anaonesha.
“Mungu wangu,” nilijikuta nimetamka wa sauti kubwa, Junaitha akaniwahi na kuniziba mdomo.

“Huku huwa hatumtaji ovyo Mungu, si unajua kuna amri katika vitaabu vitakatifu ambayo inasema usilitaje bure jina la Bwana Mungu wako?” alisema Junaitha kwa sauti ya kunong’ona, nikatingisha kichwa kama ishara ya kukubaliana naye lakini bado moyoni nilikuwa nimepatwa na hofu kubwa mno.
Joka kubwa lililokuwa limesimamia mkia na kujiinua, likiwa na macho mekundu yanayowaka huku ulimi wake mrefu wenye ncha mbili ukichezacheza, lilikuwa likitutazama, mita chache kutoka pale tulipokuwa tumembananisha yule mwanamke mzee.
“Huyu ni nani?”
“Mkuu.”
“Anahusikaje katika hili?”
“Maagano yote wanayoyafanya watu wanaoishi Kusini mwa Jangwa la Sahara na kuzimu hupitia kwake na yeye ndiye anayeidhinisha.”
“Anataka nini?”
“Anataka mniachie niende zangu,” alisema yule mwanamke huku akitetemeka. Muda wote huo, macho yangu yalikuwa yameganda kwenye lile joka, kuna wakati nilihisi kama haja ndogo inanitoka kwa hofu. Likawa linageuza kichwa huku na kule, likiendelea kuchezesha ulimi huku likitutazama.
Mara likaanza kuteleza taratibu likitusogelea, Junaitha akanipa ishara kwamba nisogee tusaidiane kumshika yule mwanamke, nikafanya hivyo. Ndani ya dakika sifuri tayari tulikuwa tumemshika yule mwanamke, mimi upande wa kulia na Junaitha upande wa kushoto.
“Inabidi tuondoke, fuatisha ninachokifanya,” alisema Junaitha, akapiga mguu wa kushoto chini, na mimi nikafanya hivyo, akapiga tena, na mimi nikapiga mpaka mara tatu kisha akanionesha ishara kwamba tunatakiwa kuanza kuzunguka kutengeneza duara, tukifuata uelekeo wa kinyume na mshale wa saa au kwa Kizungu wanaita Anti-Clockwise, yaani kutoka kulia kwenda kushoto.
Tulipozunguka mara moja tu, ghafla upepo mkali ulianza kuvuma, Junaitha akanionesha ishara kwamba tuendelee kuzunguka kwa kasi zaidi, kufumba na kufumbua kikaibuka kimbunga kikali na kutuzoa, kwa mbali nikawa nasikia sauti ya lile joka likinguruma kwa hasira, sauti zikafifia masikioni mwangu na ikafika mahali nikawa sijitambui tena.
Nilipokuja kuzinduka, nilijikuta nikiwa nimelala kwenye zulia, ndani ya kile chumba tulichokuwa tumekaa mimi, Junaitha, Raya, Shamila na Firyaal. Kama ilivyokuwa mara ya kwanza tulipotoka kumuokoa Shamila, mwili wangu ulikuwa umechoka mno, karibu kila kiungo kikiniuma.
Nilipofumbua macho, nilimuona Junaitha akiwa anasumbuana na yule mwanamke mzee, ilivyoonesha ni kama alikuwa akitaka kujifungua kamba tulizomfunga, akamzabua kibao kwa nguvu na kumtaka atulie.
Nilijikakamua na kusimama, japo kwa taabu, miguu yangu ikiwa inatetemeka kwani sikuwa na nguvu kabisa.
“Hebu njoo tukamfungie huyu mshenzi naona anataka kushindana na mimi,” Junaitha alisema, kijasho chembamba kikimtoka. Kwa kuwa mle ndani kulikuwa na mwanga tofauti na kule kwenye ulimwengu mwingine tulikotoka, niliweza kumtazama vizuri yule mwanamke. Ama kwa hakika alikuwa anatisha.
Ngozi yake ilikuwa imeweka utando mweusi juu yake, kuonesha kwamba ulipita muda mrefu sana bila kuoga au kugusa maji, kucha zake nazo zilikuwa ndefu, zilizojaa uchafu, huku kichwani nako akiwa na nywele ndefu, chafu, zilizonyonyoka na mdomoni alikuwa na meno machafu, yaliyochongoka kama ya mnyama wa porini.
“Mbona unashangaa? Shika tumpeleke ndani,” alisema Junaitha, akawa ni kama amenizindua kutoka kwenye lindi la mawazo ya kutisha. Nilimshika yule mwanamke japo kwa woga, nikamuona akinitazama na kunikazia macho.
“Sura yako siyo ngeni, tumewahi kukutana mahali,” alisema yule mwanamke huku akiendelea kunitazama kwa kunikazia macho. Alipozungumza, harufu mbaya ilimtoka mdomoni na kusababisha hali ya hewa ichafuke, sikumjibu kitu, akawa anaendelea kunitazama.
Sikuwahi kumuona kabla wala sikuwahi kukutana na kiumbe cha mfano wake, nilishangaa ananiambia sura yangu siyo ngeni, nikahisi anataka kunichezea mchezo wa kunirubuni.
“Donda lako la kifuani lilishapona?” aliniuliza swali lingine lililonishtua mno. Ni kweli nilikuwa na kidonda kifuani ambacho kilinitesa kwa kipindi kirefu lakini alijuaje? Nikajikuta nikiwa kwenye mtihani mgumu uliokosa majibu. Nilimtazama Junaitha lakini alifanya kama vile kunipotezea fulani hivi, akijifanya hajasikia kilichozungumzwa na yule mwanamke.
“Hukupaswa kuwepo hapa leo, ulimwengu huu siyo sehemu yako, unatakiwa kuwa sehemu nyingine sasa hivi,” alizidi kusema yule mwanamke wakati tukimkokota kuelekea kwenye chumba cha ndani kabisa ambacho Junaitha hakuwa akiruhusu mtu yeyote kuingia.
“Naongea na wewe, unajifanya hunisikii si ndiyo?” alifoka yule mwanamke baada ya kuona nimemchunia, akawa anatishia kama anataka kuning’ata na meno yake kama mnyama wa porini, Junaitha akamzibua kibao kingine cha uso, akatoa ukelele kuonesha kilikuwa kimemkolea.
“Kanisubiri chumbani kwangu,” alisema Junaitha, akawa amenizuia kijanja kuingia kwenye kile chumba chake cha siri ambacho hakuna aliyekuwa anajua ndani yake kuna nini kwa sababu hakuna aliyewahi kuingia. Hata Shamila mwenyewe, alinidokeza kwamba hakuwahi kuingia hata mara moja.
Alimuingiza yule mwanamke kisha akafunga kwa ndani, nikamsikia yule mwanamke mzee akitoa sauti ya kuugulia, sikujua nini kilichokuwa nikaendelea humo ndani. Nilijivuta na kuelekea chumbani kwa Junaitha kama alivyioniambia.
Kila kitu kilikuwa kikitokea kwa kasi kubwa mno kiasi cha kunifanya nijihisi kama nipo kwenye ndoto za kutisha. Nilirudi mpaka kwenye kile chumba nilichowaacha akina Shamila, bado walikuwa wamelala fofofo kama mizigo, nikarudisha mlango taratibu na kuelekea chumbani kwa Junaitha lakini kabla sijafika, nikiwa napita kwenye chumba alichokuwa amelala Shenaiza, nilimsikia akikohoa.
Harakaharaka nikafungua mlango nikiwa ni kama siamini nilichokisikia, nikamkuta Shenaiza akihangaika kujigeuza, jambo ambalo hakuwa amelifanya kwa kipndi kirefu tangu akiwa kule hospitalini.
“Shenaiza! Shenaiza,” nilisema huku nikipiga magoti pembeni ya kitanda chake. Bado hakuwa amefumbua macho yake.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...