Tuesday, December 19, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 53


ILIPOISHIA:
Tukaanza kuulizana maana ya kile kilichofanyika mpaka tukafanikiwa kumuokoa Shamila ambapo Junaitha alianza kutufundisha mambo ambayo hakuna aliyekuwa akiyajua kati yetu, ambayo kama hujui ungeweza kusema ni uchawi wa hali ya juu.
“Hata ukitaka kuingia benki na kuchukua kiwango chochote cha fedha unachotaka, inawezekana, mbona rahisi tu, nitawafundisha,” alisema.
SASA ENDELEA...
“Mh!” niliguna kama ishara ya kutoamini kile alichokisema, akanigeukia na kuniambia hakuna kitu kisichowezekana chini ya jua. Alianza kutufafanulia jinsi nguvu zisizoonekana kwa macho zilivyo na uwezo wa kufanya chochote na kikatimia.
“Hujawahi kuona mtu anakunja kijiko kwa kukitazama tu au mtu anahamisha glasi ya maji kwa kuitazama tu?” alisema. Nilishawahi kusikia habari hizo lakini sikutaka kabisa kuziamini mpaka nishuhudie mwenyewe.
“Kabla ya yote nataka kujua nini kilichotokea mpaka tukafanikiwa kumuokoa Shamila?” niliuliza, nikamgeukia Shamila ambaye muda wote alikuwa kimya kabisa, akionesha bado kuwa na hofu kubwa ndani ya moyo wake.
“Eti kwani wewe ulihisi nini wakati tumekuja kukuokoa?”

“Yaani hata sielewi kilichotokea, nakumbuka nilikuwa nimewekwa chini ya ulinzi, tena mambo yakiwa yamenikalia kooni kwelikweli kwa sababu jambo la kwanza nilitakiwa kulipa bili za matibabu za wewe na Shenaiza ambazo kimsingi ni kubwa sana kisha baada ya hapo ndiyo taratibu za kisheria zingefuatia.
“Nilishaanza kuwasikia wakisema kwamba kwa jinsi tukio lenyewe lilivyokuwa limenikalia vibaya, ningeenda kufungwa, tena si kifungo cha chini ya miaka saba,” alisema Shamila, akaendelea:
“Nikiwa nimekaa pale ndani ghafla nikaanza kuhisi kama upepo hivi unavuma, mara wale askari waliokuwa wakinilinda wakapitiwa na usingizi mzito na kufumba na kufumbua, nilishangaa nikisombwa na kimbunga kikali na sikuelewa tena kilichoendelea mpaka nilipozinduka na kujikuta humu ndani. Kwani ilikuwaje?” Shamila naye alinigeuzia mimi swali.
“Labda tumuulize mama mdogo,” na mimi nililikwepa swali, wote tukamgeukia Junaitha ambaye alishusha pumzi ndefu kisha akatuambia hawezi kueleza kilichotokea kwa maneno machache tukamuelewa, tunahitaji kukaa darasani na kupata muda wa kutosha kujifunza.
“Ila kwa kifupi kilichotokea ni uthibitisho wa jinsi kila mmoja wetu hapa alivyo na nguvu kubwa ndani yake ambayo iwe anajua au hajui, ina uwezo wa kufanya mambo makubwa sana. Na tukiunganisha nguvu hiyo ndiyo tunaweza kufanya mambo makubwa yakautingisha ulimwengu wote.
“Ukishajua kucheza na nguvu hizi unao uwezo hata wa kwenda kuzimu na kurudi, yaani roho ikatengana na mwili kabisa na kila mmoja akaamini kwamba umekufa kisha baada ya muda ukazinduka tena na kuwa hai,” alisema Junaitha huku akinitazama, nikajua alikuwa akinilenga mimi jambo fulani ingawa sikuwa na uhakika.
“Hayo tutaendelea nayo baadaye lakini niwape onyo, kama kuna yeyote anayeshiriki mapenzi nje ya ndoa aache kwa sababu hiyo ni sumu kubwa sana katika udhibiti wa nguvu za ndani na najua hakuna aliyeoa au kuolewa kati yenu. Tuna kazi ya kumzindua Shenaiza kwa hiyo lazima kila mmoja ajitahidi mwili wake kuwa msafi vinginevyo hakuna kitakachofanyika,” alisema Junaitha.
Akilini mwangu nilielewa kwa nini ameyasema maneno hayo, ndani ya kichwa chake alishahisi kwamba miongoni mwa wale wasichana lazima kuna ambaye natoka naye kimapenzi na kwa sababu tayari nilishamuonjesha asali, alikuwa tayari kuchonga mzinga ila hakutaka mtu mwingine yeyote aendelee kuchangia naye.
Aliposema hivyo niliwaona wote watatu, Shamila, Raya na Firyaal wakinitazama kwa macho ya chinichini kama wanaosema ‘potelea mbali’. Alituchukua wote na kutupeleka kwenye chumba alichokuwa amelala Shenaiza akiwa hana fahamu.
“Roho yake imekwenda mbali kabisa na mwili, tunatakiwa kuivuta mpaka irudi mahali pake na hilo likifanyika tu, atazinduka. Tutakuwa na kazi kubwa kwa sababu licha ya kuwa roho yake imekwenda mbali, pia nguvu za ubongo wake zimevurugwa na madawa makali aliyokuwa anachomwa kule hospitalini, haitakuwa kazi nyepesi,” alisema Junaitha kwa msisitizo.
Wote tukawa kimya kabisa tukisubiri maelekezo yake, akatuambia kwamba itabidi wenye nguvu kati yetu ndiyo watoke kuifuata roho yake mahali ilipo na wale wengine wajazie nguvu zao kwetu.
“Narudia tena, haitakuwa kazi nyepesi na pengine tutachoka kuliko hata ilivyokuwa mwanzo,” alisema, sote tukashusha pumzi ndefu na kuendelea kumsikiliza. Akatuambia kabla ya yote, kila mmoja anatakiwa kwenda kuoga kwa maji mengi na kuhakikisha amevaa nguo safi, akatuambia kama hatukuwa na nguo safi tusijali atatupa mavazi maalum ambayo huwa anayatumia kwenye shughuli kama hizo.
“Shughuli kama hizi? Zipi?”
“Za kusaidia watu wenye matatizo kama wewe,” alijibu Junaitha huku akinitazama kwa macho ambayo yalimaanisha yupo kikazi zaidi. Kwa kututazama, usingeweza kuamini kwamba ndiyo sisi ambao muda mfupi uliopita tulikuwa tukisakata kabumbu kwenye uwanja wa fundi seremala. Tofauti na wanawake wengine, Junaitha alionesha kuwa na uwezo mkubwa wa kuzimudu vyema hisia zake.
Hakukuwa na muda wa kupoteza, harakaharaka tulienda kuoga, kwa kuwa karibu kila chumba kilikuwa na bafu la ndani, muda mfupi tu baadaye tayari wote tulikuwa tumeshaoga, ingawa ilibidi mimi nijitenge peke yangu ili kuzuia mtafaruku unaoweza kutokea.
Muda mfupi baadaye wote tulikuwa tumevalia mavazi maalum kama yale yanayotumika kwenye hoteli kubwakubwa kwa ajili ya kulalia, yote yakiwa na rangi nyeupe.
“Hamuoni mmependeza?” alisema Junaitha, wote tukacheka, tukarudi kwenye chumba alichokuwa amelala Shenaiza. Ilibidi tusaidiane kumshusha kutoka pale kitandani mpaka chini kwenye jamvi, kisha na sisi tukakaa mkao maalum wa kukunja miguu na kutengeneza duara kumzunguka Shenaiza ambaye hakuwa akielewa chochote.
“Tunafanya kama tulivyofanya wakati wa kumuokoa Shamila,” alisema Junaitha, kwa sababu wote tulikuwa tunakumbuka tulichokifanya, tulishikana mikono na kufumba macho, kila mmoja akaanza kuvuta hewa kwa utaratibu maalum na kuiachia, haikuchukua muda eneo lote likatawaliwa na utulivu wa hali ya juu.
Ile hali ilianza tena kunirudia kama mwanzo, nikaanza kuhisi kama napaa huku nikishuhudia jinsi mwili wangu usioonekana ulivyokuwa ukiachana na huu unaoonekana. Tofauti na mwanzo ambapo nilikuwa nahisi hofu kubwa ndani ya moyo wangu, safari hii nilikuwa najisikia ku-relax sana.
Kuna muda nilitamani hata maisha yangu ya kila siku niwe kwenye ulimwengu huo mwingine. Hata hivyo, hali niliyokuwa naisikia ilikuwa ya muda, ghafla nikaanza kuhisi mtikisiko mkubwa, ukasikika mlio mkali wa radi na mandhari yakabadilika hapohapo.
Kelele za vyuma vingi vilivyokuwa vikigongana, pamoja na muungurumo wa kutisha sambamba na moshi mwingi mweusi unaopalia kooni vikanizingira kila upande.
“Mbona kama nimewahi kufika kwenye haya mazingira?” niliwaza lakini cha ajabu nikasikia sauti ya kile nilichokuwa nakiwaza ikijirudia kama mwangwi mkali, nikajua kazi imeanza.
Nilipogeuka huku na kule, nilijikuta nimekaa kwenye kiti cha chuma kilichokuwa na kutu nyingi, nikageuka tena na kutazama huku na kule, nikagundua kwamba nipo kwenye lile treni ambalo siku ile nilipojeruhiwa na kupoteza fahamu kisha kuhamia kwenye ulimwengu mwingine, nililipanda.
Kwa mbali niliwaona watu kadhaa wakiwa wamevaa nguo zilizokuwa zikifanana na zile nilizovaa, lakini kila mmoja akiwa ameinamisha kichwa kuonesha kwamba yupo usingizini. Kasi ya treni ilizidi kuongezeka na kadiri tulivyokuwa tunasonga mbele, milio ya ajabu ilianza kusikika kwa mbali, ukichanganya na muungurumo wa treni lile la ajabu, na giza totyoro lililokuwepo, hali ilikuwa ya kutisha mno.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

2 comments:

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...