Wednesday, October 25, 2017

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 48


ILIPOISHIA:
Nilichopanga kichwani, ni kuchukua maelekezo vizuri kwa yule mtu aliyesema marehemu ni jirani yake kisha kwenda kwanza mpaka eneo la ajali na baada ya hapo, nitakwenda Tumbi kujionea hali ya mgonjwa na hiyo maiti kama nitapata nafasi. Nilikuwa na shauku kubwa ya kujua kila kitu maana moyo wangu ulikuwa na hatia kubwa, hasa kutokana na jinsi taarifa za ajali ile zilivyowaumiza mioyo abiria wengi.
SASA ENDELEA...
Safari iliendelea na hatimaye tukawasili Kibaha, gari liliposimama tu, nilimuwahi yule abiria aliyekuwa akisimulia kuhusu ile ajali, nikamsalimu na kumuomba anielekeze ulipo msiba kwa sababu aliyefariki ni ndugu yangu.
“Ni Mlandizi, ukishuka tu pale kituoni, uliza mtu yeyote eti kwenye msiba wa mtoto aliyekufa kwenye ajali ni wapi? Huwezi kupoteza, mtoto alikuwa anafahamika sana yule kutokana na jinsi alivyokuwa na heshima,” alisema yule abiria, nikamshukuru.
Nilipoachana naye, nilimfuata dereva ili anielekeze sehemu gari lilipopata ajali kwani kuna muda nilimsikia akisema kwamba eneo hilo ni baya sana, ajali huwa zinatokea mara kwa mara. Eneo lenyewe nilikuwa nalifahamu lakini sikujua naweza kufikaje.

“Siyo mbali sana kutoka hapa, hata kwa miguu unaweza kufika, panaitwa machinjioni,” alisema yule dereva, nikamshukuru na kuanza kutembea kuelekea eneo la tukio. Tayari kulishaanza kupambazuka na lile giza la afajiri lilianza kupungua na kumezwa na nuru ya alfajiri.
Kila nilipokuwa napita, wafanyabiashara na wasafiri walikuwa wakizungumzia ajali iliyotokea usiku wa siku hiyo. Kila mtu alikuwa akizungumza lake lakini kama baba alivyoniambia usiku, eneo hilo huwa linatumiwa sana na wachawi, hasa waliopo mafunzoni kama mimi kusababisha ajali.
Kila mtu alikuwa anashauri eneo hilo watafutwe waganga waliobobea au wachungaji wakaliombee kwani kulikuwa na nguvu za giza au ‘nyoka chunusi’ anayesababisha ajali. Njiani sikuwa peke yangu, baadhi ya watu nao waliposikia kuhusu ajali hiyo, walitaka kwenda kujionea wenyewe.
Niliongozana na vijana kadhaa, tukawa tunatembea pembeni ya barabara na dakika kadhaa baadaye, tulifika eneo ajali hiyo ilipotokea. Nilipofika eneo hilo, nilishangaa nywele zikianza kusisimka kuliko kawaida huku harufu ya damu ikitawala kwenye pua zangu. Gari lililopata ajali bado lilikuwa eneo la tukio, pembeni ya barabara, yaani kwa jinsi lilivyokuwa limeharibika, kila mmoja alibaki kushika kichwa.
Mjadala uliotawala kwa wote waliokuwa wamefika kushuhudia ajali hiyo, ulikuwa ni nini kilichosababisha ajali hiyo. Kwa sababu kulishapambazuka, niliweza kuliona vizuri eneo hilo, lilikuwa ni tambarare kabisa, hakukuwa na kona wala mteremko, achilia mbali mlima wa kuweza kusababisha ajali mbaya kiasi kile.
Nilitazama kule tulikokuwa tumekaa na baba na baba yake Rahma, ambako baada ya kuuchukua ule mwili wa yule mtoto niliupeleka, nikashangaa kuona kwamba eneo lote lilikuwa jeupe kabisa kiasi kwamba ungeweza kuona umbali wa karibu mita mia tano.
Hakukuwa na miti wala vichaka, eneo lote lilikuwa jeupe kabisa. Nikawa najiuliza pale kwenye migomba tulipokuwa tumekaa ni wapi? Ule mgomba uliokatwa kisha nikapewa ulitoka wapi? Nikahisi labda nimechanganya upande, nikageukia upande wa pili wa barabara, nako kulikuwa kweupe kabisa, nikawa ni kama nimechanganyikiwa.
“Vipi kijana, mbona unaonesha kutotulia? Unatafuta nini?” niligeuka baada ya kusikia sauti hiyo, nikamtazama aliyekuwa akinisemesha. Alikuwa ni mzee mmoja mwenye ndevu nyingi zilizofunika mdomo wote. Mkononi alikuwa na mkongojo na kwa jinsi alivyokuwa amevaa, ilionesha haishi mbali na eneo hilo.
“Aah! Hamna kitu, nashangaa tu jinsi hii ajali ilivyotokea.”
“Mh! Hebu nitazame usoni,” alisema, nikamtazama na yeye akanitazama. Kitendo cha kutazama naye tu, nilihisi ile hirizi niliyoivaa mkononi ikinibana. Maelezo aliyonipa baba, ni kwamba nikiona inanibana ghafla, lazima kutakuwa na mtu eneo hilohilo mwenye nguvu za giza anajaribu kunipima.
Akaniambia nikishaona hali hiyo, haraka sana nizibe kucha ya mkono wa kushoto kwa kutumia kidole gumba cha mkono huohuo, jambo ambalo nililifanya bila yule mzee kunishtukia. Nikashangaa ameanza kupiga chafya mfululizo, tena kwa nguvu. Alipiga chafya kama kumi hivi, kamasi na machozi vikawa vinamtoka kwa wingi, mpaka watu wengine waliokuwa eneo hili wakawa wanamshangaa.
“Mtoto mbaya sana wewe, mtazame bichwa lake,” alisema mzee huyo kwa hasira, akawa anaondoka huku akiendelea kunitukana na kupiga chafya.
“Hivi vizee ndiyo vichawi vyenyewe, unakiona kile kibabu kilivyokuwa kinapiga chafya, inaonesha kimenogewa na harufu ya damu,” alisema mmoja kati ya watu waliokuwa eneo lile, wengine wakacheka huku wengine wakiendelea kusikitika.
“Mbona yule mzee anakutukana, kwani umemfanya nini?”
“Mzee gani?”
“Yule aliyekuwa anapiga chafya?” mwanamke mmoja wa makamo aliniuliza, kumbe alikuwa ameshuhudia kila kitu, nikaamua kuvunga maana kuendelea kuzungumza kungefanya watu waanze kunitazama kwa makini, jambo ambalo sikuwa tayari kuona likitokea.
“Mh! Labda umeangalia vibaya, mbona mimi simfahamu na wala sijaongea naye chochote?” nilijibu huku nikigeuka na kumpa mgongo yule mwanamke, nikaona bado ananifuata kwa manenomaneno.
“Itakuwa kuna jambo baya umemfanyia, haiwezekani mzee kama yule aanze tu kukutukana, nataka uniambie, unajua yule ni nani kwangu,” alisema mwanamke huyo huku akizidi kunisogelea mwilini. Kitendo cha kunisogelea tu, nilishtukia ile hirizi ikianza tena kunibana, safari hii kwa nguvu kuliko mwanzo.
Ikabidi nikae chonjo kwa sababu ubanaji wake ulikuwa wa nguvu na baba alishaniambia kwamba ukiona inabana kwa nguvu, ujue upo jirani na mtu mwenye nguvu kubwa ambaye usipokuwa makini anaweza kukudhalilisha mbele za watu.
Haraka niliibana kucha ya kidole kidogo kwa kidole gumba changu na safari hii, nilitumia mikono yote miwili. Kwa mtu asiyejua, angeweza kudhani labda nachezea tu vidole vya mikono yangu kumbe nilikuwa na shughuli nyingine kabisa.
Kitendo hicho kilisababisha mwanamke yule awe ni kama amepandwa na mashetani, akaanza kukimbia huku na kule huku akiongea maneno yasiyoeleweka, akawa anasema kwamba eti pale eneo la tukio pamejaa wachawi na yeye ni miongoni mwa hao wachawi.
Kila mtu alibaki kumshangaa, ikabidi niachie vidole haraka maana kwa jinsi alivyokuwa akiongeaongea huku mara kwa mara akinigeukia na kunitazama kwa macho ya woga, angeweza kunisababishia kizaazaa.
Nilipoachia tu vidole vyangu, alidondoka chini na kuzimia, wanawake wengine wawili ambao inaonesha ni kama alikuja nao, wakawa wanampepea huku wakinitazama kwa macho mabaya. Kwa hali ilivyokuwa, ilibidi tu nianze kuangalia utaratibu wa kuondoka eneo hilo maana hali ilishaanza kuwa tete na sikutaka akizinduka anikute bado nipo eneo hilo.
Nilizugazuga kisha nikajichanganya na watu waliokuwa wakielekea kule upande wa stendi, tayari kulishapambazuka na kijua cha asubuhi kilishachomoza. Kilichonishangaza, ni kugundua kwamba licha ya ajali yenyewe kutokea katika mazingira ya kishirikina, bado kulikuwa na wachawi miongoni mwa watu waliokuwa wakishuhudia kilichotokea.
Nilipanga niende kwanza msibani kisha nikiwa narudi ndiyo nipitie kule Hospitali ya Tumbi kwenda kumwangalia majeruhi wa ajali ile na kama ikiwezekana nikaione na maiti ya huyo mtoto maana ukweli ni kwamba mimi ndiye niliyemchukua kutoka eneo la tukio na sehemu yake nikaweka kipande cha mgomba.
Nilikuwa na shauku kubwa sana ya kutaka kujua mambo mengi ambayo kwangu yalikuwa mageni kabisa. Nilipofika stendi, sikuwa na muda wa kupoteza, nilipanda kwenye gari linaloenda Mlandizi ambalo nalo ilikuwa ni lazima lipite pale eneo la ajali.
Safari ilianza, tulipokaribia eneo hilo, nilitoa kichwa nje ili nichungulie tena, nikamuona yule mwanamke aliyekuwa akinichokoza akiwa amekaa kitako chini kuonesha kwamba fahamu zimemrudia, ndugu zake wakawa wanajaribu kumuinua. Nilijikuta nikitabasamu huku moyoni nikijisikia fahari kubwa kuwashikisha adabu waliokuwa wakitaka kunichokoza.
Baada ya muda, gari liliwasili Mlandizi, hiyo ndiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza kukanyaga ardhi ya eneo hilo. Niliposhuka, niliwauliza wenyeji mahali kulikokuwa na msiba ambapo bila hiyana walinionesha. Tayari watu wengi walikuwa wamekusanyika nje ya nyumba moja nzuri na ya kisasa, huku wengine wakihangaika kuweka maturubai.
Nilipofika, na mimi nilijifanya ni mwombolezaji wa kawaida tu, nikawasalimia baadhi ya watu kisha nikajichanganya na waombolezaji wengine. Ghafla nilishtuka baada ya kuona kitu ambacho sikukitarajia, nikahisi kijasho chembamba kikianza kunitoka, mara hirizi yangu ikaanza kunibana kwa nguvu, kufumba na kufumbua kamba yake ikakatika, ikadondoka chini!
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...