Thursday, September 7, 2017

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 38


ILIPOISHIA:
“Wewe sasa hivi una mambo ya kikubwa, hutakiwi kuwa unachanganyikana na wenzako, inabidi uanze kukaa na sisi baba zako, vuta kiti kaa hapa,” alisema baba, akawa ametibua shoo nzima, nilitaka kutoa visingizio lakini hakutaka kusikia chochote kutoka kwangu, ikabidi nikae na kujiinamia, wote wakawa wananitazama.
SASA ENDELEA...
“Una matatizo gani?” baba aliniuliza baada ya kuniona nikiwa nimekaa huku uso wangu nikiwa nimeukunja.
“Unajua hata sisi wote unaotuona hapa, kuna kipindi tulikuwa kama wewe, sote tulikuwa vijana hapa na tulipitia yote unayoyapitia, kwa hiyo usitake kujifanya mjanja, umenisikia?” baba alisema kwa msisitizo.
“Na nyie mlipitia mauzauza kama yangu? Kwa nini kila siku huniambii ukweli mimi ni nani?” kwa mara ya kwanza nilimpandishia baba sauti mbele ya baba yake Rahma, nikaona wameacha kucheza karata, wakawa wanatazamana kisha wote wakanigeukia.
“Sisi ni baba zako, hutakiwi kuzungumza kwa namna hiyo, umesikia mwanangu,” alisema baba yake Rahma huku akinipigapiga begani. Tofauti kati ya baba na baba yake Rahma, yeye alikuwa na busara na mpole lakini baba yeye alizoea kufokafoka tu.
“Hapana mimi nimechoka, kila siku nikimuuliza baba aniambie ukweli hataki, mauzauza yanazidi kunitokea kila siku, mambo ya ajabu yananikumba mimi tu, mbona ndugu zangu hakuna anayepata shida kama mimi,” nilisema kwa uchungu huku machozi yakianza kunilengalenga.

Baada ya kusema ya moyoni, niliegamia meza na kujilaza huku machozi yakinitoka, kiukweli nilikuwa na dukuduku kubwa sana moyoni. Hakuna kitu ambacho kilikuwa kikinikasirisha kama kitendo cha baba kuwa ‘ananikontroo’ kama roboti bila kunieleza ukweli uliokuwa nyuma ya maisha yangu.
“Najua kwamba mimi ni mwanaye, tena anayenipenda kuliko watoto wengine wote lakini kwa nini nipo tofauti? Kwa nini haniambii ukweli?” nilisema kwa kulalama, machozi yakiwa yanaendelea kunitoka.
“Kama anaweza kufikiria haya maana yake ni kwamba ameshapevuka kiakili, nafikiri ni muda muafaka wa yeye kuujua ukweli.”
“Hapana, bado hajakua huyu, ana mambo ya kitoto sana, mimi ndiyo namjua,” baba alisema, kauli ambayo ilinifanya niinuke pale mezani na kumkodolea baba macho. Yaani kumbe alikuwa anashindwa kunieleza ukweli kwa kipindi chote hicho kwa sababu tu alikuwa anahisi kwamba mimi bado nina akili za kitoto?
Kauli ile ilinifanya nijiulize maswali mengi yaliyokosa majibu. Kwa nini baba alikuwa ananiona mimi kama bado mtoto wakati tayari nilishapevuka na kuwa mwanaume kamili? Hata Rahma aliniambia kwamba mimi ni kidume cha mbegu, achilia mbali Isri aliyekuwa akinisifia sana. Na kama ni hivyo, mbona pale aliponiita alisema nimeshakua mkubwa kwa hiyo natakiwa kukaa nao?
“Kwa nini unaniona bado mdogo?”
“Kwa sababu huwezi kuelewa kitu kwa kuelezwa mara moja. Kila unachokatazwa kufanya wewe unafanya,” alisema baba na kurudia kauli yake kwamba hawezi kuniamini kwa asilimia mia moja mpaka nitakapomuonesha ukomavu wangu wa akili.
Kiukweli kwa kipengele hicho baba alikuwa amenishinda kwa pointi na udhaifu wangu mkubwa nilikuwa nimeuonesha kwenye suala zima la mapenzi. Nakumbuka tulianza kutofautiana na baba baada ya kukutana na Isri kwenye basi, akawa ananikataza kuwa naye karibu lakini nikampuuza.
Pia hata tulipofika kwa akina Rahma, mara kadhaa alishagundua kwamba tulikuwa na ukaribu usiofaa na akanikataza kwa msisitizo kwamba nisijaribu kukutana kimwili na Rahma, tena mpaka wakatumia kigezo kwamba sisi tulikuwa ndugu lakini bado tuliangukia dhambini, tena siyo mara moja.
Kubwa zaidi, hata hapo tulipokuwa tukizungumza, licha ya baba kunikataza kwamba endapo nitakutana kimwili tena na Rahma basi atakufa, kama wasingeniita na kunizuia, pengine muda huo ningekuwa ‘nikilitafunilia mbali tunda la mti uliokatazwa’ na Rahma.
Kama kigezo hicho pekee ndicho kilikuwa kinaonesha kwamba mtu amekuwa mkubwa, basi ni kweli nilikuwa nimefeli mtihani uliokuwa mbele yangu, nikawa mdogo kama ‘piriton’.
“Eti ni kweli anachokisema baba yako?” aliniuliza baba yake Rahma, nikakosa cha kujibu.
“Unajua kwa jinsi sisi baba zako tulivyo, na pengine wewe ukija kupata nafasi hiyo, hakuna kitu ambacho kinaheshimika kwenye jamii yetu kama utii. Ukiambiwa jambo ni lazima ufanye vilevile ulivyoambiwa na si vinginevyo, kosa dogo tu linaweza kusababisha matatizo makubwa mno ndiyo maana baba yako anakuwa mkali,” alisema baba yake Rahma.
Kauli hiyo ilinifanya nijiulize maswali mengine mengi zaidi. Aliposema ‘jamii yetu’, baba yake Rahma alikuwa akimaanisha nini? Nilianza kupata picha kwamba huenda naye alikuwa anafahamu kila kitu kinachoendelea na kama alikuwa jamii moja na baba, basi moja kwa moja na yeye alikuwa akishughulika na mambo kama yale ya baba.
Tangu tumefika, baba yake Rahma hakuwahi kutoka kwamba labda anaenda kazini au kwenye biashara zake, muda wote alikuwa nyumbani tu lakini alikuwa na maisha ya hali ya juu sana. Nikiwa bado naendelea kujiuliza maswali mengi, baba yake Rahma alinisogelea.
“Baba yako anasema hakuamini kwa sababu bado una akili za kitoto lakini mimi nikikutazama nakiona kitu kikubwa sana ndani yako, tucheze dili?” aliniuliza kwa sauti ya chini huku akinikonyeza kwa jicho moja. Sikujua ni dili gani ila kwa sababu nilikuwa nataka kujua ukweli wa maisha yangu, nilitingisha kichwa kuonesha kumkubalia.
“Inatakiwa mimi na wewe tukazungumze lakini hatuwezi kuzungumzia humu ndani, inabidi tutoke nje! Lakini hapohapo, baba yako ameniambia kwamba kuna ‘madhambi’ mengine umeyafanya kiasi kwamba wewe na yeye hamuwezi kutoka mpaka giza liingie, ni kweli au si kweli?”
“Ni kweli.”
“Sasa mtihani wa kwanza, unatakiwa ukazivunje hizo nguvu zako za giza ulizozitega pale mlangoni.”
“Mimi sina nguvu zozote za giza wala sijatega chochote...” nilimkatisha lakini alinitazama usoni na kunikumbusha kwamba utii ni jambo muhimu sana, nikaufyata mkia.
“Unauona ule mlango, inatakiwa utembee kinyumenyume mpaka pale, ukiukaribia, unaugeukia lakini unatakiwa kufumba macho, kisha unakojoa mkojo wa kutosha kulowanisha eneo lote la mlango,” alisema baba yake Rahma, macho yakanitoka kama mjusi aliyebanwa na mlango.
“Hakuna kitu kinachoweza kuvunja na kumaliza kabisa nguvu za giza kama mkojo, haya fanya kama nilivyokwambia,” alisema baba yake Rahma. Ama kweli huo ulikuwa mtego mkali sana kwangu, yaani nikakojoe mlangoni, tena mahali ambapo watu wote waliokuwa sebuleni wangeweza kuniona?
Sikujua ndugu zangu watakichukuliaje kitendo hicho, wala sikujua Rahma na wadogo zake nao watanichukuliaje ila kwa sababu nilikuwa na shauku ya kuujua ukweli, nilipiga moyo konde.
Wakati nikijiandaa kwenda, nilimsikia Rahma akiimba huku akitoka koridoni na kwenda kule sebuleni, nadhani alishachoka kusubiri na kuamua kunifuata, mtihani ukazidi kuwa mgumu. Ningemjibu nini Rahma endapo angeniuliza kwa nini nakojoa mlangoni wakati choo kipo, tena siyo kwamba nimelewa au naumwa, nina akili zangu timamu kabisa!
Baba na baba yake Rahma walikuwa wametulia wananitazama huku nikimuona baba uso wake ukionesha ishara kama anayesema ‘hawezi huyu, akili zake bado za kitoto’. Niliamua kujilipua, nikasema liwalo na liwe, nilisogea usawa wa mlango, nikageuka na kuupa mgongo, nikaanza kutembea kinyumenyume kuuelekea kisha nikafumba macho, nilipoukaribia, niligeuka, macho nikiwa nimeyafumba.
Nilifungua zipu kisha nikaanza kufanya kama vile nilivyoelekezwa. Nikiwa naendelea na kitendo kile cha aibu na cha aina yake, nilisikia watu wote waliokuwa sebuleni wakishtuka, nadhani waliniona nilichokuwa nakifanya, sikuwajali, nikaendelea kuumwaga, mara kilisikika kishindo kikubwa ambacho kilinifanya nishindwe kuendelea kufumba macho, nikayafumbua.
“Mungu wangu!” nilisema kwa sauti ya juu.

Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...