Monday, September 25, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 40


ILIPOISHIA:
“Nimekikuta kwenye kitanda cha Shenaiza, na anaonekana kama hana fahamu, rangi ya ngozi yake imebadilika na kuwa ya kijivu,” nilimwambia, akashusha pumzi ndefu na kunitazama usoni.
SASA ENDELEA...
“Benzodiazepam,” Shamila alisema kwa sauti ya juu, akitamka maneno yaliyokuwa yameandikwa kwenye kile kichupa nilichokikuta pembeni ya kitanda cha Shenaiza.
“Kwani ni dawa gani?”
“Mungu wangu! Wameamua kummalizia kabisa mdada wa watu. Hii ni dawa ya usingizi ambayo hairuhusiwi kutumika bila uangalizi wa kutosha wa daktari. Mtu anapotumia dozi kubwa, husababisha muda wote awe analala tu na kama hali hii ikiendelea kwa muda, husababisha mgonjwa kupoteza kumbukumbu na kuwa kama mtu aliyechanganyikiwa.”
“Haa! Na siyo kwamba dawa hii hutumika kuwatibu wagonjwa wa akili?”
“Hapana Jamal, hii hutumika tu kuwatuliza watu wenye msongo mkali wa mawazo au stress kiasi kwamba wanakosa usingizi. Wakitumia dawa hii chini ya uangalizi wa daktari, huwasaidia kupata usingizi na kuwapunguzia msongo mkali au ‘stress’, lakini narudia tena, ni lazima itumiwe chini ya uangalizi mkali wa daktari.”
“Sasa kwa nini wanampa Shenaiza?”
“Jibu ni moja tu, wanataka watu wote waamini kwamba kweli amechanganyikiwa. Kama kwa siku chache tu alizokaa hapa hospitalini kichupa kimeshaisha, maana yake ni kwamba anapewa dozi kubwa sana ambayo ndani ya muda mfupi tu, itamfanya apoteze kumbukumbu na kuwa mwendawazimu.”

“Shamilaa! Cant we help her?” (Shamilaa! Hatuwezi kumsaidia?)
“Its none of our business Jamal.” (Hilo halituhusu Jamal)
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Nikukumbushe tu kwamba mambo yote hayo yanafanywa kwa maagizo ya baba yake mzazi. Unataka kusema wewe una uchungu na Shenaiza kuliko baba yake?” alisema Shamila na kunifanya nikose cha kujibu, nikajiinamia huku nikijisikia uchungu mkali sana ndani ya moyo wangu.
Ni hapo ndipo nilipoanza kuelewa kwa nini Shenaiza alikuwa akihitaji sana msaada kutoka kwangu. Ni hapo pia ndipo nilipoelewa kwa nini alikuwa anashindwa kunieleza moja kwa moja ni msaada gani aliokuwa anauhitaji na alikuwa akisumbuliwa na tatizo gani. Nilishusha pumzi ndefu na kukaa vizuri pale kitandani.
“Utakapojaribu kutoka tena wodini na kwenda unakokujua mwenyewe, kitakachokupata mimi sitahusika maana naona hunielewi,” alisema Shamila huku akionesha kukasirishwa na kitendo changu cha kutoka wodini bila ruhusa yake, wakati nikijua kwamba nilikuwa nikisakwa na watu wenye nia ovu.
“Nisamehe Shamila, lakini muda mwingine nakuwa sina namna zaidi ya kuvunja sheria zako,” nilisema kwa upole, akanisogelea, tukawa tunatazama, nikambusu kwenye paji lake la uso.
“Kwa nini unaonekana kuguswa sana na matatizo ya Shenaiza?” Shamila aliniuliza huku akikaa vizuri, nikashusha tena pumzi ndefu nikitafakari nianzie wapi kumueleza. Kwa jinsi hali ilivyokuwa, kumsaidia Shenaiza peke yangu lilionekana kuwa suala gumu, ilikuwa ni lazima nimueleze Shenaiza ukweli ili kwa pamoja tujue namna ya kumsaidia.
Ilibidi nianze kumsimulia Shamila kila kitu kuhusu mimi na Shenaiza. Nilimueleza kilichotokea kuanzia siku ya kwanza msichana huyo alipopiga simu yangu na baadaye kuniambia kwamba alikuwa amekosea namba. Nilimueleza alivyoendelea kunisumbua akidai kwamba hata kama amekosea namba, anaamini mimi naweza kumsaidia kumtoa kwenye matatizo makubwa yaliyokuwa yanamkabili.
“Nilimueleza Shamila jinsi nilivyoendelea kuwasiliana na msichana huyo, jinsi tulivyoenda kukutana na kumkuta akiwa na hali mbaya hospitalini baada ya kuvamiwa na kujeruhiwa vibaya. Sikumficha kitu, niliendelea kumueleza jinsi alivyonishawishi nimtoroshe hospitali na yote yaliyotokea baada ya hapo.
Shamila alikuwa kimya kabisa akinisikiliza, kadiri nilivyokuwa naendelea kumsimulia kuhusu sakata hilo la Shenaiza, taratibu nilianza kumuona na yeye akiguswa, nilimfafanulia kila kitu isipokuwa kilichotokea baada ya mimi kushambuliwa na kunusurika kufa, na kujikuta nikizinduka nikiwa kwenye ulimwengu mwingine.
Nilimficha kuhusu kipengele hicho kwa sababu maalum kwani nilijua hata nimueleze kwa lugha gani, hawezi kunielewa, sanasana atahisi labda na mimi nimeanza kuchanganyikiwa.
Nashukuru Mungu kwamba maelezo yangu kuhusu Shenaiza yalimuingia sana moyoni mwake, naye akaguswa kama nilivyokuwa nimeguswa mimi lakini kabla ya yote akanitahadharisha.
“Mara kwa mara nimemsikia Raya akilalamika kwamba wewe una uhusiano wa kimapenzi na  Shenaiza,” alisema Shamila, kauli ambayo ilinishtua sana. Nikajua kwamba kumbe hata kabla sijaanzisha uhusiano naye wa siri, Shamila alikuwa akinifuatilia kwa karibu sana na tayari alikuwa anajua mambo yangu kadhaa.
Akaendelea: “Sasa isije kuwa mi nakusaidia kumuokoa Shamila kumbe nakurahisishia mpango wako wa kumuokoa mpenzi wako, nikija kujua kwamba ni kweli mna uhusiano naye wa kimapenzi nitafanya jambo hilo ambalo hutakuja kulisahau maishani mwako.”
“Siyo hivyo Shamila, wala sina uhusiano naye wa kimapenzi, ni kama nilivyokueleza na hakuna chochote zaidi ya hayo niliyokwambia.
“Ndiyo nimeshakwambia hivyo, kwa jinsi ninavyokupenda sitaki kuona mtu mwingine akikusogelea, hata huyo Raya naandaa mpango wa kumtoa kwenye maisha yako, nataka nibaki peke yangu, wewe ndiyo mume wangu mtarajiwa,” alisema Shamila na kunibusu na lipsi zake laini, mkondo wa raha za kipekee ukapita kwa kasi kwenye mishipa yangu ya damu, nikajikuta nikisisimka mno hasa nilipokumbuka asali aliyonilambisha.
“Nakuhakikishia, suala kama hilo haliwezi kutokea,” nilisema kwa kumnong’oneza sikioni, akaruka kidogo kwa msisimko na kunibusu tena, akaniambia kwamba ananipenda sana na anaamini mimi ndiyo baba mtarajiwa wa wanaye.
“Kwa hiyo utanisaidia kuhusu suala la Shenaiza,” nilimchombeza, akanihakikishia kwamba yupo tayari kunisaidia kwa chochote ambacho nakihitaji, hata kama kitayagharimu maisha yake.
Nilifurahishwa mno na majibu yake kwani kiukweli, naomba Mungu anisamehe! Hilo ndiyo lilikuwa lengo langu kubwa la kuanzisha naye uhusiano wa kimapenzi, nilitaka nimtumie kukamilisha baadhi ya mambo yangu!
Siyo jambo zuri hata kidogo kucheza na hisia za mtu anayekupenda, nawashauri watu wenye tabia hii waache mara moja kwa sababu mapenzi huwa hayajaribiwi, kama ambavyo ilitokea kwangu na Shamila, Raya na Shenaiza. Nitafafanua kwa kina baadaye jinsi ujanja wangu wa kucheza na hisia za wote watatu kwa wakati mmoja zilivyonigharimu.
Tulichokubaliana na Shamila ilikuwa ni kufanya kila kinachowezekana kwanza kumjua daktari aliyekuwa akisimamia matibabu yake, na ikiwezekana kumbadilishia dawa bila mwenyewe kujua, kwamba badala ya kuendelea kumpa sumu Shenaiza, ampe dawa zitakazomsaidia mwili wake kurudiwa na nguvu zake upya na akipata nafuu tu, tufanye utaratibu wa kumtorosha.
Tulijadiliana pia kwa kina juu ya nini cha kufanya baada ya kugundua mchezo haramu uliokuwa ukifanywa na baba yake Shenaiza kwa kutumia Shirika la Black Heart, wa kuwasafirisha watu na kwenda kuwauza kisha kuwaua na kuwatoa viungo muhimu miilini mwao, kwa kivuli cha kujifanya wanaenda kuwasomesha, kuwapatia matibabu au kuwatafutia kazi.
Kutokana na upana wa mtandao wa baba yake Shenaiza, Shamila alinishauri kwamba kwa sababu tayari nilikuwa nimeshapata pa kuanzia, niendelee kukusanya taarifa kimyakimya kisha nikishapata nafuu na kuruhusiwa kutoka hospitalini, ndiyo tukae tena na kuamua nini cha kufanya kuhakikisha tunamuangusha baba yake Shenaiza na kuokoa maisha ya watu wengi waliokuwa wakienda kutolewa kafara bila wenyewe kujua chochote.
“Lakini sitakiwi kuendelea kukaa hapa hospitalini zaidi, wanaweza kuja hata huku na kunichukua kiulaini, wakaenda kuniua au kunifanya chochote wanachotaka ili kuniziba mdomo,” nilimwambia Shamila, akaniondoa wasiwasi kwamba naye analijua hilo lakini hatutakiwi kufanya mambo kwa kukurupuka. Akanihakikishia kwamba kila kitu kitaenda vizuri, nimuachie yeye.
Wakati tukiendelea kuzungumza, Raya alifungua mlango na kuingia akiwa na kikapu cha chakula, mazungumzo yakakatika ghafla, Shamila akajifanya yuko bize kwenye meza ya dawa, akipangapanga vitu.
“Habari za saizi nesi,” Raya alimsalimia Shamila kwa unyenyekevu, jambo ambalo hakuwahi kulifanya kabla. Shamila naye akajibu kwa uchangamfu, nikabaki njia panda. Sikujua walizungumza nini muda ule mpaka wakamaliza tofauti zao. Raya akaja mpaka pale kitandani na kunibusu mdomoni, Shamila akageuka na kulishuhudia tukio hilo.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...