Friday, September 22, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 39


ILIPOISHIA:
Akaendelea kuniambia kwamba Shenaiza alikuwa akifahamu kinachofanywa na baba yake na kwa sababu ilifika hatua akawa amechoshwa na ukatili huo, alimtishia baba yake kuwa atatoa siri, jambo lililosababisha ateswe sana, ikawa mtu yeyote akionekana kuwa karibu naye, baba yake anahisi anaweza kupewa siri hiyo hivyo anauawa haraka kabla hajafumbua mdomo wake.
“Kumbe ndiyo maana na mimi wananiwinda kutaka kuniua?” nilijikuta nikisema kwa sauti kubwa.
SASA ENDELEA...
“Na bado wataendelea kukuwinda mpaka watakapoyakatisha maisha yako, unapaswa kuwa makini sana mpenzi wangu,” alisema Shamila lakini alichokisema ni kama hakikuingia akilini mwangu.
Akili yangu ilianza kunienda mbio kuliko kawaida, nikawa naunganisha matukio, kuanzia siku Shenaiza aliponipigia simu na kuniambia kwamba ana tatizo kubwa na anahitaji nimsaidie, baada ya awali kuwa amekosea namba.
“Lazima nikazungumze na Shenaiza, atakuwa anajua mambo mengi zaidi,” nilisema huku nikijaribu kuinuka, Shamila akanizuia na kuniuliza kama ninakumbuka kilichotokea muda mfupi uliopita kwenye maegesho ya magari.
Japokuwa nilikuwa na shauku ya kwenda kuonana na Shenaiza, maneno hayo ya Shamila yalinivunja nguvu kabisa. Nilikumbuka jinsi wale wanaume wenye asili kama ya Shenaiza walivyokuwa wakiniwinda kwa udi na uvumba.

“Kama usingepata akili ya kuingia kwenye wa ile teksi unafikiri nini kingetokea?” alisema Shamila huku akinibusu kwenye paji langu la uso.
Kitu ambacho ningependa kukieleza hapa, ndani ya muda mfupi tu tangu nifahamiane na Shamila na kujikuta nikianguka naye dhambini, dada huyo mrembo alionesha kuchanganyikiwa kabisa na penzi langu.
Kila mara alikuwa anapenda kunibusubusu, mara anishike hapa, mara anisafishe kucha, mara anidekeze basi ilimradi roho yake ifurahi! Moyoni nilikuwa najisikia raha sana kwa sababu siyo siri, sikuwa mzoefu wa mambo hayo ya kikubwa.
Unajua kwa nini wanaume wengine huwa wanafikia hatua ya kutelekeza familia zao? Unakuta katika maisha yako, hujawahi kukutana na mwanamke anayejua kukupetipeti kama ilivyokuwa kwa Shamila. Sasa ukishaangukia kwenye mikono yake, na wewe ni mgeni wa mambo hayo, lazima utelekeze mke na watoto na kuhamia kwake.
“Kwani Shamila wewe ni mtu wa wapi?”
“Mbona unaniuliza swali ambalo haliendani kabisa na mada tunayozungumza?” aliniuliza Shamila huku akinitazama kwa yale macho yake ambayo muda wote yapo kama yana usingizi!
Nikachekacheka pale na kupotezea mada, akaendelea kunisisitiza kwamba huo haukuwa muda muafaka wa mimi kutoka na kwenda kwenye wodi aliyokuwa amelazwa Shenaiza, wala kuzungukazunguka kwa sababu ya usalama wangu.
“Lakini Shamila, kuna kazi ambayo ni lazima niikamilishe haraka iwezekanavyo, au wewe unaridhishwa na kinachofanywa na huyu mzee pamoja na kundi lake?”
“Siyo kwamba naridhishwa mpenzi wangu, Wazungu wanasema ‘dont hurt what you cant kill’ (usiwinde kitu ambacho hutaweza kukiua), hata ukifuatilia na kuujua ukweli, utafanya nini?”
Shamila alikuwa amenizidi kwa hoja, ikabidi nitulie tu wodini huku nikiendelea kutafakari nini cha kufanya kwa sababu ile hoja ya kwamba niache kufuatilia suala lile kwa sababu sikuwa na cha kufanya, sikuliona kama ni sahihi kwangu.
Baadaye, nilijifanya kama nimepitiwa na usingizi, lengo lilikuwa ni kumpumbaza Shamila, kweli aliponiona nimelala alikuja nakunifunika vizuri kisha akatoka na kwenda kuendelea na shughuli zake.
Nilisubiri kwa dakika kadhaa, nilipoona kumetulia kabisa, niliamka na kuvaa viatu, nikatazama huku na kule, niliporidhika kwamba Shamila hakuwepo, nilinyata hadi kwenye chumba cha manesi, nikachukua koti la kidaktari lililokuwa limetundikwa ukutani, nikalivaa na kusogea kwenye kioo kilichokuwa pembeni, nikajirekebisha vizuri.
Kama ungenitazama haraka, ungeweza kudhani na mimi ni muuguzi hospitalini hapo, niliamini hiyo ndiyo itakuwa njia nyepesi ya kwenda kuonana na Shenaiza kule wodini kwake bila kushtukiwa na mtu yeyote.
Harakaharaka nilitoka huku nikiwa makini jeraha langu la kifuani lisije kufumuka tena, nikaingia kwenye lifti na kushuka hadi ghorofa ya chini, nikashuka na kuanza kutembea harakaharaka kuelekea kule kwenye wodi ya wagonjwa wa akili, wanawake alikokuwa amelazwa Shenaiza.
Nilifanikiwa kufika kwenye wodi ya wagonjwa wa akili, kama ilivyokuwa kawaida ya wodi hiyo, nilipokelewa na vurugu na kelele za kila aina kutoka kwa wagonjwa, nikawa nawapita mmoja baada ya mwingine mpaka nilipofika kwenye kitanda cha Shenaiza.
Tofauti na nilivyotegemea kumkuta Shenaiza akiwa amekaa kitandani kwake akilalamika, nilishangaa kumkuta akiwa amelala tuli, akionesha kabisa kwamba hakuwa kwenye hali ya kawaida.
Nilisimama kwa sekunde kadhaa na kuanza kumtazama, kwa zile saa chache tu nilizokaa mbali naye, alikuwa amebadilika kabisa. Ngozi ya mwili wake, iliyokuwa na weupe wa kung’aa, ilikuwa imebadilika na kuwa na rangi kama ya kijivu hivi, macho yalikuwa yamefumbwa nusu na nusu yapo wazi, mdomo pia haukuwa umefumbwa, nikajikuta nikishindwa kujizuia kutokwa na machozi.
“Shenaiza! Shenaiza!” nilimuita lakini hakuitika, nilijaribu kumtingisha lakini hakutingishika, nikabaki nikihaha huku na kule, nikiwa sijui cha kufanya. Nilipotazama pembeni ya kitanda chake, kulikuwa na kichupa kidogo juu ya droo ya kitanda chake, kilichokuwa na maandishi yaliyosomeka Benzodiazepam.
Harakaharaka nilikichukua kichupa kile na kukiweka kwenye mfuko wa koti, nikatazama huku na kule kujaribu kuangalia kamakuna mtyu aliyekuwa akinitazama. Katika hali ambayo sikuitegemea, miongoni mwa wale wagonjwa wengi wa akili waliokuwa ndan ya wodi hiyo, kuna mmoja alikuwa ametulia, muda wote akinikodolea macho.
Kwa kumtazama tu, hakuonesha kwamba ni mwendawazimu kama wale wenzake kwa sababu macho yangu na yake yalipogongana tu, harakaharaka alikwepesha macho pembeni na kuvunga kama hakuwa akinitazama. Kitendo hicho tu kilitosha kunifanya niamini kwamba hakuwa mgonjwa kama wale wengine.
Niliendelea kumkazia macho, akawa ananitazama kwa wiziwizi, nikamsogelea pale kwenye kitanda alichokuwa amelala juu yake, nikashtuka kumuona akiwa na simu kubwa ya kisasa ambayo harakaharaka aliificha kwenye shuka.
“Wewe ni nani?” nilimuuliza kwa sauti ya chinichini, akanigeukia, tukatazamana.
“Kwani unataka nini?” naye aliniuliza kwa sauti iliyoonesha dhahiri kwamba ni mwanamke mjeuri sana na alikuwepo pale kwa kazi maalum.
“Naomba kuzungumza na wewe, unamfahamu Shenaiza?” nilimuuliza lakini badala ya kunijibu, alinitazama kuanzia juu mpaka chini kisha akageukia pembeni. Kengele ya hatari ililia ndani ya kichwa changu, harakaharaka nikageuka na kuanza kutembea kuelekea kwenye mlango wa kutokea.
“Unahatarisha maisha yako, achana na mambo yasiyokuhusu,” alisema yule msichana, nikageuka na kumtazama, naye akawa ananitazama. Sikuelewa kwa sababu gani amezungumza maneno yale, nikaendelea kutembea harakaharaka na kutoka.
“Mungu wangu, mbona sielewi kinachoendelea?” nilisema huku nikiendelea kutembea kwa haraka, nikaenda mpaka kwenye lifti na kupanda, nikabonyeza namba ya ghorofa ilipokuwa wodi ya ‘private’ niliyokuwa nimelazwa, lifti ikaanza kupanda.
“Unatoka wapi?” Shamila aliniuliza nilipofungua mlango tu, kumbe alikuwa amerejea muda mrefu na akawa anahangaika kunitafuta.
“Nilitoka mara moja,” nilijitetea huku nikijisikia aibu ndani ya moyo wangu.
“Kwa nini hujihurumii mpenzi wangu? Mimi sitakwambia tena kuhusu suala la kuzingatia usalama wako,” alisema huku akinisaidia kuvua lile koti la kidaktari huku akiendelea kunitazama kwa macho ya mshangao.
“Samahani, eti hii ni dawa gani?” nilisema huku nikitoa kile kichupa nilichokichukua kwenye kitanda cha Shenaiza. Akakishika na kukitazama.
“Umekipata wapi?”
“Nimekikuta kwenye kitanda cha Shenaiza, na anaonekana kama hana fahamu, rangi ya ngozi yake imebadilika na kuwa ya kijivu,” nilimwambia, akashusha pumzi ndefu na kunitazama usoni.

Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...