Friday, September 8, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 33


ILIPOISHIA:
“Nakuapia kama ningekutana na wewe kabla ya Raya, huenda wewe ndiyo ungekuwa mpenzi wangu na si ajabu ningeshakuwa nimekuoa, naogopa kukueleza ukweli wa moyo wangu kwa sababu mtu mwenyewe unakuwa mkali kwangu,” nilizidi kumseti kwa maneno matamu, akashindwa kujizuia na kuniinamia pale kitandani, akanibusu kwa hisia za hali ya juu na kunikumbatia bila kujali kwamba anaweza kunitonesha tena jeraha langu la kifuani.
SASA ENDELEA...
“Hata mimi nakupenda sana Jamal lakini nilikuwa nashindwa namna ya kukufikishia ujumbe, ahsante kwa kuzielewa hisia zangu,” alisema Shamila huku akiwa amenikumbatia, akaendelea kunibusu sehemu mbalimbali za mwili wangu.
Niliona jinsi kitendo changu cha kuingiza masuala ya mapenzi kilivyomfurahisha, tukaendelea kupiga stori mbalimbali huku mara kwa mara akinikumbatia na kunibusu, na mimi nikawa nazidi kumsifia kwani miongoni mwa ‘maradhi’ ya wanawake, ni kupenda kusifiwa! Dalili za kutimia kwa nilichokuwa nakitaka zikaanza kuonekana waziwazi.
Hatukuwa nesi na mgonjwa kama ilivyokuwa awali, sasa tukawa zaidi ya hapo, nikamuona Shamila akizidi kuninyenyekea, kunipa huduma bora zaidi na muda mwingi akiwa pembeni ya kitanda changu.

Sikujihisi tena kama niko hospitali, ungeweza kusema nipo tu nyumbani. Japokuwa siku hiyo Shamila alikuwa na ‘shift’ ya kutoka saa kumi na mbili jioni, hakutaka kuondoka, akaniambia kwamba ataenda kuongea na kiongozi wao ambadilishie zamu, alale tena kazini mpaka kesho yake ndiyo arudi nyumbani.
“Nimechoka kukaa hospitali mpenzi wangu, naona kama kuna mambo ya muhimu yanazidi kuchelewa, sijui utanisaidieaje?” nilimwambia Shamila, akiwa amekaa pembeni yangu, muda wote mikono yake ikiwa mwilini mwangu.
“Kwani unataka kwenda kufanya nini Jamal, mi nakuonea huruma bado hujapona vizuri. Kuna kazi ya muhimu inatakiwa nikaifanye.”
“Kwa nini usiniagize mimi nikakufanyie?”
“Hapana, ni lazima niifanye mimi mwenyewe labda kama utanisindikiza tu.”
“Lakini bado hujapona.”
“Kwani haiwezekani nikatoka asubuhi halafu baadaye nikarudi?”
“Sasa madaktari wakipita ‘raundi’ na kukukosa wodini itakuwaje? Si unajua wewe bado unatakiwa kuwa chini ya uangalizi maalum na ndiyo maana umeletwa huku kwenye wodi ya peke yako mpenzi?” alisema Shamila.
Kimsingi hakukuwa na uwezekano wowote wa mimi kutoka kirahisi hospitalini lakini nikaona niendelee kumbembeleza Shamila. Kwa kuwa sasa nilikuwa mpenzi wake na nilishaanza kumpa ahadi kemkemu kuhusu maisha yetu ya kimapenzi yatakavyokuwa, nilifanikiwa kumteka akili.
“Basi kesho inabidi mimi asubuhi nisiondoke mapema, nitasubiri mpaka madaktari wakishapita raundi wodini tu, tutaondoka wote mpaka nje ya hospitali. Nitawaambia walinzi umeandikiwa vipimo ambavyo hapa hospitalini havipo,” alisema Shamila, nikaachia tabasamu pana.
Waliosema mapenzi yana nguvu hawakukosea. Shamila alikuwa tayari kuhatarisha kazi yake kwa sababu ya kutetea penzi! Basi tulifikia muafaka, ukaribu wa mimi na Shamila ukazidi kuongezeka utafikiri tulifahamiana miaka mingi iliyopita.
Hata yale masihara aliyokuwa ananiletea awali, nikaona yamepungua sana, muda mwingi akawa anapenda tuzungumzie kuhusu penzi letu. Unajua wanaume wengi huwa wanafanya makosa sana kushindwa kufahamu namna ya kuishi na mwanamke ambaye anaonesha hisia za kukupenda.
Tofauti na wanaume ambao akimpenda mtu huweza kumwambia moja kwa moja kwa ujasiri, wanawake huwa hawana ujasiri huo labda wachache. Kama mwanamke anakupenda, kuna baadhi ya dalili atakuwa anakuonesha akiamini ukiziona, utajiongeza mwenyewe kichwani.
Ukishaziona dalili hizo, hata kama huna malengo ya kuanzisha naye uhusiano wa kimapenzi, kuna namna ya kumuonesha kwamba umemuelewa hata kabla hajatamka chochote na kwamba unaziheshimu hisia zake.
Ikitokea anakuonesha dalili fulani lakini wewe unaendelea kujifanya kipofu, kihulka wanawake ni wepesi sana wa kujisikia vibaya, atahisi umemdharau, ataamini hajakuvutia ndiyo maana umeshindwa kuelewa hisia zake na mwisho utashangaa anaanza kujitenga mbali na wewe na kukujengea chuki.
Kwangu mimi niliamua kupiga ndege wawili kwa mpigo kwa Shamila, japokuwa kiukweli hakuwepo kwenye mawazo yangu kwa sababu tayari nilishaamua kumkabidhi moyo wangu Raya, niliamua kumuonesha kwamba nampenda sana kwa sababu mbili; kwanza sikutaka ajisikie vibaya kwamba ananionesha ishara kwamba ananipenda lakini nampuuza lakini kubwa, nilitaka anisaidie kwenye ile kazi kubwa iliyokuwa inanisubiri.
Malengo yangu yalianza kutimia haraka kuliko hata nilivyotegemea kwa sababu tayari jambo moja muhimu lilikuwa likienda kutimia; kwenda kuonana na Firyaal, mdogo wake Shenaiza ambaye angenipa bahasha yenye taarifa kuhusu baba yao na biashara hatari alizokuwa anazifanya.
Usiku huo Shamila wala hakwenda kukaa kwenye chumba cha manesi kama utaratibu ulivyo, muda wote alikuwa na mimi wodini na hata muda wa kulala ulipofika, alisogeza kitanda tupu kilichokuwa pembeni karibu kabisa na kitanda changu, akajilaza juu yake huku tukiendelea kupiga stori za hapa na pale mpaka nilipopitiwa na usingizi.
Kesho yake asubuhi, Shamila aliwahi kuamka na kuniamsha na mimi, akanisaidia kubadilisha shuka pale kwenye kitanda changu, akaniandalia mswaki na taulo na kuniambia inatakiwa nikaoge ili nipate nguvu. Akanisisitiza kwamba nihakikishe maji hayagusi kwenye jeraha langu.
Nilijikaza na kuamka, nikaenda bafuni ambako nilioga kwa mara ya kwanza tangu nirudiwe na fahamu zangu, nikajisikia mwili ukipata nguvu kubwa, nikarudi wodini ambako nilikuta Shamila akiandaa kahawa, niliporudi kitandani tukakaa pamoja na kuanza kunywa, sote tukachangamka.
Baadaye madaktari walipita kwa ajili ya kutazama maendeleo yangu, wakafurahishwa sana na jinsi nilivyokuwa nikipona haraka, wakawa wanampongeza Shamila kwamba amefanya kazi yake ipasavyo ndiyo maana nilikuwa napona haraka, wote tukafurahi.
“Bila shaka sasa unaweza kutusimulia kuzimu kulivyo maana naamini ulifika na kukutana na mtoa roho ila akaamua kukusamehe tu,” alisema yule daktari kijana aliyezoea kunitania, wote tukacheka.
Nikaandikiwa dawa nyingine za kukausha jeraha langu kisha wakaondoka na kuendelea kuwatembelea wagonjwa waliokuwa wamelazwa kwenye wodi nyingine, Shamila akanitazama, macho yetu yakagongana, nikamuona akishusha pumzi ndefu na kunisogelea huku akitabasamu.
“Sasa itabidi uwe makini sana, mtu yeyote akituuliza tunaelekea wapi utamjibu kwamba nakufanyisha mazoezi, sawa?” Shamila aliniambia kwa sauti ya mamlaka, nikatingisha kichwa kuonesha kukubaliana naye.
Tukajiandaa kisha akachukua mkoba wake, tukatoka taratibu huku tukiendelea kupiga stori za hapa na pale. Kwa kuwa Shamila alikuwa akifahamika hospitalini hapo, hatukupata usumbufu wowote, tukatoka mpaka nje kabisa ya geti bila kuulizwa chochote na mtu yeyote.
Tukaenda mpaka kwenye maegesho ya teksi, madereva wakatudaka juujuu na kuanza kutukaribisha, tukaingia kwenye teksi moja kisha Shamila akanigeukia.
“Tunaanzia nyumbani kwangu, sawa?”
“Hapana, naomba kwanza twende Kurasini halafu ndiyo tutaenda kwako, niko chini ya miguu yako nakuomba,” nilimwambia, akanitazama kwa macho yake mazuri na kutingisha kichwa kuonesha kukubaliana na nilichokisema.
“Naomba tupeleke kwenye Mtaa wa Mama Zayumba, Kurasini,” Shamila alimwambia dereva huyo. Alishakuwa anaujua mpaka mtaa kwa sababu aliniuliza na nikamuelekeza kama na mimi nilivyokuwa nimeelekezwa na Shenaiza, safari ikaanza.
Safari iliendelea na hatimaye tukawasili kwenye mtaa huo ambao ndiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza kufika, tukafuata ramani aliyonipa Shenaiza na hatimaye tukatokezea kwenye jengo la kisasa la ghorofa tatu, likiwa na geti kubwa lililozungushiwa nyaya zinazopitisha umeme upande wa juu huku kukiwa na mlinzi mwenye silaha.
Tukasogea na teksi mpaka jirani kabisa na lile geti, yule mlinzi akamuonesha dereva ishara ya kusimama kisha akatusogelea na kutusabahi,mimi nidyo nikawa mzungumzaji mkuu.
“Nikajitambulisha kwamba ni rafiki yake Shenaiza na kuna kitu alikuwa amenituma kuja kukichukua kwa mdogo wake, Firyaal. Kwa jinsi nilivyompa maelezo, wala hakututilia mashaka, hasa alipomuona pia Shamila akiwa amevaa nguo zake za kazini, akajua tumetoka kuonana na Shenaiza hospitalini.
Nikamuona akiingia kwenye chumba cha walinzi na kushika mkonga wa simu, akawa anazungumza na upande wa pili kisha akarudi pale tulipokuwa tumepaki gari na kutuambia tusubiri hapohapo. Tulikaa kwa zaidi ya dakika tatu, tukaona mlango mdogo uliokuwa pembeni ya geti ukifunguliwa, wote tukakazia macho kutaka kuangalia ni nani aliyekuwa anatoka.
Je, nini kitafuatia? Usikose Jumatatu kwenye Championi Jumatatu.


No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...