Thursday, September 7, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 31


ILIPOISHIA:
Alionesha kama kuna jambo muhimu anataka kuniambia kuhusu Shenaiza na baba yake ingawa sikujua ni jambo gani.
“Ha..pa...na! Hapana!” nilijibu kwa kubabaika huku nikiwa makini kutaka kusikia ataniambia nini.
SASA ENDELEA...
“Kuwa makini, baba yake siyo mtu mzuri,” alisema nesi huyo ambaye baadaye nilikuja kugundua kwamba anaitwa Shamila.
“Unamaanisha nini?” nilimuuliza kwa sauti ya chini, akanisogelea zaidi na kukaa pembeni ya kitanda changu.
“Kuwa tu makini, nakupenda na sitaki jambo lolote baya likutokee,” alisema huku akinitazama kwa macho yake mazuri, macho yetu yakagongana. Tulitazamana kwa sekunde kadhaa, akakwepesha macho yake huku aibu za kikekike zikiwa zimetawala uso wake.
“Ahsante kwa kunisaidia kunifunga upya jeraha langu,” nilimwambia tena, nikamuona akitabasamu kisha akanishika mkono wangu.
“Usijali, hiyo ni kazi yangu ila inabidi uijali afya yako. Hata kama angekuwa ni mgonjwa mwingine, ningemsaidia kama nilivyokusaidia wewe.”
“Ahsante pia kwa fulana uliyonipa, ni nzuri na inanukia vizuri,” nilimwambia kwa sauti ya chini, akatabasamu tena na kuniambia:

“Nilijinunulia hiyo fulana kama zawadi siku ya Valentine Day.”
“Kwa nini ujinunulie mwenyewe zawadi katika siku muhimu kama hiyo? Kwani shemeji hakukupa zawadi?”
“Shemeji? Shemeji gani? Niliamua kujionesha upendo mwenyewe.
“Unataka kusema msichana mrembo kama wewe unaweza kuwa huna mtu?”
“Huwezi kuamini, sina mtu yeyote karibia mwaka unaelekea kuisha sasa. Niliyekuwa naye aliniumiza sana moyo wangu na kunifanya niyachukie mapenzi,” alisema Shamila kwa sauti ya upole, nikawa namtazama usoni alivyokuwa anaongea.
“Mbona unaniangalia sana usoni? Mi nasikia aibu bwana,” alisema huku akiniachia mkono wake na kusimama, aibu zikiendelea kutawala uso wake.
“You are so beautiful Shamila!” (Wewe ni mrembo sana Shamila) nilimwambia, akacheka sana na kurudi tena kukaa pale pembeni ya kitanda changu, akaniambia zimepita siku nyingi hajasikia kauli kama hiyo kutoka kwenye kinywa cha mwanaume mzuri kama mimi, wote tukacheka na kugongesheana mikono.
Kuna jambo kubwa lilikuwa limebadilika maishani mwangu, kwa kipindi kirefu sikuwa na mazoea ya kukaa karibu na wasichana wala kupiga nao stori.
Mtu pekee niliyekuwa nimezoeana naye alikuwa ni Raya ambaye hata hivyo mara kwa mara nilikuwa nikimkwepa lakini cha ajabu, katika siku za karibuni, nilijikuta nikivutiwa na wasichana wawili, Shenaiza na sasa Shamila, achilia mbali Raya ambaye tayari tulishaanza naye uhusiano wa kimapenzi.
Hata ujasiri wa kuzungumza pia ulikuwa umeongezeka. Nikaendelea kupiga stori za hapa na pale na Shamila, nikawa namchangamsha kwa sababu nilijua kuna jambo nilikuwa nimemkera lakini pia nilitaka kumuingia ili nipate habari kumhusu Shenaiza na baba yake kwani ilionesha kwamba nesi huyo anawajua vizuri.
“Hujaniambia ubaya wa baba yake Shenaiza, kwani amefanya nini?”
“Tuachane na hayo, usije ukaenda kumwambia binti yake bure, inaonesha unampenda sana. Hivi nikuulize, kwani wewe una wapenzi wangapi?”
“Nijibu kwanza swali langu na mimi nitakujibu la kwako. Ubaya wa baba yake Shenaiza ni upi?” nilimkomalia Shamila, akashusha pumzi ndefu na kugeuka huku na kule kama anayehakikisha kwamba hakuna mtu aliyekuwa akitusikiliza.
“Anafanya biashara za hatari sana, siyo mtu mzuri hata kidogo.”
“Biashara za hatari ndiyo biashara gani? Anauza madawa ya kulevya?”
“Si bora hata angekuwa anauza madawa ya kulevya! We elewa kwamba anafanya biashara za hatari sana, kama huamini endelea kumchunguza taratibu.”
“Nitamchunguza vipi wakati hata simfahamu?”
“Humfahamu?” aliniuliza Shamila kwa mshangao, nikamhakikishia kwamba simfahamu kabisa. Aliniambia inawezekanaje nikawa na ukaribu na Shenaiza lakini nisimfahamu baba yake? Sikuwa na cha kumjibu lakini ukweli ni kwamba sikuwa nimewahi kumuona zaidi ya kusikia tu habari zake.
Akaniambia kuwa muda mwingi huwa hakai nchini na hata akija, huwa haonekani kwa urahisi. Nikamuuliza yeye amemfahamia wapi? Akanijibu kwamba huwa anakuja mara kwa mara hospitalini hapo kwa sababu ana marafiki wengi ambao ni madaktari.
“Kwani na yeye ni daktari?”
“Hapana.”
“Sasa iweje awe na marafiki madaktari?” nilimuuliza, akashusha pumzi ndefu na kuniambia kwamba ana urafiki nao kwa sababu huwa anashirikiana na baadhi yao wasio waaminifu kwenye hizo biashara zake.
Nilijaribu kumbana aniambie ni biashara ya namna gani anayofanya na madaktari lakini hakuwa tayari kuniambia chochote kwa maelezo kwamba anahofia maisha yake. Nilimbana sana lakini alikataa katakata kuniambia zaidi ya kunitaka niendelee kufuatilia mwenyewe nitaujua ukweli.
Kiukweli alinichanganya kichwa lakini alinipa mwanga. Ukichanganya na yale maelezo ya Shenaiza, tayari nilikuwa na sehemu ya kuanzia, nikajiapiza ndani ya moyo wangu kwamba ni lazima nitaujua ukweli na nitafanya kazi niliyotumwa, ya kumzuia kuendelea kufanya alichokuwa anakifanya japokuwa sikujua ni kitu gani.
Ni kazi ambayo nilipewa nikiwa kule kwenye ulimwengu mwingine kama masharti ya kurejea kwenye ulimwengu wa kawaida. Sikujua nitafanya nini lakini nilichojiapiza ni kwamba ilikuwa ni lazima nifanikiwe kumzuia alichokuwa anakifanya.
“Mbona kama umezama kwenye dimbwi la mawazo?” Shamila aliniuliza na kunizindua kutoka kwenye mawazo mazito, nikashusha pumzi ndefu na kumtazama usoni.
“Haya na wewe nijibu maswali yangu!” alisema Shamila huku tabasamu likianza kuchanua kwenye uso wake. Jambo ambalo sikuwa na uhakika nalo, ni juu ya uchangamfu wa Shamila. Sikujua huwa anachangamka hivyohivyo akiwa na watu wengine au ni kwangu tu.
“Nimekuuliza una wapenzi wangapi?”
“Mmoja tu, anaitwa Raya, yule niliyekuwa namkimbilia muda ule.”
“Muongo wewe, na Shenaiza?”
“Shenaiza siyo mpenzi wangu, ni rafiki yangu tu.”
“Rafiki yako ndiyo mna-kiss? Yaani hamjifichi kabisa, inaonesha ni mpenzi wako.
“Siyo mpenzi wangu, kweli tena,” nilimwambia Shamila lakini akaendelea kukataa, akaniambia hata Shenaiza mwenyewe alikuwa akiwaambia manesi kwamba mimi ndiyo mpenzi wake na tuna mipango ya kuja kufunga ndoa, kauli iliyonishangaza sana.
Shamila aliendelea kunishutumu kwamba sijatulia, naonesha nina wanawake wengine wengi na ndiyo maana nashindwa kuwathamini watu wanaonipenda kwa dhati. Sikuelewa msingi wa lawama zake ni nini kwa sababu mimi na yeye ndiyo kwanza tulikuwa tumejuana, akaendelea kuniambia kwamba kwa sababu sijatulia nitakosa vitu vizuri.
Akaonesha kususa na kutoka wodini kwa hasira, akaniacha nikiwa na maswali mengi yaliyokosa majibu, wakati anatoka mlangoni, alipishana na Raya aliyekuwa akiingia akiwa na kikapu ambacho hata bila kuuliza nilijua kwamba kina chakula. Nilipomtazama usono, macho yake yalikuwa mekundu na yamevimba kuonesha kwamba alikuwa amelia kwa muda mrefu, hata ule uchangamfu wake haukuwepo tena. Macho yake yakatua kwenye fulana niliyokuwa nimevaa, akanikazia macho.

Je, nini kitafuatia? Usikose Jumatatu kwenye Championi Jumatatu.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...