Tuesday, September 5, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 30


ILIPOISHIA:
“Ukikamilisha kazi nitakupa zawadi ya ushindi,” alisema Shenaiza huku akinifinyia kijicho kimoja, nilishaelewa alimaanisha nini. Nikasimama na kumshukuru, nikambusu kwenye paji la uso wake na kugeuka nyuma ili nirudi kule wodini kwangu.
SASA ENDELEA...
Sijui Raya alikuwa amefika muda gani eneo hilo kwani nilipogeuka tu, macho yangu na yake yaligongana, japokuwa alikuwa umbali wa mita kadhaa, niliweza kuona hali aliyokuwa nayo. Ilionesha hata kitendo cha mimi kumbusu Shenaiza alikiona kwa macho yake, nikamuona akianza kububujikwa na machozi.
Nilijikuta mwili wangu ukipigwa na ganzi, nikabaki nimesimama nikihisi hata miguu ilikuwa mizito kuinyanyua. Raya alipoona nimemuona, aligeuka na kuanza kutembea harakaharaka huku akiendelea kulia. Niljihisi kuwa na hatia kubwa sana ndani ya moyo wangu.
Japokuwa mimi na Shenaiza hatukuwa tumebusiana kwa nia mbaya, nilijaribu kujiweka kwenye nafasi ya Raya na kuhisi maumivu ambayo alikuwa anayahisi kwa wakati huo. Kwa wale ambao wamewahi kupitia maumivu ya mapenzi watakuwa wanaelewa vizuri ninachomaanisha!
Ukimpenda mtu halafu ukasikia au ukahisi mtu mwingine pia anampenda, ukiwaona pamoja lazima moyo uume sana, na hapo ni ukiwaona kawaida tu, iwe wameongozana barabarani au wamekaa sehemu! Raya alishajua kwamba kuna kitu kipo kati yangu na Shenaiza na kama hakipo basi kinakuja lakini kibaya zaidi, alikuwa amenifuma laivu nikimbusu msichana huyo!
Uso wangu ulinishuka kwa haya, sikujua nitatumia maneno gani kumlainisha Raya, nikawa nazidi kuongeza mwendo kumfuata lakini ghafla nikahisi kitu kikinipasua pale kwenye jeraha langu kifuani ambalo japokuwa nilikuwa na nafuu kubwa, bado halikuwa limepona kabisa.

Licha ya maumivu niliyoyasikia, sikutaka kurudi nyuma, nilijikaza kisabuni na kuendelea kujikokota kumfuata Raya ambaye naye alizidi kuongeza mwendo, akiwa hataki hata kugeuka nyuma kunitazama. Nilivuka kwenye mlango wa kuingia kwenye ile wodi niliyokuwa nimelazwa, nikawa naendelea kumfuatilia Raya aliyekuwa akielekea kwenye geti la kutokea kwa kasi.
Hatua chache mbele nilishindwa kuendelea kumfuatilia baada ya kuhisi maumivu yakizidi pale kifuani kwenye jeraha, nikainama kidogo ule upande wenye jeraha, katika hali ambayo sikuitegemea, nilishtuka mno kugundua kuwa kumbe damu zilikuwa zikinitoka pale kwenye jeraha kiasi cha kulowanisha shati nililokuwa nimevaa.
Nilipogeuka nyuma, niliona michirizi sakafuni kuonesha kuwa kumbe damu ilianza kunitoka pale nilipohisi kitu kikinipasua kifuani, hofu kubwa ikatanda moyoni mwangu. Nikawa nahaha kutaka kujifuta damu na kuzifuta sakafuni kabla mtu yeyote hajaona maana ningeonekana mzembe nisiyejijali afya yangu na huenda madaktari wangenifokea sana lakini sikuwa na nguvu ya kufanya hivyo.
Niligeuka huku na kule kutazama kama kuna mtu alikuwa akiniangalia, pande zote hakukuwa na mtu yeyote zaidi ya Raya aliyekuwa akiishia kwa mbali, lakini nilipotazama kwenye mlango wa ile wodi niliyokuwa nimelazwa, macho yangu yaligongana na ya yule nesi ambaye kumbe muda wote alikuwa akitazama kila kilichokuwa kikiendelea, akiwa ametulia tuli.
Nilishindwa cha kujibu zaidi ya kuendelea kuhaha huku na kule, yule nesi aliendelea kunitazama huku akitingisha kichwa kwa masikitiko. Maumivu yalinizidi, ikabidi niegemee kweye ukuta wa korido huku nikipumua kwa shida.
Harakaharaka yule nesi alikuja mpaka pale nilipokuwa nimeegemea ukuta lakini tofauti na nyakati zote, safari hii hakuwa akicheka wala kutabasamu, kwa mara ya kwanza nilimuona akiwa ‘serious’.
“Help me please!” (Nisaidie tafadhali) nilisema huku nikiendelea kupumua kwa shida, hakunijibu kitu zaidi ya kunipa ishara kwamba nimshike begani, nikafanya hivyo, akapitisha mkono wake mmoja kiunoni kwangu, wa kwangu nikaupitisha kwenye bega lake, akanisaidia kutembea kuelekea wodini huku damu zikiendelea kunitoka.
Yule nesi alinipeleka mpaka kitandani kwangu, akanisaidia kupanda na harakaharaka akanivua lile shati nililokuwa nimevaa, akatoka mbiombio na muda mfupi baadaye alirejea akiwa na kisinia kilichokuwa na vifaa vingi vya tiba.
Kimyakimya akaanza kunisafisha pale kweye jeraha, akanifungua bandeji iliyokuwa imeachia, akanipaka dawa ya kuzuia damu kutoka, akanifunga plasta na bandeji nyingine kisha akanipa dawa za kutuliza maumivu. Akachukua lile shati lililokuwa limeloa kwa damu na kutoka nalo.
Muda mfupi baadaye alirudi akiwa na fulana nyeupe, akanipa nivae huku pia akiwa na vifaa vya kupigia deki, wakati navaa ile fulana kwa umakini ili nisijiumize tena, yeye alikuwa akifuta damu harakaharaka pale chini ya kitanda changu, akaendelea kufuta mpaka kule koridoni nilikokuwa nimechafua.
Yaani hata kama ulikuwa unaumwa vipi, ukikutana na nesi wa namna hii, lazima upone, nilijihisi kuwa na bahati ya kipekee kuhudumiwa naye. Ile fulana aliyonipa nivae ambayo hata sikujua ameipata wapi, ilikuwa imepuliziwa manukato mazuri yaliyofanana na yale aliyokuwa amejipulizia mwilini mwake, nikajisikia raha fulani ndani ya moyo wangu, nikabaki sina la kusema zaidi ya kumshukuru ingawa mwenyewe wala hakunijibu chochote.
Aliendelea kusafisha mpaka nje, aliporudi wodini, niligundua kwamba kumbe wakati akinisaidia kuniingiza wodini, nilimchafua gauni lake jeupe kwa damu, nikazidi kujihisi kua na hatia kubwa. Kumbe na yeye alishagundua kwamba nimemchafua, bila kuzungumza chochote alienda mpaka kwenye chumba cha manesi na kubadilisha gauni, akarudi akiwa amevaa gauni jingine safi.
Kama ilivyokuwa mwanzo, hakutabasamu wala kucheka, hata yale masihara yake hayakuwepo tena, nikahisi nimemkwaza sana kwa nilichokifanya. Alinisogelea pale kitandani, akanipima joto la mwili wangu kisha nikamsikia akishusha pumzi ndefu.
Bila kuzungumza chochote, alienda kukaa kwenye meza iliyokuwa inatazamana na mlango, nikamuona akifunua mafaili mengi, akawa anajaza vitu ambavyo sikujua ni nini, nilihisi ni katika kutimiza majukumu yake ya kazi. Aliendelea kuwa kimya huku mara kwa mara akinitazama kwa kunikazia macho, nikimtazama anakwepesha macho yake na kujifanya hakuwa ananitazama, na mimi nikawa najifanya kama simuoni.
Japokuwa alikuwa ameamua ‘kunichunia’, moyoni nilishukuru kwa msaada alionipa kwani muda mfupi baadaye, yale maumivu yalitoweka kabisa na zile damu nazo zikaacha kutoka, moyoni nikajiapiza kwamba sitainuka tena kitandani mpaka kidonda kikauke kabisa.
Nikiwa pale kitandani, nilizama kwenye dimbwi la mawazo kuhusu mfululizo wa matukio yale yaliyonitokea maishani mwangu mpaka wakati huo, nilikuwa na shauku kubwa ya kupona haraka ili niende kule nilikoelekezwa na Shenaiza kwamba nitakutana na mdogo wake atakayenipa bahasha yenye maelezo ya nilichokuwa nakitafuta.
Hata hivyo, niliamua kujipa muda kidogo ili nipone kidogo na mwili wangu upate nguvu, mawazo mengi yakawa yanaendelea kukizunguka kichwa changu. Niliendelea kujiuliza maswali mengi kuhusu ule ulimwengu mwingine niliouona na maajabu yake, pia jinsi nilivyokuwa naweza kutoka kwenye mwili wangu halisi na kukaa pembeni kisha nikaanza kujitazama mwenyewe.
Ndani ya kipindi kifupi tu nilikuwa nimetokewa na matukio mengi ya kutisha na kustaajabisha ambayo hakuna ambaye angeweza kuniamini endapo ningemsimulia na ndiyo maana mwenyewe niliamua kubaki nayo moyoni, mtu pekee ambaye nilitaka nipate muda wa kutosha kuzungumza naye, alikuwa ni Shenaiza ambaye naye alionesha kutokewa na hali kama na iliyokuwa nayo mimi.  
“Umefahamiana vipi na yule dada aliyelazwa kwenye wodi ya vichaa?” aliniuliza swali yule nesi lililonizindua kutoka kwenye lindi la mawazo, nilipogeuka na kumtazama, alionekana kuwa bize na simu yake ya kisasa, nikashusha pumzi ndefu na kuendelea kumtazama.
“Si naongea na wewe Jamal?” alisema, nikashtuka zaidi alipolitaja jina langu kwa ufasaha mno, kama vile linavyotakiwa kuitwa, tofauti na watu wengi waliokuwa wakilikosea.
“Ni rafiki yangu tu.”
“Baba yake unamjua?” aliniuliza swali lingine ambalo liliufanya moyo wangu ulipuke paah! Tayari alikuwa amesimama na kunisogelea pale kitandani, ule ‘u-serious’ wake ukawa umepungua kiasi. Alionesha kama kuna jambo muhimu anataka kuniambia kuhusu Shenaiza na baba yake ingawa sikujua ni jambo gani.
“Ha..pa...na! Hapana!” nilijibu kwa kubabaika huku nikiwa makini kutaka kusikia ataniambia nini.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...