Wednesday, August 30, 2017

The Graves of the Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia) - 33


ILIPOISHIA:
Muda huo kwa makadirio ilikuwa ni kama saa nane za usiku maana kuna sehemu nilipita nikasikia redio kwa mbali ikitangaza kwamba ni saa nane kasoro za usiku.
“Mbona umeshtuka Togo!” alisema huku akinisogelea. Siwezi kuficha, mshtuko nilioupata nusura nidondoke na kuzimia.
SASA ENDELEA...
Alikuwa ni yule msichana ambaye mchana wa siku iliyopita alinifia gesti tukiwa kwenye mechi ya kirafiki na kunisababishia matatizo makubwa mpaka nikapelekwa mahabusu nikikabiliwa na kesi kubwa ya mauaji.
Nilitaka kukimbia nikahisi mwili wangu ukiishiwa nguvu, nilitaka kupiga kelele lakini sauti ikawa haitoki, nikabaki nimesimama palepale nikitetemeka kama mbwa mbele ya chatu, akawa ananishangaa usoni kama anayejiuliza maswali mengi yaliyokosa majibu.
“Wewe si ulikufa wewe?” nilisema huku safari hii miguu yangu ikiwa imeanza kupata nguvu, nikawa narudi nyuma nikiangalia upenyo wa kukimbia. Ni kama alishagundua ninachotaka kukifanya, akacheka na kunisihi nisikimbie bali kuna jambo la muhimu anataka kuniambia.
Maneno yake yaliingilia sikio moja na kutokea la pili, akili yangu ilinifanya niamini kwamba hakuwa yeye bali mzimu wake, akawa anazidi kunisogelea mwilini.
“Najua unafikiri labda mimi ni mzimu, siyo, nipo hai wala sijafa na leo nitakutajia mpaka jina langu,” aliniambia huku akizidi kunisogelea. Mazungumzo yake hayakuonesha kama alikuwa mzimu au alikuwa na nia mbaya na mimi lakini bado niliendelea kurudi nyuma, naye akawa anazidi kunifuata.

“Jina langu naitwa Isrina au wengi huwa wanapenda kuniita Isri. Nakuomba unipe japo dakika chache nikueleze kilichotokea leo na historia fupi ya maisha yangu, pia nataka nikueleze kitu ambacho hukijui kuhusu wewe ambacho kitakusaidia sana,” alisema kwa sauti ya upole.
Sijui nini kilitokea lakini nilijikuta nikishawishiwa na maneno yake matamu, nikasimama, akazidi kunisogelea mwilini na kunikumbatia kimahaba. Kitendo hicho kilisababisha hofu yote niliyokuwanayo iyeyuke ghafla kwa sababu nimewahi kusikia kwamba tofauti ya mtu na mzimu, ni kwamba mzimu unakuwa na mwili ambao japo unauona, hauwezi kuushika ukashikika.
Nimewahi kusikia kuwa miili ya mizimu inakuwa kwenye mfumo wa hewa, kwamba unamuona mtu lakini ukitaka kumkumbatia anakuwa kama hewa, hashikiki. Ili kuwa na uhakika, na mimi nilimshika kiuno chake, kweli kikashikika vizuri kabisa, tukawa tunatazamana usoni.
Tukiwa bado tunaendelea kutazamana, alinibusu kwenye shavu langu la kushoto, nikajikuta mwili mzima ukisisimka na ndani ya sekunde chache tu, ile hali iliyokuwa inanisumbua sana, ya kuwa na kiu kubwa ya kucheza mchezo wa kikubwa ilinianza tena.
Ni kama Isri alielewa nilichokuwa nakihitaji, alichokifanya ilikuwa ni kuendelea kunitoa hofu huku akiendelea kunichokoza hapa na pale, hali ikazidi kuwa tete kwa upande wangu.
Usiku huo kulikua kimya kabisa, hakukuwa na mtu yeyote aliyekuwa akuipita barabarani, kelele pekee zilizokuwa zinasikika zilikuwa ni za mbwa waliokuwa wakibweka mitaani. Ilibidi tusogee pembeni ya barabara, hakukuwa na muda wa kupoteza, kila mmoja alijiweka kwenye mkao wa kula na kazi ilianza palepale.
Kwa jinsi nilivyokuwa na ‘kiu’, nilimsambaratisha vilivyo Isri mpaka ikabidi aweke mpira kwapani. Hata hivyo, angalau kidogo nilianza kujisikia vizuri, akili yangu sasa ikahamia kwenye kutaka kuujua ukweli kwa sababu nilishahakikisha kwamba Isri hakuwa amekufa.
“Haya niambie kilichotokea.”
“Kwanza nashukuru,” alisema huku akinikumbatia na kunibusu huku tabasamu pana likiwa limechanua kwenye uso wake.
“Usijali, ahsante na wewe,” nilisema, akazidi kucheka. Alivuta pumzi ndefu na kunitazama usoni, Japokuwa ilikuwa ni usiku, kwa msada wa mbalamwezi niliweza kumtazama vizuri jinsi alivyokuwa ananiangalia kwa macho yaliyojaa ujumbe.
Alishusha tena pumzi ndefu kisha akanikumbatia na kujilaza kifuani kwangu, akaniambia kama sitajali, tutafute sehemu na kukaa kwa sababu alikuwa amechoka sana. Nilimkubalia, tukasogea kwenye nyumba ambayo ilikuwa ikijengwa lakini bado haijakamilika, tukakaa kwenye msingi na kuanza kuzungumza.
Aliniambia kwamba aligundua kwamba nina kitu fulani cha kipekee siku ya kwanza tulipokutana ndani ya basi, wakati tukisafiri kutokea Mbeya kuja Dar es Salaam. Aliniambia kwamba yeye amezaliwa katika ukoo wa kichifu kwani babu yake mzaa baba, alikuwa ni kiongozi wa mila wa Wanyakyusa waliokuwa wakiishi kandokando la Mlima Rungwe na alikuwa akiheshimika sana. Aliniambia kwamba hata babu yake huyo alipofariki, alimrithisha mikoba yake baba yake ambaye licha ya kuwa msomi, akiwa ni daktari kwenye Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, pia alikuwa akiendelea na shughuli za kimila na ndiyo maana yeye alikuwa na uwezo wa tofauti na watu wengine kwani ndani kwao yeye ndiye aliyekuwa wa kwanza kuzaliwa.
Maelezo hayo bado hayakuwa yamenisaidia kuelewa chochote, niliona kama ananizungusha tu lakini sikutaka kumkatisha, nikatulia na kuendelea kumsikiliza.
Aliniambia kwamba kwa kuwa yeye ndiye mtoto wa kwanza kwenye familia yao, na kawaida zile kazi za kimila huwa zinarithishwa kwa mtoto wa kwanza, baba yake alikuwa amefanya kitu kimoja kibaya sana kwenye maisha yake ndiyo maana siku aliponiona mimi alifurahi sana.
“Unamaanisha nini?”
“Mimi ni kaburi la wasio na hatia Togo, nimeamua kukueleza ukweli kwa sababu wewe ndiye mwanaume pekee ambaye umeweza kuuvuka mtego wa kifo,” aliniambia, nikawa simuelewi kabisa. Sikuelewa anamaanisha nini anaposema yeye ni kaburi la wasio na hatia na anamaanisha nini anaposema mimi nimeweza kuuvuka mtego wa kifo?
Nikiwa bado na shauku kubwa ya kutaka kumsikiliza alichomaanisha, nilipoinua uso wangu na kutazama upande wa barabarani, nilishtuka sana kuona kulikuwa na watu wengi wamekusanyika, wote wakiwa wanatutazama.
“Mungu wangu,” nilisema kwa mshtuko kwani ilionesha kuna jambo halikuwa sawa kwetu na ndiyo maana walikuwa wakitutazama. Tofauti na mimi, yeye alipowatazama wala hakushtuka, akaniambia ni haki yao kushangaa kwa sababu hatukuwa tukionekana wa kawaida.
“Unamaanisha nini?”
“Umewahi kusikia stori za majini?” aliniuliza, nikamgeukia na kumtazama usoni kisha nikawatazama tena wale watu, walikuwa wakizidi kuongezeka kwa wingi, safari hii baadhi yao wakawa wanatupiga picha kwa kutumia simu zao. Niliweza kuligundua hilo kwa sababu ya mwanga wa flash uliokuwa ukitumulika.
Nilimtaka tuondoke lakini akasema wala nisiwe na wasiwasi, hawawezi kutufanya jambo lolote na hawana uwezo huo. Alipoona situlii, aliniambia nimpe mkono wangu wa kushoto, nikafanya hivyo, akashika kidole changu cha mwisho kisha akaniambia na mimi nifanye hivyohivyo, nikamshika.
“Nahesabu mpaka tatu, nikifika tatu fumba macho na usifumbue mpaka nitakapokwambia,” alisema, nikatii kile alichoniambia. Alipofikisha tatu, nilifumba macho, nikashtukia ghafla tumehama pale tulipokuwa na kwenda upande wa pili, kule barabarani ambako watu wengi walikuwa wamesimama wakishangaa, tukajichanganya na wale watu.
“Hebu angalia wanachokishangaa,” alisema huku akinitaka nitazame pale tulipokuwa tumekaa awali. Macho yalinitoka nikiwa ni kama siamini.
Je, nini kitafuatia? Usikose Jumatatu kwenye Gazeti la Championi Jumatatu.


No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...