Tuesday, August 1, 2017

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 8


ILIPOISHIA:
 Dereva alizidi kuyumba huku gari likiongeza kasi, hali iliyofanya abiria waanze kupiga kelele kwa nguvu, wengi wakilitaja jina la Mungu.
Gari lilizidi kuongeza kasi, likawa linashuka kwenye mteremko huo kwa kasi kubwa huku likiendelea kuyumba huku na kule, kelele ndani ya basi zikazidi kuongezeka.
SASA ENDELEA...
Katika hali ambayo hata sielewi ilikuwaje, nilijikuta nikipata nguvu na kusimama, nikawa natazama nje kwa kupitia kioo cha dereva. Cha ajabu na cha kushtua, nilimuona baba akiwa anapigana na mtu ambaye sikumtambua ni nani, pembeni ya barabara.
Kwa macho yangu, nikamshuhudia baba akimpiga yule mtu kwa nguvu, akamdondosha chini na kuanza kumbamiza kwenye lami, damu nyingi zikatapakaa eneo lote.
Kufumba na kufumbua, nilishtukia baba akiwa ameshika usukani wa lile basi tulilokuwa tukisafiria, sikuwahi kumuona baba hata siku moja akiendesha gari lakini eti siku hiyo ndiyo alikuwa ameshika usukani. Sikukumbuka ameingiaje ndani ya basi, tena likiwa katika mwendo mkali kiasi kile.
Kila kitu kilifanyika kwa kasi kama ya radi, akamtoa dereva na kumsukumia pembeni, akaanza kubadilisha gia huku akiwa ameung’ang’ania usukani, katika hali ambayo hakuna aliyeitegemea, gari liliacha kuyumbayumba ingawa halikupunguza mwendo, likawa linazidi kukimbia kwa kasi kubwa, likishuka kwenye mteremko mkali maarufu kama Mlima Nyoka.
Abiria wote walitulia, hata wale waliokuwa wakipiga kelele, walikaa kimya, wakawa wanaendelea kumuomba Mungu ndani ya mioyo yao, hakuna aliyeona mabadiliko yaliyofanyika upande wa dereva zaidi ya mimi nadhani na watu wachache waliokuwa wamekaa mbele.
Nilimshuhudia baba akiendelea kupangua gia kwa kasi, gari likaanza kupunguza mwendo na mita chache mbele, alifunga breki, gari likaserereka na hatimaye likasimama kandokando ya barabara, watu wote waliokuwa ndani ya basi walianza kushangilia na kumpongeza dereva huku wakikimbilia kwenye mlango wa kutokea nje.
Harakaharaka na mimi nilielekea kule mbele lakini lengo langu kubwa ilikuwa ni kwenda kumuuliza baba nini kilichotokea maana sikuwa naelewa chochote.
Cha ajabu, nilipofika pale kwenye siti ya dereva, nilimuona yule dereva ambaye ndiye aliyetoka na sisi Mbeya mjini akiwa ameegamiza kichwa kwenye usukani, akiwa ni kama amepitiwa na usingizi.
Nilibaki nashangaa kwa sababu kitendo cha kuinuka kutoka pale kwenye siti niliyokuwa nimekaa mpaka pale kwa dereva, sikuwa nimetumia hata dakika moja kamili, zilikuwa ni sekunde tu lakini eti baba hakuwepo tena na aliyekuwa amekaa pale kwenye usukani alikuwa ni dereva.
Niligeuka huku na kule kutazama kama nitamuona baba lakini sikumuona, abiria walikuwa wakiendelea kugombea kutoka na muda mfupi baadaye, wote walikuwa wameshateremka, kila mmoja akawa anamshukuru Mungu wake. Yaani kama ingetokea ajali, kwa jinsi mteremko ulivyokuwa mkali, sidhani kama kuna mtu angetoka salama ndani ya basi lile.
Ilibidi nimguse begani yule dereva ambaye bado alikuwa amelala na kuegamia usukani ili nimuulize nini kilichotokea. Cha ajabu, nilipomgusa, alishtuka sana, akawa ni kama aliyezinduka kutoka kwenye usingizi mzito, akawa anageuka huku na kule. Hakukuwa na mtu mwingine yeyote ndani ya gari, isipokuwa mimi na yeye tu.
“Nini kimetokea? Hatujapata ajali? Mungu wangu,” alisema yule dereva huku akianza kujikagua mwili wake. Nilishangazwa sana na hali ile, yaani kumbe na yeye hakuwa anaelewa kilichotokea kwa hiyo kama zisingefanyika jitihada zile, ni kweli tungepata ajali mbaya sana.
“Kwani wewe unakumbuka nini?” nilimuuliza.
“Wakati tunauanza huu mteremko wa Mlima Nyoka, nilianza kuhisi kizunguzungu, nikajaribu kupunguza mwendo ili nisimame lakini cha ajabu, badala ya kukanyaga breki nilikanyaga mafuta, gari likaongeza mwendo na kizunguzungu kikazidi, sikumbuki tena kilichotokea,” alisema yule dereva huku akiendelea kugeuka huku na kule.
“Tushuke,” nilimwambia, harakaharaka akafungua mlango na kushuka, na mimi nikashuka. Wale abiria waliokuwa chini, walimzunguka dereva na kuanza kumpongeza kwa kazi kubwa aliyoifanya. Ilibidi awe anaitikia tu lakini kiukweli hakuwa anajua nini kimefanyika na imekuwaje mpaka basi limesimama.
Akiwa anaendelea kupongezwa, tabasamu la uongo likiwa limechanua kwenye uso wake, alishtuka baada ya kuanza kuona damu zikimtoka puani, abiria wote nao wakashtuka. Mara ya kwanza alipojifuta, zilikuwa ni damu kidogo lakini mara ya pili, zilikuwa nyingi, tena zikiwa na weusi fulani hivi, kila mmoja akapatwa na hofu kubwa ndani ya moyo wake.
Kwa bahati nzuri, miongoni mwa wale abiria alikuwepo daktari ambaye ilibidi amshike mkono na kumsogeza pembeni, akawataka abiria wengine wasogee pembeni ili apate hewa, akamlaza chini na kuanza kumpa huduma ya kwanza.
Nikiwa bado sielewi nini cha kufanya, nilimuona baba akiwa ng’ambo ya pili ya barabara, akanionesha ishara kwamba nimfuate. Nikaangalia kushoto na kulia, nilipoona hakuna gari, nilivuka barabara na kusogea kule baba alipokuwa amesimama.
“Huku nyuma, mama na ndugu zangu wengine walishangaa kwa nini navuka barabara, mama akaanza kuniita. Nilishangaa kwa nini ananiita mimi tu wakati pembeni yangu alikuwepo baba, nikakosa majibu.
“Vipi, umeona kilichotokea?” baba aliniuliza huku akinitazama usoni, nikawa namtazama huku nikiwa na maswali mengi yasiyo na majibu.
“Baba wewe si tulikuacha stendi? Umefikaje hapa? Halafu uliingiaje kwenye gari na kuzuia ajali isitokee? Yule uliyekuwa unapigana na...” nilijikuta maswali mfululizo yakinitoka. Alichokifanya baba, ilikuwa ni kuniziba mdomo kwa kutumia kiganja cha mkono wake, ambao bado ulikuwa na damudamu.
“Nimeshakwambia, ukiwa mwanaume maana yake unatakiwa kuwa na kifua, siyo kila unachokiona unatakiwa kukisema, umenielewa?” alinihoji baba huku akinitazama, nikatingisha kichwa.
Akaniambia kwamba safari yetu ilikuwa imeandamwa na mabalaa makubwa na mtu pekee ambaye angeweza kushirikiana naye kuhakikisha tunafika salama, ni mimi. Akaingiza mkono mfukoni na kutoa kikaratasi ambacho kilifungwa unga fulani mweusi, akaumimina kidogo mkononi na kuniambia natakiwa kwenda kumpulizia yule dereva usoni.
Akaniambia baada ya hapo, mambo yote yangekuwa sawa na akaniambia natakiwa kukaa siti ya nyuma ya dereva, nikiona jambo lolote haliendi sawa, nivue viatu kisha nivivae upya kwa kuvigeuza, yaani cha kushoto nivae kulia na cha kulia kushoto kisha nishike sehemu zangu za siri.
“Umenielewa?”
“Ndiyo baba.”
“Mimi natangulia kusafisha njia,” alisema kisha akaniambia nivuke barabara, nikafanya hivyo. Kwa bahati mbaya, wakati navuka barabara, safari hii sikutazama kushoto wala kulia, nikavuka tu kama ng’ombe. Nikiwa nimefika katikati ya barabara, nilisikia mama akipiga kelele kwa nguvu pamoja na watu wengine, wote wakinionesha ishara kwamba nikimbie.
Sikuelewa kwa nini wananiambia vile, ghafla niligeuka kutazama upande wangu wa kushoto, lori kubwa la mafuta, lilikuwa limeshanisogelea huku likiwa kwenye mwendo wa kasi kubwa, taa zote za mbele zikiwa zimewashwa.
“Mungu wangu!” nilisema kwani nilijua hakuna kinachoweza kuniokoa kutoka kwenye mdomo wa mauti, ilikuwa ni lazima linisagesage palepale kama chapati.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.











No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...