Saturday, August 19, 2017

The Graves of The Innocent (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 24


ILIPOISHIA:
Ghafla tulishtushwa na kishindo kikubwa ambacho hata sikuelewa kimetokea wapi. Watu walianza kupiga kelele kwa nguvu huku wale waliokuwa baharini wakianza kukimbia kuokoa maisha yangu. Ilibidi tugeuke kutazama kule kishindo kile kilichotokea ambako bado zile kelele zilikuwa zikitokea.
SASA ENDELEA...
Lahaula! Samaki mkubwa ambaye sikuwahi kumuona ingawa baadaye nilisikia kwamba anaitwa papa, akiwa na meno makali yaliyochongoka, aliipiga kikumbo boti ndogo ya uvuvi iliyokuwa eneo hilo na kusababisha kishindo kikubwa, wavuvi waliokuwa ndani ya boti hiyo wote wakarukia majini na kuanza kuhaha kuokoa maisha yao.
Nikiwa bado namshangaa samaki yule ambaye alijirusha kwa nguvu kutoka majini na sasa akawa anaonekana mzimamzima, wote tulishtukia akimfuata mmoja kati ya wale wavuvi, akafunua mdomo wake uliokuwa na meno makali kama msumeno, akamkamata kiunoni, kufumba na kufumbua akaubana mdomo wake kwa nguvu, yule mvuvi akagawanyika vipande viwili.
Sijui nilipata wapi ujasiri, nilijikuta nikiinuka kwa kasi kubwa pale tulipokuwa tumekaa na Rahma, akabaki anapiga kelele za kuniita huku akiniuliza nakwenda wapi na kufanya nini? Sikuelewa swali lake lilimaanisha nini kwa sababu kila kitu kilikuwa wazi, nilikuwa nakwenda kutoa msaada kwa wale wavuvi.
Nilikimbia mpaka eneo ambalo maji yalianza kunifika kiunoni, kwa kuwa nilikuwa na uzoefu wa kutosha wa kupiga mbizi, nilianza kuelekea eneo la tukio. Kadiri nilivyokuwa nazidi kusonge mbele ndivyo kelele zilivyokuwa zikizidi kuongezeka. Sikuwahi kudhani kwamba samaki ana sauti ya kutisha kiasi kile maana alikuwa akitoa milio ya ajabu.

Nikiwa naendelea kupiga mbizi, nilimshuhudia akikifuata kile kipande cha kichwa cha yule mvuvi, akaanza kukichanachana kwa meno yake makali, akararua minofu yote na kubakiza mifupa michache tu, akahamia kile kipande kingine cha kichwa, akakitafuna na kuacha kichwa tu. Nilijikuta nikipatwa na hofu ya ajabu, hakika sikuamini nilichokuwa nakiona.
Maji yote ya eneo lile yalibadilika rtangi na kuwa mekundu, mimi nikawa nazidi kupiga mbizi nikiwa hata sijui naenda kufanya nini maana uwezo wa kupambana na samaki yule kwenye maji, hakika sikuwa nao, nikasikia kelele za watu wakinizuia na kunitaka nirudi maana tayari wale wavuvi wengine walishapotea kwenye upeo wa macho yangu.
Ghafla nilihisi kama kuna kitu kimenishika kwenye mguu wangu wa kushoto na kuanza kunivutia chini, tayari nilishafika kwenye kina kirefu, nikatumia nguvu kubwa kujaribu kupambana na kile kitu kilichokuwa kimeninasa ambacho bado sikuwa najua ni nini, ghafla nikajikuta nikizama.
Nilipoibuka, nilikuwa nimemeza kiasi kikubwa cha maji ya chumvi na nikiri kwamba unaweza kuwa unajua sana kuogelea kwenye maji baridi lakini maji chumvi ni hatari sana maana yakikuingia puani au ukiyanywa, ile chumvi inakufanya uzidi kuwa kwenye hali mbaya.
Nilijaribu kupiga mbizi kwa nguvu lakini bado kile kitu kilikuwa kimenibana mguu na kuzidi kunivuta, nilitamani nigeuke niangalie ni nini lakini sikuweza kutokana na jinsi nilivyokuwa napambana na mawimbi makali. Nikajikuta nikizama tena na kunywa maji mengi zaidi ya mwanzo, nikaibuka na kuendelea kutapatapa, safari hii mwili ukiwa umeishiwa kabisa nguvu kiasi cha kuanza kuhisi giza nene machoni.
Sikuelewa tena kilichoendelea kwani giza nene lilinizingira usoni huku nikianza kuona picha za majinamizi ya kutisha.
***
“Nisaidieni jamani mchumba wangu anakufaaaa, msaada?” Rahma alipiga kelele kwa nguvu na kuwafanya watu wote waliokuwa ufukweni hapo, wakiwemo wavuvi waliokuwa wakivuta nyavu zao, kuacha kila walichokuwa wakikifanya na kukimbilia kule baharini kwenye kina kirefu.”
“Imekuwaje tena jamani?”
“Mh hata sijui nini kimetokea, hawa walikuwa wamekaa pale ufukweni na mwenzake, mara mwanaume akaanza kukimbilia baharini, tena akiwa na nguzo zake zote.”
“Mimi mwenyewe nimemuona, nikasema huyu jamaa kachanganyikiwa nini? Unaambiwa kakimbia mpaka kule, akaanza kupiga mbizi kwa kasi kubwa kama samaki, mara tunashangaa anaanza kutapatapa, mwisho maji yanamzidi anazama,” alisema mwanaume mmoja, shuhuda wa tukio lile.
“Binti kwani amepatwa na nini?”
“Nisaidie kwanza kumsaidia, mengine tutajua baadaye,” alijibu Rahma huku akilia na kurusharusha miguu kama amekanyaga siafu. Muda mfupi baadaye, wavuvi watatu tayari walikuwa wameshamfikia pale alipokuwa ambapo kwa sababu alishazama na kuibuka kwa mara ya tatu, ilibidi wazame chini kumtafuta.
Kwa bahati nzuri, walifanikiwa kumpata, wakaibuka naye na kupiga mbizi mpaka ufukweni kwenye mchanga ambapo watu wengi walikuwa tayari wameshakusanyika, zoezi la kumsaidia kurejesha pumzi zake likaanza ambapo wale wavuvi walianza kumkandamiza tumboni kwa nguvu.
***
“Kwani ilikuwaje Rahma?”
“Hata sijui baba, siwezi kuelezea maana naona ni zaidi ya maajabu,” nilisikia sauti za watu wakizungumza kwa mbali ambapo nilizitambau vyema sauti hizo kuwa ni Rahma na baba. Bado macho yangu nilikuwa nimeyafumba, nikihisi kila kiungo kwenye mwili wangu kikiwa kizito na kilichokosa nguvu kabisa.
Nilijaribu kufumbua macho mara kadhaa lakini nilikuwa nashindwa, nikawa nimelala tu lakini nikiwa na uwezo wa kusikia kila kilichokuwa kinaendelea.
“Tueleze ili angalau tupate mwanga maana mpaka sasa sote tupo gizani na wewe ndiye uliyekuwa naye kabla hajafikwa na haya matatizo.”
“Tulikuwa salama tu lakini baada ya ile simu mliyopiga ndiyo mambo yalipoharibika, kwa sababu mwanzo tulikuwa tumekaa kwenye mchanga baada ya kuwa Togo ameshacheza sana na maji ya bahari, tena akawa ananichekesha kwa kuniambia eti ukipia chakula hakuna haja ya kuweka chumvi.
“Muda mfupi baada ya kumaliza kuzungumza na simu, nilishangaa kusikia akiniambia kama nimesikia hicho kishindo kikubwa, nikawa nashangaa maana hakukuwa na kishindo chochote, mara akasimama huku akitazama baharini, akawa ni kama ameona kitu ambacho mimi hata sijui ni nini.
“Nikiwa bado nimepigwa na butwaa, nilishangaa akianza kukimbilia baharini, alipofika kwenye maji mengi alipiga mbizi kwa kasi kubwa mpaka alipofika kwenye kina kirefu, mara akaanza kutapatapa mpaka akazama, wavuvi wakaenda kumuokoa akiwa hajitambui, tumbo likiwa limejaa maji,” nilimsikia Rahma akitoa ufafanuzi ambao ulinishangaza sana.
Nilijikuta nikipata nguvu za ghafla, nikafumbua macho na mimi nikitaka kutoa ufafanuzi wa kilichotokea. Kitendo cha mimi kufumbua tu macho, kiliwafanya wote waache kila walichokuwa wanakifanya, wakanisogelea na kuzunguka pale kitandani huku nikimsikia Rahma akimuita nesi.
Wakati wao wananishangaa na kuniuliza nilikuwa najisikiaje, mimi bado nilikuwa nikitafakari maelezo aliyoyatoa Rahma ambayo niliyasikia vyema kabisa. Nilishangaa kwa nini akwepeshe ukweli wa kilichotokea? Yaani alibadilisha maelezo kwa faida ya nani?
Kwani yeye hakumuona yule papa mkubwa aliyekuwa akimla mvuvi huku wenzake wakiponea kwenye tundu la sindano? Ina maana hakusikia kile kishindo cha samaki yule mkubwa anayetisha alipoipiga kikumbo kikubwa boti ile ya wavuvi? Kwa nini hawaambii kwamba nilikuwa naenda kuwaokoa wavuvi? Nilijiuliza maswali mengi yaliyokosa majibu.
Nilianza kuwatazama mmoja baada ya mwingine, kuanzia mama ambaye uso wake ulikuwa na huzuni kubwa, baba ambaye alionesha kuwa katika tafakuri nzito na ndugu zangu wote ambao walikuwa wamekodolea macho, kila mmoja akiwa na maswali mengi yasiyo na majibu.
Mara mlango wa wodi ulifunguliwa, watu wote wakageuka kutazama ni nani aliyekuwa akiingia kwa kasi kiasi kile.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...