Thursday, August 31, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 26


ILIPOISHIA:
“Jamal! Jamal! Jamal!” nilishtuka baada ya kuisikia tena ile sauti nzito ya kutetemeka, iliyoniita kwa mara ya kwanza kabisa, ikiniita tena, ikafuatiwa na vicheko vya kutisha vya watu wengi, nikawa nageuka huku na kule lakini sikuona chochote zaidi ya giza nene, hofu kubwa ikatanda moyoni mwangu.
SASA ENDELEA...
“Hujafika hapa kwa bahati mbaya Jamal, ilikuwa ni lazima uje huku ili ufunuliwe haya mambo ambayo kwa akili ya kawaida usingeweza kuyajua, hebu nifuate,” ilisikika ile sauti nzito ya kutetemeka na kutisha, nikiwa sielewi ni nani aliyekuwa akizungumza nami na alikuwa anataka nimfuate wapi, nilishtukia nikishikwa mkono.
Kufumba na kufumbua, tulitokezea sehemu ambayo kulikuwa na watu wengi wa kila aina wamekusanyika. Wengine walikuwa wamekaa, wengine wamesimama, wengine wamejiinamia na wengine wamelala.
Walikuwa wengi mno, wakubwa kwa wadogo, vijana kwa wazee, wanaume kwa wanawake. Cha ajabu, licha ya wingi wao, wote walikuwa kimya kabisa, hakuna aliyekuwa anazungumza chochote, sauti pekee zilizokuwa zinasikika zilikuwa ni za watu wachache waliokuwa wakigugumia kuonesha wapo kwenye maumivu makali.
“Hapa ni wapi na hawa ni akina nani?” niliuliza lakini hakukuwa na mtu wa kunijibu, yule mtu aliyenileta sikumuona tena, nilijikuta nikiwa peke yangu lakini kukawa na nguvu fulani iliyokuwa inaniongoza sehemu ya kwenda.
Niliendelea kujipenyeza ndani ya lile kundi la watu, nikawa makini kuwatazama wale watu usoni nikiamini naweza kukutana na ninaowafahamu lakini sura nyingi zilikuwa ngeni kwangu. Nikiwa naendelea kushangaashangaa, nilimuona mtu ambaye nilikuwa namfahamu vizuri lakini nilishangaa iweje nikutane naye?
Hakuwa mwingine bali Mzee Muyombe, huyu alikuwa dereva wa halmashauri na nilimkumbuka vizuri kwa sababu mwanaye, Mathayo, tulisoma naye darasa moja tukiwa shule ya msingi na alikuwa rafiki yangu kipenzi. Kilichonishangaza, ni kwamba ilikuwa imepita karibu miaka tisa tangu mzee huyu afariki!
Alipoteza maisha kwenye ajali mbaya ya gari baada ya gari alilokuwa anaendesha kugonganga uso kwa uso na gari dogo lililokuwa linaendeshwa na kijana mmoja wa palepale mtaani. Nakumbuka hata siku ya mazishi yake nilikuwepo na nilikuwa miongoni mwa watu waliokuwa wanamfariji Mathayo kwa kuondokewa na baba yake.
Kumbe wakati nikiendelea kutafakari hivyo, na yeye alinikumbuka ingawa alionekana ni kama ananifananisha, akawa ananitazama kwa kunikazia macho. Kiukweli niliogopa sana maana kwa tafsiri nyepesi, yule hakuwa binadamu wa kawaida bali mzimu kwa sababu mwenyewe alishakufa siku nyingi zilizopita.
Tuliendelea kutazamana kwa muda, akaanza kunionesha ishara kama ya kunikataza jambo ambalo sikulielewa, akawa anatumia mikono yake kunizuia, nikiwa naendelea kujaribu kutuliza kichwa ili nielewe alikuwa akimaanisha nini, nilishangaa ameyeyuka na kupotea kwenye upeo wa macho yangu.
Nilifikicha macho na kutazama tena pale alipokuwepo, hakuwepo. Nikabaki na maswali mengi yaliyokosa majibu. Nilijikuta nikiendelea na safari, nikazidi kupenya kwenye ule umati huku nikimtazama kila mmoja usoni, kwa mara nyingine nikajikuta nikishtuka mno baada ya kumuona mtu ambaye nilikuwa namfahamu.
Huyu hakuwa mwingine bali Hezron, tuliyekuwa tukicheza naye enzi za utoto ambaye naye kama ilivyokuwa kwa mzee Muyombe, alikuwa amefariki dunia miaka mingi iliyopita. Nakikumbuka vizuri kifo chake, alipoteza maisha baada ya kuzama baharini wakati akiogelea na ndugu zake, akazidiwa na mawimbi yaliyomvutia baharini na baadaye mwili wake kuokotwa ukiwa ufukweni, akiwa tayari amefariki dunia.
Nilishangaa imekuwaje nikutane na mtu mwingine ambaye naye alikuwa amepoteza maisha? Kingine kilichonishangaza, wakati anapoteza maisha, Hezron bado alikuwa kijana mdogo lakini siku hiyo, naye alionekana kuwa mkubwa, akiwa analinganalingana na mimi.
Sikuwahi kusikia wala kusoma mahali popote kwamba mtu akifa akiwa mtoto, anaendelea kukua huko kwenye maisha yake mengine mpaka hatua ya kufikia utu uzima, nilibaki nimepigwa na bumbuwazi. Cha ajabu, naye alikuwa akinioneshea ishara kama ya kunikataza jambo, sikuelewa pia ni jambo gani alilokuwa akinikataza.
Nilipoendelea kumtazama, naye aliyeyuka, nikaendelea kusonga mbele ambapo sasa nilianza kukutana na watu wengi niliokuwa nawafahamu. Miongoni mwao, wote walishatangulia mbele za haki kwa maana kwamba walishakufa. Kadiri nilivyokuwa nazidi kukutana nao ndivyo hofu ilivyokuwa inazidi kupungua ndani ya moyo wangu.
Kati ya yote, ilionesha watu wote niliokuwa nafahamiana nao walikuwa wakinikataza jambo ambalo bado sikuwa nimelielewa ni nini. Nikiwa naendelea kushangaashangaa, nilisikia mlio wa kengele ya ajabu, ikalia mfululizo kisha nikawaona watu wote wakiinamisha vichwa vyao chini, giza nene likaanza kutanda.
“Tuondoke, muda huu haufai kabisa wewe kuwepo huku, unaweza kupitiliza moja kwa moja,” niliisikia ile sauti kisha nikahisi nikishikwa kwa nguvu, kufumba na kufumbua nilikuwa nimerejea tena kule kwenye giza nilikokuwepo awali lakini bado niliendelea kuisikia ile sauti ya kengele ikilia.
Sikukumbuka nimeshuka saa ngapi kwenye treni na limeelekea wapi ila nilijikuta tu nikiwa nimesimama. Mlio wa ile kengele ulipokoma, nilianza kusikia sauti za watu wengi wakilia kwa sauti za ajabuajabu, wakionesha kwamba wapo kwenye maumivu makali.
“Mbona unaonesha kuwa na hofu kubwa moyoni mwako?” niliisikia ile sauti ikiniuliza, nikashindwa cha kujibu zaidi ya kujiinamia. Wale watu niliowaona kule, walinifanya nijawe na huzuni kubwa kwenye moyo wangu. Kumbukumbu ya misiba mingi niliyohudhuria tangu nikiwa mdogo ilianza kujirudia kichwani mwangu.
Kwa mbali nikaanza kuamini maneno ya Shenaiza kwamba huenda ni kweli nilikuwa nimekufa. Nilijisikia uchungu mkali sana ndani ya moyo wangu, nilitamani nirudi kwenye maisha yangu ya kawaida kwa sababu bado sikuwa nimekamilisha mambo mengi sana kwenye ulimwengu wa kawaida.
Kama kweli huo ndiyo ungekuwa mwisho wa maisha yangu, tafsiri yake ni kwamba ingekuwa sawa na kusema kwamba sijafanya chochote maishani mwangu, yaani nimezaliwa, nikaishi kisha nikafa bila kufanya jambo lolote la maana maishani mwangu, jambo ambalo liliniumiza sana.
“Najua unavyojisikia ndani ya moyo wako, nalijua hitaji la moyo wako na ndiyo maana nataka nikuoneshe kilichofanya uletwe huku. Kama nilivyosema, hukuletwa huku kwa bahati mbaya bali kuna kazi ambayo unatakiwa kwenda kuifanya.
“Kuna mamia ya watu wanaendelea kuwa wahanga kwa sababu ya tamaa za watu wachache. Maisha yako yalikuwa yamefikia mwisho lakini umshukuru Mungu wako kwa kupata nafasi hii, huwa siyo kila mtu anaipata.
“Tabia yako njema uliyoionesha katika maisha yako tangu ulipopata akili, ikiwemo kushika ibada, kufuata maandiko kwa kuacha kufanya yale yaliyokatazwa na kuishi katika misingi ambayo ndiyo hasa binadamu anayotakiwa kuishi, ni miongoni mwa sababu zilizofanya upate hii nafasi ya kurudi tena duniani.
“Ukirudi duniani, ukawe balozi mzuri wa kuwahamasisha binadamu wenzako ambao bado wapo hai juu ya kumuabudu Mungu, kuwapenda binadamu wenzao na kuwatendea mambo mema, kuacha kufanya maovu na maasi na kubwa zaidi, kwenda kuikomesha kazi inayofanywa na baba yake Shenaiza na watu wake, maelezo mengine utakuwa unaletewa hukohuko,” ilisikika ile sauti nzito ya kutisha.
Sikuelewa aliyekuwa anayasema hayo ni nani na pale nilikuwa wapi maana nilimsikia akizungumzia kuhusu kurejea duniani, akimaanisha kwamba pale hapakuwa duniani. “Umenielewaa?” ilihoji ile sauti na kusababisha ngurumo nyingi zianze kusikika kutoka kila upande, zikiambatana na upepo mkali uliokuwa ukivuma kwa kasi kubwa.
“Ndiyooo!” nilijibu kwa sauti iliyojaa hofu kubwa, iliyokuwa ikitetemeka ambayo kama nilivyoeleza kuanzia mwanzo, ilikuwa ikitokea moyoni na siyo mdomoni, nikasikia radi kubwa ikipiga jirani kabisa na pale nilipokuwepo, sikuelewa tena kilichoendelea.
Nilipokuja kushtuka, nilijikuta nikiwa nimelala kitandani, mapigo yangu ya moyo yakinienda mbio kuliko kawaida, nikiwa nimeunganishwa mashine ya kunisaidia kupumua huku mwili wangu ukiwa umeunganishwa na vifaa vingi vya kitabibu, milio ya mashine mbalimbali ikisikika ndani ya chumba kile ambacho hata bila kuuliza, niligundua kwamba ni wodini.
“Amefumbua macho! Dokta... amefumbua macho! Njooni haraka!”
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...