Saturday, August 12, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 12


ILIPOISHIA:
Nilikuja kugundua kuwa huenda tunaelekea Mwananyamala Hospitali baada ya kuumaliza Mtaa wa Makumbusho na kushika Barabara ya Mwananyamala, moyoni nilianza kugubikwa na maswali mengi, nilijiuliza kama ni kweli nilipelekwa katika Hospitali hiyo ilikuwa ni kufanya nini?
SASA ENDELEA…
“Tumekuleta huku hospitalini kwa sababu kwanza maelezo uliyoyatoa kituoni, kwa kiasi fulani yanapishana na maelezo aliyoyatoa huyu mgonjwa kwa sababu wewe ulisema humfahamu kwa undani zaidi ya kuanza kuwasiliana naye kwenye simu siku chache zilizopita.
“Lakini yeye amesema wewe ni mpenzi wake wa siku nyingi, mna mipango ya kufunga ndoa na tayari ana ujauzito wako,” alisema askari mmoja wa kike, miongoni mwa wale waliokuja kunichukua mahabusu, wakati huo tukiwa tayari tumeshawasili Hospitali ya Mwananyamala.
Akaendelea: “Lakini kingine ni kwamba amekataa kutoa ushirikiano wa kueleza nini kilichotokea mpaka wewe uwepo ndiyo maana tumekufuata, hutakiwi kuzungumza chochote, umenielewa?”
Nilitingisha kichwa kuonesha kukubali kile alichokisema. Mfululizo wa matukio ya kushangaza ulikuwa unaendelea, nilijiuliza iweje tena Shenaiza awaeleze polisi kwamba mimi nilikuwa mpenzi wake na kwamba tulikuwa na mipango ya kufunga ndoa?
Yote tisa, kumi nilijiuliza iweje awaambie kwamba alikuwa na ujauzito wangu wakati hatukuwahi kukutana kimwili hata mara moja? Kama kweli alikuwa mjamzito, mimi nilikuwa nahusikaje? Nilikosa majibu.
“Jamal! Ooh my God! Thanks for coming my dear,” (Jamal! Ooh Mungu wangu, ahsante kwa kuja mpendwa wangu) alisema Shenaiza kwa sauti ya chini akionesha kwamba yupo kwenye maumivu makali, alizungumza kwa Kiingereza kizuri huku akitanua mikono yake kama ishara ya kunitaka nimkumbatie.
Sikuwahi kumsikia akizungumza Kiingereza, nikabaki na swali jingine lakini sikutaka kumuonesha chochote, nikalilazimisha tabasamu usoni kwangu, nikamuinamia pale kitandani alipokuwa amelala, dripu ikiendelea kutiririka kwa kasi kuingia mishipani mwake, nikamkumbatia, akanibusu shavuni na kuning’ang’ania kifuani kwake, tukiwa kwenye hali hiyo alinibusu mdomoni na kunifanya nijisikie aibu ndani ya moyo wangu.
Kwa jinsi alivyokuwa akinidekea, mtu yeyote angeweza kuamini kwamba kweli sisi ni wapenzi wa muda mrefu, nikageuka na kumtazama yule askari ambaye moyoni ni kama alikuwa anasema ‘unabisha nini sasa? Kama siyo mpenzi wako angekubusu mdomoni?’.
“Please help me Jamal, they want to kill me! You are my only savior,” (Tafadhali nisaidie Jamal, wanataka kuniua! Wewe ndiyo mkombozi wangu wa pekee) alisema Shenaiza kwa sauti ya chini akiwa bado amenikumbatia. Japokuwa yule askari alikuwa mita chache tu kutoka pale kitandani, hakuweza kusikia chochote.
Kwa kuwa nilishaambiwa sitakiwi kuzungumza chochote, sikumjibu chochote zaidi ya kumtazama usoni huku nikiwa na shauku kubwa ya kutaka kujua hao anaosema wanataka kumuua ni akina nani na ilikuwaje mpaka watake kumuua?
“Inatosha sasa, hebu kaa pembeni. Binti, naamini sasa utatoa ushirikiano maana uliyekuwa unamtaka tumeshamleta,” alisema yule askari huku akinielekeza kukaa pembeni ya kitanda cha mgonjwa, akarudi kinyumenyume na kufungua mlango, askari wengine watatu, akiwemo yule aliyenihoji mimi wakaingia na kusimama kwa kutuzunguka.
Yule askari wa kike akawaeleza jambo kwa sauti ya chini ambayo mimi na Shenaiza hatukusikia kisha tukawaona wote wakitoka, akabaki yule mmoja aliyenihoji mimi siku iliyopita, mkononi akiwa na ‘diary’, akavuta kiti na kukisogeza karibu na pale Shenaiza alipokuwa amelala.
“Si umeshaambiwa maelezo yote kwamba hutakiwi kuzungumza chochote?” yule askari ambaye nilishamtambua kwamba ni mpelelezi, aliniambia.
“Ndiyo.”
“Oke vizuri, binti unaendeleaje?”
“Naendelea vizuri,” alijibu Shenaiza, akamwambia anataka kuanza upya kumhoji na anaamini atatoa ushirikiano kwa sababu mimi nilikuwepo.
“Jina lako kamili unaitwa nani?”
Shenaiza alinitazama kabla ya kuanza kujibu, akanionesha ishara ambayo sikuielewa, nikabaki kumtazama tu huku na mimi nikiwa na shauku kubwa ya kutaka kusikia maelezo yake maana kiukweli hata mimi sikuwa namfahamu kwa undani.
“Shenaiza Petras Loris,” alijibu Shenaiza. Nilishangazwa na jina lake, sikuwahi kusikia Mtanzania yeyote akiwa na jina hilo, akilini nikaanza kupata majibu kwamba kile nilichokuwa nakihisi awali kwamba msichana huyo hakuwa Mtanzania kutokana na mwonekano wake kilikuwa kweli.
Yule askari aliendelea kumhoji maswali kama polisi wote wanavyofanya, akafikia swali la kabila na utaifa wake, Shenaiza akanitazama tena na kushusha pumzi ndefu kisha akamjibu:
“Kabila langu ni Aethikes,” alijibu, yule askari akapigwa na butwaa na kuacha kuandika, akamtazama Shenaiza kwa muda kisha akanigeukia na mimi, mshangao aliokuwa nao ulikuwa sawa na niliokuwa nao mimi.
‘Bini, hebu kuwa ‘serious’, hilo ndiyo kabila gani? Tangu nianze kufanya kazi huu mwaka wa kumi sasa sijawahi kusikia kabila kama hilo hapa Tanzania, hebu taja kabila lako,” alisema yule askari kwa sauti iliyoonesha kutokuwa na hata chembe ya masihara.
“Mimi siyo Mtanzania, natokea Greece (Ugiriki), asili yetu ni Attica, baba yangu amezaliwa na kukulia kwenye Jiji la Athens lakini mama yangu ni mpare wa Mtae, Lushoto mkoani Tanga ndiyo maana unaona naweza kuzungumza Kiswahili vizuri,” alisema msichana huyo huku akionesha kujiamini mno.
Nilimuona yule askari akiandika maelezo hayo kwenye ‘diary’ yake, akaendelea kumhoji maswali mengine ambapo niligundua kwamba msichana huyo, alikuwepo nchini kisheria na kubwa zaidi, kumbe alikuwa ni mwanafunzi wa mwaka wa kwanza katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Mahojiano yaliendelea, kikafikia kipengele cha muhimu ambacho ndiyo hasa nilichokuwa nakisubiri kwa shauku kubwa, cha kutaka kujua nini kilitokea mpaka msichana huyo mrembo akajeruhiwa vibaya na kwenda kulazwa Hospitali ya Amana kabla ya mimi kumsaidia kutoroka mpaka nyumbani kwangu, na kile kilichokuwa kimetokea nyumbani kwangu usiku.
Shenaiza alivuta pumzi ndefu baada ya kuulizwa swali hilo, akazishusha kisha akatulia, ukimya mkubwa ukapita kati yetu mle wodini. Ilibidi yule askari avunje ukimya na kurudia tena kumuuliza swali lile lakini badala ya kutoa majibu kama alivyokuwa akifanya kwa maswali yote, alikaa kimya huku machozi mengi yakimtoka na kulowanisha uso wake.
‘Kijana hebu naomba utupishe mara moja, toka nje nitakuita,” alisema yule askari, ikabidi nitii, nikawaacha wenyewe wawili mle wodini.
Je, nini kitafuatia? Usikose Jumatatu kwenye Gazeti la Championi Jumatatu.

  

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...