Thursday, August 31, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 26


ILIPOISHIA:
“Jamal! Jamal! Jamal!” nilishtuka baada ya kuisikia tena ile sauti nzito ya kutetemeka, iliyoniita kwa mara ya kwanza kabisa, ikiniita tena, ikafuatiwa na vicheko vya kutisha vya watu wengi, nikawa nageuka huku na kule lakini sikuona chochote zaidi ya giza nene, hofu kubwa ikatanda moyoni mwangu.
SASA ENDELEA...
“Hujafika hapa kwa bahati mbaya Jamal, ilikuwa ni lazima uje huku ili ufunuliwe haya mambo ambayo kwa akili ya kawaida usingeweza kuyajua, hebu nifuate,” ilisikika ile sauti nzito ya kutetemeka na kutisha, nikiwa sielewi ni nani aliyekuwa akizungumza nami na alikuwa anataka nimfuate wapi, nilishtukia nikishikwa mkono.
Kufumba na kufumbua, tulitokezea sehemu ambayo kulikuwa na watu wengi wa kila aina wamekusanyika. Wengine walikuwa wamekaa, wengine wamesimama, wengine wamejiinamia na wengine wamelala.
Walikuwa wengi mno, wakubwa kwa wadogo, vijana kwa wazee, wanaume kwa wanawake. Cha ajabu, licha ya wingi wao, wote walikuwa kimya kabisa, hakuna aliyekuwa anazungumza chochote, sauti pekee zilizokuwa zinasikika zilikuwa ni za watu wachache waliokuwa wakigugumia kuonesha wapo kwenye maumivu makali.
“Hapa ni wapi na hawa ni akina nani?” niliuliza lakini hakukuwa na mtu wa kunijibu, yule mtu aliyenileta sikumuona tena, nilijikuta nikiwa peke yangu lakini kukawa na nguvu fulani iliyokuwa inaniongoza sehemu ya kwenda.

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 34



ILIPOISHIA:
Alipofikisha tatu, nilifumba macho, nikashtukia ghafla tumehama pale tulipokuwa na kwenda upande wa pili, kule barabarani ambako watu wengi walikuwa wamesimama wakishangaa, tukajichanganya na wale watu.
“Hebu angalia wanachokishangaa,” alisema huku akinitaka nitazame pale tulipokuwa tumekaa awali. Macho yalinitoka nikiwa ni kama siamini.
SASA ENDELEA...
Watu wawili, mmoja akionesha kuwa mwanamke na mwingine mwanaume, wakiwa watupu kabisa huku miili yao iking’aa sana, walikuwa wamekaa kwenye msingi wa nyumba, wakiwa wanazungumza. Macho ya kila mmoja yalikuwa yaking’aa sana na nyuso zao zilikuwa na gizagiza fulani ambalo lilifanya iwe vigumu kwa watu kuwatambua sura zao.
“Hivi ndivyo tulivyokuwa tukionekana ndiyo maana unaona hawa watu wote wamekusanyika hapa,” alisema Isri huku akiniegamia.
Nilibaki nimepigwa na butwaa huku nikiwatazama wale watu ambao wala hawakuwa na taarifa kwamba tulikuwa tumeshajichanganya nao. Nilitamani kumuuliza Isri kwamba sasa iweje wale watu wawe wanaendelea kutuona wakati tulishahama na kujichanganya nao? Kabla hata sijamjibu, ni kama alizisoma hisia zangu, akaniambia kile walichokuwa wakiendelea kukiona, ilikuwa ni kiini macho.

Wednesday, August 30, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 25


ILIPOISHIA:
Harakaharaka, huku akilia, aliwaita walinzi ambao nao walimuita daktari wa familia hiyo, muda mfupi baadaye wote wakawa wamejaa ndani ya chumba hicho wakijaribu kuokoa maisha ya msichana huyo lakini ilionesha kwamba tayari walikuwa wamechelewa.
SASA ENDELEA...
Shenaiza alikuwa akitapatapa, akirusharusha mikono na miguu, mapovu mengi yaliyochanganyikana na damu yakimtoka mdomoni na puani, harakaharaka Shenaiza alitolewa kwenye chumba alichokuwa amefungiwa na kulazwa juu ya kitanda cha magurudumu, akakimbizwa kwa kasi mpaka nje na kupakizwa kwenye gari.
Muda mfupi baadaye, gari lililombeba lilikuwa tayari lipo barabarani, likikimbia kwa kasi kubwa, taa zote za mbele zikiwa zimewashwa huku yule daktari akiwa bize kuhakikisha anaokoa maisha ya Shenaiza.
Japokuwa baba wa msichana huyo mrembo hakuwepo nchini kwa muda huo, tayari taarifa zilimfikia huko alikokuwa juu ya kilichomtokea binti yake.
Naye akajikuta akichanganyikiwa mno kwani Shenaiza alikuwa mtu muhimu sana kwake. Bila yeye, mambo yake mengi yangekwama, jambo ambalo hakuwa tayari kuona linatokea. Muda hohuo aliwapigia simu wasaidizi wake na kuwaambia ni lazima wafanye kila kinachowezekana kuhakikisha anapona.
Baada ya kufikishwa hospitalini, harakaharaka Shenaiza alilazwa juu ya kitanda chenye magurudumu, akakimbizwa kupelekwa kwenye wodi ya wagonjwa mahututi, madaktari kadhaa, wakisaidiana na yule daktari wa familia, walianza kuhaha kuhakikisha wanaokoa maisha ya msichana huyo.
*** 
“Lakini mimi sijafa Shenaiza, mimi niko hai.”
“Ungekuwa hai ndiyo ungekuwa huku? Acha kujidanganya Jamal!”
“Hapana sijafa! Mimi sijafa! Niko haiii,” nilisema kwa sauti kubwa iliyofuatiwa na kilio.
“Sasa unalia nini Jamal? Kwani kufa ni jambo la ajabu? Mbona mimi mwenyewe nimeamua kuyakatisha maisha yangu?”

The Graves of the Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia) - 33


ILIPOISHIA:
Muda huo kwa makadirio ilikuwa ni kama saa nane za usiku maana kuna sehemu nilipita nikasikia redio kwa mbali ikitangaza kwamba ni saa nane kasoro za usiku.
“Mbona umeshtuka Togo!” alisema huku akinisogelea. Siwezi kuficha, mshtuko nilioupata nusura nidondoke na kuzimia.
SASA ENDELEA...
Alikuwa ni yule msichana ambaye mchana wa siku iliyopita alinifia gesti tukiwa kwenye mechi ya kirafiki na kunisababishia matatizo makubwa mpaka nikapelekwa mahabusu nikikabiliwa na kesi kubwa ya mauaji.
Nilitaka kukimbia nikahisi mwili wangu ukiishiwa nguvu, nilitaka kupiga kelele lakini sauti ikawa haitoki, nikabaki nimesimama palepale nikitetemeka kama mbwa mbele ya chatu, akawa ananishangaa usoni kama anayejiuliza maswali mengi yaliyokosa majibu.
“Wewe si ulikufa wewe?” nilisema huku safari hii miguu yangu ikiwa imeanza kupata nguvu, nikawa narudi nyuma nikiangalia upenyo wa kukimbia. Ni kama alishagundua ninachotaka kukifanya, akacheka na kunisihi nisikimbie bali kuna jambo la muhimu anataka kuniambia.
Maneno yake yaliingilia sikio moja na kutokea la pili, akili yangu ilinifanya niamini kwamba hakuwa yeye bali mzimu wake, akawa anazidi kunisogelea mwilini.
“Najua unafikiri labda mimi ni mzimu, siyo, nipo hai wala sijafa na leo nitakutajia mpaka jina langu,” aliniambia huku akizidi kunisogelea. Mazungumzo yake hayakuonesha kama alikuwa mzimu au alikuwa na nia mbaya na mimi lakini bado niliendelea kurudi nyuma, naye akawa anazidi kunifuata.

Monday, August 28, 2017

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 32


ILIPOISHIA:
Wote waliacha kila walichokuwa wanakifanya, wakawa wananitazama kwa macho makali. Sikuelewa nini hasa kimetokea, wakati nikiendelea kuwatazama vizuri kwa mara ya pili, kuna jambo moja lilinishtua mno mpaka nikajikuta nimetoa mkono mfukoni, giza likarudi kama lilivyokuwa mwanzo.
SASA ENDELEA...
Japokuwa kulikuwa na giza, niliweza kuonamacho ya wale watu yaking’ara kama wanyama wakali wa porini, nikawa najilaumu kwa kile nilichokifanya. Hata sijui nini kilitokea kwani kuanzia mwanzo nilikuwa nimejiapiza kwamba siku hiyo sitaleta ujuaji wowote mbele ya watu hao lakini cha ajabu, ndani ya muda mfupi tu, tayari nilishakuwa nimewekwa mtu kati.
Sikujua safari hii wataniadhibu vipi lakini niliamua kupiga moyo konde, liwalo na liwe. Bado nilikuwa najiuliza maswali mengi kuhusu kile kilichokuwa kwenye mfuko wangu, sikujua ni nini na kilikuwa na uhusiano gani na ule mwanga uliotokeza ghafla mle ndani ya mahabusu.
Sijui nilipata wapi ujasiri lakini nilijikuta nikiingiza tena mkono taratibu mfukoni, nilipokigusa tu kile kitu mle mfukoni, ule mwanga ulirudi tena vilevile, wale watu ambao safari hii walikuwa wamejikusanya na kutengeneza kama nusu duara hivi, waliinua wote shingo zao na kunigeukia tena, nikakishika kile kitu kwa nguvu huku na mimi nikiwa nawatazama.
Katika hali ambayo sikuitegemea, nilishangaa wa kwanza akisimama na kukimbilia kwenye ile kona alipokuwa amekaa yule mahabusu ambaye awali alikuwa akipiga kelele. Safari hii alikuwa amelala, tena kwa kuinamisha kichwa mbele, katikati ya miguu yake.
Nikamuona yule mtu wa kwanza, mikono yake akiwa amejiziba sehemu nyeti, akisogea mpaka kwenye kona, alipoikaribia, aligeuka na kuanza kutembea kinyumenyume, akamkanyaga yule mahabusu kisha nikashangaa akipotelea kwenye ukuta.

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 24


ILIPOISHIA:
Treni ilizidi kushika kasi, ikafika kipindi nikawa nahisi kwamba haikanyagi kwenye reli bali inapaa angani kwa jinsi ilivyokuwa ikienda kasi. Ghafla, nilipogeuka huku na kule, nilishtuka kugundua kwamba nilikuwa nimebaki peke yangu kwenye treni hilo, sikukumbuka kama kuna sehemu lilisimama, nikawa najiuliza wale abiria wengine wameenda wapi?
SASA ENDELEA...
Kuna wakati nilihisi pengine huenda nilikuwa kwenye ndoto lakini bado sikuwa na uwezo wa kuthibitisha kwamba ile ilikuwa ni ndoto, maisha halisi au kitu gani, kila kitu kilikuwa gizani. Treni lilizidi kushika kasi, moshi mwingi ukiwa unazidi kuingia ndani na kufanya hata ule mwanga hafifu niliokuwa nauona awali nao umezwe na moshi huo mweusi.
Ghafla, nilihisi kama naguswa na mtu pembeni yangu, nikajikuta nikiruka kwa hofu kubwa, nilipogeuka na kumtazama aliyenigusa, alionesha ni mwanamke kwa jinsi alivyokuwa amevaa lakini uso wake alikuwa ameuinamisha chini.
“Jamal! Jamal, ni wewe?” alisema yule mtu kwa sauti ya chini lakini ambayo ilisikika vizuri licha ya kelele ya vyuma vya treni lile, muungurumo mkubwa na upepo uliokuwa unavuma.
Badala ya kuitikia, niligeuka na kumtazama kwa hofu kubwa mno, yeye wala hakugeuka kunitazama zaidi ya kuendelea kujiinamia vilevile, akisubiri majibu kutoka kwangu. Licha ya zile kelele na yeye mwenyewe kuzungumza kwa sauti ya chini, bado niliweza kuitambua vyema sauti hiyo, haikuwa ngeni kabisa masikioni mwangu.
“Mbona hunijibu!” aliuliza tena lakini tofauti na mwanzo, sauti yake ilisikika kwa nguvu ikiambatana na mwangwi ambao uliyaumiza masikio yangu.

Saturday, August 26, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 23


ILIPOISHIA:
“Mzimu? Mzimu gani wakati sasa hivi ni mchana?”
“Nilikuwa nimelala nikatokewa na mzimu wa marehemu Jamal!”
“Mh! Au unaanza kuchanganyikiwa mwenzetu? Jamal gani unayemzungumzia?”
SASA ENDELEA...
“Nimeota kabisa naongea na Jamal wakati ameshafariki. Ninachosema ni kweli kabisa, wala siyo kwamba nimeanza kuchanganyikiwa,” Shenaiza alizidi kusisitiza lakini hakuna aliyemuamini.
Tangu aende kuchukuliwa kwa nguvu na walinzi wa baba yake na kurejeshwa kwenye makazi ya siri ya familia yao, Kurasini, alikuwa ni kama amechanganyikiwa. Muda mwingi alikuwa ni mtu wa kulia na kuijutia nafsi yake huku akimlaumu baba yake kwamba alikuwa akimuonea kwa yote aliyokuwa akimfanyia.
Alipokuwa akizidi kusumbua, daktari maalum wa familia hiyo, alikuwa akipewa kazi ya kumdunga dawa za usingizi zilizomfanya alale muda mrefu. Hali hiyo ilimfanya kwa kiasi kikubwa akose hata nafasi ya kufuatilia kilichokuwa kinaendelea kuhusu Jamal, kitu pekee alichokuwa anakijua akilini mwake, ni kwamba kijana huyo alikuwa amefariki dunia baada ya lile tukio ambalo yeye ndiye aliyekuwa chanzo.

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 31


ILIPOISHIA:
Nikiwa bado naendelea kumtazama kwa jicho baya, mara nilishtuka kusikia vishindo viwili vikubwa juu ya bati, kama vile nilivyokuwa navisikia usiku uliopita, moyo wangu ukapatwa na mshtuko mkubwa mno. Mara nilisikia vishindo vingine vitatu mfululizo, nikawa nimepigwa na butwaa huku macho yangu yote yakiwa juu.
SASA ENDELEA...
Kwa jinsi vishindo hivyo vilivyokuwa vikisikika, ilikuwa ni kama kuna watu wanaruka kutoka angani na kudondokea juu ya bati kwani vilikuwa vizito mno. Safari hii nilitaka kuwa makini kushuhudia je, kile ninachokisikia mimi, kila mtu anasikia hivyohivyo maana nilishahisi kuna kitu hakipo sawa kwangu lakini baba hataki kuniambia ukweli.
Baada ya vishindo vile vya kama watu au vitu kutua juu ya bati, mara vilianza kusikika vishindo vya mtu akitembea juu ya bati.
Unajua haya matukio kama hujawahi kutokewa nayo, huwezi kuelewa ile hofu unayokuwa nayo lakini kiukweli, ni bora tu uwe unasikia lakini yasikutokee. Hakuna hofu inayotesa kama hofu ya matukio kama haya yanapokutokea, hasa usiku kama huo.
Nilijikuta nywele zikisisimka vibaya mno, mapigo ya moyo yakawa yananienda kwa kasi maana sikujua safari hii wanakuja kwa mtindo gani. Vishindo viliendelea kusikika kisha kikasikika kishindo kingine ambacho kwa makadirio yangu ya haraka, kilikuwa ni kwenye sakafu ya mle mahabusu.

Friday, August 25, 2017

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na hatia)- 30



ILIPOISHIA:
Kwa bahati nzuri, nilipofika pale mapokezi, yule dada hakuwepo, nikatoka kimyakimya mpaka nje, nikaelekea lilipo geti kubwa huku nikijitahidi kuvaa tabasamu la uongo ili walinzi wa hoteli hiyo wasishtukie chochote.
“Aroo! We kijana... Aroo wewe,” nilisikia sauti ya mlinzi wa nje ya geti la hoteli hiyo akiniita, moyo ukalipuka paah!
SASA ENDELEA...
“Unaenda wapi?”
“Naenda dukani afande.”
“Mwenzako umemuacha wapi?”
“Yupo ndani, narudi sasa hivi, naenda kununua kinga.”
“Mbona kama una wasiwasi?” alisema yule mlinzi huku akinisogelea. Licha ya kujaribu kucheza na akili zake, ni kama alishashtukia jambo kwa jinsi nilivyokuwa na hofu. Mtu kukufia chumbani, usifanye mchezo.
Hata kama ulikuwa jasiri vipi, lazima uchanganyikiwe. Hicho ndicho kilichonitokea. Hofu ilishindwa kujificha kwenye macho yangu, nikawa nakwepesha macho kwa sababu niliamini yule mlinzi kwa jinsi alivyonishupalia, angeweza kugundua kitu. Nilitamani kufanya kitu lakini sikuwa na uwezo, harufu ya jela ikaanza kunukia.
“Mkazie macho usoni,” ile sauti ya ajabu ya baba, ilisikika masikioni mwangu, nikageuka huku na kule lakini baba hakuwepo eneo hilo. Kwa kuwa mara zote ilikuwa ikinisaidia, nilifanya kama nilivyoelezwa.
Nilimkazia macho yule mlinzi, na yeye akanitazama. Ghafla nikashangaa anakuwa mpole ghafla, mwanzo alikuwa amekunja sura lakini ghafla alitabasamu. Niliendelea kumkazia macho.

Thursday, August 24, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 22


ILIPOISHIA:
“Mzimu? Mzimu gani wakati sasa hivi ni mchana?”
“Nilikuwa nimelala nikatokewa na mzimu wa marehemu Jamal!”
“Mh! Au unaanza kuchanganyikiwa mwenzetu? Jamal gani unayemzungumzia?”
SASA ENDELEA...
“Nimeota kabisa naongea na Jamal wakati ameshafariki. Ninachosema ni kweli kabisa, wala siyo kwamba nimeanza kuchanganyikiwa,” Shenaiza alizidi kusisitiza lakini hakuna aliyemuamini.
Tangu aende kuchukuliwa kwa nguvu na walinzi wa baba yake na kurejeshwa kwenye makazi ya siri ya familia yao, Kurasini, alikuwa ni kama amechanganyikiwa. Muda mwingi alikuwa ni mtu wa kulia na kuijutia nafsi yake huku akimlaumu baba yake kwamba alikuwa akimuonea kwa yote aliyokuwa akimfanyia.
Alipokuwa akizidi kusumbua, daktari maalum wa familia hiyo, alikuwa akipewa kazi ya kumdunga dawa za usingizi zilizomfanya alale muda mrefu. Hali hiyo ilimfanya kwa kiasi kikubwa akose hata nafasi ya kufuatilia kilichokuwa kinaendelea kuhusu Jamal, kitu pekee alichokuwa anakijua akilini mwake, ni kwamba kijana huyo alikuwa amefariki dunia baada ya lile tukio ambalo yeye ndiye aliyekuwa chanzo.
“Muiteni dokta.”
“No! I dont need any more sedatives please, im not out of my mind,” (Hapana! Sihitaji tena kuchomwa dawa za usingizi, mimi sijachanganyikiwa) alipiga kelele Shenaiza lakini haikusaidia kitu, muda mfupi baadaye, daktari wao aliingia akiwa na bomba la sindano na kichupa cha dawa mkononi kilichokuwa na maandishi yaliyosomeka Diazepam, akiwa ameongozana na wanaume wawili wenye miili mikubwa.

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 29



ILIPOISHIA:
Nikiwa bado naendelea kuugulia, nilisikia ndugu yangu mmoja akiniita kutokea dirishani, nikafunua pazia na kuchungulia nje. Sikuyaamini macho yangu baada ya kumuona akiwa na yule msichana tuliyesafiri naye, harakaharaka nikafungua dirisha huku tabasamu pana likiwa limechanua kwenye uso wangu.
SASA ENDELEA...
“Mambo Togo?”
“Safi, karibu,” nilisema huku nikitazama huku nakule. Yule ndugu yangu alikuwa amesimama pembeni akikutazama kwa zamuzamu.
“Samahani nina maongezi kidogo na wewe,” alisema. Kwa hali niliyokuwa nayo, nilikuwa nikifikiria jambo moja tu kutokakwake, mapenzi.
“Nisubiri kwa kule mbele,” nilimuelekeza huku harakaharaka nikitoka na kuelekea bafuni. Nilijimwagia maji ya baridi kwa wingi ili angalau nitulie kisha nikarudi chumbani na kuvaa nguo.
Nilijitazama tena kwenye kioo, bado nilikuwa na alama za kuvilia damu usoni lakini sikujali, akili yangu ilikuwa ikihitaji kitu kimoja tu kwa wakati huo. Nilitoka kimyakimya bila kumuaga mtu yeyote mpaka nje.
Nikamfuata yule ndugu yangu na kumwambia kwamba iwe siri yetu nitampa zawadi, nikamsisitiza kwamba asimwambie mtu yeyote. Alikubali, nikamshukuru nakumfuata yule msichana ambaye alionesha kuwa na shauku kubwa ya kuonana na mimi.
Tulitoka mpaka nje kabisa, sehemu ambayo mtu yeyote aliyekuwa ndani asingeweza kutuona, akanikumbatia kwa nguvu na kunibusu shingoni. Nilijikuta nikisisimka mno, nikawa nachekacheka tu mwenyewe.
Aliniambia kuna mahali anataka rtwende pamoja kwa sababu alikuwa na jambo muhimu lililokuwa likimsumbua ndani ya moyo wake. Nilimuuliza amepata wapi ujasiri wa kuingia mpaka kule ndani? Akaniambia ilikuwa ni muhimu sana kuonana na mimi na ndiyo maana hakujali chochote.

Wednesday, August 23, 2017

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 28


ILIPOISHIA:
Baba alitoa kichupa kilichokuwa na unga mweusi lakini kabla hajafanya chochote, aliniambia nikajitazame kwenye kioo kilichokuwa humo chumbani.
“Mungu wangu,” nilisema kwa mshtuko usio wa kawaida.
SASA ENDELEA...
Uso wangu ulikuwa umebadilika na kuwa mweusi tii kama mkaa. Kilichoonekana ilikuwa ni macho na meno tu. Nilishindwa kuelewa kwa nini mimebadilika na kuwa vile, sikujua kama ni yale makofi ya nguvu niliyopigwa au ni nini.
“Usishtuke, na huo mchezo wako ukiendelea nao yatakufika makubwa zaidi, yaani unaonekana umeonja asali na sasa unataka kuchonga mzinga kabisa. Hukuwa na mambo ya kupenda wanawake, nini kimekusibu?” alisema baba lakini maneno yake yaliingilia sikio moja na kutokea jingine.
Akili yangu ilikuwa ikiwaza kuhusu mabadiliko yaliyotokea kwenye uso wangu. Nilishindwa kuelewa itakuwaje kama nitaendelea kuwa hivyo, nilijikuta nikiishiwa nguvu kabisa, nikakaa chini huku hofu kubwa ikiwa imetanda moyoni mwangu.
“Si naongea na wewe?” alinihoji baba huku akiwa amekishika kile kichupa, sikumjibu chochote kwa sababu akili yangu ilikuwa ikiwaza mambo mengine tofauti kabisa. Suala la kuacha kufaidi penzi la Rahma halikuwepo kabisa kichwani mwangu, kwa sababu hata wao wenyewe walijaribu kulizuia lakini kilichotokea kila mmoja akawa shahidi.

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 21


ILIPOISHIA:
Nikiwa naendelea kulia, nilipaliwa na mate, hali iliyofanya nikohoe mfululizo, ajabu zaidi, na ule mwili wangu pale kitandani ukakohoa, madaktari wakazidi kupigwa na butwaa, wakawa wanatazamana wakiwa ni kama hawaamini kilichokuwa kinatokea.
SASA ENDELEA...
“Amerejewa na fahamu zake, amezinduka,” alisema daktari mmoja kwa sauti, nikaona pilikapilika zimeanza tena kupamba moto mle wodini. Daktari mmoja akaja kunipima mapigo ya moyo huku akiwatazama wenzake, nikamuona akitingisha kichwa.
Niliendelea kupewa matibabu ya uhakika, kila mmoja akawa anachakarika kwa nafasi yake. Nilimuona daktari mmoja akifungua mlango na kutoka nje, akasogea mpaka pale akina Raya walipokuwa wamekusanyika.
Nikamuona akizungumza nao mambo fulani, ghafla nikamuona Raya akimrukia mwilini kwa furaha, akamkumbatia kwa nguvu kisha akainua mikono juu kama ishara ya kumshukuru Mungu.
Japokuwa sikuwa nimesikia walichokuwa wanakizungumza, niliamini kwamba lazima yule daktari atakuwa ameenda kuwaambia kwamba sikuwa nimekufa kama wanavyofikiria. Nilijikuta nikisisimka sana, yale machozi yaliyokuwa yananitoka yakaacha, nikawa namtazama Raya alivyofurahi kama mwendawazimu.

Tuesday, August 22, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 20


ILIPOSHIA:
Mpaka muda huo nilikuwa nimeshindwa kabisa kujizuia nisiendelee kuporomokea kule chini, kwa mbali nikaanza kuliona shimo kubwa ambalo ukubwa wake hata sijui nifananishe na nini lakini kwa kifupi lilikuwa kubwa mno, lisilo na mwisho, moto mkali ukiwa unawaka ndani yake. Kibaya zaidi, na mimi nilikuwa nikiendelea kuporomoka kuelekea ndani ya shimo hilo, nikajua huo ndiyo mwisho wangu.
SASA ENDELEA...
“Jamal! Jamal! Don’t go my love, come back to me! Come back Jamal,” (Jamal! Jamal! Usiende mpenzi wangu, rudi kwangu! Rudi kwangu Jamal) wakati nikiendelea kuporomokea kule kwenye lile shimo kubwa lililokuwa na moto mkali ambao siwezi kuuelezea, nilisikia sauti ikiniita.
Tofauti na sauti za kutishatisha nilizokuwa nikizisikia, hii ilionesha dhahiri kwamba siyo ngeni masikioni mwangu. Ilikuwa ni sauti ambayo niliitambua kuwa ni ya Raya, msichana aliyetokea kunipenda kwa moyo wake wote.
Raya alikuwa akipaza sauti huku akilia, maneno aliyokuwa akiniambia yalinichoma sana moyoni mwangu.
Katika hali ambayo sijui niielezeeje, nilijikuta nikipata nguvu kubwa kutoka ndani, nikajipindua kwa nguvu na kujikuta ile kasi ya kuporomokea kule chini inapungua, nikazidi kufurukuta kupambana na ile nguvu kubwa iliyokuwa inanivuta na hatimaye nikajikuta nikiangukia sehemu nyingine tofauti kabisa na kule nilikokuwa nikielekea.

Monday, August 21, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 19


ILIPOISHIA:
Kuna wakati hofu ilinizidi na kutaka nigeuze nilikotoka lakini kitu ndani ya moyo wangu kikaniambia nizidi kusonga mbele. Kadiri nilivyokuwa nazidi kusonga mbele ndivyo zile sauti zilivyokuwa zinazidi kuongezeka, nikazidi kutetemeka kwa hofu huku nikiwa sijui nini itakuwa hatma yangu.
SASA ENDELEA...
Sauti zilizidi kuongezeka, nikawa nasikia sauti nyingine zikiugulia maumivu makali mno, nilitamani nione nini kilichokuwa kinaendelea lakini sikuweza kutokana na lile giza. Ilifika mahali ikabidi niwe natembea kwa uangalifu sana kwani nilihisi nilikuwa nikipita jirani kabisa na wale watu waliokuwa wakilia kwa maumivu makali.
Kiasili mimi ni mwoga sana kiasi kwamba nikiwa nyumbani kwangu, hata panya akipita darini kwa kasi, lazima nitashtuka sana lakini nashangaa siku hiyo kadiri muda ulivyokuwa unasonga mbele ndivyo hofu ilivyokuwa inazidi kupungua.
Haikuwa rahisi kupita sehemu ambayo unasikia kabisa wenzako wanalia kwa kusaga meno kwa maumivu makali kama ile. Ukiachilia mbali sauti hizo za watu, kulikuwa pia na sauti za watoto wachanga waliokuwa wamepamba moto kulia, ungeweza kudhani wamelazwa kwenye siafu.

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 18


ILIPOISHIA:
Nakumbuka neno la mwisho nililofanikiwa kulisema, ingawa ilikuwa ni kwa taabu kubwa kutokana na midomo yangu kuwa mizito, ilikuwa ni: Mungu nisaidie! Nikafumba macho na giza totoro likatawala kila sehemu, sikuelewa tena kilichoendelea baada ya hapo!
SASA ENDELEA...
Katika hali ambayo sikuitegemea na ambayo mpaka leo huwa siwezi kuifafanua, muda mfupi baadaye nilijikuta nikizinduka lakini nikiwa kwenye hali ya tofauti kabisa. Nilizinduka nikiwa palepale nilipokuwa nimelala awali lakini katika hali ya ajabu, nilikuwa mwepesi sana.
Nikajikuta nikianza kupaa taratibu kuelekea juu. Nikiwa juu kidogo, niligeuka na kutazama pale nilipokuwa nimeangukia, nikashangaa kuona bado mwili wangu ulikuwa umelala palepale, damu nyingi zikiendelea kutoka kwenye jeraha la kifuani, tena safari hii zikitoka kwa mabongemabonge.
“Mungu wangu! Hiki ni kitu gani tena?” nilijikuta nikisema kwa sauti ya chini, ungeweza kudhani nilikuwa kwenye ndoto lakini haikuwa hivyo. Nilijiuliza kama mwili wangu bado ulikuwa pale chini, mimi niliyekuwa napaa nilikuwa ni nani? Sikupata majibu.
Niliendelea kupaa kuelekea juu mpaka nikafikia umbali wa mita kadhaa, ulioniwezesha kuona vizuri kila kitu kilichokuwa kinaendelea eneo la tukio. Niliwaona watu wakizidi kumiminika kwa wingi eneo la tukio, wengine wakishika vichwa vyao baada ya kuuona mwili wangu ukiwa kwenye hali ile.
Hali hiyo ya ajabu iliendelea kunitokea, nakumbuka niliendelea kushuhudia kila kitu kilichoendelea, jinsi mwili wangu ulivyochukuliwa kutoka eneo la tukio na kukimbizwa mpaka hospitali ambako nako niliona madaktari walivyokuwa wakichakarika kuokoa maisha yangu.
Niendelee kusisitiza kwamba wakati haya yote yakitokea, katika ulimwengu wa kawaida sikuwa na fahamu hata kidogo, nilikuwa nimefumba macho na kulala pale kitandani kama maiti, nikiwa nimeunganishwa na mashine ya kunisaidia kupumua lakini katika ulimwengu mwingine ambao hata sijui niuiteje, nilikuwa nimesimama kwenye pembe moja ya ile wodi, nikishuhudia kila kilichokuwa kinaendelea.

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 27


ILIPOISHIA:
Sikutaka kumuamsha Rahma, nilimtoa kifuani kwangu taratibu kisha nikashusha miguu chini, nikawa nimekaa huku nikitazama huku na kule. Sikuweza kuona chochote kutokana na giza lililokuwa limetanda usiku huo. Mara nikasikia kishindo kizito kama cha kitu kilichodondoka kutoka darini mpaka sakafuni, mapigo ya moyo yakaanza kunienda mbio kuliko kawaida.
SASA ENDELEA...
Nilikaza macho kwenye giza kujaribu kuangalia ni kitu gani hicho kilichodondoka, kwa mbali nikaanza kuona kama mtu amepiga magoti kwenye kona ya chumba hicho, taratibu akaanza kuinuka, nikazidi kumkazia macho na kadiri muda ulivyokuwa ukizonga ndivyo nilivyozidi kuiona vizuri taswira yake.
Nilimtambua kwamba ni mwanamke kutokana na maumbile yake ingawa alionesha kuwa ni mzee kwani niliweza kuiona ngozi yake ilivyokuwa imekunjamana, nikamkazia macho usoni nikitaka niione sura yake. Hata hivyo eneo la usoni lilikuwa na giza sana, nikamuona akiinua mikono juu kama anayetoa ishara fulani, akageuka na kuanza kujisugua makalio yake ukutani.
Mara nilisikia kishindo kingine, hofu ikazidi kutanda ndani ya moyo wangu, kijasho chembamba kikawa kinanitoka huku nikiwa nimekodoa macho kwa nguvu zote.
 Nilitamani niamke nikawashe taa lakini ujasiri huo sikuwa nao, nilitamani niingie chini ya kitanda lakini mwili wote haukuwa na nguvu, nilitamani kupiga kelele kuwaamsha nyumba nzima lakini sikuwa na uwezo huo, nikawa natetemeka kuliko kawaida.
Nilipotazama kwa makini pale chini, nilimuona mtu mwingine kama yule wa kwanza naye akiinuka taratibu lakini tofauti yake, huyu alikuwa mwanaume kutokana na jinsi mwili wake ulivyokuwa na alionesha pia kuwa mzee zaidi maana mpaka mgongo wake ulikuwa umepinda.

The Graves of The Innocent (makaburi ya Wasio na Hatia)- 26




ILIPOISHIA:
Nilipomtazama, macho yangu na yake yaligongana, akanikazia macho, ikabidi nikwepeshe macho yangu, safari ya kurudi nyumbani ikaanza huku mara kwa mara baba akichomoza kichwa na kunitazama, jambo ambalo sikulifurahia.
SASA ENDELEA...
Bado nilikuwa na maswali mengi kuhusu huyu msichana, sikuwa najua ndani ya ile bahasha kuna nini na kwa sababu gani anaonekana kunijali kiasi hicho. Baada ya dakika kadhaa, tukawa tumeshawasili nyumbani.
Magari yaliposimama tu, baba alishuka haraka na kunifuata, kabla hata dereva hajanisaidia kufungua mkanda, baba alifika na kunitazama kwa macho ya ukali, safari hii nikaona kama ananionea, na mimi nikamkazia macho, tukawa tunatazamana kama majogoo yanayotaka kupigana, huku nikiificha ile bahasha asiione maana angeweza kunipokonya kama alivyofanya kwenye simu.
“Kwa nini unakuwa huelewi unapoonywa jambo? Unataka mpaka nini kitokee ndiyo ujue kwamba yule msichana ni mtu hatari kwako na kwetu sisi sote?”
Magari yaliposimama tu, baba alishuka haraka na kunifuata, kabla hata dereva hajanisaidia kufungua mkanda, baba alifika na kunitazama kwa macho ya ukali, safari hii nikaona kama ananionea, na mimi nikamkazia macho, tukawa tunatazamana kama majogoo yanayotaka kupigana, huku nikiificha ile bahasha asiione maana angeweza kunipokonya kama alivyofanya kwenye simu.

Saturday, August 19, 2017

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na hatia)- 25




ILIPOISHIA:
Nilianza kuwatazama mmoja baada ya mwingine, kuanzia mama ambaye uso wake ulikuwa na huzuni kubwa, baba ambaye alionesha kuwa katika tafakuri nzito na ndugu zangu wote ambao walikuwa wamenikodolea macho, kila mmoja akiwa na maswali mengi yasiyo na majibu. Mara mlango wa wodi ulifunguliwa, watu wote wakageuka kutazama ni nani aliyekuwa akiingia kwa kasi kiasi kile.
SASA ENDELEA...
“Shikamooni! Samahani naomba kuuliza eti hii ndiyo wodi aliyolazwa Togo?” alisema mtu huyo lakini kabla hajajibiwa, tayari alikuwa ameshasimama sehemu ambayo ilinifanya mimi na yeye tutazamane.
Moyo wangu ulinilipuka mno kugundua kuwa kumbe alikuwa ni yule msichana tuliyekutana naye kwenye basi na kujenga naye urafiki utafikiri tumejuana miaka kumi iliyopita.
Sikuelewa amejuaje kwamba nilikuwa hospitalini hapo kwa sababu mara ya mwisho alipokuja nyumbani na kunikuta nikiwa na Rahma, tukiondoka kuelekea ufukweni, nilimueleza kwamba tunaenda Coco lakini baadaye tukabadili uelekeo na kuelekea Msasani Beach kwa lengo la kumkwepa.
Kwa harakaharaka, isingewezekana mtu ambaye ametufuata Coco ajue kwamba kumbe tulienda Msasani na kama hiyo haitoshi, ajue kwamba kuna tatizo limetokea na kujua mpaka wodi niliyokuwa nimelazwa. Kengele ya hatari ililia ndani ya kichwa changu.
“Ooh! Ahsante Mungu, Togo... umepatwa na nini baba?” alisema huku akinisogelea pale kitandani lakini baba alimzuia.
“Binti, sidhani kama nakujua. Wewe ni nani?”
“Togo alisema hawafahamiani ila walikaa siti moja kwenye basi tu, hata sijui amefuata nini,” alidakia Rahma na kuzungumza kwa chuki, moyoni nikajisikia vibaya sana kwa sababu kama mtu alikuwa amekuja kwa ajili ya kuniona, achilia mbali utata mkubwa uliokuwa nyuma ya tukio la yeye kujua mahali nilipo, hakupaswa kufanyiwa vile.

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 17


ILIPOISHIA:
Safari iliendelea mpaka tulipofika Magomeni ambako kulikuwa na foleni kubwa sana asubuhi hiyo, jambo ambalo halikuwa la kawaida.
“Nimekwambia kwamba sijui kama tutafika salama, umewahi kuona asubuhi namna hii kunakuwa na foleni kama hii?” alisema Shenaiza huku akizidi kuonesha hofu kubwa ndani ya moyo wake, nikawa nazidi kumtuliza.
SASA ENDELEA…
Tulikaa kwenye foleni kwa zaidi ya dakika ishirini, magari yakiwa hayaendi mbele wala hayarudi nyuma. Nilitegemea kwamba muda mfupi baadaye askari wa usalama barabarani (trafiki) watafika na kusaidia kuondoa foleni hiyo lakini haikuwa hivyo.
Madereva wengine walipochoka, walianza kupiga honi kwa nguvu, huku wengine wakiteremka kwenye magari yao na kusogea upande wa mbele kujaribu kuangalia kilichokuwa kinasababisha foleni hiyo.
“Nasikia kuna ajali huko mbele, hapa hatuwezi kuondoka sasa hivi mpaka trafiki waje, wapime ajali yenyewe, wayatoe magari yaliyopata ajali unafikiri itakuwa sasa hivi?” kondakta wa daladala tuliyopanda, alisema na kutufanya abiria wote tuishiwe nguvu.
“Sasa tutafanyaje?”

The Graves of The Innocent (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 24


ILIPOISHIA:
Ghafla tulishtushwa na kishindo kikubwa ambacho hata sikuelewa kimetokea wapi. Watu walianza kupiga kelele kwa nguvu huku wale waliokuwa baharini wakianza kukimbia kuokoa maisha yangu. Ilibidi tugeuke kutazama kule kishindo kile kilichotokea ambako bado zile kelele zilikuwa zikitokea.
SASA ENDELEA...
Lahaula! Samaki mkubwa ambaye sikuwahi kumuona ingawa baadaye nilisikia kwamba anaitwa papa, akiwa na meno makali yaliyochongoka, aliipiga kikumbo boti ndogo ya uvuvi iliyokuwa eneo hilo na kusababisha kishindo kikubwa, wavuvi waliokuwa ndani ya boti hiyo wote wakarukia majini na kuanza kuhaha kuokoa maisha yao.
Nikiwa bado namshangaa samaki yule ambaye alijirusha kwa nguvu kutoka majini na sasa akawa anaonekana mzimamzima, wote tulishtukia akimfuata mmoja kati ya wale wavuvi, akafunua mdomo wake uliokuwa na meno makali kama msumeno, akamkamata kiunoni, kufumba na kufumbua akaubana mdomo wake kwa nguvu, yule mvuvi akagawanyika vipande viwili.
Sijui nilipata wapi ujasiri, nilijikuta nikiinuka kwa kasi kubwa pale tulipokuwa tumekaa na Rahma, akabaki anapiga kelele za kuniita huku akiniuliza nakwenda wapi na kufanya nini? Sikuelewa swali lake lilimaanisha nini kwa sababu kila kitu kilikuwa wazi, nilikuwa nakwenda kutoa msaada kwa wale wavuvi.
Nilikimbia mpaka eneo ambalo maji yalianza kunifika kiunoni, kwa kuwa nilikuwa na uzoefu wa kutosha wa kupiga mbizi, nilianza kuelekea eneo la tukio. Kadiri nilivyokuwa nazidi kusonge mbele ndivyo kelele zilivyokuwa zikizidi kuongezeka. Sikuwahi kudhani kwamba samaki ana sauti ya kutisha kiasi kile maana alikuwa akitoa milio ya ajabu.

Thursday, August 17, 2017

The Graves of The Innocent (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 23


ILIPOISHIA:
“Tupeleke Coco Beach, kule wanakouza mihogo,” alisema Rahma, safari ikaanza lakini mita chache mbele, nilishtuka baada ya kusikia mtu akiliita jina langu kwa nguvu, tena sauti yenyewe ilikuwa ya kike, ilibidi Rahma amwambie dereva asimame, tukageuka nyuma kutazama ni nani aliyekuwa ananiita kwa sababu mimi nilikuwa mgeni na hakuna mtu yeyote aliyekuwa akilifahamu jina langu zaidi ya wale tuliokuwa tukiishi pamoja.
SASA ENDELEA...
Mimi ndiyo nilikuwa wa kwanza kushuka kwenye Bajaj, Rahma naye akafuatia, nikawa na shauku kubwa ya kumjua aliyeniita kwa bashasha kiasi kile.
“Togo, ni wewe! Ooh siamini macho yangu, sikujua kama nitakupata!” alikuwa ni yule msichana ambaye tulikaa naye siti moja kwenye basi wakati tukisafiri kutoka Mbeya kuja Dar es Salaam. Alikuwa amevaa sketi fupi na nyepesi ambayo ilimfanya maungo yake yajichore vizuri.
Juu alikuwa amevaa blauzi ndogo ambayo iliacha sehemu kubwa ya kifua chake wazi, akawa anatembea kwa maringo akinifuata huku tabasamu pana likiwa limechanua kwenye uso wake. Kiukweli na mimi nilishindwa kujizuia kutabasamu, hasa nilipokumbuka wakati mzuri tuliokuwa nao kwenye basi mpaka tulipoachana Ubungo.
“Jamani mbona ile simu niliyokupa hupatikani hewani? Nimehangaika sana kwa kweli,” alisema akiwa tayari ameshanifikia, kufumba na kufumbua nikashtukia amenikumbatia kimahaba na kunibusu mdomoni.
“Dada mambo!” alimsalimia Rahma ambaye alikuwa amesimama pembeni yake, akiwa ni kama haamini kile alichokuwa anakiona. Ilibidi nianze kuvungavunga pale maana kila kitu kilikuwa kikitokea kwa kasi kubwa mno.

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 22


ILIPOISHIA:
Nilijifungua ile sanda, na mimi nikabaki kama Rahma, nikasogea pale kwenye bomba, maji yakawa yanatumwagikia, chini damu zikawa zinaendelea kutiririka kuelekea kwenye bomba la kutolea maji machafu. Nilimshika mikono Rahma, nikamvutia kwenye kifua changu, tukawa tunatazamana huku maji yakiendelea kutumwagikia, nikajikuta nikitamani kumbusu mdomoni.
SASA ENDELEA...
“Mbona najisikia hivi?”
“Unajisikiaje?”
“Hata sijui nisemeje lakini najisikia raha ya ajabu ndani ya moyo wangu,” alisema Rahma na kabla hata sijafanya kile nilichokuwa nakitamani, yeye alinianza akanibusu kwa midomo yake milaini huku akinikumbatia kwa nguvu, na mimi nikamuonesha ushirikiano.
“Kwa nini ulitaka kujiua?” nilimuuliza, akafumbua macho yake ambayo kwa muda wote alikuwa ameyafumba, akanitazama usoni bila kusema chochote, akajiinamia. Niligundua kwamba hakulipenda swali hilo, nikaamua kubadilisha mada lakini bado hakuzungumza chochote.
Nilimsaidia kumsafisha mwili wake wote mpaka damu zote zikaisha kwenye miili yetu, nikafunga maji na kumpa khanga yake lakini aliikataa kwa sababu nayo ilikuwa na damu.
“Vaa tu kwanza tutaoga tena kwa mara nyingine, inabidi tukafanye usafi chumbani kwako,” nilimwambia, akakubali. Tulichukua ndoo za maji na vifaa vya kufanyia usafi, tukaelekea chumbani kwake ambako kila sehemu ilikuwa imechafuka kwa damu.
Tukaanza kufanya usafi lakini bado Rahma hakuzungumza chochote, muda wote alikuwa kimya kabisa na pale alipohitaji kunielekeza jambo, alikuwa akitumia zaidi ishara.
“Mbona umebadilika ghafla? Nisamehe kama kuna kitu nimekukwaza,” nilimwambia, akanitazama tena.
“Kwani nini kilitokea?”
“Wewe unakumbuka nini?”
“Nakumbuka niliamua kunywa sumu ili nife.”
“Kwa nini?”
“Kwa sababu nakupenda.”
“Sasa ukimpenda mtu ndiyo ujiue?”

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 16


ILIPOISHIA:
Nilimtazama Raya aliyekuwa bado amelala juu ya kifua changu, nikajiuliza mara mbilimbili kama nipokee au la. Mpaka simu inakata, sikuwa nimeamua nini cha kufanya, ikaanza tena kuita mfululizo ambapo nililazimika kuipokea, sauti ya Samantha ikasikika upande wa pili, ikinipa taarifa ambazo zilinishtua mno.
“Unasemaaa?” nilijikuta nikiuliza kwa sauti ya juu, iliyomzindua Raya usingizini.
SASA ENDELEA…
Wamekuja tena hapa hospitalini wanataka kuniua na wametishia kwamba wanahisi na wewe unahusika kwenye hiki kinachoendelea kwa hiyo wameapa kufanya kila kinachowezekana kuhakikisha wanatupoteza wote wawili.
“Lakini Shenaiza, hivi ingekuwa wewe ndiyo upo kwenye nafasi yangu ungejisikiaje? Yaani unajikuta tu upo katikati ya mambo ya hatari, maisha yako yanawindwa usiku kucha lakini hata huelewi chanzo ni nini, ungejisikiaje?”
“Ningejisikia vibaya Jamal lakini si nilishakwambia nitakueleza kila kitu? Wala huna haja ya kuwa na haraka wala kukasirika.”
“Utaniambia lini? Unajua kilichonitokea nilipoondoka hapo hospitalini? Bado kidogo ningekufa leo, kibaya ni kwamba sijui hasa kinachoendelea, sijui chochote kuhusu wewe wala matatizo yako ambayo sasa yameshakuwa yangu pia.”
“Huu sio muda wa kulaumiana Jamal, nakuomba kama ulivyofanya mara ya kwanza, njoo unitoroshe tena hospitali na nakuahidi safari hii tukitoka tu, nitakueleza ukweli wa kila kitu.”
“Hapana! Siwezi Shenaiza, tafuta mtu mwingine wa kuifanya kazi hiyo, sipo tayari.”
“Jamani Jamal, kwa hiyo upo tayari kuona nakufa wakati uwezo wa kunisaidia unao? Tena asubuhi hii ndiyo muda mzuri, watu wakija kuwaletea wagonjwa chai na sisi tunatumia muda huohuo kutoroka, nipo chini ya miguu yako,” alisema Shenaiza kwa sauti iliyoonesha alikuwa akilengwalengwa na machozi.

Wednesday, August 16, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 15


ILIPOISHIA:
“Aisee! Mbona hii inaonekana kuwa ngoma nzito?”
“Ni ngoma nzito kwelikweli, halafu kuna huyu kijana ameingizwa kwenye mtego bila mwenyewe kujua chochote, mpaka namuonea huruma.”
SASA ENDELEA…
“Kwa akili zako unafikiri huyu kijana atakuwa ameingia kwenye mtego mwenyewe akiwa hajui chochote?”
“Hajui chochote, hata maelezo aliyokuwa anayatoa, yanaonesha kabisa hakuna anachokijua.”
“Unafikiri inawezekana mtu akaingizwa kwenye kumi na nane za Loris kama hana umuhimu? Hata kama mwenyewe hajui naamini lazima kuna jambo ambalo limefanya aingizwe kwenye huu mtego.”
“Lakini hajaingizwa na Loris mwenyewe isipokuwa binti yake.”
“Nani ambaye hajui kwamba Loris amekuwa akimtumia mwanaye kwenye kazi zake, hasa pale anapoona mambo yameanza kuwa magumu kwake?”
“Yote yanawezekana lakini taarifa za ndani zinaonesha kwamba huyu binti mwenyewe ameshachoka kumtumikia baba yake na ndiyo maana unaona anaandamwa na matatizo makubwa!”
“Unataka kusema ndiyo maana anatishiwa kuuawa?”
“Inawezekana kabisa, nahisi kuna jambo kubwa analolifahamu lakini hataki kueleza ukweli kwa sababu hata ukifuatilia maelezo aliyokuwa anayatoa, anazungumza vitu nusunusu sana.”
“Mh! Kweli hii ngoma nzito! Kwa hiyo tunafanyaje?”
“Inabidi tuwasiliane kwanza na mkuu, si unajua mtandao wa Loris unahusisha mpaka viongozi wetu?”
***
Raya alishika taulo nililokuwa nimejifunga na kulivuta kisha akalitundika pale alipoweka khanga yake, tukabaki saresare maua! Akanisogelea jirani kabisa kiasi cha kila mmoja kuanza kuzisikia pumzi za mwenzake, tukawa tunatazamana machoni huku ‘Jamal’ wangu naye akianza kufura kwa hasira.

Tuesday, August 15, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 14


ILIPOISHIA:
“Tuondoke!” nilisema huku nikiinuka pale nilipokuwa nimekaa kwani tayari kengele ya hatari ililia ndani ya kichwa changu, Raya naye akainuka, tukaanza kuelekea kwenye lango la kutokea nje ya hospitali hiyo lakini cha ajabu zaidi, tukiwa getini tunataka kutoka, nililiona lile gari nalo likija kule tulipokuwepo.
SASA ENDELEA…
“Bodaboda! Bodaboda!” niliita kwa sauti huku tukitembea kwa haraka kuelekea nje ya hospitali, lile gari nalo likizidi kuja kwa kasi kule tulipokuwepo. Ilibidi nimshike mkono Raya kwani kwa jinsi alivyokuwa ‘mayai’ ningeweza kumuacha pale na kumsababishia matatizo.
Kwa bahati nzuri, dereva mmoja wa bodaboda alituona na harakaharaka akawasha pikipiki yake na kutufuata, mwenyewe akijiona amewazidi wenzake ujanja kwa kuwahi abiria.
“Tupeleke Kijitonyama,” nilisema huku nikimsaidia Raya kupanda, na mimi nikapanda lakini dereva wa bodaboda hakutaka kuondoka mpaka tukubaliane kwanza.
“Twende bwana nitakupa kiwango chochote unachotaka.”

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 21


ILIPOISHIA:
Hakuwa na nguo yoyote mwilini zaidi ya kipande cha sanda alichokuwa amefunikwa kuanzia juu kidogo ya mapaja mpaka kifuani ambacho nacho kilikuwa na damudamu. Baba akanitazama usoni, na mimi nikamtazama nikiwa na shauku kubwa ya kusikia kile atakachoniambia. Nilikuwa tayari kwa chochote ilimradi Rahma apone.
SASA ENDELEA...
“Mlichokifanya mkidhani ni siri yenu ndicho unachotakiwa kukifanya hapa,” alisema baba huku akigeuka na kuanza kutoka. Ilibidi nimshike mkono na kumvuta, sikuwahi kumfanyia baba hivyo hata siku moja lakini siku hiyo nilijikuta tu nikifanya hivyo.
“Baba!”
“Ambacho huelewi ni nini? Kama unataka apone fanya nilichokwambia na wakati wa tendo hakikisha hiyo sanda huivui,” alisema baba kisha akatingisha kichwa kuonesha kwamba niendelee, akanifinjia kijicho na kuachia tabasamu hafifu. Nilijikuta nikiogopa pengine kuliko kipindi chochote maishani mwangu.
Yaani mtu anaumwa kiasi kile, yupo kwenye hatua za mwisho za kukata roho, halafu eti naambiwa nifanye naye mapenzi, tena mwili wake ukiwa umelowa damu na mimi nikiwa nimevalishwa sanda! Moyo wangu ulipigwa na ganzi.

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...