Thursday, July 20, 2017

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 4


ILIPOISHIA:
Niliondoka kazini nikiwa ni kama nimechanganyikiwa, sikuwa namjua Shenaiza lakini sijui kwa nini nilihisi kama matatizo yake yalikuwa yakinihusu sana. Nikiwa kwenye kituo cha daladala nikiendelea kusubiri usafiri, ujumbe mfupi uliingia kwenye simu yangu, ulisomeka:
“Mwenye simu hii amelazwa Hospitali ya Amana, Ilala. Hali yake ni mbaya, hawezi kuzungumza.”
SASA ENDELEA…
“Mungu wangu,” nilisema baada ya kumaliza kuusoma ujumbe huo. Nilijaribu kuipiga tena namba hiyo, ikapokelewa lakini sauti haikuwa ya Shenaiza, akaniambia yeye ni Rozina, nesi katika hospitali ya Amana na kwamba yeye ndiye aliyekuwa akimhudumia msichana huyo.
Nilimuomba anitajie wodi aliyolazwa msichana huyo, akaniambia niende tu nikifika hospitalini hapo nipige kupitia namba hiyohiyo atakuja kunipokea. Niliita bodaboda na kumuelekeza kukimbia kadiri awezavyo kuelekea Amana. Abiria wengine waliokuwa pale kituoni wakisubiri daladala, walibaki kunishangaa lakini mwenyewe sikujali.
Nikaondoka na bodaboda huku nikimhimiza kuongeza mwendo ili tuwahi kufika. Baada ya kuhangaika sana kwenye foleni, kama ujuavyo Jiji la Dar es Salaam nyakati za jioni, hatimaye tuliwasili Amana. Nikapiga namba ya Shenaiza ambapo yule nesi alipokea tena, nikamweleza kwamba tayari nilikuwa nimefika, akaniambia nimsubiri mapokezi.

Sikuwa hata naijua sura ya huyo Shenaiza mwenyewe kwa sababu hatukuwahi kuonana zaidi ya kusikia sauti yake tu kwenye simu.
Muda mfupi baadaye, alitoka nesi mmoja, mwembamba, mrefu mwenye rangi ya weusi wa asili, akaniuliza kama mimi ndiye niliyekuwa nawasiliana naye kwenye simu. Nilipomjibu kwamba ni mimi, aliniuliza nilikuwa na uhusiano gani na mgonjwa?
Nikamjibu kwamba mimi ni kaka yake, nikamuona akiguna huku akinitazama kwa macho ya udadisi. Sikuelewa kwa nini ananitazama hivyo, nikajikaza kiume na kuonyesha kutobabaika.
“Nifuate!” alisema huku akianza kutembea kuelekea wodini, na mimi nikawa namfuata. Tulipita kwenye korido na kutokezea kwenye wodi za wanawake, nikawa naangaza macho huku na kule wakati tukipita pembeni ya vitanda walivyolazwa wanawake wengi, tukapita na kwenda kwenye wodi iliyokuwa imejitenga peke yake. Yule nesi akafungua mlango na kunipa ishara kwamba niingie.
Japokuwa kulikuwa na vitanda vinne ndani ya wodi hiyo, ni kimoja tu kilichokuwa kimelaliwa na mgonjwa aliyeonesha kutokuwa na fahamu. Yule nesi alinipa ishara kwamba yule ndiyo mgonjwa mwenyewe, nilimtazama kwa mshangao nikiwa kama siamini macho yangu.
Hakuwa Shenaiza yule ambaye nilimjengea picha kichwani mwangu, alikuwa mtu mwingine tofauti kabisa kiasi cha kunifanya nihisi huenda nesi amekosea kunipeleka au hatukuelewana katika mazungumzo yetu.
Hakuwa msichana wa Kitanzania kama nilivyokuwa nimemfikiria, alikuwa na mchanganyiko ambao siwezi kueleza moja kwa moja kama ni Mzungu au ni Mwarabu lakini alikuwa katikati ya jamii hizo mbili. Kiumri alionesha kuwa bado ni binti mdogo tofauti na nilivyomfikiria kwamba anaweza kuwa ni mwanamke mwenye kati ya miaka 25 hadi 30.
Alikuwa amelala tuli kitandani huku akiwa amefungwa bandeji kubwa kichwani, huku jicho lake moja likiwa limebadilika rangi na kuwa na weusi na wekundu kwenye ngozi inayolizunguka jicho kuonesha kwamba damu zilikuwa zimevilia kwa ndani. Pia mkono wake mmoja ulikuwa umezungushiwa bandeji kubwa kuanzia juu kidogo ya kiganja mpaka kwenye kiwiko cha mkono.
Dripu moja sambamba na chupa ya damu vilikuwa vikitiririka kwa kasi kuingia kwenye mishipa yake ya damu, nikajikuta nikipatwa na hali ambayo siwezi kuielezea kwa urahisi. Kwa kifupi, japokuwa bado sikuwa na uhakika kwamba yule ndiye Shenaiza tuliyekuwa tukiwasiliana naye, nilijikuta nikimuonea huruma sana kutokana na hali aliyokuwa nayo.
Nilitamani kujua nini kimemfika mpaka akawa kwenye hali hiyo. Nilitamani pia nimjue yeye ni nani na asili yake ni wapi hasa kwani hakuonesha kuwa Mtanzania japokuwa alikuwa akizungumza vizuri Kiswahili.
“Mbona unamshangaa sana? Kwani mlikuwa mnafahamiana kabla?” yule nesi aliniuliza baada ya kuniona hali niliyokuwa nayo, nilishusha pumzi ndefu na kuzugazuga, nikasogea pembeni ya kitanda cha Shenaiza na kumpa ishara kwamba tusogee pembeni ili tuzungumze zaidi.
“Samahani nesi, hebu nieleze nini kimetokea?”
“Nitakueleza lakini nataka na wewe unieleze ukweli, usije ukanisababishia matatizo kwenye kazi yangu, huyu ni nani kwako?”
“Nimeshakwambia kwamba ni dada yangu.”
“Hapana, siyo kweli! Hebu ngoja kwanza,” alisema huku akienda kuchukua simu iliyokuwa pembeni ya kitanda cha Shenaiza, akanifuata na kuniuliza kama simu yangu nilikuwa nayo, nikamjibu kwamba ninayo, akaniambia nipige namba ya Shenaiza. Nikatoa simu yangu na kutafuta namba yake kisha nikampigia.
“Unaona amekusevu vipi?” aliniuliza yule nesi huku akinionesha jina lililotokea kwenye simu yake, nikabaki nimepigwa na butwaa kutokana na jinsi alivyokuwa amenisevu.
Sikutaka kuendelea kumbishia yule nesi kwa sababu angeweza kupata sababu ya kukataa kunipa ushirikiano baada ya kuamini kwamba nilikuwa nikimdanganya, nikaamua kukubali yaishe, nikamuacha aamini kile mwenyewe alichotaka kukiamini (nitafafanua zaidi baadaye jinsi alivyokuwa amenisevu).
Baada ya kuelewana na nesi huyo, alianza kunieleza kwamba walimpokea mgonjwa huyo majira ya saa tisa za jioni baada ya kuletwa na wasamaria wema ambao walidai wamemkuta amepigwa na kujeruhiwa vibaya nje ya nyumba yao.
“Alikuwa akitokwa na damu nyingi huku pia akiwa na majeraha sehemu mbalimbali za mwili wake, ikabidi tumpokee hivyohivyo na kuanza kumpatia matibabu lakini mpaka sasa hakuna anayejua jina lake, ametokea wapi na nini kilichomsibu, tunasubiri labda akirejewa na fahamu au ndugu zake wakija ndiyo watueleze kilichotokea,” alisema yule nesi, nikashusha pumzi ndefu na kugeuka kumtazama Shenaiza pale kitandani.
Baada ya kumaliza kuzungumza na nesi, nilimuomba niende kukaa pembeni ya Shenaiza mpaka atakaporejewa na fahamu zake lakini aliniambia kuwa ni kinyume na taratibu za hospitali hiyo, akanitaka nikakae nje ya wodi na kama kuna chochote, atanipa taarifa lakini akasisitiza kwamba mgonjwa alikuwa anahitaji damu zaidi kwa sababu amepoteza nyingi, akanitaka kama nipo tayari kumchangia anielekeze nini cha kufanya.
Sikuwa na kipingamizi, nilikubali kumchangia damu, yule nesi akanichukua mpaka kwenye wodi nyingine ambapo alinitambulisha kwa madaktari wenzake na kuwaeleza kwamba nilikuwa nataka kumtolea damu mgonjwa wangu Shenaiza. Nikachukuliwa vipimo vya awali na baada ya kuonekana nilikuwa fiti, niliingizwa kwenye chumba kingine na kuanza kutolewa damu.
Nikiwa naendelea kutoa damu, niliendelea kujiuliza maswali mengi kuhusu Shenaiza yaliyokosa majibu. Kuna wakati nilijilaumu sana kukataa kuonana naye mapema kwani niliamini pengine ningeweza kumsaidia asipatwe na kilichomtokea. Hata hivyo nilijipa moyo kwamba sikuwa nimechelewa, nikawa namuombea kwa Mungu apone na kurudi kwenye hali yake ya kawaida.
Baada ya kumaliza kutolewa damu, nilirudi pale nje ya wodi na kukaa huku nikiendelea kutafakari mambo mengi. Tayari kigiza cha jioni kilishaanza kuingia lakini moyo wangu haukuwa radhi kuondoka hospitalini hapo, nilijiapiza kwamba hata ikibidi kukesha usiku kucha, nitafanya hivyo mpaka nifahamu kilichomsibu Shenaiza.
Ilipofika majira ya kama saa moja za jioni, yule nesi, Rozina alinifuata na kunipa habari ambazo zilinifanya mapigo ya moyo yanilipuke kuliko kawaida. Aliniambia Shenaiza amerejewa na fahamu na jambo la kwanza alilouliza ni kama nilikuwa nimempigia simu.
“Nimemwambia kwamba upo hapa nje, akaniomba sana akuone, lakini anazungumza kwa shida sana,” alisema nesi huyo, nikainuka na kuanza kumfuata harakaharaka kuelekea wodini.

Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...