Wednesday, December 24, 2014

KUTUBU KWANGU (MY REPENTANCE)- 2


ILIPOISHIA:
Naomba umpe namba yangu mwambie anitafute au nipe yake nijue namna ya kumfikishia mzigo wake,” alisema dereva wa ile Carina kwa sauti ya kiungwana mno.
 Nilishusha pumzi ndefu na kuachia tabasamu, nikamwambia kwamba mimi ndiyo Flaviana, nikamsikia akicheka kidogo kisha akaniuliza nipo wapi kwa wakati huo. Nilipomuelekeza, aliniambia nimsubiri hapohapo anakuja.
SASA ENDELEA... 
Kweli baada ya kama dakika tano hivi, ile Carina ilipaki upande wa pili wa barabara, akanipigia simu na kuniuliza kama nilikuwa naliona gari. Nikatoka mbiombio na kukimbia kuvuka barabara. Kwa kuwa bado mvua ilikuwa inanyesha, nilipolifikia gari lake, alinifungulia mlango, nikaingia na kukaa kwenye siti ileile niliyokuwa nimekaa awali, nikamgeukia, na yeye akanitazama, macho yetu yakagongana.

“Pole kwa usumbufu,” aliniambia kwa sauti ya kiungwana, nikaachia tabasamu hafifu huku nikiendelea kujifuta maji ya mvua, nikwamwambia mimi ndiyo napaswa kumpa yeye pole kwani licha ya kunipa lifti bure, nilimpa kazi nyingine ya kunitafuta.
Alinipa begi langu na kuniuliza nilikokuwa nakwenda.
“Naenda chuo, pale jirani na mnara wa askari.”
“Unasomea nini?”
“Nasomea uhasibu.”
“Ooh! Safi sana, mimi pia nilisomea uhasibu pale IFM sasa hivi nafanya kazi benki,” alisema yule dereva huku na yeye akiachia tabasamu, akaniomba kama sitajali anisindikize jirani na chuo ili nisiendelee kulowa.

Nilikubali haraka na kumshukuru sana. Akawasha gari na kwenda mpaka mbele kidogo, akageuza gari na kurudi barabarani, akawa anaendesha gari taratibu huku tukipiga stori za kawaida.
Ndani ya kipindi kifupi tu nilichokaa naye, niligundua kuwa yule kaka alikuwa mtu mmoja mstaarabu sana, asiye na maneno mengi, anayejiheshimu na anayeheshimu watu wengine pia bila kujali umri, jinsia au hali ya kiuchumi.
Alinisogeza mpaka jirani na chuoni kwetu, akalitoa gari barabarani na kupaki pembeni huku mvua kubwa ikiendelea kunyesha. Nilitaka kushuka lakini akaniambia nisubiri mvua ipungue kidogo kwani yeye hakuwa na haraka sana kwani ofisi anayofanyia kazi ni jirani na pale.

Tofauti na wanaume wengi niliokuwa nakutana nao kila siku katika pilikapilika zangu, yeye wala hakuonesha papara ya kuniomba namba yangu ya simu wala hakuonesha kabisa nia ya kutaka kunitongoza hasa ukizingatia kwamba licha ya umri wangu mdogo, nilikuwa nimejaliwa uzuri wa kipekee kuanzia sura mpaka umbo.
Mvua ilipungua na hatimaye ikaisha kabisa, nikarudia tena kumshukuru yule kaka ambaye mpaka muda huo wala sikuwa nikilijua jina lake. Tukaagana, nikashuka kwenye gari lake na kuanza kutembea harakaharaka kuelekea chuoni bila hata kugeuka nyuma.
Japokuwa nilikuwa nimechelewa, nilipoingia darasani, nilikuta wanafunzi wachache tu wakiwa wameshafika, nikajua ni kwa sababu ya hali ile ya hewa. Kwa kuwa jana yake sikumaliza kazi tuliyopewa chuo, sikutaka kupoteza muda, nikakaa kwenye kompyuta yangu na kuendelea na kazi.
Bado kumbukumbu za yule kaka zilikuwa zikiendelea kuja na kupotea kwenye kichwa changu. Sijui ni kwa sababu gani lakini nahisi ni kwa sababu ya uungwana alionionesha. Ndani ya muda mfupi tu niliokaa naye, nilijikuta nikianza kumzoea na kutamani kama niendelee kumuona au kuisikia sauti yake nzuri.
Haikuwa kawaida yangu kuvutiwa kirahisi namna hiyo na mwanaume, katika historia ya maisha yangu, wanaume ndiyo walikuwa wakinipapatikia kutokana na uzuri wangu, wala mimi sikuwahi kufanya hivyo hata mara moja, nikabaki najishangaa.
Nilijitahidi kujitoa kwenye mawazo hayo bila mafanikio, kila nilipofumba macho, sura ya yule kaka ilinijia akili mwangu na kujikuta nikitabasamu.
Kibaya zaidi, wala hakunipa namba yake ya simu na sikuwa nikijua anafanya kazi wapi zaidi ya kuniambia kuwa ofisi yao ilikuwa jirani na chuo chetu. Ghafla nilikumbuka kitu kilichonifanya nitabasamu. Nilikumbuka kwamba yeye ndiye aliyenipigia simu wakati niliposahau mkoba wangu kwenye gari lake.
Harakaharaka nikatoa simu yangu na kuanza kuangalia kwenye namba zilizoingia. Macho yangu yalitua kwenye namba yake, nikaitazama kwa muda kisha nikaiandika pembeni ya kitabu changu cha Financing. Nikafanya kama najaribu kumtumia hela kwa njia ya mtandao wa simu ili nione jina gani litatokea.
Baada ya kubonyezabonyeza namba fulani, likatokea jina la Ibrahim Mnasy, nikatabasamu tena na kushusha pumzi ndefu.
“Kumbe anaitwa Ibrahim!” nilijisemea huku nikiisevu namba yake. Kama kuna mtu angekuwa ananifuatilia ninachokifanya, angeweza kudhani nataka kurukwa na akili. Angalau sasa roho yangu ilitulia kwani nilijua naweza kumpata endapo nikihitaji kuwasiliana naye.
Mvua ilikuwa imekatika kabisa, wanachuo wengi wakawa wanakuja darasani na baadaye kidogo, walimu waliwasili, tukaanza masomo japo kwa kuchelewa. Masomo yaliendelea mpaka saa nane mchana, tukatoka kwa ajili ya chakula cha mchana kisha tukarejea tena darasani mpaka saa kumi ambapo kwa kawaida ndiyo ulikuwa mwisho wa vipindi.
Tukatawanyika na mimi kuongoza mpaka kwenye kituo cha daladala cha Posta ambacho kila siku huwa napandia magari ya kurudi kwetu, Kinondoni. Kama ilivyokuwa asubuhi, usafiri ulikuwa wa shida sana jioni hiyo. Hatimaye nilipanda daladala ingawa ilikuwa ni kwa kugombania sana, safari ya kurudi nyumbani ikaanza.
Njiani bado kumbukumbu juu ya Ibrahim ziliendelea kunisumbua, nikajiapiza kuwa jioni nikimaliza kazi zangu zote, lazima nimpigie simu japo nisikie sauti yake. Baada ya kusota kwa muda mrefu kwenye foleni, hatimaye tuliwasili Morocco, nikashuka na kuvuka barabara, nikatembea kidogo kuelekea nyumbani kwani hatukuwa tukiishi mbali sana na kitu hicho.
Nilipofika nyumbani, siku hiyo sikutaka stori na mtu, nilipitiliza chumbani kwangu, baada ya kupumzika kidogo nikaenda kuoga na kurudi sebuleni kusubiri chakula cha usiku kwani tulikuwa na desturi ya kukusanyika familia nzima kila jioni.
Tulipomaliza kula, harakaharaka nilirudi chumbani kwangu na kujifungia, nikachukua simu na kujitupa kitandani, nikatafuta namba ya Ibrahim na kumpigia huku nikiwa nimeshajiandaa nini cha kuongea.
Simu ilipoita kidogo tu, ilipokelewa, nikajikuta nikisisimka mno baada ya kuisikia sauti ya Ibrahim, mapigo ya moyo wangu yakawa yananienda mbio mno.
“Haloo!”
“Haloo kaka Ibrahim.”
“Naam! Naongea na nani?” Ibrahim alizungumza kwa sauti iliyotulia mno, nikazidi kuchanganyikiwa mtoto wa kike. Nilishusha pumzi ndefu na kujitambulisha, nilipomkumbusha tu mazingira tuliyokutania, alinikumbuka na kunichangamkia.
“Umelijuaje jina langu?”
“Si ulinitajia mwenyewe, au umesahau,” nilidanganya, nikamsikia akiguna kama anayekumbuka kitu kisha tukaendelea na mazungumzo. Nilimwambia nimempigia simu ili kumshukuru kwa wema wote alionifanyia siku hiyo, akafurahi na kuniambia nisijali.
Tuliendelea kuzungumza mambo ya hapa na pale, mimi nikiwa ndiyo mzungumzaji sana, nilichokuwa nakitaka ilikuwa ni ukaribu wake na kumzoea, jambo ambalo lilishaanza kuonekana kuwa litafanikiwa kwa jinsi alivyokuwa ananichangamkia.
Baadaye mazungumzo yaliisha, nikamtakia usiku mwema kisha nikakata simu. Nilishusha pumzi ndefu na kuanza kushangilia moyoni, sijui kwa nini nilifurahi sana kuongea na Ibrahim.
Kama hiyo haitoshi, nilimtumia ujumbe mfupi mzuri wa kumtakia usiku mwema, naye akanijibu ndani ya muda mfupi tu, nikalala na kuukumbatia mto wangu huku joto tamu likiendelea kuzunguka kwenye mwili wangu.
Niseme tu wazi kwamba nilishampenda sana Ibrahim tangu nilipomuona kwa mara ya kwanza tu, na sasa nilikuwa tayari kufanya chochote, hata ikibidi kujitongozesha ilimradi awe mpenzi wangu. 
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue. Unaweza kuisoma pia Facebook kwa ku-like page ya Simulizi za Majonzi.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...