Wednesday, November 5, 2014

MBINU 10 ZA KUFUFUA PENZI LILILOKUFA

HASH POWER 7113
NI matumaini yangu kwamba msomaji wangu uko poa. Ni wiki nyngine tunapokutana kwenye busati letu ambapo tunajuzana na kujadiliana mambo mbalimbali kuhusu uhusiano wa kimapenzi.
Nakushukuru wewe unayetuma ujumbe mfupi ukitoa maoni, kuchangia au kutaka ushauri kuhusu mambo mbalimbali, hata kama hujajibiwa elewa kwamba ujumbe wako umefika na utafanyiwa kazi.
Mada ya leo ni maalum kwa watu ambao tayari mpo kwenye uhusiano wa kimapenzi, iwe ni wapenzi wa muda mrefu, wachumba au wanandoa.
DALILI ZA PENZI LILILOKUFA
Umewahi kuhisi kwamba penzi lako limefikia mwisho japo bado upo na mpenzi wako, mchumba au mumeo/mkeo? Yaani upoupo tu, zile hisia tamu za mapenzi
ulizokuwa nazo wakati mnayaanza mapenzi yenu hazipo tena, hufurahii kuwa naye, hamzungumzi mkaelewana badala yake kila siku ni ugomvi na migogoro isiyoisha!
Kila unachokisema au atakachokisema hata kama ni kizuri vipi kinakuwa sawa na petroli kwenye moto, kinazidi kuchochea uhasama na chuki kati yenu. Kila mnapoanza kuzungumza, hata kama ni jambo zuri lazima muishie kutukanana, kufokeana au kupigana.
Unaishi naye nyumba moja lakini kila mmoja analala kwenye chumba chake, hata mkilala pamoja kila mmoja anageukia upande wake, hujisikii chochote juu yake, hata akiugusa mwili wako unaona kero na hutaki hata kumtazama usoni. Hujisikii hamu tena ya kuwa naye faragha, kila unachokifikiria kuhusu yeye kinakupandisha hasira na kukuudhi!
Unatamani uhusiano wenu ufikie mwisho hata sasa hivi ingawa hujui uanzie wapi… unatamani mwenza wako afe kwa ajali au apate mabalaa makubwa yatakayowatenganisha.
Ukiona hayo yote niliyoyataja na mengine mengi yanakutokea, huo ni uthibitisho kwamba unaishi kwenye mapenzi yaliyokufa, Wazungu wanasema Dead Love. Kwa wale ambao wameishi kwenye uhusiano wa kimapenzi kwa muda mrefu watakuwa wananielewa vizuri zaidi, kama upo kwenye penzi jipya, huwezi kuelewa vizuri.
KUACHANA NDIYO SULUHU?
Wengi wanapofikia hatua hii ya kuishi kwenye mapenzi yaliyokufa, huwa wanakosea sana kuamini kwamba njia pekee ni kuachana. Hata kama ni wanandoa na walishafanya mambo mengi pamoja ikiwa ni pamoja na kuzaa, wataishia kupeana talaka! Inasikitisha sana.
Hata hivyo, hiyo siyo dawa kwani ni kuyakimbia matatizo! Utaachana na wangapi? Wataalamu wa mahusiano na mapenzi wanasema kila penzi lililokomaa, lazima lipitie kwanza kwenye hatua ya kufa, ukweli ambao ni wachache huweza kuukubali. Wahenga wanasema dhahabu ili ing’ae lazima ipitie kwanza kwenye moto.
NINI CHA KUFANYA?
1. Hatua ya kwanza, jiwekee nadhiri kutoka ndani ya moyo wako kwamba upo tayari kulifufua penzi lako lililokufa. Yawezekana wewe umeamua hivyo lakini mwenzako hayupo tayari, hilo lisikukatishe tamaa. Jiambie moyoni kwamba utafanya kila kinachowezekana kurudisha furaha, amani, hisia za mapenzi, msisimko na upendo kama ilivyokuwa wakati mnaanzisha uhusiano wenu.
2. Jipe muda wa kutafakari nini kilisababisha mwanzo mkawa na furaha na kupendana sana. Jaribu kukumbuka mambo uliyokuwa ukimfanyia mwanzo mpaka akakupenda na kuwafanya muishi kwa amani na upendo.
Anzia hapohapo, anza kufanya yale yaliyomfanya akupende mwanzo, kuwa mpole kwake, acha kumuonesha kisirani, dharau, jeuri au kujibizana naye. Badili hisia zako za ndani, badala ya kufikiria mabaya yake, fikiria yale mazuri aliyowahi kukufanyia.
3. Kubali kuwajibika. Japokuwa wengi huwa wanashindwa kwenye kipengele hiki, jibebeshe mzigo wa lawama wewe mwenyewe hata kama si kweli kwamba wewe ndiyo mwenye makosa. Jiambie mwenyewe kwamba wewe ndiyo umesababisha mfikie hapo mlipofika kwa sababu kama alikukosea, ungeweza kumsamehe kuanzia siku ya kwanza na wala msingefikia hatua hiyo.
Ukishakubali kuwajibika, utakuwa kwenye hatua nzuri ya kuzidi kumkaribia, hata ile chuki uliyokuwa nayo, utashangaa inayeyuka kama barafu iyeyukavyo juani na mapenzi yanaanza kuchanua upya moyoni mwako.
4. Muoneshe kwamba unajisikia vibaya kwa aina ya maisha mnayoishi na hata kama hajakuomba msamaha, jiambie ndani ya moyo wako kwamba umemsamehe bure na upo tayari kufungua ukurasa mwingine mpya.
Lilazimishe tabasamu kwenye uso wake, badala ya kuwa mnapishana ndani kama wanyama, anza kuwa unamtazama usoni kwa upole, hata kama yeye hatakuangalia lakini ataanza kuhisi kitu cha tofauti ambacho kitaanza kumbadilisha naye taratibu.
5. Msaidie kazi ndogondogo za nyumbani. Kama wewe ni mwanamke na kwa kipindi chote cha ugomvi hukuwa ukimfulia nguo, kusafisha chumba anacholala au kumuandalia chakula kizuri, jilazimishe kuyafanya hayo hata kama moyo wako unakataa. Yafanye akiwa hayupo.
Kama ni mwanaume, jitoe fahamu kwa kumsaidia kazi za nyumbani hata zile ambazo hukuwahi kuzifanya. Msaidie kuosha vyombo, kusafisha nyumba, kuwaogesha watoto (kama mlishazaa), kumfulia nguo zake au kuwaandalia watoto chakula.
Hata kama utakuwa hujamwambia neno lolote, atayaona mabadiliko na taratibu utaanza kuzigusa hisia zake kwa mara nyingine. Muda mwingi atakuwa anajiuliza kwa nini unayafanya yote hayo kwa ajili yake na mwisho atajipa jibu kwamba kumbe bado unampenda na unamhitaji.
6. Rejesha mawasiliano. Mnapokuwa kwenye penzi lililokufa, si ajabu hata salamu mkawa hampeani wala hamzungumzi vizuri tena. Baada ya kuwa umeshayafanya yote niliyokueleza hapo awali, anza kumsemesha. Msalimu kila asubuhi unapoamka na kila unaporudi kutoka kazini au mpigie simu na kumtumia sms nzuri. Hata kama atakuwa hakujibu kwa uchangamfu, usichoke, endelea na taratibu utaanza kuona naye anakusemesha na kukujibu vizuri.
Katika mawasiliano hayo mapya, jitahidi kutokuwa mzungumzaji sana bali msikilizaji. Lazima atakuwa na dukuduku la mambo mengi uliyomfanyia kipindi ambacho hamuelewani au yaliyosababisha mkafikia hatua hiyo, kuwa msikilizaji na muoneshe kwamba unamuelewa kwa kila anachokwambia. Epuka kubishana naye hata kama unaona anachokwambia siyo sawa.
Uzuri wa mbinu hizi, ukizifanyia kazi, matokeo yake yanaonekana kwa macho.


7. Rejesha mapenzi kwake. Yawezekana ikawa vigumu kwako kuanza kumpenda tena baada ya kuishi kwenye migogoro kwa kipindi kirefu lakini kama kweli unataka kufufua penzi, anza kumuonesha kwamba unampenda.
Kama unapata wakati mgumu kurudisha mapenzi, jaribu kujenga taswira kichwani mwako kwamba umekutana na mpenzi mpya na ndiyo mnaanzisha uhusiano wa mapenzi. Kuna usemi wa Kizungu usemao: Love conquers all (Mapenzi yanashinda nguvu vitu vyote). Ukimuonesha mapenzi, migogoro, chuki na uhasama vitayeyuka vyenyewe taratibu kwa sababu penzi la kweli lina nguvu sana.
8. Muoneshe uaminifu wa asilimia 100. Kama awali ulikuwa na tabia ya kuchelewa kurudi nyumbani bila sababu za msingi, badilisha ratiba zako. Kama ulikuwa unaweka password kwenye simu yako, itoe na mruhusu kushika simu yako kwa uhuru. Usiende kupokelea simu nje au pembeni, kuwa muwazi kwake kadiri uwezavyo.
Kama ulikuwa na ‘michepuko’, achana nayo kabisa na elekeza nguvu zote kwa mpenzi wako. Taratibu utaona anaanza kukuamini tena na endeleza uaminifu kadiri uwezavyo. Utaugusa moyo wake na penzi lake kwako litaanza kuchanua upya.
9. Mkumbushe maisha yenu wakati wa furaha. Mnaweza kutazama picha zenu za harusi mkiwa pamoja au mlizopiga kipindi cha mwanzo cha uhusiano wenu. Utazirudisha kumbukumbu zake nyuma na atakumbuka matukio ya furaha zaidi kuliko maudhi.
Unaweza pia kumfanyia mambo mliyokuwa mkiyafanya pamoja kipindi mlipokuwa na furaha kama kutazama movie nzuri pamoja, kusikiliza muziki anaoupenda au kumtoa ‘out’ kwenye mazingira mliyokuwa mkienda kipindi mapenzi yenu yalipokuwa motomoto.
10. Mfanyie mambo mazuri. Jitahidi kadiri ya uwezo wako kufanya mambo yatakayokuwa yanamfurahisha. Mnunulie zawadi, hata kama ni ndogo zitaufurahisha moyo wake. Mwambie maneno mazuri ambayo pengine ulishaacha kumwambia kwa kipindi kirefu.
Msifie kama yeye ni mrembo au hendisamu, mueleze kuwa hujawahi kupenda kama unavyompenda yeye na mchombeze kwa maneno mazuri kila mara unapokuwa karibu naye. Rudisha upendo kwa ndugu zake, marafiki zake na watu wake wa karibu.
Jitahidi kutafuta muda wa kutosha wa kukaa naye kila siku, hata kama ubize wa kazi unakuelemea, tenga muda kwa ajili ya kuwa naye, kula naye chakula cha jioni, kutoka ‘out’ pamoja na kwenda kwenye matembezi mkiwa pamoja huku muda mwingi ukijitahidi kuwa na tabasamu usoni mwako.
Uzuri wa mbinu hizi, ukizifanyia kazi kwa ukamilifu, matokeo yake yanaonekana haraka kuliko unavyotegemea. Kama huamini, anza leo na zingatia mbinu zote kisha utaona matokeo mwenyewe. Utakuwa umefanikiwa kurejesha furaha kwenye penzi lenu na atakupenda zaidi kuliko hata ilivyokuwa mwanzo. Cha msingi ni kujizuia kurudia maudhi mara kwa mara.
Mwisho.

13 comments:

  1. Safi sn imenigUSA hiI ntazingatia nifufue la kwangu lililokufa

    ReplyDelete
  2. Nimekuelewa sana, tatizo Mimi yuko mbali tunaishia kwenye cmu cwezi kumfata

    ReplyDelete
  3. somo nzur, nimejifunza mengi yatakayoendeleza furaha kwenye maisha ya mahusiano.

    ReplyDelete
  4. Nimejifunza kitu nitafufua penz langu lililokufa🙏🙏

    ReplyDelete
  5. Dah paka nmelia..wengine hapa ndo kila cku ya mungu ugomvi..moyo unakataa kabisa kupenda tena..ila umenisaidia..ntaweka nia na nijaribu..asante sana

    ReplyDelete
  6. Mimi langu ndio linaelekea kufa nataka nijitahidi in Shaa Allah kwa uwezo wa Allah ntafanikiwa nilikuwa kwenye sintofaham nifanyeje ila nimepata suluhisho ubarikiwe ndugu!

    ReplyDelete
  7. Asante sana, nakomaa na namba 6 hadi kieleweke

    ReplyDelete
  8. Mimi mpaka anataka kuondoka akaanze upya maisha yake yaani mwanaume amechoka mpaka sielewi naanzaje

    ReplyDelete

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...