Wednesday, July 9, 2014

MY REPENTANCE-1 (KUTUBU KWANGU)-1


Naitwa Flaviana Joel, mwanamke mwenye umri wa miaka ishirini na nane. Nilibahatika kuolewa miaka kumi iliyopita, nikiwa bado msichana mbichi katika umri wa miaka kumi na nane tu.

Niliolewa na mume wangu kipenzi, Ibrahim au Ibra kama mwenyewe nilivyozoea kumuita ambaye alikuwa akifanya kazi kwenye benki moja maarufu ambayo sitaitaja jina kwa sababu maalum, iliyopo hapa jijini Dar es Salaam.https://www.facebook.com/simulizizamajonzi
Kabla Ibra hajanioa, tulidumu kwenye uchumba kwa kipindi cha takribani mwaka mmoja, kipindi hicho nikiwa nasoma chuo kimoja cha uhasibu kilichopo Posta, katikati ya Jiji la Dar es Salaam, nikiwa ndiyo kwanza nimeanza mwaka wa kwanza.
Baada ya ndoa, mimi na Ibra tulihamia Mbezi Beach kwenye nyumba yetu ambako tuliishi pamoja mpaka tulipokuja kutengana kwa sababu ambazo ndizo hasa zilizonifanya nitafute nafasi hii ya kutubu hadharani na kukiri kwa kinywa changu yote niliyowahi kuyafanya.
Nimesukumwa kuja kusimulia mkasa wangu huu kwa sababu nataka watu wajifunze kupitia maisha yangu na Ibra. Najisikia aibu sana, najikaza tu kwa sababu nataka wanawake wenzangu waelewe kilichonitokea na kamwe wasifuate njia kama ambazo mimi nilipita. Pia iwe funzo kwa wanaume, hasa wale ambao wapo ndani ya ndoa.
Nasikitika kwamba nimekuwa kikwazo kikubwa katika maisha ya Ibra, mwanaume niliyetokea kumpenda kwa moyo wangu wote lakini kwa sababu ya mapungufu ya kibinadamu ambayo nitayaelezea, nikageuka na kuwa mwiba mkali kwenye maisha yake.
Nilisema tangu awali na nitaendelea kusema kwamba sijawahi kutokea kumpenda mwanaume kama nilivyompenda Ibra ila hata sielewi ni kitu gani kilichosababisha haya yote yatokee.
Najisikia uchungu sana ndani ya moyo wangu hasa nikiwatazama wanangu Joel, James na Mahiza ambao bado walikuwa wakihitaji malezi ya baba na mama lakini kwa kukosa akili kwa mama yao (mimi) leo wanateseka mno.
Siwezi kumlaumu Ibra kwa sababu alijitahidi kwa kadiri ya uwezo wake kufanya yale ambayo mwanaume anapaswa kuyafanya katika ndoa yake ingawa pia alikuwa na udhaifu mkubwa ambao ndiyo uliosababisha leo hii nipate nguvu ya kuja kutubu hadharani na kuwa sauti ya wengine ambao waume zao wana matatizo kama aliyokuwa nayo mume wangu Ibra lakini hawana pa kusemea.
Naamini kutubu kwangu na kueleza ukweli wa kila kitu kwenye maisha yangu, kutakuwa chachu ya mabadiliko katika nyumba nyingi na utaokoa ndoa nyingi.
Ukimya unaua, naamini kuna wanawake wengi sana ambao wanakufa taratibu kwa sababu hawataki kuyasema matatizo ya ndoa zao hadharani, matokeo yake wanazalisha matatizo mengine kwa waume zao ambayo mwisho wake ni kama huu ulionitokea.
Kama kujiua isingekuwa dhambi, hakika ningeyakatisha maisha yangu lakini naogopa nitakachokutana nacho siku ya kiyama. Naamini kwa kuyasimulia haya, angalau kidogo nitapunguza mzigo unaonielemea ndani ya nafsi yangu.
Nawaomba radhi wote mlioumizwa na matendo yangu na mtakaoumizwa na ushuhuda huu, hasa kipenzi changu Ibra, watu wote wanaotufahamu na kubwa zaidi kwa mama yangu ambaye matendo yangu yamemfanya adharaulike na kila mtu kwani inaonekana alishindwa kunilea katika maadili mema.
Pia naomba Mungu wangu anisamehe na nitaendelea kumlilia kila siku kama nilivyofundishwa na mtumishi wa Mungu, Mchungaji Mwakatobe ambaye ndiye aliyeniongoza katika sala ya toba.
***
April 8, 2003
Dar es Salaam.
Ilikuwa ni asubuhi yenye mvua kubwa ambayo ilisababisha hali ya taharuki kwa wakazi wengi wa Jiji la Dar ambao tulikuwa tukitegemea usafiri wa daladala. Nakumbuka vizuri ilikuwa ni tarehe 8 ya mwezi wa nne, mwaka 2003. Naikumbuka vizuri tarehe hii kwa sababu ambayo baadaye nitaielezea.
Nilikuwa nimebeba begi langu begani na kujikunyata pembeni ya kituo cha daladala cha Morocco, kwenye makutano ya Barabara za Ali Hassan Mwinyi na Old Bagamoyo Road (hivi sasa inaitwa Mwai Kibaki Road), nikisubiri usafiri wa kuelekea chuoni, Posta.
Daladala siku hiyo zilikuwa za taabu sana kwa sababu ya hali ya hewa iliyosababisha foleni kubwa karibu kwenye barabara zote za Jiji la Dar es Salaam. Kama ujuavyo Jiji la Dar mvua ikinyesha kidogo tu basi barabarani hakupitiki kutokana na foleni.
Ilikuja daladala ya kwanza iliyokuwa inaelekea Posta lakini ilikuwa imejaza mno kiasi cha watu wengine kuwa wananing’inia mpaka mlangoni. Nikashindwa kupanda. Ikaja ya pili nayo ikiwa katika hali hiyohiyo, ikanibidi niendelee kusubiri.
Mvua nayo ilikuwa inaendelea kunyesha, safari hii ikiambatana na upepo uliosababisha wote tuliokuwa tumejibanza pale kituoni kuanza kulowa. Nilitamani kurudi nyumbani kwani ukiachilia mbali kero ya mvua, muda nao ulikuwa umeenda sana.
Nikiwa najishauri cha kufanya, gari dogo aina ya Toyota Carina lilikuja na kusimama pale kituoni, jirani kabisa na pale nilipokuwa nimesimama. Kioo cha upande wa kushoto kikashushwa kisha tukamsikia dereva akituambia kuwa kama kuna wanaoenda Posta, anataka kuwabeba watu wanne tu kwa sababu daladala zinasumbua.
Mimi nilikuwa wa kwanza kulifikia gari hilo dogo lakini zuri, nikawahi kufungua mlango wa mbele na kujitoma ndani. Abiria wengine wengi wakafuata na kuanza kugombania lakini kwa sababu gari lilikuwa na uwezo wa kubeba abiria wanne tu, watatu nyuma na mmoja mbele, ilibidi wengine wabaki.
Nilijiona kuwa na bahati kubwa, nikamgeukia dereva na kumsabahi huku nikimshukuru kwa msaada wake. Abiria wengine nao walifanya hivyohivyo, akaondoa gari na safari ya kuelekea Posta ikaanza. Kwa kuwa sote tulikuwa tumelowa, hakuna aliyekuwa na stori na mwenzake, kila mmoja akawa anajifuta maji.
Safari iliendelea taratibu kutokana na foleni na baada ya muda mrefu, hatimaye tulifika Posta. Kila mmoja alifungua nauli na kutaka kumpa dereva lakini mwenyewe alikataa na kutuambia kuwa ametusaidia tu kwa hiyo tusimlipe.
Tulimshukuru sana, sote tukashuka na kila mmoja akaendelea na hamsini zake. Baada ya lile gari kuondoka, nilikumbuka kuwa nilikuwa nimesahau begi langu lenye madaftari, vitabu na vifaa vyangu vingine vya kusomea. Nilijikuta nikichanganyikiwa ghafla, nikawa najilaumu kwa uzembe nilioufanya.
Ilibidi nianze kulifukuzia lile gari kwa nyuma lakini tayari nilikuwa nimechelewa, lilishajichanganya na magari mengine, hali iliyonipa wakati mgumu kulitambua kwani kulikuwa na magari mengi aina ya Carina Posta, tena yote yakiwa yanafanana.
Nilitoa simu yangu mfukoni lakini nilishindwa kuitumia kwa sababu sikuwa nikizijua namba za dereva. Nikajikuta nikiishiwa nguvu kabisa. Safari yangu yote haikuwa na maana tena kwa sababu nisingeweza kwenda chuo nikiwa sina vifaa vya kusomea.
Kwa kuwa bado mvua ilikuwa ikimwagika, nilisogea kwenye korido ndefu za Posta Mpya na kujibanza hapo pamoja na watu wengine wengi waliokuwa wamejisitiri mvua. Nikiwa bado najiuliza cha kufanya, simu yangu ilianza kuita. Nilipotazama namba ya mpigaji, ilikuwa ngeni kwangu.
Sina kawaida ya kupokea namba za simu nisizozijua lakini siku hiyo niliipokea haraka ilipoita mara moja tu.
“Halloo!”
“Haloo, nani mwenzangu.”
“Samahani, unamfahamu Flaviana Joel?”
“Ndiyo namfahamu, kwani vipi?”
“Kuna watu niliwapa lifti kwenye gari langu muda mfupi uliopita sasa kuna mmoja amesahau begi lake la vitabu, nilipopekua ndiyo nikaikuta hii namba imeandikwa nyuma ya kitabu kimoja. Naomba umpe namba yangu mwambie anitafute au nipe yake nijue namna ya kumfikishia mzigo wake,” alisema dereva wa ile Carina kwa sauti ya kiungwana mno.

Nilishusha pumzi ndefu na kuachia tabasamu, nikamwambia kwamba mimi ndiyo Flaviana, nikamsikia akicheka kidogo kisha akaniuliza nipo wapi kwa wakati huo. Nilipomuelekeza, aliniambia nimsubiri hapohapo anakuja.
Kweli baada ya kama dakika tano hivi, ile Carina ilipaki upande wa pili wa barabara, akanipigia simu na kuniuliza kama nilikuwa naliona gari. Nikatoka mbiombio na kukimbia kuvuka barabara. Kwa kuwa bado mvua ilikuwa inanyesha, nilipolifikia gari lake, alinifungulia mlango, nikaingia na kukaa kwenye siti ileile niliyokuwa nimekaa awali, nikamgeukia, na yeye akanitazama, macho yetu yakagongana.

Usikose next issue! Unaweza pia kusoma katika Gazeti la Risasi Jumamosi.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...