Saturday, January 7, 2012

MIMBA KUCHOROPOKA (MISCARRIAGE)

HASH POWER 7113
Tatizo la mimba kuharibika na kutoka (kuchoropoka) kabla ya umri wake unaotakiwa kukamilika, limekua likiwasumbua wanawake wengi. Kutokana na maombi ya wasomaji wetu, tutalijadili kwa kina tatizo hili ambalo kitaalamu huitwa Miscarriage.

MISCARRIAGE NI NINI?
Kwa kawaida, ili mtoto azaliwe, ni lazima mwanamke afanye tendo la ndoa akiwa katika siku zake za kupata ujauzito ambapo mimba hutungwa. Baada ya mimba kutungwa, mtoto hukaa tumboni kwa muda wa miezi tisa mbapo hupitia hatua mbalimbali za mabadiliko hadi kuwa binadamu aliyekamilika.

Inapotokea kuwa kitoto kimetoka tumboni kwa namna yoyote ile, kikiwa na umri wa chini ya miezi mitano (wiki ishirini), tatizo hilo huitwa Miscarriage.
Katika hali hii, kitoto kinakuwa hakijakamilika na hakiwezi kujitegemea chenyewe kwa mahitaji muhimu kama kupumua, jambo ambalo husababisha kifo.

NB: Mtoto akitoka akiwa ameshapita umri wa miezi mitano, tatizo hilo huitwa pre-mature birth (kuzaa njiti).


NINI HUSABABISHA MISCARRIAGE?
Zipo sababu nyingi zinazosababisha ujauzito uchoropoke.

  1. Matatizo ya Vinasaba (Genetic Factors)
Hitilafu katika kromosomu (Chromosomal abnormalities) ambayo husababisha vinasaba kuwa katika hali isiyo ya kawaida, inatajwa kuwa sababu kubwa zaidi inayosababisha ujauzito uchoropoke ukiwa na umri wa chini ya wiki 13.
Matatizo haya husababisha damu ya mama ishindwe kuendana nay a mtoto na kusababisha reactions ambazo humdhuru mtoto na kumfanya ashindwe kuhimili hali ya tumboni kwa mama. Hivyo ujauzito kuharibika.

2. Upungufu wa Homoni (Progesterone Deficiency)
Homoni ya Progesterone hufanya kazi kubwa kuanzia mamba inapotungwa mpaka mtoto anapozaliwa. Progesterone ndiyo huchochea uimara wa ukuta wa placenta ambao mtoto hujishikiza. Upungufu wa homoni hii husababisha ukuta wa mji wa mimba kushindwa kuhimili uzito wa mtoto, hali ambayo husababisha ujauzito kuharibika na kutoka kabla ya muda wake.


3. Umri Mkubwa
Kwa kawaida, mwanamke anapofikisha umri wa miaka 35 au zaidi, misuli (sphincters) ya mji wake wa uzazi hulegea na kupungua nguvu za kuweza kuhimili na kutunza kiumbe kinachokuwa ndani ya mji wa uzazi. Kulegea kwa misuli hii husababisha mimba kuchoropoka kwa urahisi.

4. Magonjwa
Wanawake wanaosumbuliwa na magonjwa kama kisukari, unene kupindukia (obesity), Polycystic Ovary Syndrome, malaria kali, magonjwa ya zinaa na mengineyo huwa katika hatari kubwa ya mimba zao kutoka.

5. Hitilafu Katika Kizazi
Baadhi ya wanawake huwa na mfuko wa mimba (uterus) ambao muundo wake siyo wa kawaida (T- Shaped Uterus). Wanawake wenye tatizo hili, huwa na hatari kubwa ya mimba zao kuharibika kabla ya kutimiza umri wa miezi tisa.

6. Maambukizi ya bakteria au fangasi
Maambukizi ya bakteria au fangasi husababisha misuli ya kizazi kushambuliwa na kisha kupoteza uwezo wake wa kuhifadhi ujauzito, jambo ambalo husababisha mimba kuchoropoka.

Sababu nyingine ni pamoja matumizi ya pombe kali, uvutaji sigara, matumizi ya dawa za kulevya, kemikali, matatizo ya kurithi n.k


DALILI ZA MIMBA KUCHOROPOKA (Symptoms of a miscarriage):

 1. Kutokwa na damu sehemu za siri
Dalili kubwa za miscarriage ni mama mjamzito kutokwa na damu (nzito au nyepesi) sehemu za siri kwa vipindi au mfululizo. Damu hizi hutoka kama zile zitokazo mwanamke anapokuwa kwenye siku zake na huambatana na maumivu makali ya tumbo chini ya kitovu.

 2. Maumivu makali ya viungo

Dalili nyingine za mimba inayotaka kuchoropoka ni maumivu makali ya mgongo, kiuno, nyonga na tumbo chini ya kitovu. Maumivu haya huanza taratibu lakini huongezeka kadiri muda unavyozidi kusonga mbele. Pia huambatana na kutokwa na damu kama ilivyoelewa hapo juu.


3. Kutokwa na uchafu sehemu za siri
Dalili nyingine kubwa ya Miscarriage ni mama mjamzito kuanza kutokwa na uchafu wenye rangi sambamba na mabonge ya damu sehemu za siri.

ANGALIZO: Dalili hizi pekee hazitoshi kuashiria kuwa tayari ujauzito umeharibika ila mama mjamzito anapoona moja kati ya dalili hizi au zote, anashauriwa kuwahi hospitali kuonana na daktari haraka iwezekanavyo.

 Endapo mama atachelewa, atakuwa anajisababishia matatizo zaidi kwani sumu za kiumbe kilichoharibika huharibu mfuko wa uzazi na kusababisha matatizo makubwa siku za mbeleni ikiwemo ugumba.


JE, KUFANYA MAPENZI UKIWA MJAMZITO KUNA MADHARA?
Swali: Pole na kazi dokta, mimi ni mwanamke mwenye umri wa miaka 22. Nimeolewa na hivi sasa nina ujauzito wa miezi mitano. Tatizo linalotusumbua mimi na mume wangu ni kuwa, tangu nipate ujauzito hamu ya kushiriki tendo la ndoa imeongezeka sana lakini tunaogopa kufanya kwa sababu tuliwahi kuambiwa kuwa tunaweza kumdhuru mtoto tumboni na ujauzito kutoka. Tunaomba ufafanuzi wako daktari, je ni kweli kuna madhara kufanyamapenzi ukiwa mjamzito?
Msomaji, Hanang, Manyara

Jibu: Siyo kweli kwamba kufanya mapenzi ukiwa mjamzito kutasababisha mimba kuharibika na kutoka. Jambo la kuzingatia ni kutotumia staili zinazobana au  kuumiza tumbo au kufanya mapenzi kwa muda mrefu. Tendo la ndoa linalofanywa kwa wastani husaidia kulainisha njia ya uzazi hivyo kupunguza matatizo wakati wa kujifungua. Inashauriwa kuwa ujauzito ukifikisha miezi nane, wanandoa waache kufanya tendo hilo mpaka mama atakapojifungua na kupona.

KUZUIA MIMBA KUCHOROPOKA
Hakuna tiba ya moja kwa moja inayoweza kuzuia tatizo la mamba kuchoropoka ila kwa kuzingatia vyanzo vya tatizo hili, ni rahisi kuliepuka.

  1. kuacha tabia hatarishi
Tabia kama ulevi wa kupindukia, matumizi ya dawa za kulevya na sigara kwa wanawake wajawazito yakiepukwa, hupunguza hatari ya miscarriage.

  1. Kufanya mazoezi
Inashauriwa kuwa, mama mjamzito ajenga mazoea ya kufanya mazoezi mepesi angalau mara tatu kwa wiki kwa muda usiopungua nusu saa. Mazoezi kama kutembea na mengine mepesi husaidia kuimarisha misuli ya kizazi na hivyo kupunguza hatari ya mamba kuchoropoka.

  1. Vyakula
Inashauriwa mama mjamzito kula vyakula vyenye madini ya Zinc, Magnesium, Vitamin B6 na Vitamin C kwa wingi ili kulinda ujauzito wake. Vyakula vitokanavyo na nafaka, mimea jamii ya mikunde, karanga, kiini cha yai, mboga za majani na matunda  husaidia kuimarisha afya ya mama na mtoto hivyo kuzuia tatizo hili.

  1. Kupata chanjo
Akina mama wajawazito wanashauriwa kuhudhuria kliniki mara kwa mara kwa ajili ya kupatiwa chanjo za magonjwa hatarishi ambayo husababisha ujauzito kuharibika na kutoka.

  1. Kupima afya mara kwa mara
Akina mama wajawazito ni lazima wajenge mazoea ya kwenda kupima afya zao mara kwa mara na kuangalia uwepo wa magonjwa kama ya zinaa na mwengineyo, na kama yapo watibiwe haraka ili kulinda kiumbe kilichopo tumboni.




No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...