Monday, April 25, 2011

MY HEART mwisho

Akatii amri na kuwapeleka kwenye chumba walichojificha Bi Miriam na wanae. Yale majambazi hayakuwa na simile, yalianza kupekua chumba kizima. Baada ya muda mfupi yaligundua kuwa walikuwa ndani ya kabati la nguo. Yakawatoa na kuanza kutembeza kichapo bila huruma.
"Mumeo na wanao wengine wako wapi?" Jambazi moja lilimuuliza Bi. Miriam kwa ukali. Hakuwa na jibu la kuwapa, hali iliyofanya apigwe na kitako cha bunduki na kudondoka chini. Yakambana mke wa mwalimu Kihiyo aliyekuwa anatetemeka kwa hofu, akawaongoza kwenye chumba cha pili alikokuwa amejificha mzee Khalfan na wanae wawili, hawakumkuta mtu... Wakati wakiendelea kupekua, wakasikia purukushani kubwa uani.
Mzee Khalfan alikuwa akipambana na lile jambazi lililomfuata uani. Kwa kasi ya ajabu alichomoka kutoka chini ya kibanda cha kuku alikokuwa amejificha na kulikaba shingoni kwa nguvu, wakawa wanavutana huku na kule hadi jambazi likazidiwa nguvu. Mzee Khalfan akafanikiwa kulipokonya bunduki na kufyatua risasi mbili zilizopenya sawia ubavuni na kulifanya lile jambazi lipige yowe kuu. Kwa kasi ya ajabu mzee Khalfan akaanza kupanda ukuta kuelekea upande walikokuwa wamerukia Girbons na Khaleed. Alipofika juu ya ukuta, alishangaa kuona anamulikwa na tochi zaidi ya tano, milio mfululizo ya risasi ikasikika, moja ikapenya kwenye mguu wa Khalfan na kumfanya adondokee kwa nje. Akatua kwenye mikono ya wanae, Khaleed na Girbons ambao bila kupoteza muda walianza kutimua naye mbio kuelekea porini.
Yale majambazi yakabaki kutoa huduma kwa mwenzao aliyepigwa risasi ubavuni. Mengine yakaruka ukuta na kuanza kuwafukuza porini. Je nini kitaendelea? Usikose wiki ijayo.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...