Monday, August 2, 2010

URAIBU WA MADAWA YA KULEVYA (DRUG ADDICTION)

Hapa tutalitazama kwa upana tatizo linalowasumbua vijana wengi ambao wako katika kipindi cha mpito cha kutoka utoto kuingia utu uzima (Adolescence). Pia kuna idadi kubwa ya watu wazima ambao nao wanasumbuliwa na tatizo hili, hivyo ni matumaini yangu kuwa mada hii itakuwa ni ya manufaa makubwa.

URAIBU(ADDICTION) NI NINI ?
Uraibu ni ile hali ambayo mtumiaji wa dawa za kulevya anakuwa sugu, mtegemezi na asiyeweza kujitoa mwenyewe kutoka kwenye tatizo la utumiaji wa dawa za kulevya au pombe. Watu wenye uraibu wa dawa za kulevya hujikuta katika hali ngumu sana wakikosa kutumia dawa hizo hata kwa muda mfupi tu. Wengine husinzia na kuwa kama wagonjwa, wengine hutetemeka viungo vya miili yao huku wengine wakitokwa vidonda mdomoni mpaka wapate dozi nyingine ndiyo wachangamke.

URAIBU HUANZAJE?
Vijana wengi wamejikuta wakitopea katika matumizi makubwa ya dawa za kulevya kutokana na kutaka kujaribu. Utafiti wa kisayansi umebaini kuwa madawa kama Heroine na Cocaine yana kiwango kikubwa cha Uraibu (Addiction) ambapo mtu akianza kujaribu kutumia mara moja, hujikuta akitamani kurudia tena, huku kiwango cha dozi kikiongezeka taratibu, mpaka kufikikia hali ya uraibu (Uteja). Dawa nyingine kama bangi, Mirungi na Mandrax hazina kiwango kikubwa cha Uraibu na humchukua mtu muda mrefu mpaka kufkia uteja, lakini Uraibu wake hudumu zaidi akilini kuliko madawa mengine.

Ni dhahiri kwamba, mtu akitumia dawa za kulevya au pombe, akili yake hubadili namna ya utendaji kazi wake. Umakini hupungua, uwezo wa kufikiri na kuchanganua mambo hupungua, kupoteza kumbukumbu na hata maamuzi yake huwa siyo ya kueleweka. Mtu huyu anapoendelea kutumia dawa za kulevya, hali hii huota mizizi katika akili yake, na kama asipopata tiba ya haraka, anaweza kuishia kwa kurukwa na akili na kuwa kichaa au kupoteza fahamu.

KWA NINI VIJANA WENGI NI WARAIBU?
Utafiti wa kina umebaini kuwa vijana hususan wa kiume ndiyo wanaoongoza kwa kusumbuliwa na uraibu. Hii ni kutokana na ukweli kwamba vijana wa kiume huwa na tamaa ya kutaka kujaribu kila kitu wanachokiona au kukisikia, huyafikia kwa urahisi maeneo kunakouzwa madawa ya kulevya, na hukutana kirahisi na watumiaji wengine na kasha kuunda urafiki ambao mwishowe huishia kwenye uraibu. Ni jukumu la kila kijana kutojihusisha na matumizi ya dawa za kulevya, kwani athari zake kwa mwili wa binadamu ni kubwa.

DALILI ZA MTU MWENYE URAIBU
Japokuwa dawa za kulevya hufanya kazi tofauti katika mwili,. Madhara yake huwa hayatofautiani sana, na kwa maana hiyo waraibu wa zina zote za dawa za kulevya huwa na dalili zinazofanana. Dalili za uraibu (Addiction) ni kama ifuatavyo:
-Kushindwa kutimiza majukumu: Watu wenye uraibu hushindwa kutimiza majukumu yao katika sehemu zao za kazi au shuleni. Kama ni mwanafunzi ataanza kutoroka vipindi, atakuwa mvivu na kama jitihada zisipotumika anaweza kuacha kabisa masomo.

- Kuhatarisha maisha mara kwa mara:
mraibu huwa na kawaida ya kurahisisha mamabo hata yale ambayo kiuhalisia ni ya hatari. Waraibu huendesha magari kwa kasi kubwa wakiwa wamelewa, hujidunga kwa sindano moja waraibu zaidi ya mmoja, hufanya ngono hovyo bila ya tahadhari yoyote, hali ambayo huongeza hatari ya kupata magonjwa ya Zinaa na Ukimwi.


DALILI ZA MTU MWENYE URAIBU
Wiki iliyopita tulianza kuliangalia tatizo la uraibu wa dawa za kulevya, tukaangalia maana ya uraibu, unavyotokea na dalili za mtu mwenye uraibu. Leo tunaendelea na mada yetu, na tunaendelea kuziangalia dalili anazokuwa nazo mtu mwenye tatizo la uraibu.

-Kuvunja sheria
Dalili nyingine ya uraibu ni kuvunja sheria kwa makusudi. Watumiaji wa madawa ya kulevya hujikuta wakikabiliwa na mkono wa sheria mara kwa mara kutokana na kujihusisha katika vitendo viovu kama ujambazi, ugomvi na kukamatwa na madawa ya kulevya.

- kuvurugikiwa akili unapokosa dawa za kulevya
Watu wenye uraibu wa dawa za kulevya huwa kama wamechanganyikiwa akili wanapokaa hata kwa muda mfupi bila ya kupata dozi. Dalili za kuvurugikiwa akili ni kama kuzungumza peke yako, kuchekacheka hovyo bila ya sababu ya msingi, kushindwa kuzuia mate kutoka mdomoni n.k

- kuzidi kuongeza dozi ya dawa ya kulevya
Mwili ukifikia hatua ya uraibu, huhitaji kiwango kikubwa zaidi cha madawa ili kufikia hali ya kulewa kama ilivyokuwa awali. Kama mwanzoni mtu alikuwa akitumia kete moja kulewa, akifikia hatua ya uraibu huweza kutumia kete tatu, nne au zaidiya hapo ili kuelewa kama mwanzoni. Hali hii ikizidi huweza kusababisha tatizo la Kujiovadozi ambalo husababisha kifo cha ghafla.

-Kushindwa kuyamudu maisha
Uraibu wa madawa ya kulevya humfanya mtumiaji kushindwa kuyamudu maisha kwa kushindwa kupangilia muda wake vizuri. Badala ya kutumia muda mwingi kufikiria masuala ya maendeleo, mraibu hutumia muda mwingi kufikiria namna atakavyopata dozi nyingine ya madawa, au jinsi atakavyopata pesa kwa ajili ya kununulia dozi nyingine.

-Kupoteza kumbukumbu
Matumizi ya dawa za kulevya huufanya ubongo wa mhusika kushindwa kutunza kumbukumbu na kupoteza umakini. Ni kawaida kabisa kwa mraibu kupoteza kumbukumbu juu ya mambo ya muhimu, na kama ni mwanafunzi hujikuta katika wakati mgumu sana kutokana nakusahau sahau yale anayofundishwa darasani.

-Kuendelea kuwa mtumwa wa dawa za kulevya
Matumizi ya dawa za kulevya yakifikia hatua ya uraibu, mhusika hata kama anazijua athari zake, hawezi kujitoa mwenyewe mpaka apate msaada mkubwa wa kisaikolojia na kitabibu. Hata kama atakuwa anazijua athari zake, bado mraibu ataendelea kutumia tu dawa za kulevya.

-Kupoteza furaha ya vitu ambavyo zamani ulikuwa unavifurahia
Mraibu wa dawa za kulevya hupoteza furaha aliyokuwa nayo kabla ya kuanza matumizi ya dawa za kulevya, na hata yale mambo ambayo awali alikuwa anayapendas sdana hugeuka na kuwa kero kubwa kwake. Kama alikuwa ni mwanamichezo, taratibu ataanza kuichukia michezio na hatimaye atakuwa hashiriki tena.

-Kubadili marafiki kila mara
Mraibu wa dawa za kulevya hubadili kabisa marafiki na kuachana na wale ambao alikuwa akiwapenda kabla ya kuazna matumizi ya dawa za kulevya, na kujiunga na waraibuwenzake ambao ndiyo huwa marafiki zake makubwa.

HATUA TANO ZA KUANZA KUONDOKANA NA URAIBU
Uraibu kama yalivyo magonjwa mengine ya akili hutibika. Tofauti ni kwamba mhusika mwenye we lazima awe tayari kuachana nahali hiyo na kuziona hatari zilizopo mbele yake kama ataendelea kutumia dawa za kulevya. Zifuatazo ni hatua tano muhimu ambazo kama zikifuatwa kwa umakini zinaweza kumsaidia mtu mwenye tatizo la uraibu kuondokana na tatizo hilo.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...