Wednesday, May 19, 2010

USILIE TENA GENEVIV -22

Mchuma janga hula na wa kwao. Binti mdogo Geneviv anajikuta katika matatizo makubwa baada ya kupata ujauzito wakati akifanya biashara haramu ya Uchangudoa. Kwa msaada wa rafiki yake Alice, wanaenda kwenye Dispensari moja maarufu inayofanya kazi hiyo, kwa ajili ya kufanya abortion, huku wakijitahidi kuficha siri ili mama yake Geneviv asigundue chochote. Daktari waliyemkuta anamtamani Geneviv, na kabla ya kumfanyia abortion anamuingilia kimwili.

Geneviv anayakubali yote kutokana na hali aliyokuwa nayo. Bahati mbaya Daktari anakosea kumtoa mimba, hali inayomuingiza kwenye matatizo makubwa sana. Upande wa pili mama yake anaingiwa na wasiwasi baada ya kutomuona mwanae kwa siku mbili mfululizo. Kwa kuwa hali yake tayari imeshakuwa nzuri, anaruhusiwa kutoka Hospitali. Je atafanikiwa kugundua kilichomsibu mwanae? Atafanikiwa kumuokoa? Nini kitafuatia? Twende pamoja.

Bi Patricia alishangaa kuona muda wa chakula cha mchana unapita bila ya Geneviv kumpelekea chakula wakati haikuwa kawaida yake. Akawa anaangaza macho huku na kule akidhani labda atamuona akija. Mpaka jioni inafika alikuwa hajafika. Muda mfupi baadae Alice alienda kumpelekea chakula akiwa peke yake, hali iliyomshtua sana. “Mwenzio yuko wapi, mbona hata mchana hakuja?” Bi Patricia alimdaka juu juu Alice na kuanza kumhoji maswali mfululizo. Ikabidi Alice adanganye…

“Geneviv anajisikia vibaya mama, kichwa na tumbo vinamuuma tangu asubuhi tulivyotoka hapa. Nimemuacha amepumzika lakini anaendelea vizuri”
Bi patricia hakutaka kuhoji zaidi, akaishia palepale ingawa alipomkazia macho Alice alisoma kitu kwenye macho yake. Muda wa kuoa wagonjwa ulipoisha akaondoka na vyombo kurudi nyumbani. Bi Patricia alishaingiwa na wasiwasi juu ya mwanae Geneviv, akabaki kumuachia Mungu.

Tumbo liliendelea kumuuma Geneviv bila kupata nafuu. Japokuwa alikuwa amepewa dawa za kumaliza maumivu na kusafisha tumbo, aliugulia usiku kucha akijigalagaza kitandani kwa Alice. Alikuwa akisikia maumivu makali sana ambayo yalikuwa yakiongezeka kadri muda ulivyokuwa unaenda. Mpaka kunakucha, alikuwa hajapata hata tone la usingizi. Kutokana na maumivu, alishindwa kumuandalia kifungua kinywa na kumpelekea mama yake hospitalini. Ikabidi Alice aende tena peke yake.

“Vipi mbona umekuja tena peke yako, ina maana bado Geneviv hajapata nafuu, au ni Malaria? Lakini bahati nzuri na mimi nimesharuhusiwa, nisubiri tuondoke wote kurudi nyumbani,” aliongea Bi Patricia, kauli ambayo ilimshtua sana Alice. Akajua siku yao ya kubainika imefika.

“Sijui itakuwaje huko nyumbani akienda kumuona Geneviv, leo tumepatikana” alikuwa akijisemea Alice wakati akimsaidia mama Geneviv kufungasha vitu vyake tayari kurudi nyumbani baada ya kupona na kuruhusiwa kutoka hospitali. Baada ya muda mfupi, Bi Patricia alikuwa tayari ameshakusanya vitu vyake vyote tayari kwa safari ya kurudi nyumbani baada ya kukaa Hospitali kwa muda mrefu. Alice alikuwa akimsaidia na muda mfupi baadae wakawa ndani ya gari tayari kwa kurudi nyumbani.

Alice alishindwa kuificha hofu yake kwani alikuwa akifahamu fika hali aliyomuacha nayo Geneviv. Alijua lazima tatizo lingine kubwa lingetokea baada ya Bi Patricia kufahamu mchezo mchafu walioucheza na Geneviv. Akaamua kufanya kitu ili kunusuru shari iliyokuwa jirani kutokea.
***
Geneviv alikuwa akiendelea kuugulia maumivu makali ya tumbo, mara ujumbe mfupi wa simu ukaingia kwenye simu yake ya mkononi aliyoinunua siku za karibuni. Ulikuwa umetoka kwa Alice na ulisomeka hivi…

… “Shosti leo tumepatikana, sijui utamweleza nini mama yako…lazima atagundua tu kuwa umefanya abortion. Hivi saizi ndio tunatoka nae hospitali, amesharuhusiwa na baada ya muda mfupi tutakuwa tayari tumefika!”

Baada ya kumaliza kuusoma ujumbe ule kwenye simu yake, Geneviv alijikuta ameshtuka
Kupita kawaida. Hakutegemea kuwa mama yake angetoka Hospitali siku ile, na zaidi kilichomchanganya ilikuwa ni hali aliyokuwa nayo.

Alijua lazima mama yake angemgundua na alijua ataumia sana akiufahamu ukweli. Akajikuta amepona ghafla… alijitahidi kuinuka kitandani na kwa haraka akavaa vizuri.

Lengo lake ilikuwa ni kumkimbia mama yake ili kuepusha matatizo mengine ambayo yangetokea baada ya mama yake kuujua ukweli.

Alipokuwa tayari alitoka mpaka ndani mwao na kwa haraka akachukua kalamu na karatasi na kuandika ujumbe akimdanganya mama yake kuwa kichwa na tumbo vimemzidia hivyo ameenda hospitali. Akili yake ilikuwa ikifanya kazi kwa spidi ya ajabu. Alipomaliza kuandika uongo alitoka na akawa anajivuta kuelekea mtaa wa nyuma. Alipohakikisha amefika mbali na kwao, alimpigia simu dreva teksi aliyekuwa anakuja kuwachukua usiku na Alice, na akamwambia aende haraka kumchukua.

Muda mfupi baadae akawa ameshafika na kumfungulia Geneviv mlango. Akaingia ndani ya gari nakumuamuru dereva aondoe gari upesi.

“Mbona leo mapema aunt, si nikupeleke kiwanja kilekile cha sikuzote?” Aliuliza dereva Taksi wakati akiwasha gari na kuondoka. Alikuwa amezoea kuwachukua Alice na Geneviv na kuwapeleka kwenye biashara yao ya Uchangudoa, akajua na muda huo ndiko Geneviv alikokuwa anaenda.

Geneviv hakujibu kitu zaidi ya kuendelea kuugulia tumbo. Alipanga kwenda gesti yoyote na kupanga chumba mpaka apate nafuu ndio arudi kwa mama yake. Alijua yale maumivu ni ya muda mfupi na yangeisha kama daktari Maguru alivyokuwa ameahidi na kumpa moyo.

“Nishushe hapo kwenye hiyo gesti…aliongea Geneviv kwa sauti ya chini akionyesha namna alivyokuwa akisikia maumivu. Alimlipa dereva pesa yake na akajikongoja mpaka ndani alikochukua chumba self contained na kujifungia. Tumbo liliendelea na sasa alishindwa kuvumilia, akawa analia kimyakimya.

“Eeeh Mungu nisamehe dhambi zangu! Niponye tumbo langu nirudi nyumbani kwa mama, why me my Lord!” alikuwa akiongea Geneviv huku akilia.

Je nini Kitaendelea? Usikose wiki ijayo.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...