Sunday, October 11, 2009

MY HEART IS BLEEDING! (MOYO WANGU UNAVUJA DAMU) -I


MY HEART IS BLEEDING! (MOYO WANGU UNAVUJA DAMU) -I

(SWAHILI VERSION)
“Beyond The Seen Scene!… Beyond The Grave Yards… There Laid…
The Hearts That Bleeds, Hearts Of Desperately Broken Victims, The Weak!! Their Hearts Are Bleeding…, But Finally A Healing Balm For Every Wound Is Found, When The Darkness Takes Its Flight…”
My Heart Is Bleeding…
(moyo wangu unavuja damu)
Novel story by:
Aziz Hashim-Hash power
amenibarikihash@rocketmail.com

EPISODE I
SEHEMU YA KWANZA
Ilikuwa ni jumatatu ya kwanza ya mwezi Septemba, asubuhi tulivu yenye anga lililopendezeshwa na rangi ya bluu, jua la asubuhi likiwa ndio linachomoza na kuzidi kuipendezesha siku ya kwanza ya juma.
Umati mkubwa wa watu waliokuwa wamefurika katika viwanja vya mahakama kuu ulitosha kumfanya yeyote asiyejua kilichokuwa kinaendelea mahali hapo kupigwa na butwaa. Ilikuwa ni idadi kubwa kabisa ya watu kuwahi kutokea tangu mahakama hiyo ilipoanza kufanya kazi rasmi miaka kadhaa iliyopita…




Kwa kadri muda ulivyokuwa unaenda, ndivyo watu walivyokuwa wanazidi kuongezeka katika eneo la kuizunguka mahakama. Wote walikuwa wamekuja kwa lengo la kutaka kusikiliza mwendelezo wa kesi nzito ya mauaji iliyokuwa ikimkabili kijana mdogo kabisa, ambaye kwa haraka haraka ungeweza kumkadiria kuwa na umri usiozidi miaka ishirini.

Hiyo haikuwa kesi ya kwanza ya mauaji kutolewa hukumu mahakamani hapo, lakini kesi hii ilionekana kuwa tofauti na kesi nyingine, kwani ilionekana kuzigusa hisia za watu wengi sana.

Iliwawia vigumu askari wa kutuliza ghasia na wale wa jeshi la polisi kuweza kuwatuliza watu wote waliofurika eneo hilo kwani walikuwa ni wengi sana na walikuwa bado wanazidi kuongezeka kwa kadri muda ulivyokuwa unaenda.

Ving’ora vya magari ya polisi na kelele za mbwa wa polisi vilizidi kufanya hali ya mahali hapo izidi kuzizima, huku kila mtu akiwa na hamu ya kutaka kujua nini kingeendelea. Vurugu zilizidi kupamba moto na utulivu na amani vikatoweka kabisa katika viwanja vya mahakama wakati gari lililombeba mtuhumiwa likiwa linaingia mahakamani hapo.
Watu walikuwa wakipiga kelele na kukanyagana kila mmoja akitaka japo amwone mtuhumiwa wa kesi hiyo nzito. Kila mtu alikuwa analikimbilia gari lililombeba mtuhumiwa na muda mfupi baadae gari lote likawa limezingirwa kila upande, kiasi cha kushindwa kuelekea kwenye lango kuu la mahakama .

Akina mama waliokuwepo eneo hilo walisikika wakiangua vilio kama wanaomboleza msiba mzito, huku vijana na watu wazima wakishindana nguvu na polisi wa kutuliza ghasia waliokuwa wakiwazuia wasimuone mtuhumiwa.

Kilichoendelea sasa ikawa ni vurugu mtindo mmoja, Polisi virungu na mabomu… raia mawe na fimbo. Polisi wa kutuliza ghasia walioneka kuanza kuzidiwa nguvu na raia hali iliyowalazimu kuanza kufyatua hovyo risasi hewani na kurusha mabomu ya machozi ili kuutawanya umati mkubwa wa watu waliokuwa wamelizingira gari alimokuwemo mtuhumiwa.

Baada ya nguvu kubwa kutumika kuwadhibiti raia, hatimaye ikalazimu gari lililombeba mtuhumiwa lirudi kwenye gereza kuu mpaka hali itakapokuwa shwari. Baada ya patashika lililodumu kwa takribani masaa mawili, hatimaye hali ilitulia.

Polisi wa kutuliza ghasia walikuwa wameongezwa maradufu, wengi wakiwa ni wale wa kikosi maalum cha mbwa wakiwa wametapakaa karibu kila sehemu sehemu kuizunguka mahakama.

Baada ya hali kuwa shwari hakimu aliamuru mtuhumiwa akaletwe na kupandishwa kizimbani tayari kwa kusomewa mashtaka mazito ya mauaji yaliyokuwa yakimkabili.

Safari hii ilibidi gari lililombeba mtuhumiwa liingie kwa kupitia mlango wa nyuma “Emergency exit” ili kuzuia hali kama ile iliyojitokeza awali.

Hatimaye mtuhumiwa aliingizwa mahakamani chini ya ulinzi mkali na akapandishwa kizimbani. Utaratibu wa kawaida wa kuendesha mashtaka ukaanza huku Jaji mkuu Profesa kadir Mudhihir Simba akiwa ndiye anayetakiwa kuisikiliza kesi ile na kuitolea hukumu ya mwisho.

Minong’ono ya chinichini ilikuwa ikisikika kutoka pande zote za mahakama huku watu wakiwa hawaamini kuwa ni kweli yule aliyekuwa kizimbani upande wa kushoto wa hakimu ndio mtuhumiwa aliyeifanya nchi nzima kutetemeka kwa hofu kutokana na mauaji makubwa na ya kutisha aliyokuwa ameyafanya.

Huyo ndio alikuwa mtuhumiwa aliyezigusa hisia za watu wengi kuliko kawaida kiasi cha kufanya kila mtu awe na hamu ya kutaka kumuona na kujua nini hatma yake. Kijana mdogo kabisa, mrefu wa wastani mwenye rangi ya maji ya kunde, ambaye ungemkadiria kuwa na umri usiozidi miaka ishirini.

Usoni hakuonyesha wasiwas hata kidogo na alikuwa akitabasamu japokuwa alikuwa akikabiliwa na kesi nzito sana ya mauaji ya kutisha ya idadi kubwa ya watu, akiwa amewaua wote kwa mkono wake. Alikuwa ametulia kimya akisubiri kuona nini hatma yake.

Minong’ono ilikuwa ikizidi kuongezeka, na zaidi akinamama ambao hawakuweza kujizuia kulia kwa uchungu kwani hakika hukumu ambayo ilikuwa ikisubiriwa huenda ndio ingekuwa kali zaidi kuliko zote zilizowahi kutolewa.

Kilichovuta hisia za watu wengi ni sababu ambazo zilifanya kijana huyu mdogo kufanya mauaji makubwa na ya kutisha kiasi kile. Ni sababu ambazo ilihitajika mtu makini sana kuweza kutoa hukumu. Na hii ndiyo iliyosababisha kesi hii kuahirishwa mara saba mfululizo licha ya kwamba upelelezi ulishakamilika siku nyingi na vithibitisho vyote vilikuwa vimefikishwa mahakamani.

Mahakimu wote walikuwa wakijitoa katika hatua za mwisho za kesi hyo huku kila mmoja akitoa sababu zake binafsi. Mwishowe ilibidi jaji mkuu aingilie kati na kuamua kuisikiliza mwenyewe kesi ile baada ya mahakimu karibu wote kuonekana wanaikwepa.

Waliokuwa wakifahamu kisa na mkasa kilichopelekea kijana yule mdogo kufanya vile, walikuwa wakimsikitikia kwani walijua hakika asingeweza kukwepa adhabu nzito iliyokuwa inamngoja. Hakuna aliyeonekana kuwasikitikia wahanga wa mauaji yale kwani wote walistahili kufa kwa waliyoyafanya.
“Mwachieni huru mwanetu!”

Alisikika mama mmoja akiongea kwa jazba iliyofuatiwa na kilio cha kwikwi. Kwa mujibu wa taratibu na sheria za mahakamani hapo, hakuna yeyote aliyeruhusiwa kuongea chochote wakati kesi ikiendelea. Lakini kwa jinsi kesi hiyo ilivyozigusa hisia za watu, mama yule alijikuta ameropoka na kuungwa mkono na umati wote uliokuwemo mle ndani. Ilibidi jaji mkuu atumie busara zake kurudisha utulivu mahakamani kwani vurugu ilikuwa almanusra ianze tena bada ya wanausalama kutaka kumtia nguvuni mama yule kwa kuvunja taratibu za mahakama.

Baada ya muda mfupi hali ikarudi kuwa shwari. Zilisikika kelele za karatasi tu, za jalada la kesi zilizokuwa zinapekuliwa na jaji mkuu, Profesa Kadir Mudhihir Simba. Watu walikuwa wakiwatazama mtuhumiwa na hakimu kwa zamu zamu. Ungeweza kudhani ni mchezo wa kuigiza kwenye luninga au tamthilia nzuri , lakini haikuwa hivyo.

Jaji mkuu aliuvunja ukimya uliokuwepo mahakamani hapo kwa kuanza kumsomea mashtaka mtuhumiwa, na kabla hajaendelea kutoa hukumu akamuuliza mshtakiwa…

“Je! Ndugu mshtakiwa una lolote la kujitetea kabla hukumu haijatolewa?”
Swali lile lilizua upya minong’ono ambayo iliongeza shauku ya umati ule kutaka kusikia mshtakiwa atajibu nini.

“Mtukufu hakimu, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Kwangu mimi huu sio utetezi bali ni ushuhuda wa yale yaliyonifanya niwaue mashetani hawa.Ninachoweza kusema ni kwamba, nakiri kufanya mauaji makubwa na ya kutisha kwa mikono yangu. Mikono yangu imetapakaa damu… damu ya kisasi. Sijuti kwa yale niliyoyafanya, zaidi najiona kama shujaa kwa kuweza kulipa kulipa kisasi cha damu kufidia maisha ya ndugu zangu waliouawa mikononi mwa mashetani hawa. Nahitaji kwenda kuungana na familia yangu kuzimu tukapumzike. Nihukumu kunyongwaaa! Nataka kufa! Mungu ibariki kazi ya mikono yangu! Amen.”

Mahakama yote ililipuka kwa vilio na makelele ya watu waliokuwa wakimsikitikia kijana yule na kuanza kushinikiza aachiwe huru. Watu wote walikumbwa na taharuki na kugubikwa na wingu zito la sintofahamu. Kwa ushuhuda ule mfupi alioutoa, hata wale ambao walikuwa wakimuona kama muuaji na gaidi hatari walianza kumuonea huruma.

Kila mmoja alionekana kusononeka sana moyoni, hata polisi waliokuwa wamejaa mahakamani mle kila mmoja alionekana kuingiwa na simanzi huku wakijitahidi kuonyesha ukakamavu wao kwa kuyazuia machozi. Hakuna aliyeonekana kuwaonea huruma watu waliokuwa wameuawa mikononi mwa kijana yule, kila mmoja aliunga mkono alichokifanya hata kama ilikuwa ni kinyume na sheria za nchi lakini kwa waliyoyafanya wote walistahili kufa.

Hali ilitisha. Kelele zile na maombolezo ya watu waliokuwa wakisikiliza kesi ile vilimtisha jaji mkuu ambaye sasa utulivu ulimuisha. Ni kweli kabisa kuwa kijana yule alikuwa na hatia kubwa mbele ya sheria na vithibitisho vyote vya kumtia hatiani vilikuwepo, lakini sababu zilizomfanya kuua ndizo zilizoifanya kesi ile kuonekana kuwa ngumu sana.

Jaji mkuu alikuwa akihaha kutafuta msaada kutoka kwa wazee wa baraza kuu la mahakama ili kujua nini kifanyike. Tai aliyokuwa ameivaa ilionekana kuwa mzigo kwake, akaivua na kuiweka juu ya meza huku kijasho chembamba kikianza kumtoka. Koti maridadi la suti alilokuwa amelivaa lilionekana kuwa mzigo pia, akalivua na kuliweka nyuma ya kiti alichokuwa amekalia.

Baada ya vuta nikuvute iliyoendelea kwa muda mrefu, hatimaye Jaji mkuu aliamua kusoma hukumu. Watu wote wakawa kimya kutaka kusikia hukumu ya mwisho ambayo jaji mkuu Profesa Kadir Mudhihir Simba angeitoa.

No comments:

Post a Comment

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 1

Mtunzi: Hashim Aziz (Hashpower) 0719401968 “Ngo! Ngo! Ngo! Fungua!” “Nanii?” “Fungua!” “Jitambulishe kwanza, wewe nani?” “Nimese...